Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu.

Kwanza kabisa ningependa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anawajali wana wa Tarime. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana kwa sababu kulikuwa na tatizo kubwa sana katika Jimbo letu la Tarime Mjini ambapo kulikuwa na madai ya muda mrefu ya fidia katika Mtaa wa Kinyambi na Bugosi ambapo kulikuwa na mgogoro kati ya Jeshi na Wananchi wa Mtaa ule. Mheshimiwa Rais alitoa pesa na wale wananchi wakalipwa. Kwa niaba ya wana wa Tarime nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo aliweza kusikiliza kilio chao na kuweza kuwalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tulikuwa na tatizo kubwa la ukosefu wa soko katika Mji wetu wa Tarime. Ametoa zaidi ya shilingi bilioni 9.5 na ujenzi ule sasa unaelekea kukamilika na sisi tunategemea wafanyabiashara wa Tarime wapate sehemu ya kufanyia biashara ambayo ilikuwa ni tatizo kubwa katika kipindi cha muda mrefu. Hizi ni baadhi ya mambo makubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameyafanya katika kipindi cha miaka mitatu cha uongozi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nichangie Mpango kuelekea katika upande wa vijana. Ukizingatia kwamba vijana ni wengi katika nchi hii na vijana wengi hawana ajira, ningependa niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Mipango pamoja na Waziri wa Fedha kwa namna ambavyo wamekuja na Mpango mzuri ambao umezingatia vile vile vijana kwa upande wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2024/2025 ulikuwa umelenga kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi ambao ni jumuishi unaopunguza umasikini, unaozalisha ajira kwa wingi, unaotengeneza utajiri na unaochochea mauzo ya bidhaa nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningependa nilenge sana upande wa ukosefu wa ajira kwa vijana. Tatizo la ajira katika Nchi yetu ni kubwa sana na ni kubwa, kubwa, kubwa, kubwa. Imekuwa tatizo kubwa mpaka watu wanapoanza kuomba ajira wanadanganya kwamba ni walemavu ili waweze kupata upendeleo wa kupata ajira. Mwaka uliopita waombaji kazi 419 walidanganya kwamba ni walemavu ili waweze kupata ajira na hii inadhihirisha ni namna gani tatizo hili ni kubwa katika Nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walioomba kazi walikuwa 171,916 na waliopata kazi katika upande wa walimu walikuwa 13,130. Katika upande wa Afya waliopata kazi walikuwa ni 5,319. Kwa hivyo jumla ya waliopata ajira kati ya 171,916 walikuwa 18,449. Kwa hivyo waliobaki 153,512 hawa walibaki bila ajira wakienda mtaani. Jumla mwaka 2014 watu 1,000,000 kwenda kuomba kazi katika idara ya uhamiaji na huku watu 70 ndiyo walikuwa wanahitajika kwa mwaka huo. Kwa hivyo watu 930 walitoka pale bila ajira na walienda mtaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ripoti ya Taasisi ya Utafiti na Kupunguza Umasikini Tanzania (REBOA) ya mwaka 2019, vijana 1,000,000 wanahitimu katika vyuo mbalimbali na uwezo wa Serikali pamoja na Sekta Binafsi wa kutengeneza ajira ni 2,500. Unaweza kuangalia namna tatizo hili lilivyo kubwa ndiyo maana tunao machinga wengi mitaani, tunao boda boda wengi ambao hawapendi kufanya ile kazi lakini kwa sababu hawana kazi ndiyo maana wamejiingiza katika kazi ile ili waweze kupata at least kipato cha kuwaweka waendelee kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo letu la Tarime Mjini wapo watu waliojiwekeza kuchimba madini wadogo wadogo. Katika kuchimba wanapokuwa wametoka shimoni wamechimba madini yao, wanapotoka nje tayari wanatozwa ushuru bado hawajauza lakini bado hata hawajapata chochote kutokana na wanatozwa kulingana na udongo waliopata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna vijana ambao wanatoa bidhaa Kenya wanakuja kuuza Mji wa Tarime. Kutokana na kwamba bidhaa nyingi ambazo zinatoka Kenya kuja Tarime pale at least bei yao inakuwa chini. Anapokuwa amepita na cement 10 kwamba aje auze Tarime hawezi kulipa kodi kwa sababu mfumo hauruhusu kulipa kodi bidhaa ndogo ndogo. Hii inasababisha vijana wale wapite kwa njia ya magendo na Serikali inapoteza fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili ndilo lililosababisha Serikali ikaja na Mpango wa Maendeleo 2024/2025 na katika Mpango huu kuna Program ya Taifa ya kukuza ujuzi Nchini lakini pia kuna Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Ningependa nizungumzie Program ya Taifa ya Kukuza Ujuzi Nchini. Program hii iliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Serikali pamoja na Sekta Binafsi kwamba waweze kutoza fedha kwa ajili ya kugharamia kukuza ujuzi wa vijana wetu kwa lengo la kuzalisha ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, makubaliano yalikuwa kwamba asilimia moja ya tozo hizo iweze kupelekwa kwa ajili ya kuendeleza ujuzi wa vijana. Kwa mwaka 2021 na 2022 makusanyo halisi yalikuwa shilingi bilioni 291 na kwa asilimia moja ilipaswa shilingi bilioni 97 ziende kuendeleza ujuzi wa vijana wetu lakini mambo yalikuwa tofauti. Mwaka 2015/2016 walipeleka shilingi bilioni 15, 2016/2017 walipeleka shilingi bilioni 15, 2017/2018 walipeleka shilingi bilioni 15, 2018/2019 walipeleka shilingi bilioni 15, 2019/2020 walipeleka shilingi bilioni 18, 2020/2021 walipeleka shilingi bilioni 18. Kuanzia 2021 mpaka 2022 walipeleka shilingi bilioni tisa, 2022/2023 wamepeleka shilingi bilioni tisa. Hii imesababisha vijana ambao walikuwa wananufaika 42,000 imeshuka sasa mpaka vijana 12 peke yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na Mpango, vijana 681,000 walipaswa wanufaike na Mpango huu ndani ya miaka mitano lakini kwa namna ambavyo wanapeleka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)