Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kama ambavyo wengi waliotangulia wamesema, kwamba mpango huu ni matokea ya kazi nzuri ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi na mipango mingine. Kwa hiyo na mimi naomba niungane nao kwa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ameonyesha umahili mkubwa tangu alipoingia madarakani na kuwa na mipango mingi inayotekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuirudisha Tume ya Mipango. Hii ni dalili njema ya kuonyesha kwamba Watanzania tumeamua kupanga, na kupanga ni kuchangua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaona ndugu zangu wawili pale kutoka Iramba, wanaosimamia mpango huu. Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba. Nawapongeza kwa namna ambavyo mmeonyesha kwamba mmejipanga kupanga kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nishiriki kwenye kupanga kwa kuwashauri wapangaji wenzetu. Nadhani wote tunafahamu, ili nchi iendelee inahitaji kuwa na mipango thabiti na endelevu, mipango ambayo Watanzania wakilala wakati wanaamka wanajua nini kitatokea. Kwa hiyo, ninaomba sana Serikali, tunapokubaliana kwamba tumepanga jambo fulani basi sote kwa pamoja tutumie nguvu zetu kulitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutakuwa tunakutana hapa kupanga mipango mipya wakati mipango ya zamani hatujaitekeleza, tutakuwa hatutendi haki. Kwa hiyo, niaombe sana ambao mmepewa dhamani hii ya kumsaidia Mheshimiwa Rais kutekeleza maono yake kwenye taifa hili, mhakikishe kwamba kila tunachokipanga mnakisimamia kinatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nitoe mfano mdogo, kwa sababu mimi ni moja ya Wabunge wengi wanaotoka vijijini. Mazingira ya vijijini kidogo nayafahamu. Vijiji vyetu wakazi wake wengi ni wakulima na wafugaji. Wakulima wanalima mazao ambayo ni malighafi za viawanda na mazao mengine yanasafirishwa yakiwa ghafi hivyo hivyo kwenda nje ya nchi na kulipatia taifa fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vyetu vinapata malighafi kutoka mashambani kwa asilimia kubwa. Mazao ambayo yanaenda nje moja kwa moja bila kuchakatwa kama hii wanaita korosho, choroko, dengu na pamba inachakatwa kidogo inapelekwa nje; mazao yote haya ni chanzo kikubwa cha mapato ya nchi yetu. Kwa hiyo ni lazima wote tujipange katika mopango yetu kuhakikisha mazao haya yanakuwa na tija. Tija kwa Serikali kukusanya fedha lakini tija kwa wakulima wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tuna shida moja kwenye kupanga. Maeneo ya vijijini ambako mazao haya yanatoka tumekuwa tukiyasahau. Kwa hiyo nataka niwakumbushe wenzangu, na nitumie mfano huu kumkumbusha kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu; tangu niwe Mbunge wa Sumve na tangu awe Waziri wa Fedha kwenye kila mpango na bajeti tumekuwa tukizungumza kuhusu Miundombinu katika Jimbo la Sumve. Kaka yangu huyu amekuwa mtu mwema sana kwangu. Amekuwa ananiahidi na kuonyesha kwamba atafanya. Kwa kweli kwenye kuniahidi na kunionyesha kwamba utafanya, mimi nakupa big up kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi zimekuwepo za uhakika lakini hazitekelezwi. Kwa hiyo ndugu yangu ili twende pamoja na ili tuanzishe mpango mwingine ahadi yako uliyonipa hapa tarehe 22 Juni, 2022, ya kwamba utanijengea kilometa zangu 71 za kutokea Magu – Bukwimba – Ngudu mpaka Nhungumalwa, kwa kiwango cha lami na ukaniambia umepata na mkopo, jenga basi. Ili mpango huu uende uje na mwingine. Lakini kama tutakuwa na mpango ule ule hautekelezwi halafu Watanzania hawa hawa tunakata tena Wabunge wao wasimame wapange mipango mingine inakuwa siyo sawa. Naomba na ninasisitiza kwamba tilichokipanga tukitekeleze (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Kitila Mkumbo akiwa back bencher huku, aliwahi kusema hapa kuhusu Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Madiwani. Kwamba, wale ndio wanaosimamia fedha zetu kule vijijini. Mheshimiwa Ng’wasi Kamani amesisitiza hapa kuhusu Ripoti ya CAG, na kwa mfumo wetu wa Bunge kuna Kamati Maalum kabisa inakagua Hesabu za Serikali za Mitaa. Kwa nini Kamati hiyo inazikagua? Na kwa sababu fedha nyingi tunazipeleka kule na kwa mujibu wa mfumo wetu Waheshimiwa Madiwani ndiyo wasimamizi wa hizo fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiamua wenyewe kupiga mpira, tunajirudishia pasi na tunajipiga chenga wenyewe. Wale wanaotakiwa kusimamia fedha hizi hayujawawezesha. Kwa hiyo Mheshimiwa Halima Mdee na Kamati yake wataendelea kila siku kutuletea madudu hapa na Serikali itaendelea kulalamikia wizi na Waheshimiwa Mawaziri mtaendelea kupanga kupeleka fedha na kutumbua watu kama hamjajipanga kuweka walinzi halisi wa hizi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napitia Taarifa za Serikali. Naona juzi kuna nyaraka ilitoka ambayo inawa-exclude Wenyeviti wa Halmashauri kwenye kusaini mikataba. Sijui tunaona shida gani kama Madiwani watasimamia ile mikataba. Yaani tunataka Wakurugenzi wetu hawa ambao wakati mwingine hawana uwezo wa kutosha kufanya kazi ya ukurugenzi kwa sababu hawana uzoefu, waende kwa kutumia vichwa vyao wasaini mikataba bila kusimamiwa na Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatengeneza mwanya wa fedha zetu tunazozipeleka huko, ziende zikapotee. Kwa hiyo, mimi naomba niishauri Serikali kwamba, baada ya kupanga kutafuta fedha na kupeleka maendeleo, pia tupange kulinda na kuzisimamia fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nataka kuzungumzia Sekta ya Utalii. Sekta ya Utalii ni sekta ambayo inatuingizia mapato mengi sana; na wote tunafahamu kwamba tuna mbuga nzuri kabisa ya Serengeti na mbuga zingine, lakini wote tunafahamu kutokea Mwanza kwenda Serengeti ni karibu zaidi kuliko popote pale katika viwanja vya ndege nchini. Uwanja wa Ndege wa Mwanza uko karibu zaidi na Serengeti, lakini kwa nini watu hawautumii? Kwa sababu Serikali haijapanga kuuboresha uwanja ule kuufanya uwe wa Kimataifa. Kwa hiyo, hautumiki na sekta yetu ya utalii inakuwa imeng’ang’ania eneo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitokea Mwanza, ukaenda kwenye Jimbo la Kisesa kwa kaka yangu Mheshimiwa Mpina, pale Mwandoya ukaongea na wananchi kuhusu wanyama pori, ni viumbe anaowachukia kuliko viumbe wowote. Wanajiuliza kwa nini tunafuga tembo ambao wanaharibu mazao yao na wanaua watu wao. Kwa sababu hawafaidiki kabisa na huu utalii, lakini Serikali imeamua kuyatelekeza maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupanga sekta ya utalii, wekeni miundombinu ya kiutalii Mwanza. Kuna barabara za msingi kabisa za kiutalii. kwa mfano ukitokea Bujingwa kupitia Nyambiti kwenda Malya, ukaenda Ngulyati, ukaenda Itilima, ukaenda Mwandoya mpaka Sakasaka kwenye geti lile la Maswa Game Reserve ni karibu zaidi kuliko mtu atokee KIA mpaka aje huku. Sasa kwa nini hizi barabara hamziboreshi, hamzijengi halafu tunakutana hapa tunapanga kuboresha sekta ya utalii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba niishauri Serikali kwamba, sasa imefika wakati Maeneo ya Kanda ya Ziwa nayo yaboreshwe ili kukuza sekta ya utalii na iwe na manufaa kwa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)