Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa maoni yangu katika hoja zilizopo mbele. Nitoe pongezi kwa mapendekezo mazuri yaliyoletwa na Mawaziri wetu wote wawili. Sina wasiwasi juu ya utendaji wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais wetu, Mama yetu Samia kwa kazi nzuri anazozifanya hususan katika utekelezaji wa miradi mikubwa na mingine ya vielelezo. Kwanza ni utekelezaji wa mradi wa umeme wa Mwalimu Julius Nyerere ambao hadi Juni, 2023 ulikuwa umefikia asilimia 91 na malipo yake hadi Julai yalikuwa asilimia 84.3. Kutekelezwa kwa mradi huu kunatuletea uhakika wa kupata umeme na tukiwa na uhakika wa kupata umeme, mambo mengi yataenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunahitaji uhakika wa umeme? Hata mapendekezo yaliyoletwa na Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji katika kuanzisha viwanda ambavyo vitafanya mchakato wa awali vinahitaji uhakika wa umeme. Tunahitaji uhakika wa umeme ili kupunguza gharama ya uzalishaji katika viwanda vyetu ili zile bidhaa ziweze kushindana na bidhaa zinazotoka nje ili kuweza kuwavutia wananchi wetu wanunue bidhaa zinazozalishwa nchini zikiwa na gharama ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanalazimika kununua vitu vya nje kwa sababu vitu vile vinazalishwa kwa gharama ndogo, lakini changamoto mojawapo inayosababisha kuwa na gharama kubwa ya uzalishaji ni kutokuwa na uhakika wa umeme. Kwa hiyo, mimi naunga mkono Mpango huu na ninawatakia kila la heri katika utekelezaji au kutuletea mpango ujao ukiwa na uhakika wa upatikanaji wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Mipango, katika mapendekezo aliyoyatoa katika kuchochea na kuimarisha maendeleo ya kiuchumi ya jamii vijijini yaliyopo katika ukurasa wa 21 na moja ya hatua atakazozichukua ni kuweka mazingira maalum katika kuvutia ujenzi wa viwanda vidogo vijijini kwa lengo la kufanya ongezeko la awali la thamani katika sekta za kimkakati kwa lengo la kuongeza ajira na kubakisha thamani vijini. Maeneo ya kimkakati mojawapo ni kilimo, madini, uvuvi pamoja na mifugo. Nilikuwa nataka nitoe mapendekezo yangu au maoni yangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninadhani kwa upande wa kilimo, mazao yanayotegemewa kufanyiwa mchakato wa awali, mojawapo ni zao la alizeti. Ni ukweli usiopingika, mwaka huu zao hili bei yake iliporomoka vibaya sana na hivyo kukatisha tamaa wakulima kulilima tena. Natambua thamani ya mafuta ya alizeti, yanahitajika katika nchi za wenzetu. Kwa hiyo, maoni yangu, baada ya kufanya mchakato wa awali, basi tutengeneze mazingira ya kuwepo wengine wengi ambao watafanya final processing. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwa na wengi, bado kutakuwa na wachache watakaoweza kuhodhi malighafi hii. Mathalani, katika mwaka huu, wananchi wa Wilaya ya Meatu walichukua alizeti na kupeleka kwenye kiwanda ambacho siwezi kukitaja. Walinunua debe kwa shilingi 6,000/= na walipofika kule walikutana na bei ya shilingi 4,000/=, kwa hiyo, elfu mbili ziliwakata wananchi wetu na yule aliyekuwa anapelekewa alizeti ile anai-process na kuipeleka moja kwa moja nje, ambapo inatuletea fedha za kigeni. Sasa naye anaposema kwamba soko la alizeti limeshuka, nakuwa sielewi. Kwa hiyo, Serikali inavyoweka hii mipango, iwahakikishie wananchi wetu masoko ambapo hakutakuwa na ukiritimba wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hoja zilizoletwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika maelekezo ya maandalizi ya mpango wa bajeti wa 2024/2025 ni kuhusu mazingira na mabadiliko ya tabia nchi. Naomba kuwepo na mpango kabambe wa kutekeleza matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuendelea kufanya uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2022 kama tutakumbuka, katika kongamano la nishati safi ya kupikia, Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo ya taasisi kuanza kutumia nishati safi. Mheshimiwa Waziri wa Mazingira, alitoa tamko kwamba matumizi ya kuni mwisho Januari, 2024. Wakati anatoa yale matamko, tayari sisi huku Bungeni tulikuwa tumeshapitisha bajeti, kwa hiyo, ilikuwa ni ngumu kufanya utekelezaji au itakuwa ni vigumu by Januari, 2024 kwamba matumizi ya nishati ya kuni yawe mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi naomba Serikali iwe na mpango kabambe. Kama ni kukopa fedha katika mfuko wa hazina ikope, kwa sababu taasisi hizo zinatakiwa zipate hii nishati safi na wakati huo huo bado zitaendelea kufanya matumizi kwa nishati iliyokuwa inatumika awali. Kwa hiyo, tukichukua kwa pamoja zile fedha tukajenga ule mfumo, na zile taasisi zinahitaji kupika kila siku, itakuwa ni ngumu kutekeleza mpango huu. Kwa hiyo, naiomba Serikali ije na mpango kabambe katika mapendekezo kuhusu suala zima la nishati safi ya kupikia katika taasisi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu maoni ya Kamati yaliyopo katika ukurasa wa 50 kuhusu Wizara, Idara, Mamlaka na Taasisi za Umma kutoshirikiana wakati wa kupanga na kutekeleza miradi. Hali hii imesababisha baadhi ya taasisi kutekeleza miradi katika ngazi ya Serikali za Mitaa huku utaratibu na usimamizi wa ufanyikaji ukitoka Serikali Kuu moja kwa moja na hivyo miradi hiyo kukosa uangalizi ama kutekelezwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika, tunapoteza fedha nyingi kutokana na huu mpango wa kutozihusisha Serikali za Mitaa. Kama utakumbuka, jana niliongelea mfano, mojawapo wa utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji ambapo watekelezaji walitoka moja kwa moja DASIP bila kuishirikisha halmashauri, tukapoteza shilingi bilioni 1.2, wananchi hawana kitu. Ukienda pale kwenye ule mradi utafikiri ni uwanja wa mpira, hakuna kinachoendelea pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maji nayo ilitekeleza Bwawa la Mwanjolwa kwa shilingi bilioni 1.8, limebomoka na sasa wananchi wanahangaika na maporomoko ya maji na mradi ule haujawahi kunufaisha hata siku moja. Sasa basi, kama Meatu ni shilingi bilioni tatu, ukiingiza na uhamilishaji wa mifugo 1,000 ambao ulifanywa moja kwa moja kwa Wizara, leo hii ukienda Meatu huwezi kuona ng’ombe mmoja aliye bora aliyetokana na uhamilishaji, lakini fedha nyingi za Serikali zilipotea. Kama Meatu ni shilingi bilioni tatu: Je, nchi nzima itakuwa ni shilingi ngapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ione namna inavyopoteza fedha kwa kutozishirikisha halmashauri na viongozi waliopo katika level ya mkoa pamoja na halmashauri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)