Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nyasa nianze na kumshukuru sana sana sana Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake yote na kwa bajeti hii inayoongozwa sasa na Mheshimiwa Waziri Mwigulu kwa jinsi ambavyo wameweza kutekeleza shughuli za kimaendeleo katika Jimbo langu la Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa usimamizi wao kwa kazi zote zinazoendelea. Kwavile siyo rahisi kumshukuru kila mmoja, niseme tu nawashukuru wote waliohusika katika kuleta maendeleo katika Jimbo langu la Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuishukuru Serikari kwa kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami, barabara ya kutoka Kitai kwenda Litui hadi Ndumbi. Pia naomba watusaidie juu ya Daraja la Mitomoni ambalo liko katika Mto Ruvuma ambalo kwa kweli limekuwa ni kilio kikubwa kwa wananchi na wananchi wamekuwa wanapata shida wengine kiasi cha kufariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati nzuri yalipotokea yale maafa, Serikali ilipeleka timu wakafanya feasibility study kiasi kwamba lile daraja sasa liko tayari kwa kuanza kujengwa. Ni imani ya wananchi kwamba daraja hilo litajengwa ili kuondoa adha iliyopo na pia hata hali ya kimawasiliano ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii napenda nizungumzie kama ushauri kwa upande wa Serikali. Serikali imetufundisha jambo moja kubwa sana kupitia mkopo wa masharti nafuu ambao uliletwa kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa madarasa. Katika hilo nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo mkopo huu ulifanyiwa kazi. Fedha iliyotolewa ni Shilingi trilioni 1.3, lakini fedha hii inajulikana na kila Mtanzania, kila mtu anajua kwamba kuna mkopo wa Shilingi trilioni 1.3 umeenda kufanya kazi hii na hii na hii, kiasi kwamba mpaka unaweza kufikiria kwamba ah, hivi ina maana kumbe kwa mwaka mzima yawezekana fedha iliyofanya kazi ni hiyo tu. Kwa sababu zile fedha nyingine tunazokusanya tumeambiwa ni karibu Shilingi trilioni 20 na kitu, hazioneshi moja kwa moja zimeenda katika matumizi yapi? Pamoja na kwamba kweli tunajua zimeenda kwenye wilaya zetu, lakini hazijawekwa kwa uwazi mzuri kama zilivyoweka hizi fedha za COVID-19. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kuona kwamba, kwa kuwa tunafanya hayo makusanyo na tumekuwa tukipeleka fedha huko, basi kila Wizara iwe inatoa orodha ya vitu ambavyo vinaenda kutekelezwa huko kunakotekelezwa, tuweze kuona kabisa Wizara hii ilipata fedha kiasi fulani na zimeenda mahali fulani ili tuweze kusimamia kwa karibu kama ambavyo tulisimamia haya madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijaribu kuona kwamba kama shilingi trilioni 1.3 ilifanya kazi kubwa hiyo nchi nzima, haya matrilioni mengine je, ukiondoa ile mishahara ya wafanyakazi na vitu vingine! Tukiamua hata Shilingi trilioni tatu tu hizi kwamba sasa zitaenda kufanya hili na hili, nina uhakika na tukijipangia muda tutaweza kupiga hatua kubwa sana katika maendeleo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ninalopenda kuchangia ni eneo la Wamachinga na ile asilimia 10 iliyozungumzwa kwamba ipunguzwe asilimia tano kwa ajili ya miundombinu. Kwa bahati nzuri eneo hili nimelifanyia kazi kwa kipindi kirefu. Niseme tu kwamba kundi hili la Wamachinga, siyo kwamba Wamachinga ni wale wanaotembea tu. Wamachinga wamekuja kutoa jina hilo kutokana na ule ubunifu wao wa kufanya biashara kiasi kwamba sasa hata wale wajasiriamali wadogo wenye mtaji kuanzia shilingi 1,000 mpaka shilingi milioni 50 wanaangukia katika kundi hilo la Wamachinga. Kimsingi ni wale wajasiriamali wadogo wadogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuzungumza kwamba ipo haja ya kuiga mtindo tunaowafanyia nyuki. Nyuki unamtengenezea mzinga, yeye anakupa asali. Sasa na hawa Wamachinga wanafanya biashara ambazo ukijumlisha katika ile thamani ya kazi wanayofanya ni fedha nyingi sana na wanatengeneza ajira nyingi sana katika nchi yetu. Ila kwa kuwa kundi hili hatujalitambua kikamilifu na kulipa haki kamili ya maeneo ya kufanyia kazi, ndiyo maana wakati mwingine tunampa pressure hata Mheshimiwa Rais, Wamachinga wetu wapate maeneo ya kufanyia kazi; wote tunachangia humo. Leo linapokuja suala la kusema kwamba tuanze sasa kutengeneza mazingira bora ya hawa watu kufanyia kazi, wote tunaruka. Tunasema ah, bora watu wakakopeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie ukweli, katika baadhi ya maeneo, hata ufuatiliaji wa hawa watu wanaokopeshwa unakuwa ni mgumu kwa sababu hawajulikani waliko. Unakuta watu wanapewa fedha tu kwenye kikundi wanaganagawana mambo yanakwisha. Imekuwa ni kama fedha za msaada badala ya kuwa ni fedha za kuwawezesha katika masuala ya kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya nasema mimi kama mimi na ninasimama mimi kama mimi. Najua Waheshimiwa Wabunge wengi wamekuwa upande tofauti, lakini kazi ya Bunge ni kila mtu anashauri anavyoona. Nasema wazo hili ni zuri sana, isipokuwa tunaweza tukaamua kuanza na maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Jimbo langu la Nyasa natamani liwe mfano, nami naunga mkono asilimia tano ikatengeneze miundombinu na asilimia tano wakopeshwe, na wale watakaokuwa wamekosa, waendelee kwenda benki kwa sababu benki zipo. Benki ya NMB ipo, CRDB ipo na mabenki mengine yapo. Hayo ndiyo tuwape sasa kazi ile ya kukopesha zaidi. Isitoshe mifumo yetu ya ukopeshaji inabidi na yenyewe itengenezewe utaratibu kama wa kibenki. Kwa sababu sasa hivi hata ukopeshaji wake saa nyingine hata taarifa haziko sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano. Pale kwangu Bambabay palikuwa hapana mazingira mazuri kabisa ya kupata chakula, nikaamua bora nitafute fedha ili waweze kupewa sehemu ya kufanyia kazi. Nikakaa nao, nikawashawishi, tukavunja mabanda yale ya biashara ambayo yalikuwa ya ovyo kabisa. Baadaye tukajenga mabanda mazuri, sasa hivi kila mtu anaenda pale na shughuli za kibiashara zimekuwa kubwa zinazidi kuongezeka. Huu ni mfano mdogo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mialo yetu mingi ni mibaya, ya ovyo kabisa. Ninazo picha hapa nitawaonesha. Hawasaidiwi hawa watu, kila siku wanakuwa ilimradi tu, ndiyo maana hawakui. Tunajiuliza kila siku, kwa nini hawa wafanyabiashara wadogo wadogo hawakui? Moja ya sababu ambayo kiutaalam imeelezwa ni maeneo ya kufanyia kazi ni hafifu. Siyo lazima kujenga soko kubwa sana, labda eneo kubwa kama labda tulivyofanikiwa Dodoma, hapana. Hata kama ni maeneo madogo madogo, lakini mtu afanye kazi zake kiunadhifu; na wanapokaa pamoja, wanapeana ujuzi na pia wanasaidiana hata katika mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasimama, nasema Serikali hata kama wazo hili itatokea kwamba wengi wamelikataa, mimi naliunga mkono. Naomba mkafanye pilot, yaani kama sehemu ya kujifunzia; kwenye Wilaya yangu ya Nyasa naliunga mkono. Yaani ninachoomba, tutoe flexibility. Wanaotaka zote kukopesha, hiyari yao; wanaotaka 50 kwa 50, hiyari yao; ilimradi taarifa ziwe wazi na watu waweze kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja.