Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nachukua nafasi hii kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu Utamaduni na Michezo kwa taarifa nzuri ambayo amewasilisha mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia nampongeza Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wote kwa namna ambavyo wanaiongoza Wizara katika kufikia malengo yake na kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla nasema kwamba Wizara tumepokea maelekezo na michango ya Waheshimiwa Wabunge ambayo tunaahidi tutakwenda kuifanyia kazi katika kuboresha sekta za utamaduni, sanaa na michezo ili ziweze kufanya vizuri zaidi kuliko ambavyo iko sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niruhusu kutoa ufafanuzi kwenye baadhi ya maeneo pamoja na michango yangu. Eneo la kwanza ni kuhusu ukarabati wa uwanja wa Benjemin William Mkapa. Uwanja huu ndiyo uwanja pekee ambao unatambulika na Shirikisho la Soka Barani Afrika kwa sasa katika nchi zote za CECAFA. Ndiyo maana tumepata nchi nyingi na vilabu vingi nje ya Tanzania kuomba kuja kutumia uwanja huu, vikiwemo vilabu vyetu pendwa vya Simba na Yanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanatumia uwanja wakati ukarabati unaendelea hivyo mkandarasi analazimika kusimama kipindi fulani ili kuruhusu mechi ziweze kucheza. Kama pale ambapo tumekuwa na African Football League, tumekuwa na mechi za Simba na Yanga za kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumekuwa na nchi ya Burundi na Gambia wakitumia uwanja huo, hiyo inasababisha ucheleweshaji kidogo. Pia, wakati muda wa mkandarasi umekwenda kwa asilimia 40, kazi aliyofanya imekwenda kwa asilimia 24, hii inatokana na sababu hizo ambazo nimezisema. Pia, fedha ya awamu ya pili ambayo Wizara ya Fedha imeitoa kwa wakati ndiyo imefika kwa mkandarasi. Akiitumia fedha hii yote atafika sambamba na muda na fedha ambayo imetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya mkutano na mkandarasi pamoja na consultant ambaye ni TBA na Kamati ilivyotembelea niliwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba TBA anafanya kazi nzuri sana kusimamia mradi ule. Ahadi ya mkandarasi ambayo na mimi naomba kuitoa katika Bunge lako hili tukufu ni kwamba atamaliza ukarabati kwa wakati. Sisi kama Wizara, kama Serikali, tunatarajia Tarehe 24 Agosti, 2024 mkandarasi atukabidhi uwanja uliokarabatiwa. Endapo atachelewa tutam-charge liquidated damages ili aweze kuwajibika kwa uzembe wowote ambaoo atakuwa ameufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ni AFCON 2027 ambapo sisi Tanzania, Kenya na Uganda tutakuwa wenyeji. Sisi nchi hizi tatu tumeipa jina AFCON hii inaitwa Pamoja AFCON. Kwa sababu ni kwa mara ya kwanza katika historia ya Bara la Afrika, nchi zaidi ya moja zinaandaa mashindano kama haya, kwa hiyo tunaita Pamoja AFCON.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya Pamoja AFCON mwaka huu Septemba nchi hizi tatu zitakuwa wenyeji wa pamoja wa mashindano ya CHAN. CHAN ni AFCON ya wachezaji wa ndani, inatumika kama rehearsal kabla ya kwenda kwenye AFCON kubwa. Kwa hiyo, tayari tunaendelea na maandalizi hayo, sisi Tanzania tutakuwa na vituo viwili, Dar es Salaam na Zanzibar, Kenya vituo viwili na Uganda pia watakuwa na vituo viwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongelea AFCON ya 2027. Kwa upande wa Tanzania tutakuwa na viwanja vitatu. Kiwanja cha kwanza ni cha Benjamin William Mkapa ambacho kama ambavyo nimesema kitakuwa tayari Agosti mwaka huu. Kiwanja cha pili ni kiwanja cha Amani pale Jijini Unguja Zanzibar na tunaona kabisa Disemba mwaka jana uwanja ule ulizinduliwa rasmi kwa maana uko tayari. Uwanja wa tatu ni uwanja wa Arusha ambao tayari tunategemea ndani ya mwezi huu wa pili mkandarasi atakabidhiwa site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeyasema haya ili kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge na kuwatoa hofu Watanzania wote kwamba maandalizi ya AFCON 2027 yanakwenda vizuri. Tayari viwanja viwili vipo na cha tatu kwa maelekezo na ahadi ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan tutaumaliza kwa wakati na sisi tutakuwa wenyeji hatuwezi kukubali kupoteza heshima hii ambayo Bara la Afrika limetupatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo nachukua nafasi hii kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kwamba maandalizi ya AFCON yanakwenda vizuri tutakwenda kwa wakati. Kwenye hili nampongeza sana Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri wa Fedha, yuko kwenye hatua za mwisho kuhakikisha kwamba program ya EPC+F inakamilika na ndani ya mwezi huu wa Februari uwanja wa kisasa kabisa utajengwa katika Jiji la Arusha. Uwanja huu tayari sisi tumeshaupa jina, unaitwa Uwanja wa Samia Suluhu Hassan. Utakuwa uwanja mzuri zaidi katika ukanda wetu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeongelewa Uwanja wa Dodoma; Uwanja wa Dodoma siyo sehemu ya maandalizi ya AFCON. Uwanja wa Dodoma ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi hususan katika Ibara ya 243 capitals (A). Chama cha Mapinduzi kiliahidi kitajenga uwanja wa kisasa jijini Dodoma sasa huu ndiyo utekelezaji wa hayo. Tunasema kwamba uwanja huu utakwenda sambamba na ule wa Dodoma ili tuweze kukaa vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwa mwenyeji si tu kuwa na uwanja bali ni pamoja na kuwa na timu nzuri. Tunajipanga, kama mmeona timu yetu ambayo imekwenda AFCON sasa hivi ilikuwa na wachezaji takriban saba ambao wana umri wa miaka chini ya 22. Wengi hawakucheza walikuwa wamekaa benchi lakini pale benchi ni darasa la wao kujifunza. Mwaka huu wamekaa benchi AFCON, AFCON ya mwakani 2025 tunataka tupambane ili wacheze angalau nusu. Ikifika 2027 hawa under 23 ndiyo watakuwa wachezaji ambao watatuvusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nasisitiza, ukiangalia tulikuwa na wachezaji 27 waliokwenda AFCON, 13 wanatoka kwenye vilabu vya ndani, 14 wanatoka kwenye vilabu vya nje. Napenda kuongelea hivi vilabu vya ndani, ni vilabu vitano ambavyo vyote ama vinashiriki au vimeshiriki mashindano ya Afrika. Hivyo, ushiriki wa vilabu vyetu katika mashindano ya Afrika unawakomaza wachezaji wetu kuweza kufanya vizuri zaidi kwenye Timu ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri hapa, timu yetu ya Taifa imesifiwa sana kwamba ilikuwa na ukuta mzuri ndiyo maana tumeweza kutoa suluhu zile mechi mbili. Ukuta ule mzuri tunaongelea wachezaji wawili pale katikati kwenye central defense, Mwamnyeto na Baka. Hao ni wachezaji ambao wanachezea Dar es Salaam Young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Yanga walifika fainali mwaka jana, na safari hii wanacheza Champions League. Uzoefu ambao kina Baka na Mwamnyeto wameupata wakiwa Yanga ndio unatusaidia sasa. Hivyo, tunaendelea kuimarisha ushiriki wa vilabu vyetu katika mashindano ya Afrika ili tukichanganya na wachezaji wale wa nje tuweze kupata timu nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imesemwa hapa kwamba Uwanja wa Taifa wa Benjamin Mkapa unatumika sana, hata sisi tumeliona. Tunakarabati Uwanja wa Uhuru, tayari tumeshampata mkandarasi na tayari tunafanya vizuri katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kwamba sekta hizi tatu, Utamaduni, Sanaa na Michezo zinaendelea kufanya vizuri na sisi wasaidizi wake tutaendelea kumsaidia hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema moja la mwisho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa muda umekwenda.

WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ametuagiza sisi wasaidizi wake kwamba tuchukulie hizi sekta tatu za utamaduni, sanaa na michezo kama ajira na uchumi. Sisi tumepokea falsafa hiyo, tunaifanyia kazi; na ndiyo maana sekta hizi zinaongoza kwa ukuaji kwa asilimia 19. Tunachotaka kukifanya sasa asilimia hizo asilimia 19 tuweze kuzitafsiri katika uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naunga mkono Taarifa ya Kamati. (Makofi)