Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kulipongeza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu mwaka huu limepitisha sheria ambayo imerejesha Tume ya Mipango. Halikadhalika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha sheria ile na kuitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaye Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo amekaa hapo na ametuandalia taarifa nzuri sana. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Profesa ns Waziri wa Fedha, taarifa zenu nimeanza kuzisikiliza, kwani mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti, tumezichambua na ushauri wetu ni kama ambavyo umewasilishwa na Mwenyekiti wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, nianze kwa kuangalia eneo la umuhimu wa utafiti katika kuandaa mipango ya maendeleo ya nchi kwa sababu kuna mjumbe mmoja Mheshimiwa Zaytun Swai nilimsikiliza, alitoa tafsiri ya Mpango. Alisema; “kupanga ni kuchagua.” Maana yake unakuwa na vitu vingi, unachagua lipi lianze na lipi lifuatie kutegemeana na umuhimu wake na vipaumbele vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naona kwamba eneo la utafiti ni nyenzo muhimu sana katika kupata mipango mizuri. Sasa tukiangalia kwenye Mfuko wa Utafiti wa Maendeleo (COSTECH) naona kwa mwaka 2024/2025 kwenye hii taarifa ya Mpango inaonesha kwamba mwaka 2022/2023 fedha ambazo zilitengwa kwa ajili ya utafiti ni shilingi bilioni 4.9 ambayo ni sawa na 0.003% ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kinyume kabisa na lengo la nchi yetu ambapo tumejiwekea malengo ya kila mwaka kwenye pato la Taifa angalau 1% iende kwenye eneo la utafiti. Hii 1% hatujaweza kuifikia. Kwa hiyo, naishauri Serikali vipindi vinavyokuja iongeze bajeti kwenye eneo la utafiti. Katika lile pato la Taifa angalau tuweze kutimiza hii 1% ya pato la Taifa. Kwa sababu tafiti na ripoti mbalimbali zinaonesha kwamba nchi nyingi ambazo zimepata maendeleo, utafiti umesaidia sana katika kuweka mipango ambayo ni madhubuti na endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa utafiti unasaidia sana watunga sera katika kufanya maamuzi ambayo ni sahihi. Kwa mfano, tukiangalia Benki ya Dunia, taarifa yake ya mwaka 2023 inaonesha kwamba Taifa la China limefanikiwa kupata maendeleo makubwa sana kwenye nyanja za afya, elimu, teknolojia na ubunifu kutokana na kuwekeza kwa kiwango kikubwa kwenye eneo la utafiti. Halikadhalika, hata nchi kama vile Rwanda na Korea Kusini zinaonesha kwamba wameweza kuzisaidia nchi zao katika kujenga, kuimarisha na kuendeleza uwezo wake wa ndani. Kwa hiyo, naishauri Serikali yangu iweze kutimiza angalau hili lengo la 1% ya pato la Taifa kwenye eneo la utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo vyuo mbalimbali hapa nchini; tuna Chuo Kikuu cha Sokoine SUA, vinaweza vikatumika katika kufanya tafiti kwenye maeneo mbalimbali. Kwenye eneo la kilimo nampongeza sana Waziri wa Kilimo amekuja na mikakati na mipango mizuri kwenye eneo la kukuza kilimo nchini. Ameungwa mkono na Serikali kwa kuongeza bajeti kwenye eneo la kilimo, lakini kwa kiwango gani tunavitumia vyuo vikuu vyetu kwenye eneo la utafiti ili viweze kuboresha mipango na mikakati ile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, eneo la tafiti naona ni eneo ambalo ni nyeti sana. Litatusaidia katika kuendeleza eneo la kilimo na masoko ya bidhaa mbalimbali hapa nchini. Kwa mfano, eneo la kilimo, tuna hawa watu wa NFRA, ukiwaangalia wao jukumu lao la msingi kisheria ni kuhifandhi tu chakula ili kukitokea tatizo waweze kusaidia maeneo yale yenye upungufu wa chakula. Tuna chombo gani ambacho kinasaidia haya mazao ya chakula kutafuta masoko kwa mfano mahindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri asubuhi amejibu vizuri swali la wakulima kucheleweshewa malipo yao ya mahindi. Alitoa ufafanuzi mzuri na nina imani kwamba Serikali itawalipa, kwa sababu sasa hivi mvua zimeshaanza, wanaanza kilimo, wanazitegemea kwa ajili ya shughuli. Kwa hiyo, tumewaambia watulie, wasubiri maelekezo aliyoyatoa asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tafiti katika maeneo haya ya masoko, kuongeza thamani ya mazao na vitu vingine yatasaidia sana kupata mipango madhubuti ambayo itachangia kwa kiwango kikubwa kuleta maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niongelee eneo la ardhi, mipango miji na maendeleo ya makazi. Tukiangalia eneo hili tunaona linakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinasababisha washindwe kufikia malengo. Tukiangalia kwa mfano eneo la makusanyo ya kodi za ardhi, kuanzia Julai, 2022 mpaka Mei, 2023 malengo yalikuwa ni shilingi bilioni 250.1 lakini ilifanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 132 ambayo ni 53.2% ya malengo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia changamoto ambazo zinaisababishia Wizara ya Ardhi ishindwe kufikia malengo: moja; uhaba mkubwa wa watumishi. Tuna vyuo vikuu vinatoa wahitimu kila mwaka, lakini ajira zake hazijatoka muda mrefu. Kwa hiyo, Wizara hii ingeweza kuongezewa wapima ardhi, maafisa mipango miji kwa sababu kuna ripoti ambayo inaonesha kwamba kasi ya ukuaji wa makazi holela ni 67%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, makazi holela yanakua kwa kasi na kasi ya upimaji wa ardhi haiendani na kasi ya ongezeko la idadi ya watu. Vilevile, tunatambua kwamba ardhi ikipimwa, kodi itaongezeka kwenye Serikali lakini wananchi watakuwa na usalama wa milki zao, vilevile watakuwa na dhamana ambayo itawawezesha kupata mikopo kwenye taasisi za fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili eneo nadhani tungeliangalia kwa kuongezea vifaa, lakini hata kupitia vile viwango ambavyo tunatoza kodi kulingana na eneo husika na matumizi ya ardhi. Je, ni rafiki? Zinalipika? Ule mfumo ambao tunautumia kudai kodi tungeutumia kama wa watu wa maji, muda ukifika unatumiwa message kwenye simu yako na control number kwamba unadaiwa kiasi hiki. Huo mfumo ukiwa rafiki, tutaweza kuongeza mapato eneo hili la kodi ya pango la ardhi. Kwa hiyo, napenda kusisitiza kwamba viwango vile viangaliwe lakini mifumo iboreshwe iwe rafiki inamvutia mlipaji kuweza kulipa kodi ya pango la ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile watumishi waliopo natambua kwamba ni chini ya 15% ya mahitaji yote yaliyopo nchini. Bajeti wanayopewa wangeweza kuongezewa ili wapime kwa kasi kubwa sana. Katika hili nampongeza sana Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Jerry Silaa, watu wa Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, wamefanya kazi nzuri sana Makete na Ludewa. Kwa hiyo, naomba waendelee kuongezewa fedha ili wafanye kazi nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile eneo ambalo napenda kuliangazia ni eneo la matumizi ya makaa ya mawe. Tunatambua kwamba kuna makubaliano huko ya Kimataifa ambayo yanakwenda kuondoa kabisa matumi ya makaa ya mawe ifikapo 2030. Sisi tuna zaidi ya tani bilioni tano ambazo hatujazichimba. Walau Kiwira na Ngaka kidogo tumeanza ambapo Ngaka wanatoa tani 250,000 na Kiwira tani 150,000. Lini tutazifikia hizi tani bilioni tano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukiangalia logistics, namna ya kutoa mkaa kule unakopatikana mpaka kupeleka kwenye bandari miundombinu nayo bado ni changamoto. Kulikuwa na mpango ule wa kujenga reli inayoanzia Mtwara mpaka Mbamba Bay, Tawi, Mchuchuma na Liganga. Sasa mradi huu wabia ambao wanatarajiwa, wanaanza kuangalia sasa Serikali inafanya nini kwenye kuanza kwa mradi wa Liganga na Mchuchuma? Kwa sababu bila kupata uhakika wa mzigo wa kusafirisha tunaweza tukachelewa sana kupata mbia wa kujenga ile reli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali yangu iharakishe majadiliano na mwekezaji ili kuwe na uhakika wa mzigo wa kutosha wa chuma na makaa ya mawe kwenda Bandari ya Mtwara. Vilevile, naishauri Serikali yangu iangalie uwezekano wa kupitia hizi sheria hii Reli ya Tazara ambayo inahusisha pia nchi ya Zambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama inawezekama kufanya majadiliano, kungekuwa na tawi pale, litoke Makambako liende pale Liganga ili nayo iweze kusaidia kusafirisha mzigo, kwa sababu siyo mzigo wote utasafiri kupitia Bandari ya Mtwara. Mzigo mwingine unaweza kuhitaji bandari nyingine. Kama itawezekana, itakua njema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, majadiliano yale yafikie kikomo na tuangalie multiply effects kwa sababu kuna ajira nyingi pale zimelala na sasa hivi kuna uhaba wa dola, lakini madini yale yamechanganyika na madini ya Titanium na Vanadium ambayo ni madini yenye thamani zaidi ya mara tano ya chuma chenyewe. Kwa hiyo, ule uhaba wa dola, mradi ule ukianza kwa kiasi kikubwa itakuwa ni mwarobaini. Tunaweza tukapata fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia miradi hii itaongeza pato kubwa sana kwenye Taifa letu na hasa uhaba wa dola kama nilivyoeleza. Kwa hiyo, nashauri kwenye Mpango huu, yale majadiliano yafikie mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda umenitupa mkono. Baada ya kusema hayo machache, nitamke kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)