Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya mpango. Kwa kuanzia, napenda niwapongeze Mawaziri wetu wote wawili kwa kazi nzuri ambayo wameifanya, kazi ambayo inakuja kuleta dira ya nchi yetu kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma vizuri hotuba zote mbili, nimeangalia sehemu za vipaumbele, kwa upande wa Wizara ya Fedha wameandika vipaumbele 12, Wizara ya Mipango wameandika vipaumbele nane, kidogo nilishituka, lakini nilipofanya uchunguzi wa kina nikaona vile vipaumbele vyote ni sawa. Huku wamechanganua, huku wameunganisha, lakini vyote ni sawa. Hii ni kuonesha kwamba Serikali iko katika single unit, yaani ni ya aina moja. Kwa hili, nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utaanza sehemu ya biashara. Nimeona hapa wamesema kwamba katika mpango watasimamia One Stop Center. Kwanza napongeza. Hili jambo ni zuri ambalo linasababisha kufanya biashara vizuri na nchi ambazo zimetuzunguka. Hiki ni kilio cha Watanzania wengi, wanapofika kwenye mipaka yetu wanakwama sana na wakati mwingine wanatumia gharama kubwa kuweza kuvuka border nyingine, kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa kuja na mpango huu. Napenda sana mpango huu usije ukakwama, tumalize mwaka huu na mwaka unaokuja tusizungumzie kabisa Mpango huu wa One Stop Center.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo hili, nasisitiza Zanzibar nayo inahitaji kuwa na One Stop Center kwa sababu nayo ni border. Kwa hiyo, katika mpango huu nayo ije; Waziri akiwa ana-wind up, atuambie kwamba biashara kati ya Zanzibar na Tanzania Bara zimepewa kipaumbele gani? Kwa sababu gani nasema hivyo? Ni kwa sababu biashara inapotoka Zanzibar kuja Tanzania Bara, ama inapotoka Bara kwenda visiwani kunakuwa na stop nyingi. Kule kuna stop na huku kuna stop, kwa hiyo, hii One Stop Center, tunataka biashara inapoondoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar ikifika kule iwe ni kulipa handling charge siyo jambo lingine, na vile vile ikija huku iwe ni kulipa handling charge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kasumba hapa inasemwa kwamba ushuru wa Zanzibar ni mdogo, jambo hili siyo kweli. Maana yake ushuru wa Zanzibar kweli uko chini, lakini ukiangalia gharama za Wazanzibar wanazolipa, ni zaidi ya ushuru unaotozwa Tanzania Bara. Nichukue mfano mmoja, freight charge kutoka nchi za nje, mfano kutoka Dubai kuja Zanzibar kontena moja ni dola 8,000 lakini kuja pale Dar es Salaam ni dola 2,600. Kwa hiyo, hii difference tu tayari inaleta gharama kubwa. Vile vile kutoa mzigo Zanzibar kuuleta Dar es Salaam kuna handling charge pia, kuna transport. Kwa hiyo, gharama ni za juu. Kumtoza mfanyabiashara differential tax, siyo halali. Jambo hili liondolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalotaka kuzungumza, tumesema One Stop Center, hii ni kwa upande wa borders. Tunataka kujua, wakati Mheshimiwa Waziri unakuja ku-wind up hapa, Mheshimiwa Waziri wa Biashara, alisema kwamba leseni zote zitakuwa na mfumo wa aina moja. Maana yake, ukiomba leseni hii utakuwa umemaliza shughuli. Kwa hiyo, mara hii kwenye mpango tuje tuambiwe kwamba jambo hili limeanza katika mwaka unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la usafiri kwa upande wa nchi zetu hizi mbili, Zanzibar na Tanzania Bara. Usafiri siyo rafiki. Usafiri uliopo ni wa watu wenye uwezo. Wananchi hawana uwezo wa kulipa nauli ya shilingi 30,000 kwenda Zanzibar ama kurudi. Napenda hasa Serikali ichukue jukumu la kuleta public transport ambayo itakuja kuwa na gharama ya chini ili wananchi wetu hawa wasafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja, Serikali haituambii hapa, lakini ndugu zetu wanaotoka Tanga kwenda Pemba ama wanaotoka Tanga kwenda Unguja pale, wengi sana wanakufa ndani ya Mitumbwi. Sasa Serikali hailioni hili? Naomba mpango huu utuelezee kupata public transport ili kuokoa maisha ya wananchi wetu. Tusiwe kila siku tunapuuzia jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye upatikanaji wa dola. Naipongeza Serikali kwa kutuambia kwamba wana dola za kutosha na benki zetu zinapata dola, lakini cha kushangaza wafanyabiashara wadogo wadogo hawapati hizo dola kule benki. Kwa hiyo, tunataka Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa atueleze upatikanaji wa dola na wananchi watazipata vipi? Kwa sababu inawezekana benki zinafanya ulanguzi, sasa itueleze kwamba itafuatilia vipi? Pia kila mfanyabiashara au anayehitaji dola azipate vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri, leo nilikuwa nahitaji dola mia tano kwa kumchangia jamaa yangu alikuwa anakwenda kupata matibabu, nimekosa. Mpaka nimekwenda kumuomba mtu ambaye anasafiri anipunguzie. Dola mia tano anakosa basi Benki? Basi hili naomba kama Serikali ilisimamie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze suala la mkataba wa bandari ambao umezungumzwa hapa katika Mpango. Mkataba wa Bandari mimi binafsi naupongeza, ilikuwa ni mkataba mzuri na ninaipongeza TPA kwa kuingia huu mkataba wa utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa katika Mpango nimeona huu mkataba kutoka batch zero mpaka batch three, batch four mpaka batch seven. Naona kwamba, mkataba huu ni mzuri na unakuja kuleta tija. Mpango haujatueleza. Tuliambiwa hapa kwamba, kwa sasa bandari inakusanya asilimia 10 ya bajeti lakini tukishaingia mkataba huu tutakuja klukusanya asilimia 62. Sasa, Mpango utueleze, je, ni mwaka huu au mwaka unaokuja? Hili napenda kwenye mpango huu mje mtueleze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kulichangia ni suala la Liganga na Mchuchuma. Suala hili ni suala ambalo tumeona Mheshimiwa Rais, kwanza tunapongeza sana kwa kuweza kulipa fidia kule kwa wenzetu ambako iko miradi hii. Hata hivyo, ningependa kujua sasa huu mpango umetaja jambo hili, tunakweda kwenye step gani? Kwa sababu tuliambiwa kuna Mkataba wa wale wenzetu wa kampuni ya kachina. Tunalipa hili ili kuwaokoa watanzania. Je, nataka kujua sasa status ya mkataba ule sasa utakuwa umekufa au tunakwenda kwenye mpango kwa kujisukuma ili baadaye tuje tushitakliwe ama tutakuwa kuwalipa share hawa wachina? Tunataka kujua katika Mpango huu tuje tuelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, nataka nimalizie suala la utawala bora. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hapa, aje aeleze huo utawala bora tunaoufuata ni wa aina gani? Kwa sababu bila utawala bora hata huo Mpango hautafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana, katika Jimbo langu, juzi watu wameshukiwa wanafanya Magendo ya Karafuu bila kukamatwa na bidhaa yoyote. Cha kushangaza wamekamatwa, wamepigwa mpaka mimi nikawajibika kwenda kuwaomba polisi kwenda kuwafanyia matibabu. Jambo hili haliwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana Wizara au Serikali itueleze kwa uyakini kwamba utawala bora umekaaje ili kusiwe kuna kunyanyasa wananchi. Nakushukuru.