Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa maono yake, kwa uongozi wake thabiti na imara sana na kwa namna anavyowatumikia wananchio wa Taifa hili. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake wote kwa namna walivyobeba maono ya Mheshimiwa Rais na kuwasilisha bajeti katika Bunge lako Tukufu, bajeti ambayo ni moja kati ya bajeti bora ambazo nimeshuhudia nikiwa Bungeni hapa. Jukumu letu ni kutoa ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitachangia kwenye maeneo kama manne iwapo muda utaniruhusu na kwa kuanzia nitaanza na eneo la elimu. Kwenye hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 51, ameongelea maamuzi ya Serikali kuanzisha dirisha kupitia TASAF, kusaidia watoto ambao hawana uwezo wa kulipa ada. Ni jambo jema, lakini kwenye eneo hili ningeshauri watu wanaonufaika na Mfuko wa TASAF haujajumuisha wale wote ambao wangestahili kufaidika na Mfuko ule. Kwa mfano, kuna viongozi wa Serikali za Vijiji, kuna Viongozi wa Vyama vya Siasa, haijalishi kama kiuchumi hayuko vizuri, lakini kwa sifa hiyo tu ya kuwa kiongozi hanufaiki na Mfuko wa TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo tafsiri yake ni kwamba, watoto ambao kutokana na baba yao kutokuwa na uwezo kiuchumi hawawezi kunufaika na Mfuko huu. Kwa hiyo, ningeshauri kwenye eneo hili iangaliwe namna nyingine bora ambayo itabainisha watoto ambao watanufaika na mfuko huu na dirisha hili la TASAF ambapo kwa kuanzia Mheshimiwa Waziri amesema unaweka bilioni nane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la elimu vilevile niipongeze Serikali kwa kufuta ada ya kidato cha tano na cha sita. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi huu, lakini niombe pamoja na kuondoa ada bado sehemu kubwa ya wanafunzi wetu na vijana wetu wanaathirika sana na michango mbalimbali. Kwa hiyo, ningeshauri Serikali iangalie namna bora ya kudhibiti michango hii na kuwe na chombo kama ni Wizara ya Elimu na chombo kingine chochote ili kuainisha ni michango ipi ambayo itapaswa kutozwa kwenye shule zetu, isiwe kikwazo kwa watoto wanaoenda kupata elimu kupata yale manufaa ya kufuta ada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mipango yetu, sera zetu zinapaswa kujibu matatizo ya vijana wa Taifa hili, vilevile kwa dhamira hii njema ya kufuta ada ya kidato cha tano na cha sita, lakini na kuweka dirisha hili kupitia TASAF, bado kuna umuhimu wa Serikali kuona haja ya kugharamia ada za vijana wanaoingia kwenye vyuo vya kati, Vyuo vya VETA, tunajenga vyuo vingi sasa hivi, kuna Vyuo vya Maendeleo ya Jamii, ni daraja ambalo linatengeneza vijana wengi sana ambao wanaingia kwenye soko la ajira, lakini wengi wanashindwa kuendelea kwa kukosa pesa za kugharamia mafunzo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaishauri Serikali ione umuhimu vilevile wa kugharamia level hii ya kati ambayo ndiyo ya watenda kazi ambao tunawaingiza kwenye soko la ajira lakini vilevile kuanzisha shughuli mbalimbali za kiuchumi na baadae kuwa walipa kodi wazuri na kuweza kusaidia Taifa letu kujijenga kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni eneo la utalii. Ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa kutengeneza filamu ya Royal Tour. Dhamira ya Mheshimiwa Rais ni njema na ina matokeo chanya, kwa mujibu wa Ilani yetu ya uchaguzi ni kweli na kwa kupitia Royal Tour itatusaidia sana, lakini nishauri pamoja na dhamira hii njema ya Mheshimiwa Rais ambapo ameonesha njia ametengeneza skelton wajibu wetu sisi Wizara nyingine nyingi, taasisi na watu binafsi ni kujaza nyama sasa kwenye skelton hii ili hii Royal Tour iwe na taswira iwe na impact chanya kwenye eneo la utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo vivutio vingi sana vya utalii lakini bado hatujaweza kuvitangaza ni jukumu sasa la Wizara mbalimbali Wizara ya Uwekezaji, Wizara ya TAMISEMI kwenye miundombinu, Wizara ya Utalii yenyewe na maeneo mengine yote ili kuweza sasa ku-compliment hiki alichokifanya Mheshimiwa Rais ili kiweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kuna vivutio vingi kwa mfano mimi kwenye eneo langu la Ukerewe kuna vivutio vingi. Kuna jiwe linacheza kule, kuna beach ya Rubya kuna mapango ya Andebezi ambayo tokea shule za msingi tunasoma na maeneo mengine ninaamini hata maeneo mengine kuna vivutio vingi vya utalii lakini bado havijaweza kutambulika na kutengenezewa miundombinu ili hawa sasa tunaowashawishi waje kutembelea Taifa letu waweze kuvijua na kuweza kuvitembelea. Kwa hiyo, tu-compliment hii Royal Tour sisi kama Wabunge lakini na taasisi nyingine zote ili angalau iweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo ningetamani kuchangia ni eneo la kilimo. Ninaipongeza Serikali kwa mara ya kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais bajeti ya Wizara ya Kilimo imepanda kutoka Bilioni 294 mpaka Bilioni 954, haya ni mapinduzi makubwa sana na kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri lengo ni kuongeza uzalishaji kwenye kilimo cha umwagiliaji kutoka asilimia 10 mpaka asilimia 50, ninaamini tunaweza tukafikia lengo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia trend ya kukua kwa uzalishaji kwenye eneo la kilimo imekuwa siyo nzuri sana. Ukiangalia kwa mfano, mwaka jana kwenye Pato la Taifa kilimo kimechangia asilimia 26.4 mwaka jana tukashuka mpaka 26.1 lakini kwa haya mapinduzi na mtizamo wa Serikali sasa kuongeza bajeti, ninaamini tutaenda mbele zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuweka nguvu kwenye kilimo hiki cha umwagiliaji ninaamini tuna maeneo ambayo tunaweza tukayatumia tuna-quick wins nyingi sana, ni vizuri tukaangalia sasa maeneo ambayo tunaweza tukawekeza kidogo kwa kuanzia lakini tukapata tija hasa kwenye maeneo ambayo yanazungukwa na maji, kuna vyanzo vya maji tayari badala ya kwenda kwenye maeneo ambayo tunahitaji kuweka uwekezaji mkubwa, kuna maeneo yanayozungukwa kwa mfano na maziwa, yanazungukwa na mito tunaweza tukawekeza kwa kuanzia na kukawa na matokeo chanya kwa sababu tayari kuna vitu vya kuanzia kuna chanzo cha maji. Sisi Ukerewe pale kwa mfano, tuna hekta zaidi ya 2000 ambazo tungeweza kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji tukapata mavuno mengi sana mavuno makubwa, sambamba na Ukerewe lakini kuna maeneo mengine vilevile yana taswira kama hiyo, ni vizuri tukaangalia maeneo haya kwa kuanzia tukawekeza tukaweza kupata tija kwenye eneo hili la umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunawekeza nguvu kubwa kwenye kilimo cha umwagiliaji ni lazima tuangalie tumejiandaaje kwa sababu tumewekeza lazima tutapata matokeo chanya, tutapata mavuno mengi, tumejiandaaje sasa kupata soko la mavuno haya ambayo tutayapata kutokana na kilimo hiki cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri siyo vibaya Serikali vilevile ikatengeneza matajiri wazalendo kwenye Taifa hili, ikatengeneza watu ambao inaweza kuwatengenezea njia, kuwatafutia masoko ikawapa mitaji ili wakiwa wazalishaji wazuri na wakawa wametengenezewa masoko wakaweza ku-supply mavuno hayo ambayo tutakuwa tunayapata. Kwa sababu moja kati ya changamoto ambazo tumekuwa nazo kwenye Taifa hili ni kwamba tunazalisha chakula, tunapata masoko nje ya nchi, lakini sasa kunakuwa hakuna consistence ya uzalishaji wa mazao yale, kitu ambacho kinapelekea wale tunaowasambazia bidhaa zile wanakata tamaa na kuingia mikataba na watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kulea watu wetu, tukawapa mitaji, tukawajengea mazingira wakawa wazalishaji wazuri, ina maana itatusaidia hata kuweza kupata masoko ya uhakika lakini tukaweza kuwasambazia na kusaidia Taifa letu kwenye kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la mifugo na uvuvi ninaipongeza Serikali kuongeza bajeti kutoka Bilioni 100 mpaka Bilioni 268, kwenye eneo la uvuvi pekee imeongezeka karibu Bilioni 176. Ninaendelea kuisisitiza Serikali iwekeze nguvu kwenye ufugaji wa Samaki kupitia vizimba, yatakuwa mapinduzi makubwa sana na kwenye eneo hili, itasaidia hata ajira kwa vijana wetu ambao tumekuwa tunawasemea ili waweze kupata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la nne na la mwisho ni kwenye eneo la ufanisi wa miradi ya maendeleo. Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 21 umeongelea juu ya eneo hili, ukasema Mheshimiwa Rais amekuelekeza kuangalia upya taratibu za ununuzi na thamani ya fedha kwenye miradi ya maendeleo, ni kweli tunapoteza pesa nyingi sana kwenye eneo hili, wamesema wachangiaji wengine kama tutaangalia vizuri kwenye eneo hili itatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano kwenye eneo langu la Ukerewe, mwaka jana nashukuru tumepata pesa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya lakini kuna sintofahamu namna gani mradi huu unatekelezwa, ni vizuri kwenye eneo hili Serikali ikasimamia kwa makini, tunapoteza pesa nyingi sana hasa kwenye Halmashauri zetu kwa sababu ya mifumo hii kwa kutumia sheria zetu za manunuzi, kwa hiyo, kama tutaliangalia vizuri jambo hili itatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)