Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika mpango huu. Kwanza naanza kwa kuzungumzia suala la Bandari Kavu ya Tunduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunajua hata Serikali inajua umuhimu wa mpaka wa Tunduma hasa kwa kuzingatia kwamba mpaka wa Tunduma ni lango kuu la SADC. Mpaka wa Tunduma unapitisha mizigo zaidi ya asilimia 73 inayoshuka katika Bandari ya Tanzania. Mizigo yote hii inapita katika mpaka wa Tunduma ambalo ni lango kuu la SADC. Katika michango yetu mbalimbali tumeendelea kuisisitiza Serikali na kuiomba, ione umuhimu mkubwa wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma ili kurahisisha huduma za usafirishaji wa mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajabu ni kwamba, tangu nimeanza kuusoma Mpango huu, sijaona mahali ambapo Serikali imeweka kipaumbele cha kuhakikisha inajenga bandari kavu katika Mji wa Tunduma ili kurahisisha huduma kwa watu ambao wanatumia mpaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifahamike wazi kabisa kwamba sasa hivi mataifa yapo katika ushindani wa kibiashara ikiwemo Tanzania. Tunaona mataifa mengi ambayo yanaandaa mipango ya kujenga bandari kavu katika mataifa yao. Ni lazima Serikali ione umuhimu wa kujenga bandari kavu katika Mji wa Tunduma hasa ukizingatia kuwa ni lango kuu la SADC ili kurahisha huduma na kuendelea kuwashawishi watu ambao wanatumia mpaka huu wa Tunduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua umuhimu wa bandari kavu na sisi sote tunaona namna Halmashauri ilivyolichukua jambo hili kama kipaumbele. Halmashauri ya Mji wa Tunduma imetenga zaidi ya ekari 2,000 kwa ajili ya kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma. Tumeomba miundombinu, tumeona reli imepita katika lile eneo, tunaona hospitali kubwa imejengwa katika yale maeneo, tunaona stendi imejengwa katika yale maeneo. Tunaiomba Serikali ione umuhimu wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma ili kuleta ushindani wa kibiashara na mataifa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba kuzungumzia suala la kilimo. Nazungumzia upatikanaji wa mitaji katika Sekta ya Kilimo. Mimi ninatokea Mkoa wa Songwe, Mkoa ambao asilimia kubwa ya wananchi wake wanaishi vijijini na ni wakulima wakubwa, na ni wakulima wazuri kabisa ambao wanategemewa na Taifa hili. Tunaona katika pato la Taifa namna kilimo ambavyo kimekuwa na mchango mkubwa, zaidi ya asilimia 26 kilimo kinachangia katika pato la Taifa. Hivyo, kilimo ni kipaumbele kikubwa ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona katika upatikanaji wa mitaji ya sekta ya kilimo kwa mwaka 2022/2023, taarifa inasema zaidi ya shilingi trilioni 2.622 zilitengwa na benki kwa ajili ya shughuli za kilimo kwa riba isiyozidi asilimia 10, lakini katika fedha hii shilingi trilioni 2.622 ambayo ilitengwa na hizo benki, 7% tu ndiyo ilikwenda katika uzalishaji wa mazao, asilimia 93 ilikwenda katika biashara ya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni hatari kwa Taifa letu. Tunaona namna watu ambavyo wamezama kwenye biashara na wamesahau kwenye suala zima la uzalishaji wa mazao ndani ya Taifa letu. Ndiyo maana tunatumia fedha nyingi kuagiza baadhi ya mazao nje kwa kuwa huku ndani tumeshindwa kuwekeza. Tuna wakulima wengi sana ambao wamejitoa kwenye suala zima la kilimo, lakini wengine wanashindwa tu kwa sababu ya mitaji. Tuna ardhi ya kutosha ambayo hata nusu, hata robo bado hatujaifikia, lakini bado tuna changamoto kubwa ya kuagiza baadhi ya vyakula nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali, ione umuhimu wa kuwekeza fedha nyingi ambazo zinatengwa na benki, ziende kwenye uzalishaji wa mazao na siyo biashara. Ni lazima tuzalishe mazao ya kutosha, ni lazima tuzalishe mazao ya aina mbalimbali ya kutosha ndani ya Taifa letu na ikiwezekana tuuze nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona kuna changamoto. Ukisoma katika taarifa utaona ya kwamba Magereza yetu yanatumia zaidi ya shilingi bilioni 10 kila mwaka kwa ajili ya chakula. Wakati huo tunaona namna ambavyo Magereza yana ardhi kubwa na nzuri ya kutosha ambayo inaweza kutusaidia katika uzalishaji wa mazao. Changamoto kubwa ambayo Magereza wanashindwa ni kukosa mtaji na fedha za kuendeshea kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali ione umuhimu wa kuwekeza fedha na kuwakopesha watu wa Magereza ili waweze kuzalisha chakula kingi na ikiwezekana wajiendeshe, wajikwamue kiuchumi na waweze kutusaidia katika suala zima la uzalishaji wa chakula ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuzungumza jambo moja. Kumekuwa kuna changamoto, kwamba wakulima wetu wanatumia muda mwingi kupambana na kuhakikisha wanajikwamua katika suala zima la kiuchumi kupitia kilimo. Nasema wazi, tumeona katika mkoa wetu na maeneo mengine, Serikali imewatangazia wakulima kwamba iko tayari kununua mazao na wakulima bila kusita wamejitoa kwa moyo wote kuiuzia Serikali mazao. Ajabu ni kwamba, NFRA Wakala wa Chakula, inaeleweka hiyo!

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajabu ni kwamba, tangu mwezi wa Tisa, wa Nane, wa Kumi, watu wamechukua mazao lakini wakulima hawajalipwa fedha zao, pamoja na Serikali kuchukua haya mazao. Tunaomba, watu wamelipwa wachache na wengine bado hawajalipwa na ukizingatia katika mikoa yetu, tumeingia katika msimu wa kilimo. Huyu mkulima mnamweka kwenye eneo gani? Mimi ninachojua wakulima wanalima mazao wakiwa na malengo.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella, kuna Taarifa.

TAARIFA

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Mbunge, Serikali ilinunua mazao yenye thamani ya shilingi bilioni 194. Mpaka kufika siku ya jana, Serikali imemaliza madeni yote ambayo ilikuwa inadaiwa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella, Taarifa rasmi hiyo unaipokea?

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei Taarifa.

MWENYEKITI: Aaah!

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa kwa sababu, sisi mwezi huu na mwezi uliopita tayari tumeingia kwenye maandalizi ya kilimo. Mnawaletea wakulima wetu vidonda vya tumbo! Nina uhakika hata Momba huko Isanga hawajalipwa. Labda kama mmelipa jana, ndiyo mtuambie. Kama watu wamepimiwa mazao kutoka mwezi wa Nane wamelipwa jana, hii inakaa sawa? Kwamba hawa wakulima hawana malengo? Hakuna anayefanya kazi bila malengo. Acheni kuwasababishia wakulima umaskini usio na lazima. Ni lazima tuseme ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuzungumzia suala zima la barabara. Sisi wote tunajua zaidi ya asilimia 80 mpaka 90 ya mizigo na abiria wanatumia barabara. Hivyo, ni wazi kwamba barabara ina mchango mkubwa kwenye uchumi wa Taifa letu na maendeleo ya kijamii. Hata hivyo kumekuwa na changamoto, na ndiyo maana kila Mheshimiwa Mbunge anayesimama hapa, anazungumzia suala la barabara. Barabara imekuwa ni changamoto kwenye nchi yetu. Maeneo mengi barabara zinakufa, zina hali mbaya kabisa. Kuna maeneo hata barabara za kuunganisha mikoa na mikoa zina hali mbaya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa, kengele ya pili.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, lakini muda wangu mwingine ulichukuliwa na Mheshimiwa Waziri. Nashukuru.