Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia taarifa za Kamati zetu hizi mbili, Kamati ya TAMISEMI pamoja na Kamati ya Utawala Katiba na Sheria. Niende moja kwa moja kwenye kuchangia kwa sababu muda wetu ni mdogo, nitachangia mambo mawili, kwanza ni Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na la pili nitachangia linalogusa pia TAMISEMI juu ya kugawa maeneo ya utawala wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuifanya sasa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ifanye kazi pande zote za Muungano (Tanzania Bara na Zanzibar), kwa mujibu wa marekebisho ya Sheria yake Namba 8 ya Mwaka 2006 inaifanya sasa Tume hii iweze kufanya kazi maeneo yote mawili ya Muungano au ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume hii ya Haki za Binadamu iko Kikatiba na kwenye Katiba ukurasa wa 108 na 109 majukumu ya Tume hii yametajwa yako mengi na mimi niyataje machache. Moja, ni kufanya shughuli za kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu. Jingine ni kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora. Jingine ni kama ikibidi kufungua mashauri Mahakamani ili kuzuia vitendo vya uvunjaji wa haki za binadamu na jingine ni kuchunguza mienedo ya mtu yeyote anaehusika au taasisi yeyote inayohusika na masharti ya Ibara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu haya ukiyaangalia ni majukumu makubwa, majukumu mazito na ni majukumu yenye upana wake. Ukiangalia nchi yetu kwa kuiangalia Tanzania Bara na Zanzibar nayo ni kubwa sana. Sasa kwa majukumu haya ambayo Tume hii imepewa napata shida kuona utendaji kazi wao kama unaridhisha ili wananchi waweze kufikiwa na Tume hii ya Haki za Binadamu. Kusema ukweli ufikiaji au utendaji kazi wa Tume hii hauwapati wanachi wetu kwa ujumla wake. Moja, ni kwa sababu Tume hii ina Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti na Makamishna na Wasaidizi wa Makamishna halafu wako Dodoma Makao Makuu ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watumishi kwanza ni wachache lakini pia hawapo kwenye Mikoa na Wilaya zetu. Sasa kama wako Dodoma haya malalamiko yaliyosemwa kwenye majukumu yao wanayapata kwa njia ipi. Kama wanayapata wanawezaje kuwafikia hao wanaolalamika kuzingatia uchache walionao na vifaa wanavyovitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa kweli nataka kuishauri Serikali kwamba kama tumekubali kuwa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala bora basi Tume hii iwezeshwe kwa namna ya watumishi tuwe na watumishi mpaka kwenye Mikoa au Wilaya ili wananchi wetu wanapopatwa na madhila yanayohusiana na kuvunja kwa haki za binadamu wawe na mahali ambapo wanaweza kupeleka pa karibu zaidi, kuliko mwananchi kutokea Wilayani kwangu kule Maswa alete hoja yake hapa Dodoma, sasa nashindwa kuelewa itatatuliwa saa ngapi, malalamiko hayo yatatuliwa saa ngapi, shida hizo zitatatuliwa saa ngapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani assumption iliyokuwepo tulipokuwa tunaweka Tume hii ni kwamba Tume hii labda inahusika na viongozi tu lakini kuvunjwa kwa haki za binadamu hakufanywi na viongozi peke yao hata raia wanavunja haki za binadamu. Pia mambo mengine yanatokea kule kwenye maeneo yetu ambako hakuwezi kuonekana kwa urahisi. Kama Tume hii ingejulikana ipo na inafanya kazi kushughulikia matatizo haya, malalamiko hasa ya uvunjaji wa haki za binadamu, Tume hii ingeweza kupunguza sana kitu ambacho mwenzangu aliyenitangulia amesema malalamiko ya wananchi ambayo viongozi wetu wanakutana nayo wanapokuwa wanafanya mikutano yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kwamba Tume hii kwanza iongezewe watumishi, Watumishi wake wasifanye kazi kutokea Dodoma peke yake waende Mikoani na Wilayani, pia waongezewe rasilimali fedha. Rasilimali fedha kama haijaongezwa hawawezi kufika huko kwenye maeneo yetu. Jambo la tatu miundombinu kama majengo na vifaa vya TEHAMA viweze kupatikana kwa Tume hii ili waweze kufanya kazi yao vizuri na kuwahudumia wananchi wetu vinginevyo kwa rasilimali chache na kwa uchache wa watumishi waliopo hii Tume itabakia kwenye Katiba na itabakia kwenye maandishi yetu lakini utendaji kazi wao hatuwezi kuuona kama wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende suala la pili la kugawa maeneo ya utawala wa nchi yetu. Naelewa kwa sababu suala hili limekuwa likizungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge kwa njia ya maswali ya nyongeza na Serikali imekuwa ikijibu hapa kwamba pengine upatikanaji wa fedha utakapokuwepo suala linaweza likatazamwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ni kubwa. Nchi yetu sisi ni kubwa kiasi kwamba unaweza ukajumlisha nchi nne za Afrika Mashariki Uganda, Kenya, Rwanda na Burundi, bado hujapata eneo la ukubwa wa nchi yetu. Sasa nchi yetu kwa sababu ni kubwa mimi sihesabu kama ni balaa kwa nchi yetu kuwa kubwa, tuhesabu kama ni fursa! Siyo kosa kosa nchi yetu kuwa kubwa. Inavyoelekea ni kwamba tunaona sasa kama ni tatizo, mimi sioni kama ni tatizo, ni fursa na tukijielekeza vizuri bado tunaweza kufanya nchi yetu ikatawalika vizuri na suala la utawala bora na lenyewe likaenda sawa sawa lakini kwa kugawa maeneo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kugawa maeneo ya nchi yetu, wilaya kubwa kama Kilosa ambayo ni zaidi ya Mkoa wa Kilimanjaro, wilaya kubwa kama ya Maswa yenye square kilometers zaidi ya 3,000, ni kubwa; sasa maeneo kama haya kuyahudumia kwa watu walioko kule ni shida sana. Ni tabu sana kwa Mkuu wangu wa Wilaya, Mkurugenzi na watumishi wengine waliopelekwa na Serikali kule kuhudumia eneo kubwa lililo pana namna hii, haya maeneo yagawiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunashindwa kuyagawa, basi kwa neno lile la Tawala za Mkoa, kwa kuwa na mkoa au kuwa na wilaya ili tuwe na DC, basi tugawe kwa upande huu wa pili, Serikali za Mitaa. Tugawe ziwe halmashauri mbili na maeneo ya vijiji yale makubwa ambayo yanafanana na kata na yenyewe yagawiwe angalau tuwe na halmashauri mbili kwenye eneo la halmashauri moja ambayo ni kubwa na vijiji au kata. Kwa sababu utakuta kata nyingine ni sawa na tarafa kabisa, lakini imeachwa kuwa kata moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tugawe halmashauri, tugawe kata na vijiji. Haya maeneo yakigawiwa, ndiyo maeneo muhimu kwa wananchi wetu kufikishiwa huduma kule kwa ukaribu sana. Tunaweza kufikiria kugawa kuwa na Mkuu wa Mkoa na kuwa na Mkuu wa Wilaya baadaye lakini kuwa na Mkurugenzi na kuwa na Mtendaji wa Kata, kuwa na Mtendaji wa Kijiji ni suala ambalo tunaweza kulifikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza kufanya hata kwa awamu kuliko tukiacha maeneo kama yalivyo. Maeneo mengine hayafikiwi kabisa na huduma za Umma, hayafikiwi kabisa na watumishi wa Serikali kwa sababu ya ukubwa wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine tumekuwa tukilalamika hapa kwamba rasilimali fedha zinazoenda kule labda hazisimamiwi vizuri, lakini tatizo mojawapo ni ukubwa wa haya maeneo. Tunapeleka miradi mingi. Kwa mfano, mradi uliopelekwa kijiji changu kimoja kinaitwa Mwandu, kilomita 120 kutoka Makao Makuu ya Wilaya, sasa huyu DC na Mkurugenzi, Afisa Elimu, Afisa Kilimo atafika saa ngapi kule na kusimamia kazi ya mradi au pesa zilizopelekwa kule ukizingatia pia vifaa kama magari na pikipiki na vyenyewe bado ni pungufu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya maeneo tukiyagawa itakuwa ni karibu kuyahudumia, mtu anaweza kwenda hata kwa pikipiki bila matatizo yoyote. Mtu anaweza akaenda hata kwa pick-up bila shida yoyote, mgongo usimuume kwa sababu mwendo atakaoenda ni mfupi. Kama maeneo yatabaki makubwa namna hii, bado watumishi wataendelea kupata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzuri wa kuyagawa haya maeneo, itarahisisha usimamizi wa shughuli na miradi ya Serikali.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mashimba Ndaki, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Jumanne Sagini.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa fikra alizonazo Mheshimiwa Ndaki ya kupendekeza kuyagawa haya maeneo zaidi, lakini naomba kumpa taarifa zaidi kwamba mpaka mwaka 2012 Mkoa wa Shinyanga ulikuwa unaibeba Mkoa karibu wote wa Simiyu. Serikali kwa kutambua hayo, iliweza kuugawa Mkoa wa Shinyanga na baadhi ya Wilaya za Shinyanga zilizokuwa tatu zikagawanyika tukapata halmashauri sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri atambue kwamba juhudi zimekuwa zikifanyika, lakini haitakuwa na tija sana iwapo utagawa bado ukashindwa kuweka miundombinu stahiki kuiwezesha Serikali kutimiza wajibu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa hiyo taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante; Mheshimiwa Ndaki taarifa hiyo unaipokea?

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa sehemu; natambua Mkoa wangu wa Simiyu ulimegwa kutoka Mkoa wa Shinyanga mwaka 2012, lakini hiyo haizuii kugawa wilaya kubwa kuwa halmashauri mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na wilaya kubwa kama ya Maswa, anaifahamu Mheshimiwa Sagini, kubwa, lakini ni halmashauri moja. Huyu Mkurugenzi atatoka damu kifuani kufuatilia miradi kwenye kata zake 36 na vijiji karibu 140 kwenye wilaya hiyo. Tutampa shida bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba hapa ni kwamba, sawa Serikali imefanya juhudi kubwa, lakini bado tunahitaji kuyagawa haya maeneo hata kama ni kwa awamu. Mwaka huu basi halmashauri hizi kubwa tuzigawe ziwe halmashauri mbili. Halmashauri tano kubwa tuzigawe, halmashauri tano nyingine mwaka unaofuata tuzigawe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)