Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na kutuwezesha kuwepo hapa. Kwa nafasi ya pekee niwapongeze wawasilishaji wa taarifa zote mbili, ni taarifa nzuri na mpango ni mzuri. Nami mapema kabisa nitamke kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu kama ulivyosomwa inaonesha namna gani kiuchumi tunaenda vizuri. Kwa mujibu wa taarifa hii, kwa taarifa iliyotolewa na Benki ya Dunia mwezi Septemba, kwa miaka mitatu mfululizo uchumi wetu kama Taifa umeendele kukua. Achilia mbali kwamba kidunia uchumi umekuwa unapungua lakini kwetu imekuwa kwa asilimia kadhaa uchumi unaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matarajio kwamba mwakani uchumi utaendelea kuongezeka. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa sababu pamoja na changamoto kadhaa, kwa miaka takribani minne mitano mfululizo ame-stabilize hali na uchumi wetu umeendelea kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kukua kwa uchumi, kimaandishi uchumi wetu unakua, ni lazima sasa tutakafari zaidi je, hali ya watu wetu inaendana na kukua kwa uchumi huu katika maandishi (katika tarakimu)? Ni lazima tuone je, kuna uwiano? Kwenye mpango kama ulivyosomwa na Mheshimiwa Waziri, kuna mabadiliko makubwa yamefanyika kwenye hali ya kiuchumi ya watu wetu na hili limetokea kwa sababu ya uwekezaji uliofanyika kwenye sekta za kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tufanye vizuri zaidi na ili tufikie athari chanja kwenye eneo hili, ni lazima uwekezaji zaidi uwe kwenye maendeleo ya watu, hasa kwenye eneo la kijamii na kwenye maeneo ya kiuchumi hasa tukiweka mkazo kwenye maeneo ya vijijini. Ni lazima tuimarishe uwezo wa uzalishaiji kwenye sekta muhimu kama kilimo, uvuvi na nyinginezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nimekuwa najiuliza, tuna rasilimali nyingi sana kama Taifa, lakini kwa mtazamo wangu, bado hatujaweza kuzitumia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna rasilimali maji ambayo tungeweza kuitumia kwa ubora zaidi na kwa ufanisi kufanya kilimo cha umwagiliaji kuwa msingi wa Uchumi wa Taifa letu. Bado pamoja na jitahada kubwa sana zinazofanywa na Serikali ninatambua mwaka jana tumeongeza bajeti kwenye Wizara ya Kilimo, Wizara ya Kilimo inafanya kazi kubwa sana kujaribu kufufua kilimo kwenye nchi hii. Tunahitaji tufanye zaidi ya hapo tuweze kutumia rasilimali tulizonazo kama maji, tuweze kuitumia vizuri ili kukuza kilimo chetu vilevile kufanya wakulima wetu waweze kunufaika na rasilimali hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa ninatafakari eneo kama Ukerewe ambako tunazungukwa na maji. Katika eneo la square kilometa karibu 6,400 zaidi ya asilimia 90 ni maji. Tuna eneo pale, ni kwa nini Ukerewe watu walalamike kukosa chakula, kuwa na upungufu wa chakula kila mwaka? Ni kwanini, tusiwekeze kwenye umwagiliaji kwa kutumia rasilimali maji yaliyopo kwenye eneo hili kufanya kilimo cha umwagiliaji, kutumia eneo dogo lililopo kwa ufanisi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sehemu moja lakini kuna maeneo mengi ambayo kwa rasilimali tulizonazo tunaweza tukatumia vizuri tukaweza kuwekeza tukafanya watu wetu kwenye maeneo yaliyopo kule chini kuweza kutumia rasilimali hizo kujiimarisha kiuchumi. Niombe kama nilivyotoa mfano kwenye eneo la Ukerewe pamoja na maeneo mengine, tutumie rasilimali hizi kwa ufanisi ili kuweza kufanya watu wetu kule chini wawe imara kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwenye kilimo hata kwenye uvuvi bado kama alivyokuwa anachangia Mheshimiwa Sanga bado kuna vikwazo vingi sana kwa watu wetu kule chini wanapokuwa wanafanya biashara lakini wanapokuwa wanafanya shughuli za uzalishaji vilevile. Sekta ya uvuvi ni sekta muhimu sana kwenye Taifa hili katika kuimarisha uchumi wetu, wavuvi wetu wanakutana na vikwazo vingi sana vya tozo mbalimbali. Kwa mfano, leo kwenye maeneo ya kanda ya ziwa kuna kitu kinaitwa tozo ya control namba na kadhalika ni kikwazo kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ningeshauri kupitia Wizara ya Uvuvi, ondoeni tozo hii. Inaleta kero kubwa, inaathiri uzalishaji kwa wavuvi wetu kwenye maeneo yale jambo ambalo kiujumla linaathiri uchumi wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyotajwa kwenye mpango, tukiwekeza kwenye huduma za kijamii, uchumi wetu utaendelea kukuwa kwa kiwango kikubwa sana. Na hili ndiyo maana nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji mkubwa sana alioufanya kwenye Sekta ya Huduma za Kijamii, kwenye elimu, afya, kwenye maji, kazi kubwa imefanyika hata miundombinu na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna maeneo ambayo miundombinu yetu hasa ya usafirishaji kuna changamoto kubwa sana. Niki-sight kwa mfano eneo la Ukerewe, kwenye ilani yetu ya uchaguzi ili kurahisisha mazingira ya watu wetu, kufanya waimarishe uchumi wao kupitia sekta ya usafirishaji, Ilani ilielekeza kujenga vivuko kwa ajili ya kusaidia wananchi wetu kusafiri kutoka eneo moja kwenda eneo jingine kusafirisha mazao yao. Leo eneo kama la Ihugwa kisiwa cha Ilugwa pale Ukerewe, mwananchi anasafiri masaa matano eneo ambalo angeweza kusafiri kwa nusu saa kwa sababu tu mazingira ya usafiri kwenye eneo lile sio bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilani imeelekeza vivuko vitengenezwe kwenye eneo lile. Niombe Wizara zinazohusika katika mpango wa bajeti unaokuja, pesa kwa ajili ya kuelekeza kwenye eneo hili kukamilisha miradi hii iweze kutengwa na iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kitila katika hotuba yake ameelezea kwamba katika nguzo zinazoshikilia mafanikio ya utekelezaji wa mipango yetu, moja ni kuwa na nidhamu ya utekelezaji wa mambo tunayoyapanga. Wakati Mheshimiwa Sanga anachangia hapa, ameelezea namna ambavyo ni muhimu sana kuwekeza kwenye mifumo ya kiteknolojia (Mifumo ya TEHAMA), lakini mifumo hii hata kama tutaifunga, kama hakutakuwa na ufuatiliaji na tathmini ya namna gani mifumo hii inafanya kazi bado hatutakuwa na mafanikio katika mifumo hii hata kama tutaiweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita tulikuwa tunajidili Ripoti ya CAG. Mambo mengi sana, miradi mingi inakwama kwenye utekelezaji kwa sababu hakuna mfumo wa tathimini na ufuatiliaji. Ndiyo maana niombe Mheshimiwa Kitila, bado kama nilivyosema wiki iliyopita ni muhimu sana tuwe na sera ya kitaifa ya ufuatiliaji na tathmini ili mipango yote hii tunayoipanga tuhakikishe kwamba kweli inatekelezwa kwa namna ambavyo tumedhamiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, tukiwa na national policy ya monitoring and evolution itasaidia kwanza kuongeza uwajibikaji, itasaidia miradi yetu kufanyika katika kiwango bora na thamani ya pesa tuliyowekeza kwenye miradi ile kuonekana. Itaongeza uwazi kwa sababu kutakuwa na ufuatiliaji lakini kutakuwa na tathmini itakayokuwa inafanyika, kutakuwa na ujumuishaji wakati wa utekelezaji wa miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, achilia mbali hiyo bado maadili ya watumishi wetu katika kusimamia na kutenda kwenye usimamizi wa miradi hii utaongezeka jambo ambalo litasaidia rasilimali pesa tunazozitomia kuwekeza kwenye miradi mingi ya maendeleo, tathmini yake ikifanyika inakuwa na tija na inakuwa na maslahi kwa Taifa letu. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Kitila katika plan zako zote ulizonazo, bado kuna umuhimu mkubwa wa kuwa na national policy ya monitoring and evolution ili kuhakikisha rasilimali pesa tunazowekeza kwenye miradi yetu ya maendeleo inafanyika kwa tija na yale tunayotarajia kwa maslahi ya maendeleo ya Taifa letu yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nilitaka niuweke kwenye eneo hilo. Ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja.