Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ABDUL-HAFAR IDRASSA JUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na kuwa mchangiaji wa mwanzo katika hoja hizi zilizokuwa mezani.

Mheshimiwa Spika, ningeomba nijielekeze sana katika hoja iliyowasilishwa na Kamati ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali za Mitaa, kwa sababu ni sehemu ya Wajumbe wa Kamati hiyo.

Mheshimiwa Spika, Fedha za Maendeleo kwa kiwango kikubwa Serikali Kuu imekuwa ikitimiza wajibu wake. Hakuna halmashauri ambayo haijapelekewa kabisa Fedha za Maendeleo, lakini nini kilichopo katika halmashauri zetu kikubwa? Ni usimamizi usioridhisha wa Fedha za Maendeleo wa Wakurugenzi na wasaidizi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Samahani kidogo Mheshimiwa Mbunge.

Waheshimiwa Wabunge tunaposimama tutazame mchangiaji yuko wapi. Usimkate mchangiaji kwa sababu anapozungumza, anazungumza na mimi. Tuzingatie sana hilo ni la muhimu kwa sababu pia haitaleta picha nzuri kukwambia rudi kwenye kiti chako.

Mheshimiwa Juma.

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa hiyo, fedha za maendeleo Serikali Kuu inapeleka, lakini usimamizi wa halmashauri zetu katika fedha za maendeleo hauridhishi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo wanaopelekewa takribani milioni 500 mfano. Halmashauri zote zikapelekewa milioni 500 zikafanye jambo fulani, labda kujenga kituo cha afya ama kiwango fulani cha fedha kwa ajili ya kujenga skuli mpya, lakini nini kinachotokea? Wapo wanaokamilisha, wapo wasio kamilisha, wapo ambao hawafanyi kabisa, wako wengine mpaka leo wamejenga robo na fedha imekwisha.

Mheshimiwa Spika, sasa usimamizi wa fedha zinazopelekwa kwa maafisa wetu masuuli bado hauridhishi, lakini fedha kwa maendeleo zinazotengwa na wao wenyewe kutoka fedha zao za ndani hizo ndizo kabisa. Wapo wengine fedha wanazipata, sheria inawataka wapeleke asilimia 40, wanapeleka kiwango wanachotaka. Sasa nini maana ya sheria zilizotungwa na Bunge?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nadhani Halmashauri zetu Serikali iongeze umakini wa kuzisimamia ili ziweze kutimiza wajibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu asilimia 10. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuelekeza utaratibu mpya wa usimamizi wa fedha za asilimia 10 ya halmashauri. Lakini katika bajeti ya mwaka 2021/2022 ambayo taarifa yake ndio imewasilishwa hapa mbele bilioni tano haikupelekwa katika mfuko wa asilimia 10. Si kwamba ikatafutwe, fedha ilishakusanywa, lakini Wakurugenzi na maafisa masuuli wenzao waliamua tu kutokupeleka bilioni tano za vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inamaanisha kwamba, kwa kutokupeleka bilioni tano katika mwaka 2021/2022 vijana katika Taifa hili wamenyimwa shilingi bilioni mbili ya kujiendeleza kiuchumi; wanawake katika Taifa hili wamenyimwa shilingi bilioni mbili ya kujiendeleza kiuchumi, na watu wenye ulemavu wamenyimwa shilingi bilioni moja ambayo ilipatikana na sheria tumeitunga Bunge ilitaka wakapewe.

Mheshimiwa Spika, kama tungeamua kuwa na vikundi 50 tu nchi nzima, kila kimoja kikapewa shilingi milioni 100, fedha ambayo ilikuwa imeshapatikana, leo tungekuwa tumesaidia Watanzania wangapi? Lakini Wakurugenzi na maafisa wao masuuli hawakupeleka fedha hizi.

Mheshimiwa Spika, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali katika mwaka huohuo amebainisha takribani bilioni 88.4 zimekopeshwa hazijarejeshwa. Hivi ni wazimu wa aina gani ukampe mtu fedha halafu ushindwe kurejesha fedha yako ilhali ulimpa ya mkopo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ni nini ambacho kamati tuliona? Na mimi kama Mbunge ninashauri kwamba, japo Mheshimiwa Rais ameelekeza mfumo mpya wa utoaji wa utoaji wa fedha hizi ambao Serikali inaendelea kuufanyia kazi lakini zile ambazo zimeshatoka lazima zipatikane kwa sababu, amewapa watu. Vikundi hewa vilikuwepo, wametengeneza vikundi hewa, kikundi kimepewa fedha eti mtu aliandika namba yake ya simu, leo simu haipatikani, ulimpaje mtu fedha kwa namba ya simu? Inawezekana vipi kama maafisa masuuli hawapo katika sehemu ya mchezo huu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini ushauri wangu wa jumla ni kwamba; pamoja na Maazimio ya Kamati, kuna umuhimu sasa wa kufanyika tathmini ya jumla ya Halmashauri moja baada ya nyingine kupima uwezo wake wa kifedha, kupima uwezo wake wa kutoa huduma kwa wananchi na kupima umuhimu wa uwepo ama kutokuwepo kwake.

Mheshimiwa Spika, ingekuwa biashara Serikali Kuu katika fedha za matumizi ya kawaida kwa mwaka 2021/2022 Halmashauri ya Kigoma, fedha za matumizi ya kawaida, mshahara, OC na mambo mengine, kununua stationaries, wamepewa shilingi bilioni 16.3. Fedha walizikusanya wao ni milioni 700. Japo wamezidi bajeti yao kwa asilimia 3, lakini ingekuwa biashara ya kawaida hebu tutathmini jamani; unachukua bilioni 16 unakwenda kukusanya bilioni tatu?

Mheshimiwa Spika, sasa narudia tena ushauri wangu, tufanye tathmini. Muundo huu wa Serikali za Mitaa tulionao ulikuwepo tangu hakujawa na WhatsApp, tangu Mheshimiwa Nape hajasambaza minara katika maeneo mengi ya nchi hii. Sasa tufanye tathmini basi tuone Halmashauri tulizonazo tuna umuhimu wa kuendelea kuwanazo katika muundo huu? Tuzibadilishe kulingana na mahitaji ya sasa ama tuone namna gani vizuri zaidi vya kufanya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningetamani pia kuona Serikali inaboresha hatua za kinidhamu kwa watu ambao wanakuwa wamehusika kabla ya kupeleka katika hatua za kisheria. Wanaosababisha upotevu wa fedha, wakishafanya utafiti wao wanawapeleka TAKUKURU. Kule TAKUKURU mambo yanakwenda yanaenda Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda tu nikwambie; yupo Mkurugenzi ana kesi ya jinai kwa matendo aliyoyafanya kutoka katika halmashauri moja. Sasa hivi ni Mkurugenzi katika Halmashauri nyingine anatoka na gari la Serikali anakwenda kuhudhuria katika kesi yake ambayo ametenda makosa katika halmashauri fulani.

Mheshimiwa Spika, sasa utaratibu wa kinidhamu nadhani pia Serikali iuboreshe kwa Wakurugenzi wa Halmashauri, kwa wakuu wa idara na watumishi wengine kabla ya kufika katika utatuzi wa kisheria. Wapo Wakurugenzi wamebainika ndugu zao ndio walikuwa wana POS machine, wamekusanya fedha, fedha haijapelekwa, ndugu huyu hajulikani yuko wapi, Mkurugenzi yule kahamishwa, wanasema taratibu za kisheria zinaendelea, taratibu za kinidhamu ziko wapi?

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ni za Watanzania na ninaomba, pamoja na Maazimio ya Kamati, lakini Serikali ijiangalie katika uchukuaji wa hatua za kinidhamu kwa watu wanaohusika na ubadhirifu katika masuala ya halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia kabisa katika hoja yangu ileile ya ushauri mkuu wa kufanya tathmini. Wenyeviti wa Halmashauri ni Madiwani na sisi Wabunge kwa wale ambao sheria inawaruhusu ni Madiwani katika halmashauri zetu. Tumebaini, yapo maeneo Madiwani ambao wengine ni Wenyeviti wa Halmashauri kwa kushirikiana na watendaji wetu katika Halmashauri wanafanya makusudi kumharibia Mbunge aliyekuwa madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nini ushauri wangu katika tathmini hiyo. Ningetamani tathmini hiyo pia, iangalie je, hakuna uwezekano Mbunge wa jimbo akawa ndiye Mwenyekiti wa Halmashauri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali Kuu mwaka 2021/2022 imepeleka shilingi trilioni 5.9 katika Halmashauri, za maendeleo pamoja na masuala mengine ya matumizi, lakini Halmashauri zote zimekusanya bilioni 800. Kuna Mheshimiwa Diwani mmoja pale ambaye labda hamtaki na yeye anautaka Ubunge kwa sababu ndiye ameshika zile nafasi na labda kwa sababu mahusiano ya Mkurugenzi na Mbunge hayako vizuri, wanatumia nafasi hiyo kumuharibia.
Mheshimiwa Spika, sasa ile tathmini ikifanyika tuangalie nini kinachowezekana, kama mambo haya yalipitishwa muda mrefu, kama nilivyosema, tangu WhatsApp na Facebook tunatumia sana Yahoo, sasa tuko katika Gmail na mengine. Sasa tuangalie ikiwezekana basi tufuate utaratibu ambapo Mbunge wa jimbo ikiwa halmashauri ina Mbunge zaidi ya mmoja itafutwe namna, lakini Mbunge akawe Mwenyekiti wa Halmashauri, ili kujaribu kuunganisha uwajibikaji wa pamoja.

Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)