Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Mpango wetu. Kwenye Mpango wakati Mheshimiwa Waziri wa Mipango anawasilisha hotuba yake, kwenye ukurasa wa 20 aliongea kwamba, “Tutaongeza uzalishaji na uuzaji wa bidhaa nje ya nchi kupitia kilimo, mifugo, uvuvi na madini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni wazo zuri sana, hii mimi likanisukuma niangalie je, kwenye mpango huu suala la ardhi limeangaliwa kiasi gani? nilivyomsikiliza Waziri wakati anawasilisha sikusikia neo ardhi lakini nikaenda kwenye Mpango nimebahatika kupitia ukurasa wa 100 yote yanayoripotiwa ni ambayo yamekwisha kufanyika kwa sehemu kubwa. Ukiangalia zimetumika shilingi bilioni 17.2 kwa ajili ya upimaji wa vijiji lakini katika kurasimisha na viwanja 118,045 kwa mwaka 2020/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukirejea tena kwenye kuimarisha mipaka ya kimataifa. Mpaka kati ya Kenya na Tanzania umetumia kwa mwaka 2020/2023 shilingi bilioni 1.75 na ukiangalia mambo yote yaliyogusa ardhi ni yale ambayo yamekwisha kufanyika. Ukisikiliza Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wamechangia inaonyesha tunatatizo kubwa sana kwenye eneo la ardhi. Ardhi ya kilimo, ardhi ya mifugo kuna changamoto kubwa, ardhi ambayo tunaihifadhi kwa ajili ya misitu changamoto ni kubwa. Eneo hili ninaamini kwamba kwenye mpango ilipaswa kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea wananchi wangu wa Kijiji cha Diloda, Kata ya Gidafira wote wamechomewa nyumba zao wakisema kwamba eneo lile ni hifadhi. Sasa tuna Kitongoji tumefanya uchaguzi 2019, tumeweka Mwenyekiti wa Kitongoji na viongozi wote wa Serikali wanaohusika. Kwenye ramani ya vijiji Kitongoji hicho ni sehemu ya Kijiji, unaenda leo Maliasili na Utalii unasema hili ni eneo la msitu!

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi imani yangu ni kwamba tukitibu tatizo la ardhi, maendeleo mengine yanaweza yakawa ni rahisi. Tunaweza kuwa na maeneo ya uhakika ya kilimo, tunaweza kuwa na maeneo ya uhakika ya wafugaji lakini pia hata uvuvi kwa sasa kwa sababu tunataka kuchimba mabwawa, tunaweza kuwa na uhakika na maeneo ya kuchimba madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Mpango lazima uangalie vizuri eneo la ardhi, lakini kuhusu eneo hili ambalo Wananchi wamechomewa nyumba zao. Ninaomba Serikali i-act haraka kwa sababu wananchi hawa kwa sasa hawana makazi, wananchi hawa nyumba zao zimechomwa na mazao ndani na ambayo ilikuwa ni chakula. Mbegu zao zimechomwa ndani lakini pia mavazi yao kwa sababu walifukuzwa na nyumba zikachomwa watu hao hawana mavazi. Hayo yote ni mambo muhimu katika maisha ya binadamu, watu hawa wamekoseshwa haki zao tena kipindi kigumu kipindi ambacho mvua inanyesha, watoto wadogo wanalala nje, mama wajawazito. Naomba Serikali kwenye eneo hili iliangalie kwa kina na watu hawa waweze kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli ni hifadhi, ukiuliza upande wa Hanang’ upande wa Manyara wao wanasubiri kuweka beacon ya mipaka kwa sababu kuna utata wa mpaka kati ya Singida na Manyara hakuna alama zinazoeleweka, Manyara au Hanang’ hatujawahi kukaa vikao vyovyote kutenga eneo la Hifadhi ya Msitu! Ninaomba eneo hili liweze kushughuliwa haraka ili watu hawa waweze kusaidiwa na wasiendelee kukaa kwenye mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea kuchangia kwenye mpango wetu, pamoja na malalamiko haya ya wananchi wangu, nitambue kazi nzuri ambayo imefanyika kwenye eneo la kilimo. Kilimo inaajiri watu zaidi ya asilimia 65 lakini ninafarijika sana ninavyoona kwamba yenyewe ndiyo inayoongoza kwenye Pato la Taifa. Tuendelee kuwekeza, tuendelee kuboresha eneo la kilimo lakini pia tuendelee kuboresha utafutaji wa masoko ya mazao ya kilimo, ili tuboreshe eneo hili kwa sasa ni wakati wa mvua, utaratibu wa upatikanaji wa mbolea lakini mbegu za ruzuku, ili tuweze kupata mbegu bora wakulima wetu waweze kulima ili waweze kuzalisha mazao na waweze kuzalisha kwa tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto baada ya kuvuna. Tumejifunza wakati wa corona umuhimu wa nchi kujitegemea. Kipindi kile cha lock down ukitaka bidhaa za afya kwa sababu nyingi tulikuwa tunaziagiza toka nje, changamoto hata mafuta nazo tulianza kupata changamoto kwa vitu vyote tunavyoingiza nchini. Kuna umuhimu sana wa nchi kuanza kujitegemea. Maana yake ni nini? Bidhaa zile tunazozizalisha ndani ya nchi tuhakikishe kwamba zinakuwa na soko la uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano sasa hivi tuna changamoto kubwa ya nakisi ya uzalishaji wa ngano lakini wakulima wakizalisha ngano upatikanaji wa soko ni changamoto kubwa kwa sababu tumeagiza ngano nyingi kutoka nje na kwa hali ya uzalishaji wa nchi yetu bei ya ngano ya nje ni nafuu kuliko ya ngano ya ndani. Changamoto hiyo tunayo kwenye alizeti, tunayo kwenye mazao mengine. Ninachotaka kusema, vile ambavyo vinawezekana kuzalishwa hapa nchini tutoe kipaumbele kwanza, tuwe tumevitumia ili nakisi inayobaki ndiyo tuagize kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na mjadala mrefu kwenye suala la zao la ngano. Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Bashe anakumbuka vizuri kwamba wale wanaotumia ngano wanunue ngano yote ya ndani ndiyo wapewe kibali cha kuingiza ngano kutoka nje ya nchi. Ninaomba hilo lifanyike kwenye mazao yote ili kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanakuwa na uhakika wa soko wa kile wanachokizalisha mashambani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda hata kwenye upande wa nishati. Wabunge wengi wameongelea, tunayo gesi. Gesi hii husikii sana matumizi yake yakitangazwa. Ukiongea namna ya vituo hivi vinavyopatikana vibali yawezekana ni changamoto au vinachukua muda mrefu. Ninachoomba kile ambacho kinaweza kupatikana hapa nchini tuwekeze na tuweke msukumo mkubwa. Tufanye marketing ili gesi iweze kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tuendelee kuagiza mafuta kwa kiasi kikubwa wakati tungeweza kuhamasisha matumizi ya gesi kwenye magari yetu. Tukianza kuna Wabunge wameshasema kwamba magari ya Serikali yawe ya kwanza kwenye suala la gesi. Upatikanaji wa vibali vya kujenga vituo kwa ajili ya gesi urahisishwe na ikiwezekana uwe fast tracked ili gesi hiyo iweze kutumika kwa ufanisi na tuache kuagiza mafuta ili hatimae fedha zile ambazo tungezitumia kwa ajili ya kuagiza nishati nje ya nchi izunguke hapa hapa ndani ili tujitosheleze hapa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mitambo ya kuzalisha umeme, tuhakikishe mitambo yote ambayo inatumia either diesel tuibadilishe ianze kutumia gesi ili gesi hiyo iweze kutumika na iweze kutusaidia. Ni muhimu sana kuweka huo msukumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamakaa ya mawe, ni karibuni tumeanza kutumia lakini dunia nzima inafanya harakati ya kuondokana na makaa ya mawe, gesi yenyewe harakati zinafanyika mpaka 2040, 2050 iwe imeondoka sokoni na sisi bado hatujanufaika vya kutosha, lazima tuweke nguvu kubwa kwenye eneo hilo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu umeisha?

MWENYEKITI: Malizia dakika moja.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mimi naomba nihitimishe kwa kusema hivi, suala la ardhi ni suala muhimu, tuweke mkakati mzuri wa matumizi ya ardhi na yale ambayo yanaathiri watu wetu tuchukue hatua sasa. Tuone namna ya kuwashirikisha Wenyeviti wa Vijiji ambao wanakaa karibu na wananchi ili elimu iweze kwenda sawa sawa. Hawa Wenyeviti wa Vijiji wakati mwingine ndiyo wanaosababisha confusion hata kwenye maeneo yetu kwa sababu hawana mishahara kwenye kazi wanayoifanya, tutengeneze mfumo rasmi wa kuwatumia na kuwalipa, hiyo itatusaidia ili kutumia ardhi yetu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)