Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze leo kuzungumzia hoja hii. Kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha siku ya leo kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu na mimi kuchangia kwenye hoja hizi za Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati zote zilizowasilisha leo hapa, kwa kweli wamewasilisha vizuri sana hongereni sana Wenyeviti wetu lakini pia napenda nipongeze Makamu Wenyeviti wote na Wajumbe wote wa Kamati kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya katika kuwasilisha maoni na mapendekezo yetu katika Kamati hizi husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu kwanza utajikita katika maeneo mawili au matatu iwapo nitapata muda. Kwanza nitaanza katika Wizara ya Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu halafu nitakwenda kwenye Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na kama muda utakuwepo nitakwenda kwenye Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze kwanza Mheshimiwa Rais wetu. Mheshimiwa Rais wetu alitoa kauli kwamba miradi yote iliyoanza itakamilika. Mimi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia miradi ambayo ilikuwa inafanyika katika taasisi zilizopo kwenye Wizara ya Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu. Kupitia kwenye mifuko yetu ya NSSF kulikuwa na miradi mingi ambayo ilianzishwa ikiwemo mradi wa kiwanda cha sukari cha Mkulazi II. Kiwanda kile kwa kweli tulikuwa hatudhani kwamba kiwanda kile kinaweza kukamilika lakini mimi kama Mjumbe wa Kamati na wenzangu wa Kamati tumeshuhudia kwamba kiwanda cha Mkulazi II kimeanza kazi rasmi na kinafanya kazi pamoja na changamoto zingine tu za kimazingira. Hilo ni jambo kubwa kupata kiwanda chetu sisi kama Watanzania kinachomilikuwa na Serikali ubia baina ya NSSF na Magereza siyo jambo dogo ni jambo kubwa nani jambo la kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kutoa fedha kuhakikisha mradi huo unakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi kwenye miradi ya ujenzi wa majengo ya NSSF kule Dar es Salaam majengo ya Mzizima lakini hata mradi mkubwa ule wa Dege ambao ulikuwa ni mtihani katika miaka kadhaa sasa una mwelekeo mzuri. Mradi ule unaelekea kwenye kuuzwa na una majadiliano yanaendelea na Insha’Allah tuna imani mradi ule sasa utakwenda kuuzwa na ile hoja ambayo ilikuwa inatesa miaka yote ya mradi wa Dege sasa tunakwenda kuimaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee napenda niipongeze Mifuko yetu yote ya Serikali PSSSF, WCF, OSHA, NSSF na mifuko hiyo mingine yote kwa kufanya kazi nzuri. Kwa kweli matokeo tumeyaona kazi inaendelea. NSSF tunawaona wakiendelea katika miradi yao lakini PSSSF tunawaona jinsi gani sasa wastaafu wanavyopata taarifa zao kwa haraka na pensheni zao zinakuja kwa haraka kupitia mitandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukikaa wewe kama mstaafu unakuja kushtuliwa na meseji unaambiwa tayari kitu kimeingia huku, siyo jambo dogo. Tukiangalia tulipotoka watu mpaka wakafuatilie huko lakini leo unaambiwa umeingiziwa kiasi gani kwa ajili ya pensheni yako ni jambo kubwa, ni jambo la kupongeza sana sana sana lakini mfuko wetu wa WCF unatoa elimu ya fidia kwa wafanyakazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wafanyakazi wengi walikuwa hawaelewi hata nini wanapopata ajali kazini wafanye. Sasa hivi kutokana na elimu ambayo wanaitoa tunaona kwamba jamii inaanza kuelewa. Tunachoomba kwa mfuko huu bado elimu iendelee katika maeneo mbalimbali ya kazi. Wapo Watanzania ambao wanafanya kazi kwenye maeneo hatarishi sana, ni vyema mfuko huu ukaenda kutoa elimu katika maeneo ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto zao za ukosefu wa watumishi lakini wajipange vizuri kuhakikisha wanaenda kwenye viwanda na maeneo mbalimbali ya taasisi mbalimbali kwenda kuwaeleza wananchi wa Tanzania haki yao kwamba pale wanapopatwa na matatizo wakimbilie wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mfuko wa OSHA. OSHA watu walikuwa hawaielewi zamani na walikuwa wanaielewa kwa upande wa pili kama kitu fulani korofi hivi lakini sasa hivi Watanzania wameanza kuelewa umuhimu wa OSHA. Tunaona mazingira rafiki katika maeneo ya kazi yanazingatiwa, hii yote ni kutokana na juhudi ambayo wanaifanya wao, kutoa elimu, kuwatembelea, kwenda kwenye maeneo mbalimbali kwa kweli mimi niipongeze sana Taasisi hii inapiga kazi niwaombe waendelee kufanya hivyo na kutoa elimu kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye mfuko wa NSSF. Pamoja na mambo yote mazuri ambayo nimewasifia na kuona kwamba wana miradi lakini pia kwenye mazuri hapaokosi changamoto. Ipo changamoto kubwa ya madeni, Serikali NSSF wanaida Serikali takribani trilioni 13, katika kuchangia miradi mbalimbali lakini pia kwenye madeni yale ambayo ni ya watumishi wa Serikali kuletwa kwenye mfuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, PSSSF nao vile vile wana madeni mengi ikiwepo takribani bilioni 787 ambazo zipo katika mashirika mablimbali. Mimi niombe madeni haya yalipwe yaongezee ule mfuko, pamoja kwamba madeni hayo ni mashirika ambayo ya Serikali lakini haya mashirika PSSSF na NSSF vitabu vyao vinakuwa havikai vizuri. Tutawasifu, watafanya kazi nzuri lakini kama vitabu vyao vya kimahesabu havijakaa vizuri kazi yao nzuri inakuwa kama ni bure, kumbe kazi hiyo hawajasababisha wao matatizo hayo yamesababishwa na Taasisi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote ni wa aina moja tuangalie jinsi gani wa kuondoa haya madeni. Madeni megine ni ya Serikali, kama ni ya Serikali na madeni yale yamekuwa chechefu sasa hayalipiki basi ni bora wakafutiwa madeni hayo na wao waendelee kuendelea na miradi yao mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye mfuko wa CMA. Hii CMA ni mamlaka ya usuluhishi lakini wana changamoto kubwa sana wa kokosa kusimika mfumo wa kieletroniki. Hii inaendesha kazi yake sambamba na Kimahakama, tunaona jinsi Mahakama sasa zilivyoboreshwa yanaendesha mambo yake yote kupitia mfumo wa electronic. Sasa tuombe Serikali iwape fungu wao wahimize huu mfumo uendelee ili na wao waweze kufanya maamuzi ya yale mashitaka kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja sasa kwenye TAESA. TAESA hii ni Taasisi ambayo inashughulika na kutoa na kusimamia vijana na ajira. TAESA walikuwa ni taasisi ambayo inajitegemea Serikali wakaitoa wakaipeleka Wizarani wakaiweka kwenye benchi ni basic katika Wizara hiyo ya Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu sasa hawa watu hawana bajeti, wanategemea bajeti ya Wizara kupewa fungu. Lakini tunaona crisis ya vijana Tanzania ukosefu wa ajira ile ajenda ya vijhana ni ajenda ya dunia, duniani kote kuna tatizo la vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii taasisi ilikuwa inawa-train vijana wetu, inawatafutia ajira maeneo mbalimbali tofauti tofauti lakini wanashindwa kuendesha kwa sababu wao kama wao siyo Muhimili unaojitegemea wanaitegemea Wizara na Wizara hii ina bajeti ndogo kwa hivyo wanashindwa kufanya kazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii TAESA tumeshawaona wengine vijana mbalimbali wanapata ajira zile za intern, watoto wa vyuo wanavyotoka chuoni. Wanapata ajira zile za muda zile mwaka mmoja, miaka miwili lakini hata wengine wanabahatika wanatafutiwa hata ajira za kudumu ni taasisi ambayo inafanya kazi yake vizuri sana. Niombe Serikali wahakikishe kwamba wanatenga fungu kwa ajili ya TAESA. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mariam ahsante sana.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kidogo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa maliza sekunde 30.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake wa Makundi Maalum, nayo vilevile kwa ujenzi na ukarabati wa maeneo mbalimbali ya watoto, makazi ya wazee jambo hilo limefanyika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kuhakikisha anaboresha maeneo yote ya makazi ya wazee. Makazi hayo yakikuwa chakavu, hayafai lakini pia ujenzi wa Vyuo vya walemavu ni jambo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake wa Makundi Maalum haina fungu. Fungu lake ni dogo sana waongezewe bajeti ili waweze kuendeleza program zao ikiwemo zile za watoto na kupinga ukatili wa kijinsia. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)