Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii muhimu sana ya bajeti yetu ya fedha kwa ajili ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa kazi nzuri waliyofanya kwenye kuandaa Bajeti hii ya Serikali. Hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri ambayo ni Bajeti ya Mheshimiwa Rais ya mara ya pili kwenye Bunge lako Tukufu ni ya kihistoria ni hotuba ya kimapinduzi makubwa na uzalendo mkubwa sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma hotuba yote, ukurasa kwa ukurasa. Kimsingi bajeti hii imejikita katika mambo yafuatayo; kwanza ni bajeti ambayo imekusudia kuinua kilimo na kumwinua mkulima wa Tanzania. Pili, hii ni bajeti ambayo imekusudia kuhimiza sekta binafsi na biashara pamoja na wajasiriamali wa nchi. Hii ni bajeti ya kihistoria kwa sababu pia imekusudia kukuza ajira nchini; ni hotuba ya kihistoria kwa sababu imekusudia kutoa tija na motisha kwa wafanyakazi wa nchi yetu ya Tanzania; pia ni hotuba ya kihistoria kwa sababu imedhamiria kuboresha huduma za kijamii zikiwemo, afya, maji, elimu, barabara, utalii na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii imepokelewa vizuri sana na Watanzania wote nchini kote. Nampongezz Waziri kwani kwenye hotuba hii amedhihirisha wazi kwamba alichukua muda kujiandaa na kufanya utafiti, hongera sana. Pamoja na uzuri wa hotuba hii ya Waziri wa Fedha naomba ninukuu maneno ya Makamu wetu wa CCM Taifa, Comrade Kanali Abdulrahman Kinana aliyoyasema wakati akishiriki sherehe za Iftar tarehe 23 Aprili, 2022 kwenye kuadhimisha miaka 18 ya Kampuni ya Usafirishaji (Silent Ocean Company).

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kinana anasema hivi, “nataka vikao vizae matunda. Nchi hii imeharibiwa na “vikao,” nchi hii imeharibiwa na “mchakato,” nchi hii imeharibiwa na “tutafanyia kazi,” nchi hii imeharibiwa na “tupeni muda,” nchi imeharibiwa na “tutasikiliza,” nchi hii imeharibiwa na “tutakwenda kutatua kero.” Makamu wa CCM anasema yote tumesikia, tunataka vitendo. Huyu ni Makamu Mwenyekiti wa CCM, Abdulrahman Kinana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa uzuri wa hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri kwa kutembea kwenye maneno ya Kiongozi wetu wa CCM Taifa ni kwamba, hotuba hii ni nzuri sana, imejaa mapinduzi makubwa, imejaa uzalendo mkubwa, lakini haitakuwa na maana kama haya ambayo yamesemwa hayatakwenda kwenye maneno hayo ambayo Makamu wa CCM anasema, tusiendelee kusema “mchakato unaendelea, tunakwenda kufanyia kazi.” Tunakuomba Mheshimiwa Waziri, hotuba hii ikatekelezwe ili ionekane wazi kwamba tumetafsiri kwa vitendo maono ya Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na sehemu ya kilimo. Kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, ukisoma kwenye ukurasa wetu wa 29 utaona wazi kwamba Mheshimiwa Rais anatembea kwenye Ilani ya CCM. Ukurasa wa 29 ile sehemu ya kwanza inasema katika miaka mitano ijayo CCM itaielekeza Serikali kuongeza fursa za ajira katika sekta rasmi na isiyo rasmi zisizopungua milioni saba kwa kuchukua hatua mbalimbali zikiwemo zifuatazo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Ilani yetu inasema kuchochea ukuaji wa uchumi hususan katika sekta ya viwanda vinavyotumia malighafi za kilimo, mifugo, uvuvi, madini, maliasili na sekta ya huduma za kiuchumi ikiwemo utalii. Tumemwona Mheshimiwa Rais akitekeleza maono haya ya Ilani ya CCM kwa vitendo. Rais wetu kwenye sehemu hii ya kilimo kwenye hii bajeti yetu ameongeza zaidi ya shilingi bilioni 700 kwenye kilimo. Kwenye sekta ya Utalii peke yake Rais wetu amezunguka nchi mbalimbali akitangaza Royal Tour ambayo sasa imeanza kuzaa matunda makubwa kwa ajili ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa upande wa ajira, kwa mara ya kwanza kwa miaka mitano iliyopita Mheshimiwa Rais wetu ametoa ajira kwa vijana wetu zaidi ya 30,000 katika mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba Mheshimiwa Rais amedhamiria kuboresha huduma mbalimbali kwa mujibu wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. Kwenye maneno haya ambayo nimesema kwamba tunaomba vitendo, naomba Mheshimiwa Waziri, kwenye hotuba yako amependekeza maeneo mbalimbali ya kuwabana watumishi na kufuatilia kodi na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo ambayo yako chini ya uwezo wetu kama Serikali ambayo tunaweza kuongeza mapato. Kwa mfano, wananchi wa Jimbo la Lupembe kwa mfano, wana Kiwanda cha Chai ambacho Serikali imekitelekeza kwa muda mrefu. Nimekuwa naongea mara nyingi humu ndani nikisema kwamba Kiwanda hiki kama Serikali ingekuwa na nia thabiti ingeweza kuingiza fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemwambia Waziri juzi kwa barua, kwamba kwenye Wizara yako Mheshimiwa Waziri kuna jambo limekwama kuhusu Kiwanda Lupembe. Naibu Msajili au Msajili wa Hazina amekalia maamuzi ya Mahakama yanayomtaka atekeleze uamuzi wa Mahakama wa kumtaka Mwekezaji wa Kiwanda cha Lupembe Do Mecan TYRE aweze kuachilia kile kiwanda ili Serikali iweze kuendelea.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Naunga mkono hoja ya Serikali. (Makofi)