Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. KASASALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima. Niwashukuru vile vile wapiga kura wa Jimbo la Sumve kwa ushirikiano mkubwa ambao wamekuwa wakinionesha tangu nichaguliwe kuwa Mbunge wao katika kutekeleza majukumu ya kuleteana maendeleo na kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajielekeza katika hoja yangu, naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ambayo ameifanya na anaendelea kuifanya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi sisi watu wa Jimbo la Sumve, Mbunge wa Sumve anaposimama na kupongeza, anapongeza kwa mifano ambayo ipo bayana. Tangu Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aingie madarakani, sisi watu wa Sumve alitukuta tunazo zahanati 21 tu, lakini leo ninapozungumza, zahanati 10 ndani ya mwaka mmoja, yaani ninapozungumza zahanati 21 nazungumza tangu uhuru, lakini ndani ya mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu Hassan, watu wa Kijiji cha Mwashilalage, Zahanati; Kijiji cha Bung’egeja, zahanati; Kijiji cha Nyamikoma, Zahanati inaanza kujengwa; Kijiji cha Busule, Zahanati; na Kijiji cha Kinamweli, Zahanati. Naweza kuzungumza hapa vijiji vingi lakini ndani yam waka mmoja kwa hiyo tunaposema Rais Samia Suluhu Hassan anafanya kazi kubwa nadhani ni kazi ambazo zinaonekana kwa urahisi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge wa wakulima na wafugaji, katika Jimbo la Sumve tunalima pamba Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametukuta tunauza pamba kwa Shilingi 800 lakini mwaka jana tumeuza pamba kwa bei ya juu kabisa ya 1,500 lakini sasa hivi pamba tunaendelea kuiuza kwa bei ya Shilingi 2,000. Kwa hiyo tunaposema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imetusaidia wakulima mifano inaonekana na ni bayana, ndiyo maana naona kwamba nikisimama hapa nikaacha kupongeza nitakuwa sijawatendea haki watu wa Sumve. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba sasa na mimi nielekee kwenye kushauri katika bajeti ambayo Kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ametusomea humu bajeti ya Serikali yetu pendwa ya CCM.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tunatakiwa sisi ambao wenzetu hawa ambao mmepewa kazi ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika Wizara mbalimbali mnatakiwa mtumie muda mwingi kujifunza namna ambavyo Mheshimiwa Rais anavyotaka nchi iende. Mheshimiwa Rais ametuonyesha kwenye TARURA kwamba anataka kila eneo lipate kwa usawa. Wabunge ni mashahidi kwenye Majimbo yetu, Mheshimiwa Rais alipoingia tu alitupatia Milioni 500 kila Jimbo akiwa na maana kwamba hii nchi ni moja, watu wote wapate maendeleo kwa usawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye fedha maarufu za Mama Samia ambazo tulikopa Mama ametupatia kwa usawa kila Jimbo linajenga madarasa watu wanaona, kwa hiyo tunatakiwa sasa na maeneo mengine mfahamu nia ya Mheshimiwa Rais kupitia mifano hii. Katika sekta ya umeme sote tunaona nchi nzima vijiji vyote vinawekewa umeme, Mama anataka nchi iende kwa usawa. Sasa ipo shida moja kwenye eneo la miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hii kuna maeneo ambayo yanabandua lami yanaweka mpya na kuna maeneo ambayo hayana hata milimita moja ya lami. Katika jumbo la Sumve ambalo mimi ninatoka, ambalo ninadhani wote tukipitishana kwenye historia ya nchi yetu Jimbo la Sumve liko kwenye Wilaya ya Kwimba, Wilaya ya Kwimba ni moja ya Wilaya ambazo zimeachwa ni Wilaya ambazo zilianzishwa kabla hata hatujapata uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Nyanza Province kulikuwa na Wilaya ya Mwanza, Wilaya ya Kwimba, Wilaya ya Maswa, Wilaya ya Musoma, Wilaya ya Shinyanga, Wilaya ya Kahama na Wilaya ya Bukoba, baada ya Nyanza Province kutoka ukaja Mkoa wa Mwanza Wilaya Nne za kwanza Kwimba imo, Kwimba Mwanza Geita na Ukerewe lakini baada ya Geita kutoka Wilaya Kwimba bado ipo na Jimbo lake la Sumve imezaa Wilaya ya Misungwi, Wilaya ya Misungwi ina lami, imezaa Wilaya ya Magu, Makao Mkuu ya Magu na Mkoa wa Mwanza na Mikoa mingine imeunganishwa na lami, tukazaa mjukuu Busega ameunganishwa na lami. Sasa Kwimba tunashida gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri wa Fedha, naiomba sana Serikali ya CCM igawe maendeleo kwa usawa hasa kwenye sekta ya barabara. Haiwezekani kila siku tangu Rais Mkapa alisimama akatuahidi watu wa Kwimba na sisi tutapata lami haikufanikiwa, akaja Rais Kikwete akatuahidi haikufanikiwa, akaja Hayati Magufuli akatuahidi haikufanikiwa! Hapa sasa hivi tuna amani Rais Samia ameonesha dhahiri anataka nchi iende kwa usawa. Sasa nimepitia hii bajeti bado mnaonekana hamko serious kwenye jambo la barabara kwenye baadhi ya maeneo hasa Jimbo ninalotoka la Sumve.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Sumve tulikuwa tukiimba wimbo wetu hapa kuanzia bajeti iliyopita tunataka walau basi kwenye bajeti na sisi mtuone mtujengee barabara yetu ya kimkakati na ya muhimu inayoanzia Magu inapita Bukwimba inaenda Ngudu mpaka Hungumalwa, barabara yenye urefu wa kilimeta 71 katika bajeti iliyopita Serikali ikatupangia kutujengea kilomita 10 hawajajenga hata milimita moja, katika bajeti hii ndiyo sioni kabisa hata mwelekeo, sasa tukienda namna hii nchi yetu tutakuwa tunapendelea baadhi ya maeneo na kutekeleza baadhi ya maeneo,.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike wakati tufahamu kwamba ili maendeleo yafaidishe watu wetu lazima kuwe na usawa kwenye ugawanaji wa keki ya Taifa, haiwezekani wenzetu wanabandua lami sisi hatuijui, ukichukua mtoto wa Sumve ukamwambia neno lami hajui! Ninaposema hapa mnaweza mkawa hamnielewi kwa sababu ninyi wengi mnalami kwenu lakini Sumve hatuna hata milimita moja ya lami. Baada ya miaka yote hii ya uhuru sasa tufike wakati tuweke mstari na sisi sasa muda wetu umefika, eleweni Mheshimiwa Rais anataka watu wote wapate haki, watu wote wagawiwe keki hii kwa usawa, twendeni mtugawie kwa usawa zipo barabara za muhimu sana kwenyeJimbo letu, katika Serengeti ya Kusini…

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Mbunge makini, jambo hili ni jambo ambalo haliwezi kuachwa liendelee hivi. Wengine tulioko Kaskazini tunazungukwa na Wilaya zenye lami na zingine ndiyo hizo ambazo ni bandika bandua imefika wakati wale ambao wanapata barabara za lami sasa hata za zamani wasimame tupate lami wengine ili na wao waweze kupata na wale walipata kupitia TANROADS wasipewe barabara nyingine kupitia TARURA mpaka Watanzania wengine tuwe tumepata lami, tumeahidiwa haitekelezwi! Ahsante.(Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mageni taarifa hiyo unaipokea.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa naipokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema kwamba tugawiwe kwa usawa nafikiri tunatakiwa tufike wakati tuelewane, Mheshimiwa Mwigulu na wewe unatoka Iramba huko angalau labda ninyi mmeungwa kwa lami, lakini tuelewe kwamba watu wetu wanahitaji maendeleo, tunapotaka utalii ukue Serengeti Kusini kote mimi nilikuwa juzi Mwandoya wananchi wanachukia Tembo, wanachukia mbuga za Wanyama kuliko kitu chochote, kwa sababu hawafaidiki nazo. Barabara za msingi zinazotakiwa kupeleka watalii waende mpaka Meatu, waende kwenye maeneo ya utalii ya Serengeti ya Kusini zote ni za vumbi! Barabara inayotakiwa kutoka Mwanza ikaja ikapita Fulo, ikaenda ikapita Sumve, ikaenda ikapita Nyambiti, ikaenda Malya mpaka Maswa, barabara hii imekuwa ni story na barabara ya kujazwa ukurasa wa Ilani inaandikwa kila siku, haijengwi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tufike wakati jamani kama alivyosema Mheshimiwa Ole-Sendeka waliopata wasimame, Mheshimiwa Waziri angalia hii bajeti yako haiwezekani sisi watu wa Sumve tukawa tunakuja kukusindikiza humu, tunasindikiza wengine wanawekewa lami sisi tuko tu hapa tunapiga makofi, wananchi wa Sumve wameniambia nisipige makofi kwenye mambo ya hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitapiga makofi kwenye mambo ya hivi, haiwezekani sisi tukasindikiza watu tukabaki kuwa watazamaji wa lami za watu. Inafika wakati mimi wakati kwa historia mwaka 2000 kuna binti anatusaidia nyumbani, Mimi naenda Shinyanga nikapanda naye basi nilipofika eneo ambapo kuna lami, kwenye eneo la Mabuki pale, yule mtoto akaniambia Kaka hivi kumbe barabara za huku zimewekewa cement yaani haelewi lami na cement anaonaga ndani sasa ifike wakati muwakumbuke hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii nchi ni ya kwetu sote tunataka maendeleo, msisitizo wangu ni kwamba maendeleo na keki ya Taifa tuigawane kwa usawa. Nakushukuru sana. (Makofi)