Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kushukuru kwa kunipa fursa kuchangia katika hoja hii ambayo iko mbele yako. Nianze moja kwa moja kwa kumpongeza Shemeji yangu Waziri Dkt. Lameck Mwigulu Nchemba kwa wasilisho zuri alilofanya, kuwasilisha utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo na ile Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze sana Serikali yangu CCM inayoongozwa na Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutekeleza vyema sana ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. Serikali yetu inatekeleza miradi mingi sana katika Majimbo yetu yote Serikali ya Awamu ya Sita na pamoja na miradi inayotekelezwa katika Majimbo yote, Serikali inatekeleza miradi ya mikakati ambayo ni miradi mikubwa ikiwepo ile ya reli ya SGR, mradi wa Julius Nyerere, Daraja la Busisi na miradi mingine mikubwa, kwa hiyo tunaipongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sintokuwa na shukrani kama sitasema ahsante kwa kidogo ambacho Serikali imetupatia katika Jimbo langu la Moshi Vijijini. Naishukuru sana Serikali kwa sababu tumepata miradi ya kutosha kusema ukweli, tuna daraja la pale Rau, Rais wetu alikuja akalizindua ambalo liligharimu Shilingi Milioni 910, kuna Mradi wa Maji wa Telamande Waziri Mkuu alikuja akauzindua uligharimu shilingi milioni 905, kuna ujenzi wa madarasa 53 ya mradi wa UVIKO ambayo yamegharimu shilingi bilioni moja na milioni sitini, kuna mradi wa maji wa mradi wa UVIKO pia uko katika Kata za Kimochi na Mabogini ambazo ni bilioni moja, kuna ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo tumeshapata shilingi 500. Zahanati ya Uru Kusini ambayo tumeshapata shilingi milioni 500, ukarabati wa barabara saba kwa kiwango cha moramu ambapo tumepata shilingi bilioni 1.5 tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na utaalam wangu mimi nitachangia kwenye Sekta ya Kilimo na nianze kwa kumpongeza sana Waziri wetu na Serikali yetu kwa kupandisha bajeti ya kilimo kutoka shilingi bilioni 294 mpaka shilingi bilioni 954 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 308.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pesa hizi ambazo zimepeleka Wizara ya Kilimo nina hakika zinakwenda kuhudumia wakulima ambao ni karibia asilimia 65 na wataenda kunufaikia vizuri sana. Ushauri wangu kwenye hili kwamba nitaongelea kilimo cha kahawa, kilimo cha mbogamboga, nafaka na mikunde kama muda utabaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kahawa tunaiita ni dhahabu ya kijani na bei ya kahawa ya Arabica kwenye soko la dunia sasa hivi ni dola 4.2 na ile ya Robusta ni dola mbili, na mwaka ulioishia wa fedha ni kwamba kule Moshi wakulima walipata mpaka shilingi 7,000 kwa kilo moja na leo asubuhi George alisema kule Bukoba wakulima walipata shilingi 3000.

Mheshimiwa Naibu Spika, uzalishaji wa zao la kahawa hapa nchini kwa ujumla umeongezeka kutoka tani 60,651 mpaka tani 73,027 ikiwa ni ongezeko la asilimia 20.4 na ongezeko hili kwa mwaka huu ulioishia data za TRA zinasema kwamba nchi yetu mwaka 2021 ilipata kiasi cha pesa dola milioni 155 ikiwa ni zao la pili kutoka kwenye korosho ambayo ilipata dola milioni 159.

Mheshimiwa Naibu Spika, kahawa inazalishwa kwenye Mikoa mingi hapa nchini, kahawa inazalishwa Kilimanjaro, Kagera, Arusha, Ruvuma, Mbeya, Mara, Songwe na Kigoma. Sasa pamoja na umuhimu wa kahawa katika uchumi wa nchi yetu tumeshaona ni zao la pili ambalo linaliingizia Taifa letu pesa nyingi, lakini kuna changamoto ambazo zipo na ningependa tuzijadili hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote haya yanayozalisha kahawa changamoto yao kubwa ni upatikanaji wa maji ya kumwagilia ili wakulima waweze kuvuna kwa wingi hiyo ndiyo changamoto ya kwanza, changamoto ya pili ni miche bora, na changamoto ya tatu ni pembejeo. Kama wenzetu wa korosho na tumbaku wanavyopata pembejea wakulima wa kahawa walikuwa hawapati pembejeo na hii ilisababisha tusiende vizuri sana. Kwa hiyo ninaishauri Serikali kwamba zile pesa za umwagiliaji ambazo zimetoka, tuwekeze kwenye mifereko ya asili ili tuwafikikishie wakulima maji na wakishapata maji watazalisha kahawa nyingi na tutaipatia Taifa letu pesa za kutosha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya pili ni miche. Kuna ile miche Milioni 20 ambayo Mheshimiwa Waziri Bashe amesema kwamba atategemea kwenye bajeti hii tunaomba miche na pembejeo wapelekewe wakulima ili tuweze kushiriki kikamilifu katika uzalishaji wa kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni kwenye zao la mbogomboga. Mbogomboga ni zao la thamani sana na sekta hii ikiandaliwa vizuri kama tutapanga vizuri tukiwa na mikakati ya kutosha, tukiwapa vijana kazi ya kutuzalishia mbogamboga, nina uhakika kama Taifa tutawatoa vijana na Taifa litapata pesa nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka uliopita, ulioishia 2021 sekta ya mbogamboga iliingizia nchi yetu dola za Kimarekani milioni 373 na mwaka huu tunategemea mbogamboga zitaingiza dola milioni 750 na kufikia 2030 mbogamboga tunategemea zitaliingizia Taifa dola milioni mbili. Sasa niombe ukienda kwenye maeneo kama Mji wa Karatu, ule Mji umejengwa pale kutokana na zao la vitunguu. Karatu tunayoiona leo imetokana na zao la vitunguu, kwa hiyo tukiwekeza tukiwapata vijana kazi ya kuzalisha mbogamboga, tukiwawekea miundombinu ya kutosha kwanza, tuwaandae wawe kwenye vikundi, wakishakuwa kwenye vikundi tuwahamasishe wazalishe mbogamboga kwa wingi ili zile ndege tumenunua ziweze kupeleka nje na kuliingizia Taifa pesa za kigeni. Tukiboresha huduma za ugani kwa hawa vijana ambao tutakuwa tumewaandaa tunaweza tukaanzisha viwanda vidogovidogo ambavyo pamoja na kupeleka mbogomboga nje pia tutaliingizia Taifa letu pesa za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa mwisho ni kwenye nafaka na mikunde. Tanzania yetu hii inajitosheleza kwa chakula, mwaka wa 2021 nafaka na mikunde uzalishaji uliongeza kutoka tani milioni 18 toka tani 18,196,733 hadi tani 18,665,065. Mafanikio haya ya uzalishaji mzuri wa nafaka ulitokana na uwepo wa mvua ya kutosha, lakini mwaka huu kama tunavyojua wote mvua ni kidogo sana, huenda tukapata matatizo na tukawa na uhaba wa nafaka na chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Waziri wa Kilimo na kwa Serikali kwa ujumla wake ni kwamba zile scheme mpya ambazo tunazianzisha sasa hivi, zilenge Mikoa ambayo ina maji mengi ya kutosha ili tusije tukaanzisha scheme kwenye maeneo ambayo hakutakuwa na maji na hazitakuwa sustainable tunaweza tukapata hasara. Kwa hiyo mchango wangu ni kwamba scheme hizi ziwekwe kwenye maeneo ambayo yana maji ya kutosha ili hii miradi iwe endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)