Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi muhimu sana ya kuchangia taarifa hizi za Kamati hizi tatu PAC, PIC na LAAC.

Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma kwa kutujaalia afya na siku njema lakini kipekee niwashukuru sana Wabunge wenzangu. Nirudie tena; kipekee niwashukuru sana Wabunge wenzangu ambao kwa kweli kwa hizi siku mbili nimelala vizuri. Mimi sikuweza kutathmini wingi wa Wabunge ambao wamejitokeza kuongea kwa hisia kuhusu kupinga ufisadi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Biblia, Eliya siku moja alilalamika kwa Mungu kwamba yuko peke yake ambaye haabudu sanamu lakini Mungu alimwambia hauko peke yako wako zaidi ya 7,000. Na leo nimetambua ndani ya hili Bunge kumbe kuna watu 7,000 ambao tunapinga kwa dhati ubadhirifu, ufisadi na wizi. Kwa kweli Wabunge najisikia fahari sana kuwa sehemu ya hili Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze mchango wangu kwa kueleza masikitiko. Mwaka jana Bunge hili lilitoa Maazimio lakini leo ni asilimia 47 tu ya Maazimio yaliyoazimiwa na Bunge kwenye taarifa hii ya CAG yametekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mwaka huu tunakwenda tena kutoa maazimio wakati tuna asilimia 50 ya maazimio tuliyotoa mwaka jana hayajatekelezwa. Kwa mfano, Wabunge wenzangu niwarudishe nyuma, kuna hii Kampuni ya KADCO ambayo ilianzishwa na watu binafsi wawili kwa kushirikiana na Serikali kwa ajili ya kuendesha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa KIA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2009 Baraza la Mawaziri lilitoa agizo kwamba hisa zote za KADCO zinunuliwe na zikanunuliwa kwa thamani ya Dola za Kimarekani milioni tano, karibu bilioni sita za Tanzania, lakini mpaka leo uwanja huo bado haujarudi na KADCO wanaendelea kuuendesha licha ya maagizo ya Bunge hili tuliagiza mwaka jana. Nashukuru Mungu Waziri wa mwaka jana bado anaendelea na nafasi yake, bado anaendelea na hiyo nafasi yake na Bunge liliagiza na yeye akatuahidi kwamba, muda siyo mrefu TAA itachukua Uwanja wa Ndege wa KIA na kuundesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nimhoji Mheshimiwa Waziri hivi nani yuko nyuma ya KADCO? Hili ni lazima Wabunge tusiliache, tunataka tumjue nani yupo nyuma ya KADCO ambaye anakiuka maagizo ya hili Bunge na Serikali inaogopa kuurudisha ule uwanja ambao tayari ilishaununua na kulipa hisa zake. Hivi kweli Wabunge tufumbie macho na hilo? Tufumbie macho na hilo? hivi Watanzania watatuelewaje? Leo tena tutoe agizo lingine kusema Uwanja wa Ndege wa KIA urudishwe Serikalini wakati tayari maagizo yalishatolewa na hela ilishalipwa. Hivi tunaipeleka wapi nchi hii na nani huyo ambaye anamiliki hiyo KADCO mpaka ana kiburi cha kukataa Maazimio rasmi ya Bunge, Serikali na Baraza la Mawaziri ambayo vyote viliagiza?... (Makofi)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa naomba taarifa yako iwe ya afya maana yake nahutubia Taifa…

SPIKA: Mheshimiwa George Mwenisongole, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest…

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa naomba taarifa yako iwe na afya maana yake nahutubia Taifa hapa. (Kicheko)

TAARIFA

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba, hiyo KADCO inayoendesha Uwanja wa Ndege wa KIA, inaendesha bila hata Mkataba, kinyume na Sheria za Nchi na bado inaendesha huo uwanja na siyo hiyo tu bado imeisababishia Serikali hasara ya kutosha…

SPIKA: Mheshimiwa taarifa ni moja…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo taarifa yangu.

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa George Mwenisongole unaipokea taarifa hiyo?

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, kwa kichwa, mikono na miguu naipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kama hili Bunge litashindwa kuchukua hatua kuhusu KADCO, hakuna maana basi ya Taarifa ya CAG kuletwa Bungeni, hakuna maana. Hili liko dhahiri kabisa, liko dhahiri kabisa na hata tukisema kwamba, Mheshimiwa Waziri ambaye alituhaidi kwamba KADCO itarudishwa Serikalini mpaka sasa hivi bado yupo kwenye nafasi yake kwa kweli mimi nashindwa kuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Waheshimiwa Wabunge, tumetumia hizi siku mbili kulalamika, lakini niwaulize Sheria za Nchi anatunga nani, si sisi? Naomba tufanye maamuzi magumu na nikushukuru Mheshimiwa Maganga, naomba uingize jina langu katika orodha ya Wabunge wanaotaka Sheria ya Watu Kunyongwa wanaofanya ufisadi, George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, hakikisha unaandika jina langu leo, sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa sababu sisi ndiyo tunatunga sheria, naomba kabla ya Bunge hili kwisha tujitolee Wabunge tulete Muswada binafsi kwamba, taarifa ya CAG inapotoka tutunge sheria Serikali ilete taarifa ya utekelezaji wa Maagizo ya CAG na Maamuzi ya Kamati na Maazimio ya Wabunge ndani ya miezi mitatu baada ya taarifa ile kutoka. Kama Serikali haitaleta maazimio ya kuonesha utekelezaji wa hizi taarifa tutakuwa tunafanya kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, naomba Wabunge mniunge mkono na Watanzania wote wananisikia. Naomba tutoe azimio wezi wote wa kuku, wezi wote waliopora simu waachiwe. Kama hatuwezi kuwafunga watu wanaoibia ushirika, kama hatuwezi kuwafunga Wakurugenzi wanaotafuna fedha, kama hawa watu wa KADCO wanaiibia Serikali mchana kweupe hatuwezi kuwafunga, kwa nini tuwaonee wezi wa kuku? Kwa nini tuwaonee hawa wezi, hawa wezi tuwaachie. Kuna sababu gani ya kuwakamata watu wa hao wezi, wakati majizi makubwa wanaoitia hasara Serikali wanaachia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili Bunge litaingia katika historia kati ya Mabunge bora duniani kama tutatoa azimio la kuwaachia wezi wote wa kuku. Hakuna sababu ya kuwaweka ndani wakati wezi wakubwa tunashindwa kuwachukulia hatua, kuna maana gani basi ya sisi kuwa Wabunge? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tumechoka, kule kwetu Mbozi kinachoendelea ni vichekesho, kinachoendelea ni vichekesho. Watu wamekamatwa, Viongozi wa Vyama vya AMCOS wamekatwa na wamekiri kwamba wameiba hela, eti wameambiwa rudisheni hela halafu wakaachiwa. Waliyofikishwa Mahakamani ni wale ambao waligoma kurudisha hela hivi kweli mtu ameiba, amekiri…

MHE. ALLY M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: …kwamba ameiba halafu wanawaachia, hivi hii nchi tunaipeleka wapi?

SPIKA: Mheshimiwa George Mwenisongole, kuna taarifa kutoka Mheshimiwa Ally Mlaghila Jumbe.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, nimesema taarifa naomba iwe ina afya maana yake nahutubia Taifa. (Kicheko)

TAARIFA

MHE. ALLY M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hata Kyela ni hivyo hivyo kwenye AMCOS, watu wameiba pesa lakini wanasema zichangwe kokoa ndiyo zilipe wakati aliyeiba yupo anaonekana.

MHE GEORGE R. MWENISONGOLE: Lakini…

SPIKA: Mheshimiwa George Mwenisongole muda wako ulikuwa umeisha, sekunde thelathini malizia.

MHE GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, kipekee nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu. Niliomba ukaguzi maalum wa CAG na CAG ametoa taarifa yake. Nimemkabidhi Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameniahidi ndani ya wiki mbili anakuja Mbozi.

Mheshimiwa Spika, kipekee nimshukuru Waziri wa Kilimo ambaye alileta timu ya wakaguzi kule Mbozi, imeifanyia kazi na naamini Mheshimiwa Bashe ataongozana na Mheshimiwa Waziri Mkuu anapokuja Mbozi ndani ya wiki mbili tunataka tufanye mfano, tunataka tufanye Mbozi iwe pilot study, sisi hatutaki ufisadi Mbozi…

SPIKA: Haya ahsante sana…

MHE GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)