Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nizungumze kidogo kuhusu Bajeti Kuu ya Serikali. Awali ya yote, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya, kwa kweli Watanzania wanaona. Hata wale ambao wanasema hawaoni basi moyoni wanajua na wanakiri kwamba Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan anaupiga mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye barabara. Iko barabara ya Nachingwea – Masasi, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umefanyika na umekamilika zaidi ya miaka tisa iliyopita, lakini imetengewa fedha zaidi ya miaka mitano mfululizo lakini haijapelekwa hata senti moja. Kwenye hotuba ya bajeti ya Waziri wa Kisekta aliizungumzia hii barabara ya Masasi – Nachingwea kwamba iko kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia alielezea ujenzi wa kiwango cha lami barabara ya kutoka Nachingwea kuelekea Liwale. Sasa wakati Mheshimiwa Waziri wa Fedha anasoma hii Bajeti Kuu sijasikia. Sasa nikawa napitia kishikwambi changu nikasema labda hii page imeruka au namna gani? Tukiwa tunaomba hizi barabara, tunaomba kutufungua ili na sisi kimaendeleo tuwe sawasawa na maeneo mengine, hali huko ni ngumu. Ukizungumzia barabara ya kutoka Masasi – Nachingwea, Nachingwea – Liwale, Liwale - Nangurukuru, Nachingwea kuelekea Ruangwa wakati wa masika huwezi kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia hapa nilikuwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, tulikaa mahali tumesimama zaidi ya masaa mawili, hiyo barabara ni mbovu. Sasa sijui tumekosea wapi na kwenye hili nimwombe sana kaka yangu Dkt. Mwigulu Nchemba atakapokuja kuhitimisha, wananchi wale wa Masasi, Nachingwea, Ruangwa na Liwale wanataka kusikia barabara hii mpango wa kujenga ukoje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Ujenzi ametupa matumaini makubwa, lakini sasa kwa hotuba hii sielewi kama atakuja kuhitimisha mwishoni au la lakini kwa kweli wanasubiri kusikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoke hapo nijielekeze kwenye kilimo. Tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutupatia pembejeo za kilimo na hasa kwenye zao la korosho, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Kwenye hili naomba nishauri eneo moja, tuna changamoto ya upatikanaji wa hiyo Sulphur. Makisio ya mwaka huu ni kupata tani 25,000, lakini mpaka sasa imepelekwa tani 10,000, tayari msimu unakwenda. Maana yake hapa wakulima watapata pembejeo wakati muda wa kuzitumia umeshapita, sasa eneo hili nishauri sana Serikali kwa sasa tunatumia vyama vikuu vya ushirika kununua hizi pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe jukumu hili tuwape Bodi ya Korosho Tanzania, kwanza ni chombo cha Serikali, lakini pia tunaweza tukazipa taasisi zingine za Kiserikali na hii itatusaidia hata wakati wa kufanya auditing. Natambua Wizara ya Kilimo inafanya kazi nzuri basi na lenyewe walichukue ili waweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo suala la tembo. Nilisimama mbele ya Bunge lako Tukufu, nikalia sana, nikalalamika sana juu ya kadhia ya tembo na nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Sekta ya Maliasili na Utalii, tunawashukuru sana, jambo lile wamelifanyia kazi na kazi inaendelea. Tunajua kwamba changamoto haijaisha na naamini kwamba bado wataendelea kutuondolea kero hii ili wananchi wangu wa Jimbo langu la Nachingwea waweze kuishi kwa raha kama maeneo mengine. Tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo juu ya asilimia 10. Wakati inatengwa ile asilimia 4:4:2, ziko halmashauri zingine mapato yake ni kidogo sana, hayatoshelezi. Sasa leo Mheshimiwa Waziri wa Fedha anasema twende tukaondoe asilimia tano…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kuna taarifa. Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kuwa nitakuwa na muda wa kujumuisha, lakini nimehofia nisije hoja zikawa nyingi nikasahau jambo hili. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge makini kabisa anayeongea kwamba hii barabara anayoitaja ni kweli ni omission, tuliisahau kuiorodhesha, kwa hiyo iingie kwenye kumbukumbu za Hansard kwamba na yenyewe ni sehemu ya zile barabara zilizowekwa kwenye ule mpango ambao Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi aliusema. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa taarifa hiyo.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, iingie kwenye kumbukumbu kama ilivyotajwa kwenye Wizara ya Kisekta, imo kwenye utaratibu ule ule na wananchi wote na Wabunge wote wa Kusini waipate hivyo kama ambavyo ilisomeka kwenye Wizara ya Kisekta. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa taarifa umeipokea?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naendelea na mchango wangu kwenye asilimia 10, bado mahitaji ya watu wetu kwenye haya matumizi ya asilimia 10 ni makubwa kuliko hata hiyo asilimia 10 inayopatikana. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali bado hii asilimia 10 kwa maana ya 4:4:2 tuiache, badala yake sasa tutafute vyanzo vingine ambavyo tutakwenda sasa kuwahudumia wale wamachinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke kwamba hizi fedha pia na hao wamachinga ni sehemu ya wale vijana ambao wanakopa, ni sehemu ya wale akinamama ambao wanakopa. Hilo naomba lizingatiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni kwamba, kipo Chuo cha Ualimu Nachingwea, ni chuo kikongwe na cha muda mrefu sana. Tulizungumzia hapa juu ya kuiomba Serikali ione uwezekano wa kukipandisha kile chuo kuwa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuo hiki ni kikubwa, chuo hiki kina eneo, lakini pia Nachingwea ni tajiri kwa maeneo, tunayo maeneo mengi ya kutosha, wakiwa tayari tutawapa maeneo ya kutosha kabisa. Chuo hiki kinabeba wanafunzi kutoka kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Kwa hiyo, wakitupatia, hii ni fursa kwa uchumi wa Nachingwea, lakini pia tutakuwa tunasogeza elimu zaidi kwenye maeneo ambayo vijana wanatoka huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya furaha ya kusikia lile jambo la barabara, nisije nikaondoa utamu huu, hapa tayari nimeshaanza kupokea message za kupongeza. Nikushukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)