Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nami nianze kwa kuunga mkono hoja iliyoletwa na Kamati yetu na pia hoja zote mbili kwa maana iliyoletwa na Kamati ya USEMI na ile ya Utawala na Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli yamezungumzwa mengi sana nami binafsi yangu nataka kuchangia katika baadhi ya maeneo. Serikali ilikuwa inaongeza Bajeti mara kwa mara, na katika maeneo mengi sana tunashuhudia mabadiliko makubwa sana ya kimaendeleo hasa katika maeneo yanayohusu huduma za wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya hivyo, pia yako maeneo ambayo kwa kweli tunaweza kusema kwa namna moja au nyingine ongezeko hili la bajeti limeleta mchango ambao uko chanya kabisa kwa maana ya kusaidia wananchi wetu kama ambavyo imeelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, pia nataka niishukuru Kamati kwa kuweza kuangalia mambo ya msingi kabisa ambayo sisi kama Wizara kwa upande wetu yanatupatia nafasi ya kwenda kuboresha zaidi majukumu yetu, na kwa namna moja au nyingine kuendelea kuyafanyia kazi yale ambayo yanaonekana kuwa ni upungufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu mimi nataka niseme tu kwa niaba ya Serikali naunga mkono sana mawazo yote mazuri yalitolewa na watu wote waliochangia, lakini na mimi nataka niongezee kidogo katika maeneo hayo, kwa mfano katika hili eneo ambalo Kamati imeeleza kwamba walemavu ni kama wamesahaulika

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu nilihakikishie Bunge lako, lakini pia kuwaambia umma wa Watanzania pamoja na Bunge lako kwamba, Serikali imeendelea kuwaangalia watu wenye mahitaji maalum katika maana ya ajira, lakini pia katika kuzingatia wanapewa kipaumbele kikubwa, hasa nafikiri katika upendeleo hasa katika eneo hili la utoaji wa ajira. Kupitia Gazeti la Serikali lenye kumbukumbu namba 326 ambalo lilieleza juu ya mabadiliko ya Kanuni ya 17 ya usaili wa katika eneo la watu wenye ulemavu ni kwa kweli, upendeleo mkubwa sana umefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikiri mbele ya Bunge lako kwamba, bado changamoto zipo katika baadhi ya maeneo, lakini kiukweli katika kipindi cha miaka mitatu zaidi ya watu wenye ulemavu 190 wameajiriwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo wanaume 108 na wanawake 82, wote wakiwa ni sehemu ya wafaidikaji. Lakini pamoja na hilo pia, nataka niunge mkono juu ya hoja iliyoelezwa na kamati yetu kuhusiana na malimbikizo ya madeni ya watumishi. Kwa kweli, kibinadamu haipendezi, inauma na ni wajibu wetu kama Serikali, ni wajibu wetu kama Bunge kuendelea kuwasemea watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nipongeze juhudi mbalimbali ambazo zimeendelea kufanywa na Serikali yetu, hasa baada ya kutambulisha mfumo wa mishahara na taarifa za kitumishi ambao kwa lugha ya kitaalamu unaitwa HCMIS ambao mfumo huu umesaidia sana kupunguza madeni, lakini pia na malimbikizo mbalimbali ambayo watumishi wetu walikuwa wanadai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, hadi kufikia Disemba, 2023 Serikali imefanikiwa kulipa bilioni 210.67 ikiwa ni sehemu ya madai makubwa ya watumishi zaidi ya 125,147 ambao wamekuwa wanaidai Serikali. nataka nikuhakikishie katika fedha hizo ambazo zimelipwa, ndani ya makundi hayo, Serikali imelipa bilioni 157 kwa watumishi ambao walikuwa wanadai katika malimbikizo ya upandishwaji wa vyeo na kubadilishwa muundo wao wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mengi mazuri yamefanyika katika Serikali na ninataka Bunge lako niendelee kulishawishi kuamini kwamba, Serikali bado inaendelea kufanya mambo mazuri na hayo yanaweza kutafsirika katika eneo kama la bajeti ilivyoongezeka, hasa katika Ofisi yetu ya Rais, Utumishi ambapo asilimia 17 bajeti imeongezeka ambayo tafsiri yake imetafsiriwa katika eneo la kazi na ikiwemo mojawapo kwenye uundaji wa miundo au mifumo ya kiserikali, kuwezesha utoaji huduma nzuri kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hilo tu pia nataka niongee katika eneo moja ambalo limechangiwa na Wabunge wengi, hasa wakiongozwa na Mheshimiwa Janejelly Ntate ambaye alizungumzia hasa juu ya maslahi ya watumishi, hasa wanawake ambao wakipata likizo zao wamekuwa wanapunjwa, lakini wakati mwingine wanapata matatizo makubwa wanapoomba likizo hasa baada ya wenzetu kujifungua watoto njiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilieleza asubuhi juu ya utayari wa Serikali kukutana na wadau katika mabadiliko makubwa tunayokuja kuyafanya kwenye sheria zetu za utumishi, kuweza kuingiza kundi hili maalum ambalo linakwenda kutatua vilio vya walio wengi, akinamama zetu. Tunaamini katika nchi hii ambayo tuliamua kumpa Rais wa kwanza mwanamke, Dkt. Samia Suluhu Hassan awe kiongozi wetu kwa kuleta maendeleo, hatuwezi kuwaacha nyuma hawa ambao wanazaa watoto njiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuona unavyoshika kengele yako, maana yake muda wangu umetosha. Hoja nyingine zote kama zilivyotolewa na Kamati tunachukua, tutakwenda kuzifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)