Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini pia nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa haya ambayo amekuwa akiyatenda. Kwa kweli anatupeleka kuzuri na sisi wote ni mashahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze wote waliotuletea Mpango huu, Mawaziri wote pamoja na Wasaidizi wao, Mpango ni mzuri na nianze kwa kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Mpango kuna mambo mbalimbali na shabaha nyingi zimewekwa, lakini naanza na ile ya elimu, nimeangalia kwenye Mpango wa 2024/2025 ambapo kiashiria kimojawapo kinasema ni viashiria vya maendeleo ya watu, lakini kwenye shabaha inasema kuchochea na kuboresha ubora wa elimu na mafunzo katika ngazi zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizidi kusoma zaidi kwenye Mpango kumeonesha namna ambavyo kule nyuma tulikotoka kuanzia 2012 hadi 2022 udahili wa wanafunzi ulivyoongezeka kwenye Nyanja zote kuanzia Elimu ya Msingi udahili umeongezeka kutoka asilimia 94.6 hadi asilimia 113.2 mwaka 2022, hiyo ni kuanzia mwaka 2012. Kadhalika na sekondari tunashukuru sana udahili huu umeongezeka kwa sababu ya jitihada mbalimbali ambazo zimefanywa na Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uwekezaji katika Sekta ya Elimu ni mkubwa sana, ujenzi wa vyumba vya madarasa umeongeza, maabara zimeboreshwa, ujenzi wa mabweni lakini pia elimu msingi bila malipo bado inaendelea kutolewa hadi leo. Kwa hiyo ni kiasi kikubwa sana cha fedha ambacho kinaenda kwa ajili ya kuimarisha Elimu yetu kuanzia ngazi ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo kwa sababu uwekezaji kwenye Sekta ya Elimu ni mkubwa, tunategemea outcome ya wanafunzi hapo mbele na wenyewe waje wanafunzi ambao wameiva ukizingatia kwamba kuna kuchochea na kuboresha ubora wa elimu. ubora wa elimu ni pamoja na kuwa na Walimu wa kutosha ili kuweza kufundisha vizuri na wanafunzi wapate elimu bora mwisho wa siku Taifa liwe na kile ambacho tulikusudia tukawekeza kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia kwenye Mpango wetu sijaona, nashukuru kwamba zipo ajira ambazo huwa zinatolewatolewa, lakini kwa uwekezaji huu lazima tuwe na mkakati wa dhati wa kuhakikisha Walimu wanapatikana watakaoenda sambamba na idadi ya wanafunzi tulionayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi wanahangaika ukienda shule za pembezoni hakuna Walimu, Walimu ni wachache sana kiasi kwamba wanafunzi wengine anaenda anamaliza siku hapati Mwalimu, kesho anarudi tena, anakosa Mwalimu, inasababisha pia hata utoro, Kwa hiyo ili kudhibiti hali hii lazima tuwe na mkakati wa dhati utakaoendana sambamba na uwekezaji ambao Serikali imekuwa ikifanya katika Sekta ya Elimu, lakini pia tuwapunguzie wazazi mzigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uchache wa Walimu, wazazi wengi sasa hivi wamekuwa wakilipia Walimu wao ili wawafundishe watoto wao. Kwa hiyo kulipia kunamwongezea mzazi gharama ya Elimu, kwa hiyo niombe sana Serikali ili tupate output nzuri ni lazima tuwekeze na uwekezaji hatuna kwa kukwepea lazima tuajiri, tuweke mikakati ya dhati katika kuajiri Walimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimeliona katika kupitia Mpango wetu ni upande wa kilimo. Naomba ninukuu kwamba; “Kuanzia huko nyuma hadi kufikia mwaka 2000 mauzo ya bidhaa zetu kwenye kilimo, mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi yametawaliwa na usafirishaji wa malighafi bila kuongezea thamani. Hali inayosababisha ukuaji wa uchumi kutoendana na kasi ya kupunguza umaskini na ajira hususani vijijini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nime-base tu kwenye kilimo, hili ni la kweli, lakini niishukuru Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu imeendelea kuboresha Sekta ya Kilimo kwa namna mbalimbali, lakini hili la kuongeza thamani bado tunatakiwa kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao yetu ni kweli kabisa tunasafirisha au tunauza yakiwa ghafi hali ambayo inatupunguzia sana mapato Serikalini lakini kwa Mwananchi mmojammoja na hali ya umasikini sasa imeendelea badala ya kuwa inapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, kwa sababu thamani hii tutaipata kupitia viwanda vidogovidogo vingi, hivyo, Serikali ijikite katika Mpango wa namna ya kufufua viwanda ambavyo vimekufa hususani Viwanda vya Korosho. Ukienda kwenye maeneo mbalimbali yanayozalisha korosho mathalani ukienda Mtwara, Newala na Masasi kuna Viwanda vya Kubangua Korosho vilijengwa huko nyuma. Sasa hivi vile viwanda havifanyi kazi matokeo yake bado tunauza korosho ghafi ambazo hazina afya sana kwa mkulima. Kwa hiyo niombe sana ufufuaji wa viwanda vyetu ufanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali pia upande wa kilimo kwenye zao la korosho wamekuja na mpango wa kujenga Kiwanda kikubwa cha Korosho, industrial park kule Nanyamba, lengo la kiwanda kile ni kuhakikisha kwamba korosho zitakazozalishwa zinaenda pale zinabanguliwa, tunasafirisha sasa na kuuza korosho ambazo tayari zimeshaongezeka thamani. Kwa hiyo ni mpango mzuri ambao kama utasimamiwa sawasawa utatutoa sisi hapa tulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masikitiko yangu tu kidogo ni kwamba naona kuna changamoto, pamoja na Mpango mzuri wa Serikali kujenga kiwanda hiki, uzalishaji wa zao la korosho unazidi kupungua, kwanza namshukuru Mheshimiwa Rais kwamba ametuletea pembejeo, ambazo wakulima wamezitumia lengo lilikuwa kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametangulia hapa Mheshimiwa Mhata, ametaja mwaka 2021 Tanzania nzima tuliuza tani laki tatu, lakini 2022 tani laki moja na themanini na mbili, mwaka huu hatujui tutauza tani ngapi? Sasa najiuliza tu peke yangu kwamba tumeshaweka mkakati wa kujenga kiwanda kikubwa pale Nanyamba kwa ajili ya korosho, sasa tusipofanya utafiti wa kubaini ni nini kinaangusha au kinaporomosha zao letu la korosho nadhani kiwanda kile hakitaleta tija ile ambayo tulikuwa tunaifikiria. Tukumbuke kwamba ni uwekezaji mkubwa sana ambao umefanyika, kwa hiyo niiombe sana Serikali, kwenye Mpango huu tuweke kipengele cha kufanya utafiti wa anguko la zao la korosho. Iwepo kabisa, ili tukishafanya utafiti tukagundua, basi uwekezaji wetu utaenda vizuri kama vile ambavyo tunatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunaweza tukafanya utafiti, lakini akina nani watashuka kule chini, niombe pia mkakati wa kuajiri Maafisa Ugani ambao wataenda kufika mpaka ngazi ya vijiji kule chini ili kuinua uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo uwekezaji wa viwanda ambao tunao utaleta tija kwa Taifa lakini pia utainua uchumi wa mkulima mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kwenye kipengele cha Sekta ya Usafirishaji hususan reli ya kusini. Usafirishaji ndio ndio uti, tunaweza tukalima, tunaweza tukavuna, tunaweza tukafanya chochote, kama hatuna means nzuri ya usafiri, mazao, madini na bidhaa zozote hazitafika kule ambako tunatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kwamba Serikali imewekeza sana kwenye Bandari ya Mtwara, zaidi ya bilioni 168 zimewekezwa Bandarini, lengo Bandari ile ifanye kazi vizuri ili ilete tija kwa Taifa hili. Nasikitika tu kwamba pamoja na kuweka kule sijaona kwenye Mpango ujenzi wa reli hii ya kusini. Leo hii ukienda Mtwara makaa kutoka Mchuchuma kule Liganga yanasafiri kwa njia ya barabara yanaharibu barabara kiasi kwamba tutakuwa tunatengeneza kila siku. Kwa hiyo niwaombe sana wenzetu wa Wizara kwenye Mpango huu tuwe na mkakati wa dhati wa kujenga reli kutoka Mchuchuma na matawi yake ya Liganga hadi Mtwara ili tuweze kusafirisha bidhaa kwa kupitia reli na kupunguza uharibifu wa barabara ambao unajitokeza siku hadi siku.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Maimuna.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi, lakini pia niendelee kuunga mkono hoja. (Makofi)