Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE: ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi asubuhi ya leo ili nami niweze kuchangia hoja ya Waziri wa Fedha na Mipango inayohusu Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka uliopita Mpango wa Maendeleo kwa mwaka ujao lakini pia Mpango wa Mapato na Matumizi kwa mwaka ujao wa fedha wa 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze sana Wizara ya Fedha kwa kuja na mpango na bajeti ambayo inakwenda kugusa matarajio ya Watanzania. Bajeti ya mwaka huu tutakayoipitisha ni bajeti ambayo imezingatia kwa ukamilifu wake masuala ya maendeleo na ya huduma za jamii pongezi sana Wizara ya Fedha na Mipango. Wakati unatuletea mpango huu pamoja na mambo mengine tulizingatia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ambao tuliupitisha hapa Bungeni. Mpango huo wa Tatu wa Maendeleo pamoja na mambo mengine ulikuja na mikakati ya kuhakikisha kwamba tunajenga bandari za uvuvi katika maeneo yetu ya mwambao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru sana Serikali kwamba katika eneo hili tumeanza na Kilwa, na ninayoheshima kutoa taarifa kwamba mkataba wa kujenga bandari ya uvuvi pale Kilwa Masoko umesainiwa na tayari mkandarasi wa kutoka China ameanza kuoneshwa eneo la kufanyakazi. Hii ni faraja kubwa sana kwa Tanzania kwa ujumla wake lakini kwawana Kilwa kwa upekee wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo la bandari pamoja na mambo mengine ambayo Wizara ya Uvuvi na Mifugo imejiandaa ninayo ya kupendekeza. Jambo la kwanza ujenzi wa bandari ya uvuvi uendane na uwepo wa miundombinu mingine rafiki au taasisi zingine rafiki zitakazoendosha au zitakazowezesha bandari ya uvuvi kufanyakazi vizuri. Taasisi au miundombinu hiyo ni pamoja na hizi zifuatazo: -

Jambo la kwanza tunapendekeza chuo cha uvuvi kijengwe pale Kilwa Masoko ili bandari ya uvuvi na masuala ya kuelimisha watu masuala ya uvuvi yawe maeneo hayo hayo ya karibu. (Makofi)

Jambo la pili; tunapendekeza kwamba miundombinu ya barabara ya uhakika kutoka Bandarini Kilwa Masoko pale mpaka Nangurukuru kwenye Barabara Kuu (highway) ya Dar es Salam mpaka Mikoa ya Kusini ya Lindi Mtwara na Ruvuma iimarishwe ili iendane na mahitaji na kukidhi haja ya bandari ambayo tunakuja kuijenga. (Makofi)

Suala la tatu ambalo tunapendekeza; nimepitia mpango wa Wizara ya Uvuvi katika ujenzi wa bandari hii na nimeona kwamba tutajenga Soko la Uvuvi pale Kilwa Masoko. Mapendekezo yangu ni kwamba pale Kilwa Masoko tujenge kituo cha kukusanyia samaki au mazao ya bahari, badala yake soko la samaki likajengwe Kilwa Kivinje ambako kuna fursa za kutosha na kuna wadau wengi wachuuzi wengi, wavuvi wengi pale Kilwa Kivinje ambao ni mji jirani na Kilwa Masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne katika mapendekezo haya nipendekeze kwamba Uwanja wa Ndege wa Kilwa Masoko uimarishwe na ujengwe katika viwango vya kukidhi matakwa ya kimataifa. Hi ni kwa sababu sasa tunapojenga bandari ya uvuvi maana yake ni kwamba tunakuja kufungua fursa za kimataifa. Hatuwezi kufungua fursa za kimataifa kwa uwanja wa ndege tulionao sasa hivi ambao ni wavumbi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulikuwa na mpango wa kujenga uwanja huu wa ndege kwa kiwango cha changarawe. Uwanja huu unamita 1,800, Serikali imeweka changarawe mita 1,000 tu bado mita 800. Sasa niseme kwamba mita 800 zile zimaliziwe lakini tuwe na mpango sasa wa kujenga Uwanja wa Ndege wa Kilwa Masoko kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tuendane na kwenda kuwalipa fidia. Kulikuwa na mpango wa muda mrefu, na ninaomba niukumbushe hapa; upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kilwa Masoko ambapo wakazi wengi maeneo ya mashamba pamoja na nyumba zao zimewekewa alama, kwamba zitabomolewa ili kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege wakalipwa fidia na utekelezaji wa uwanja huu uanze mara moja kadri ambavyo Serikali itakuwa imejipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoka kwenye eneo hilo la masuala ya uvuvi na miundombinu yake rafiki nije katika eneo la menejimenti ya utumishi wa umma, usimamizi wa utumishi wa umma. Utumishi wa umma usimamizi wake unaanzia katika mchakato wa ajira mpaka mtumishi anastaafu. Hata hivyo kwa experience ambayo imejitokeza tokeza tumeona kwamba watumishi wa umma hawako katika hali ya kufurahi sana; kuanzia ajira zao mpaka ukomo wa ajira wanaishi maisha yaliyo ya mashaka mashaka kutokana kutosimamia vyema eneo hili la utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano eneo la pension kwa watumishi wa umma hivi tunavyozungumza bado kuna watumishi hawajalipwa mafao yao ya pension ilhali wamestaafu miaka miwili, miaka mitatu bado hawajalipwa. Vilevile kuna eneo la usafirishaji wa mizigo mtumishi baada ya kustaafu. Wapo watumishi wamestaafu miaka mitatu sasa, miaka minne bado hawajalipwa. Niikumbushe Serikali kwamba mwaka 2008, 2009 mpaka 2010 Ofisi ya Rais, Menajimenti ya Utumishi wa Umma ilikuwa na zoezi la kusafisha taarifa za watumishi maarufu kama data cleaning ili watumishi wenye sifa waweze kuwepo katika utumishi na taarifa zao zikawe sawa katika utaratibu wa kimtandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dhana hiyohiyo ya kusafisha taarifa za watumishi data cleaning niombe sasa Serikali ijisafishe yenyewe kwa kuhakikisha kwamba watumishi hawaidai Serikali yao. Sambamba na hilo kwenye eneo hilo la usimamizi wa menejimenti ya utumishi wa umma nigusie kidogo masuala ya uteuzi na utenguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uteuzi katika eneo hili uko wa namna mbili; wapo wanaoteuliwa kupata nafasi za uteuzi ndani ya utumishi wa umma, lakini wapo wanaopata nafasi nje ya utumishi wa umma. Niiombe Serikali kwamba treatment za makundi mawili haya zisiwe sawasawa. Kwa vyovyote vile mtumishi wa umma anapoteuliwa kwenye nafasi ya utumishi maana yake ametoka kwenye ajira anakwenda kule kwa mkataba utumishi wake huku haujakoma na sheria ndiyo inaelekeza hivyo tofauti na yule ambayo ameteuliwa nje ya utumishi wa umma ambaye anakwenda kwenye mkataba, ukiisha mkataba wake inakuwa basi atarudi kwenye shughuli ambayo alikuwa akiifanya awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtumishi wa umma anapoteuliwa baadaye mkataba wake wa uteuzi au mamlaka ya uteuzi ikasema kwamba sasa inatosha halafu anaachwa arudishwi kwenye majukumu yake hili lazima tulizungumze kwa masikitiko; kwasababu limetokea, watumishi wameathirika sana kisaikolojia na familia zimeathirika. Hata hivyo, nilishukuru sana, dada yangu Jenista alivyoingia tu katika Wizara hii jambo la kwanza kushughulikia ni kurudisha watumishi wote ambao walikuwa na sifa za kurudi kazini; ahsante sana Mheshimiwa Jenista. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika dhana hiyo hiyo ya kufanya data cleaning, niiombe Ofisi ya Rais, Menejiment ya Utumishi wa Umma, ifanye data cleaning kwa kuhakikisha kwamba watumishi waliobakibaki wale waliokuwa Ma-DAS, Wakurugenzi wa Halmashauri na Wakuu wa Wilaya lakini walitoka kwenye utumishi wa umma, mamlaka ya uteuzi ikasema sasa inatosha wapo wachache wamebaki Wizara izingatie ifanye data cleaning kuhakikisha wale waliobaki wanarudi katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la watumishi walioteuliwa utakapokoma muda wao wa uteuzi kushushwa; hili limezungumzwa na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba Dkt. katika hotuba yake ya bajeti. Niikumbushe Serikali, kwamba utumishi wa umma unazingatia haya yafuatayo; Sera ya Menejiment na Ajira ya Mwaka 1999, Sheria ya Utumishi wa Umma ya Mwaka 2002 na mabadiliko yake, Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003, Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma za Mwaka 2009, Kanuni za Utendaji Bora, Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini na miongozo mbalimbali inayoongoza utumishi wa umma. Kama hivyo ndivyo Serikali tunakwama wapi? Sheria hizi, miongozo hii tuliitengeneza wenyewe, tulitunga wenyewe, kwanini hatuzingatii hizi taratibu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtumishi anapoteuliwa kwenye nafasi ya uteuzi aidha alikuwa afisa daraja la kwanza, afisa mwandamizi, au afisa mkuu, anapopata barua yake ya uteuzi inasema kwamba yahusu kuteuliwa na kupandishwa cheo kuwa... Sasa unapomteua na kumpandisha cheo maana yake ni kwamba unamtoa katika daraja lile na kwa maana hiyo maslahi anayopata ikiwa ni pamoja na mshahara ni kwa sababu ulimteua na kumpandisha cheo. Utumishi au uteuzi wake unapokoma nafasi yake ya kupandishwa cheo ndiyo inayomfanya abaki na mshahara huo wa nafasi aliyoteuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, kwa dhati kabisa ninapendekeza kwamba watumishi hawa wanaoteuliwa pindi wanapotenguliwa wasishushwe mishahara yao kwa sababu wamepandishwa cheo; na kupandishwa cheo ndugu zangu siyo adhabu, kupandishwa cheo ni tija na ni faraja na niheshima inakuwaje mtu anayepandishwa cheo baadaye unamvunjia ile heshima? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri sana Serikali eneo hili mpango wake wa kuwashusha mishahara watumishi waliotumbuliwa isiendelee nao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji