Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo ili niweze kuchangia hii Ripoti ya CAG pamoja na Kamati zilizowasilishwa juzi hapa upotevu wa mabilioni uliopatikana katika Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukupongeza kuchaguliwa kuwa Rais wa Mabunge Duniani, Mungu akubariki sana na akuongoze, akupiganie katika utumishi wako, wanawake wenzako uwaonyeshe mfano kwamba wanawake kweli mnaweza, kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutuchagulia Makonda kuwa Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi. Nampongeza kwa roho ya dhati kabisa, tunamuona Makonda anavyopambana na sisi vijana niseme kwa niaba ya vijana wote Taifa hili tunamuunga mkono Makonda.

Mheshimiwa Spika, Makonda ameanza na Baraza la Mawaziri, ni kwa nini? Ni swali la kujiuliza kama ni mtu mwenye akili timamu. Ni kwa nini ameanza na Baraza la Mawaziri? Kama kweli ni hoja ya Kamati Kuu yote ile ya CCM naipongeza sana.

Mheshimiwa Spika, kiukweli kila nitakapopata nafasi kusema, nitakuwa nasema ukweli tu. Sitaki siasa za kibabaishaji na bora niache kuchaguliwa ila nimesema ukweli na siku nikifa nitaenda mbinguni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikupe taarifa tu kwamba, mpaka jana tumefika Wabunge 168 ambao tumekubaliana kwa pamoja kabisa tutengeneze mpango tupitishe sheria ya kunyonga watu. Tunaangalia mataifa yaliyoendelea, mengine yanatupa misaada na wanazo hizo sheria, ni kwa nini waliweka hizo sheria, watu ni wagumu, watu hawaelewi kabisa, watu huwezi ukawapeleka mahakamani tu na kulipa pesa hizi ambazo wameshaiba. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, sio maigizo ni suala ambalo limeorodheshwa humu na CAG. Wezi wote wanajulikana na mimi ninamuomba Mungu nisije nikaponyoka nikaanza kuwataja kwa sababu wanafahamika wezi waliotuibia kwenye hili Taifa.

Mheshimiwa Spika, isipokuwa ninaomba Mungu anisaidie sana nitumie nafasi yangu ya Ubunge kuishauri Serikali. Wananchi wana kilio kikubwa sana. Wanateseka na michango ya kila aina. Ukifuatilia michango wanayochangisha wananchi unakuta kuna shilingi bilioni 11 ambazo zimepotelea kwenye POS. Ninampongeza Mheshimiwa Halima juzi alitusomea hapa kwa wenye weledi mkubwa. Ametaja mpaka na majina ya halmashauri zilizotumika kuiba hizi shilingi bilioni 11. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimsapoti sana Mheshimiwa Simbachawene. Unajua mtu akiongea ukweli wakati mwingine anachukiwa na watu. Jana Mheshimiwa Simbachawene uliongea jambo la ukweli kabisa. Sisi Wabunge kwenye mabaraza ya Madiwani ni wajumbe wa Kamati za Fedha, ninaiomba Serikali hata chama kiwe na muda wa kuwauliza Wabunge kwanza, wewe kwenye halmashauri yako umefanya nini? Kila Mbunge ajieleze hadharani, mpaka upotevu wa fedha unapatikana wewe ulishauri nini kama Mbunge? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ukisoma hii Katiba inajieleza baina kabisa kwamba, Mbunge ni mtu wa aina gani, anatakiwa afanye majukumu gani. Humu tuna hatari, tuna Wabunge wasiojielewa wanasubiria siku ya kuja kulalamika hapa mbele yako. Lakini niwasemee kidogo wale watumishi wanaoisimamia Serikali. Wapo watumishi wengine wana roho ya dhati kuitumikia nchi yao, lakini Serikali Kuu mnawakatisha tamaa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, unakuta mtumishi anafanya kazi halipwi mshahara. Ukiangalia hapa kuna shilingi bilioni zaidi ya 11.998 hii ni malimbikizo watu hawalipwi mshahara mpaka zimefika hizi pesa. Hata kama ni wewe lazima ufikirie, mtu anafanya kazi, mlishakubaliana nae kumlipa mshahara, hammlipi, mnampelekea pesa nyingi za miradi ya maendeleo, hana pesa ya kula nyumbani, matokeo yake afanye nini? Lazima aibe, mimi hapo ndiyo maoni yangu.

Mheshimiwa Spika, shilingi bilioni 11.9 ninaiomba Serikali, kwanza watumishi hawa wana mishahara midogo, ione kila sababu ya kuweza kuwalipa watumishi hawa ili wawe na moyo ule wa kufanya kazi zao kama walivyopangiwa kwenye mikataba yao.

Mheshimiwa Spika, lakini nizungumzie hili, tuna hawa wazabuni wa ndani, kilio ni kikubwa sana kwa wafanyabiashara. Wamenituma Wafanyabishara kujaribu kuishauri Serikali. Kuna wafanyabiashara wameikopesha Serikali, wengine wamekopesha sementi, wengine mafundi wamefanya kazi kwenye shughuli za Serikali wakiamini kwamba hii Serikali ina pesa, hawalipwi. Niwaombe wasimamizi wote wa Serikali waweze kuwanea huruma hao wazabuni ili waweze kulipwa fedha zao.

Mheshimiwa Spika, nirudie tena kumpongeza Makonda na nimuombe Makonda andelee kuwa na msimamo wa hivyo hivyo, asirudi nyuma na sisi tupo nyuma yake. Tutampa ushirikiano wa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kweli anakuwa akifanya ziara tunamuona, juzi alikuwa Bukoba tulimuona, juzi amefanya kikao kwenye vyombo vya habari tukamuona, anakemea wezi lakini siwapongezi Mawaziri wale ambao wapo special kumpongeza Mheshimiwa Rais. Ukiangalia kwenye ndimi zao special kumpongeza Mheshimiwa Rais tu. Tukiwauliza wao wamefanya shughuli gani, tukitoa shughuli za Mheshimiwa Rais?

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa lakini sisi wanasiasa huwa tunasema mwisho lakini hoja nyingine zinakuja. Kwenye upande wa mchanga wa ujenzi, Serikali iliweka ushuru wa madini ujenzi. Wananchi wa Mkoa wa Geita wameniomba sana, halmashauri zinazoanzishwa sasa hivi zinashidwa kuendelea kujengwa kwa sababu ya huu ushuru wa madini ujenzi. Serikali iachane na huo ushuru kwa sababu, huo mchanga hauna madini, huo mchanga hauna madini kabisa toka miaka ya nyuma watu walikuwa wakichota bure na matela yao. Kuna wengine walikuwa wana miradi ya matela. Walikuwa wakisomba mchanga wanauza trip moja shilingi elfu tano. Wanajipatia fedha.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wameshapaki matoroli yao kwa ajili ya huo ushuru ni mkubwa, unawasababisha wasiendelee na biashara yao ya mchanga. Serikali iondoe huo ushuru ili kusudi mchanga ambao hauna madini watu waweze kuchota bure, waweze kujenga halmashauri zao.

Mheshimiwa Spika, narudia kukushukuru tena wewe kwa sababu nikiendelea kuzungumza mimi kadri hasira zinavyopanda na wezi waliotoajwa humu na CAG wanajulikana naogopa nisiharibu mchango wangu. Niwaombe tu Wabunge wenzangu wote wale waliobaki kujiorodhesha kwenye hii sheria tunayotaka kuipitisha ya kunyonga, waorodheshe kama na wao sio majambazi, ila kama ni majambazi wanaogopa wasinyongwe basi wasitupe ushirikiano.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mungu akubariki sana. (Makofi)