Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Moja ya jambo ambalo binafsi linanipa ukakasi ni suala la mgawanyo wa fedha za Muungano. Wazungumzaji wengi waliopita walimsifu Waziri na timu yake na wakamtaja Waziri kwamba ni mchumi aliyebobea, maana yake kwamba ni msomi, lakini sifa moja ya wasomi ni wale wenye kutumia taaluma yao ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo linanipa mashaka makubwa. Tukiangalia katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sura ya Saba inazungumzia masharti ya kukusanya fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ibara ya 133 naomba ninukuu: “Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itatunza akaunti maalum itakayoitwa “Akaunti ya Fedha ya Pamoja” na ambayo itakuwa ni sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambamo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili…”

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar. Hata hivyo, hadi leo hii bado Serikali haijataka kuweka wazi, je, hii akaunti ya fedha ya pamoja ipo? Je, hii akaunti ya fedha ya pamoja, kwa sababu hapa tuna ushirika, tumekubaliana tunachanga, tutakachokipata tunakiweka sehemu moja, baadaye tunafanya matumizi, tunaambiana tumetumia kiasi fulani cha fedha na kitakachobaki tunakigawa kwa mujibu wa Katiba na kwa mujibu wa makubaliano tuliyokubaliana katika hii Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kushangaza, hatuna akaunti ya fedha ya pamoja. Hatujui ni mahali gani fedha hizi zinawekwa. Ni namna gani ambazo fedha hizi zinatumika. Leo kama haitoshi, katika ibara hiyo ya 134 pia ilipendekeza kuweko na Tume ya Pamoja ya Fedha, lakini hadi leo hatujui ni namna gani tume hii inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitegemea tume hii iweze kukusanya fedha, lakini kutupa taarifa ni namna gani fedha wamekusanya kiasi gani, ni namna gani fedha hizi wametumia, ni namna gani fedha ambazo zimebaki na mgawanyo sasa tunagawaje kati ya Zanzibar na Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali hii inapelekea mgogoro na malalamiko makubwa juu ya suala zima la Muungano hususan kwa upande wa Zanzibar. Naomba ikumbukwe mwaka 2006 iliundwa tume iende ikafanye utafiti, ione namna gani ya mapato na matumizi ya fedha hizi za Muungano. Tume ile ikiitwa PWC ilianza kufanya kazi kuanzia mwaka huu 2014 hadi 2020, ilionesha ni kwa namna gani Zanzibar hatupati stahiki ya fedha zetu kwa mujibu wa Katiba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi hiki hadi 2014, zaidi ya Shilingi Trilioni 11.2 Zanzibar tukidai Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa naamini Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, atatuambia sasa ni kwa asilimia ngapi Zanzibar tulipata fedha hizi kwa mujibu wa taarifa ya Tume hii ya PWC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme. kwa sababu ya muda, mgawanyo wetu ni asilimia 4.5 lakini kwa report hii tulipata asilimia 1.1 kwa nini? Tumekuwa kama ni uhisani tunafadhiliwa wakati sisi ni washirika katika tume hii. Naomba nitoe rai au nitoe ushauri kwa Serikali. Kwanza, naomba Serikali kufuata Katiba na Nchi kwa kuanzishwa Akaunti ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa sheria ya mapato yote ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naiomba Serikali ifanye utafiti mpya wa mapato ya Muungano na matumizi kwa shughuli za Muungano tu ili kutoa takwimu sahihi kwa kipindi tulichonacho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, naiomba Serikali igawe ziada ya mapato ya Muungano kwa washirika wa Muungano kwa mujibu wa mgao na kanuni za mgao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, naiomba Serikali kumtaka CAG kufanya ukaguzi ili kubainisha mgao sahihi na fedha ambazo Zanzibar inaidai Serikali ya Muungano kwa kipindi chote toka kuanzishwe kwa jambo hili la Akaunti ya Pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)