Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo ili niweze kuzungumza na wananchi wote pamoja na nyinyi Wabunge wenzangu. Napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu huu muda mfupi wa dakika 10 nami niweze kushauri na kutoa mawazo yangu katika Bajeti Kuu hii ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza napenda nimpongeze sana Waziri jinsi proposal alivyoiweka ya bajeti kuu. Nampongeza Mheshimiwa Rais maana nina imani bajeti hii anaijua kikamilifu Waziri hawezi akaleta tu hivi vitu bila kujua Mkuu wa Nchi. Ninachotaka nishauri hapa yapo mambo mengi ambayo yamezungumziwa humu na nashukuru Mungu kabisa toka tarehe 14 nasikiliza michango ya wenzangu. Sasa naomba niweke mchango wangu tofauti kidogo nisifuatishe kule walikopita wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la asilimia 10 wenzangu wengi wamelisema sipendi nilirudie. Pia lipo suala hili la watu wenye umri wa miaka 18 nashauri hapo Mheshimiwa Waziri ajaribu kuliangalia na ushauri wangu asiliweke kabisa; kwamba kila mtu anapofikisha miaka 18 aingizwe kwenye TIN Number, hilo litatuletea double standard katika maisha yetu hayatakwenda sawa, nashauri Waziri aliache.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine hapa nikumbushie, mwaka jana nilishauri mambo mengi, mengine yalifanikiwa lakini mengine hayajafanikiwa. Naomba niyagusie yale ya muhimu ninayoyaona mimi. Kuna hawa viongozi wa Serikali za Mitaa, napenda awaweke na wao wawe wanapata posho mbalimbali, ili kusudi shughuli wanazozifanya wazifanye kwa moyo mmoja, Wenyeviti wa Vijiji pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala lingine upande wa TARURA, mwaka jana kila Mbunge tulipewa Shilingi milioni 500, mimi nikaweka mawazo yangu kwamba hizi fedha ziende kwenye vifaa vya ujenzi. Mheshimiwa Waziri alinikubalia kwamba watafanya hivyo, lakini baadaye ulitolewa Mwongozo TARURA ukikataa hayo mawazo. Naomba kwa kuzingatia kama Waziri alivyokusudia kubana matumizi, tukiangalia barabara zote zilizochongwa mwaka jana zimenyeshewa na mvua mpaka sasa hivi maeneo mengine hayapitiki, lakini hapa kama halmashauri zingepewa vyombo vya kutengenezea barabara wangeendelea kuchonga na barabara zingeendelea kupitika. Kwa kuwa, tunakwenda kwa style ya kubanana, nashauri Waziri wasirudi nyuma, sio mbaya hata watumishi wengine wakiwa wanaambulia Noah tu kulingana na hesabu zao za kwenye mishahara katika kuwakopesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana ukiangalia hesabu aliyoitaja Mheshimiwa Waziri juzi hapa na nimekaa siku tatu nikaitathmini vizuri nika-calculate kweli hizi gari kila mwaka zinakufa. Matengenezo huwa yanakwenda kufanyika garage za gharama kubwa lakini sisi wenyewe wengine humu tunamiliki hayo magari. Ukiangalia hesabu wanazotengenezea halmashauri huwa haziendani. Ukiangalia hizi ofisi za manunuzi sana sana ni hasara tupu, ni kuwaingiza hasara wananchi na kushindwa kuwasaidia wananchi kwenye masuala ya msingi. Ukiangalia wananchi wetu kuna kilio kikubwa, tunapitia kwenye kipindi kigumu mwaka huu, nikiangalia hali halisi kwanza kuna dalili ya njaa vyakula vinavyotembea kwenda nje ya Mataifa sidhani kama Serikali itakuwa na stock ya kutosha kuwalisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni mwezi wa Juni lakini mchele unauzwa mpaka Sh.2,500 mjini hapa, mwezi wa Julai tuko kwenye msimu. Mahindi yanauzwa mpaka Sh.120,000 Moshi na magari yanatembea usiku na mchana na nikiangalia watu wetu, ni kama vile hawajiandaa kabisa kwamba kunaweza kukachelewa mvua kunyesha maana hizi skimu zinazosemwa zinaweza zisitusaidie. Kwa hiyo, naishauri Serikali iliangalie hilo suala ikiwezekana tufunge mipaka kwanza ili watu wetu wasife kama hatuna stock za kutosha. Huo ndiyo ushauri wangu kwa Serikali, waliangalie sana hilo suala.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka nilizungumzie ni suala la kupoza maisha kwa mwananchi. Mheshimiwa Rais amefanya jambo jema mwezi uliopita Juni, ametoa Shilingi Bilioni 100 ili wananchi waweze kupata unafuu kimaisha, lakini hiyo fursa wananchi wale wa kawaida hawajaipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali iangalie na lazima tufahamiane kila mtu rank yake, Rais ni Amiri Jeshi Mkuu, Rais ni mwanzo mwisho akisema kitu ina maana kinatakiwa kizingatiwe, sio Rais amesema tena halafu tangazo lingine linatoka kwamba nauli hazitashuka bei. Niliona watu wa SUMATRA, baada ya kutangaza Rais kwamba natoa bilioni hizi ili maisha yapungue, lakini kuna tangazo lilitoka kwamba nauli hazitashuka. Matokeo yake hizi fedha kama vile zimepotea maana kule Rais alipokuwa amelenga ziende hazijaenda. Kwa hiyo, niishauri Serikali wawe wakali sana katika masuala ya watu wanaojaribu kuleta disturbance katika maisha ya watu hao wanaopata shida kwenye hili Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuondoa ada kwa kidato cha tano na cha sita, lakini lipo suala moja kwenye shule, michango michango, wanafunzi wamekuwa wakilia sana. Naomba nalo hili Serikali ilitolee ufafanuzi maana kuna hatari unaweza ukaondoa ada lakini michango ikawa mingi, ikawa hakuna ulichokifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine niwaombe Mawaziri, sasa hivi kidogo tunaendana nao, maana tumeshazoeana ni miaka miwili sasa. Zipo ahadi nyingi ambazo wamenipa kwenye Jimbo langu, Mawaziri wale waliofika kwenye Jimbo langu na uzuri walifika kampeni nilishaimaliza, nina imani ahadi walizokuwa wakinipa ni za ukweli kabisa. Hivyo, ni wakati sasa wa kuzitekeleza hizi ahadi, maana mimi sio mtani wao wa kusema kwamba labda walikuwa wanatania au walikuwa wanafurahisha watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine Waziri wa TAMISEMI tumeshaongea na yeye confidential, naomba nilirudie tu hapa, Wilaya yangu inakabiliwa na Makaimu, kila Idara imekaimiwa. Mkuu wa Wilaya mwenyewe sasa hivi kuna Kaimu, ukienda DMO Kaimu, kila sehemu Kaimu, wilaya yangu inakuwa haihudumii vizuri wananchi wangu, unajua Kaimu ni tofauti na bosi mwenyewe, kibarua ni tofauti na tajiri mwenyewe akikuhudumia, naomba waniangalie kwenye Wilaya yangu. Hata hivyo jamani napambana, nime-sacrifice maisha yangu kwa ajili ya hilo Jimbo kutoka Shilingi milioni 700, wilaya ilikuwa haikusanyi lakini mpaka sasa hivi tunakusanya Shilingi Bilioni tatu. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha a-sacrifice maisha kama alivyolianzisha hili asirudi nyuma, kodi zetu ziko bandarini pale, huku kwingine ni kama vifaranga tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari pale nina wasiwasi, bado kuna vitu vinapenyezwa, hebu wajaribu hata siku moja kuweka Jeshi wiki moja wasimamie Jeshi watoe hawa waliozoea kusimamia, wasikilize tutapata trilioni ngapi? Hii trilioni 41.48 naiona kwanza ni kidogo sana, hakuna haja ya kuongezea tena chanzo kingine, nashauri hivyo. Hivi vyanzo vilivyopo hebu tuvisimamie tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari ya Mtwara ikisimamiwa vizuri na Bandari ya Tanga, bado migodi, miamala, bado tunahangaikia trilioni 41 tu, hakuna hili suala haliwezekani. Nawaomba waliopewa dhamana wasimameni imara ,wengine huwa tunasali hatujui hata siasa kusema kwamba tuongee sijui tujipendekezeje. Nashauri kabisa katika roho na kweli na wala sihitaji kuleta magumashi sijui longolongo ya mara nini, mara nini, Taifa hili tutarudi nyuma. Rais wa Awamu ya Tano alitangaza vita ya uchumi nina imani haijaisha; na wakumbuke wengine walikuwa Mawaziri, wakati tukitangaziwa sisi wengine tulikuwa tunachunga ng’ombe. Ile vita ya uchumi haijaisha inaendelea mbona wamelala, mbona hatusikii viwanda, kuna vitu vingi vimelalalala, hatusikii Mawaziri wakisema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mawaziri wanatembelea V8 na tukimaliza hili Mheshimiwa Mwigulu turudi kwa Mawaziri, hizi gari ziwe zinatumika kwa utaratibu kwa vile tumeamua kubana bajeti. Ikiwezekana kila Waziri akitaka kufanya safari, lazima aangaliwe anakwenda safari gani, anatumia mafuta gani, hapo ndio tutakuwa na usawa ili na wanyonge nao wapate haki yao, ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Maganga, hiyo ni kengele ya pili lakini endelea kusimama. Waheshimiwa Wabunge Mheshimiwa Maganga tulimtangaza kuwa ni mchezaji bora katika mechi zilizopita. Kwa bahati mbaya tv ilikuwa haiku-zoom kwake na alipata unyonge. Sasa leo nampa nafasi tv zi-zoom kwake ili jimboni kwake wamuone, ndio amekuwa mchezaji bora kwenye mechi... (Makofi/Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana au umeniongezea na dakika kidogo niongezee katika mchango wangu?