Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2024/2025. Awali ya yote napenda kumpongeza schoolmate wangu wa Pugu High School, Profesa Kitila Alexander Mkumbo, pamoja na rafiki yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu, Waziri wetu wa Fedha pamoja na Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ambaye pia ni schoolmate wangu katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawapongeza kwa sababu wametuletea taarifa nzuri zenye mwelekeo mzuri, lakini sana nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuonesha dira kupitia hotuba yake aliyoitoa tarehe 19 mwezi Machi mwaka 2021 wakati alipoapishwa kushika hatamu za uongozi wa nchi yetu. Pia, kwenye hotuba yake aliyoitoa hapa Bungeni siku ya tarehe 22 mwezi Aprili, mwaka 2021, kwa kweli imezingatiwa kwa kiwango cha kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ningependa kuchangia katika sekta mbili tu; Sekta ya kwanza ni ya utalii na sekta ya pili ni ya mifugo. Tumeona kwenye taarifa ongezeko la mapato na idadi ya watalii katika nchi yetu imeongezeka sana na mapato ya Serikali yetu yameongezeka sana kupitia sekta hiyo. Takwimu zinaonesha kwamba mwaka 2021 watalii waliongia hapa nchini walikuwa 922,692, lakini mwaka uliofuata mwaka 2022, waliongezeka hadi kufikia 1,454,920 sawa na ongezeko la watalii takribani 500,000 hivi sawa na asilimia 57.7.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko hili limewezesha ongezeko la fedha zilizopatikana kutokana na sekta hii toka dola milioni 1.31 mwaka 2021 hadi kufikia dola milioni 2.53 mwaka 2022. Ni ongezeko kubwa na hili linaonesha namna ambavyo tumekuja kunufaika kutokana na maono ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia ile Filamu ya Royal Tour. Narudia kumpongeza Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia vizuri hizi taarifa zote tatu, sijaona mwendelezo wa Royal Tour. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiri tuone namna ambavyo tutaendeleza mwenendo mzuri uliotokana na Filamu ya Royal Tour. Kwa sababu hata taasisi za Kimataifa ambazo zilifanya assessment ya shughuli za utalii zinavyoendeshwa hapa Tanzania na nchi nyingine za kiafrika imei-rank nchi yetu kuwa namba moja kwa vivutio vingi vya utalii. Duniani imekuwa ranked kama namba 12. Kwa hiyo, haya ni mafanikio makubwa. Haya hayatufanyi tubweteke, tunatakiwa tubuni vyanzo vipya kama ambavyo malengo yetu ambayo yameandikwa kupitia huu mpango yalivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napendekeza au naishauri Serikali, tuwe na mkakati wa kuwa na Royal Tour Na. 2 au Phase II. Naomba tuweze kuzingatia maeneo yafuatayo: moja, katika hii Royal Tour Na. 2 tuyatazame maeneo ya hifadhi zetu za Taifa, tukianzia na ile ya Ruaha, tuangalie kule misitu ya Udzungwa, pori la Akiba la Selous, twende tukaioneshe dunia maajabu ambayo Mwenyezi Mungu alituumbia sisi Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niliona tunahitaji kuwekeza katika malikale kupitia hiyo Royal Tour Na. 2. Pale Kilwa kuna Magofu ya Kilwa Kisiwani yaingie, Songo Mnara yaingie, viboko albino pale Pindiro, Makangaga yaingie, viboko katika Bwawa wa Maliwe au Ziwa la Maliwe pale Mitole liingie, vilevile kumbukizi za mambo mbalimbali ya kale kama vile Vita vya Majimaji kule Kilwa pale Nandete, Kibata na maeneo mengine na kule Songea pia, yaingie katika Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi juzi hapa alikuja hata Mheshimiwa Rais wa Serikali ya Shirikisho la Ujerumani, alifika mpaka Songea. Hiyo inaonesha kwa jinsi gani hata watu walio nje ya nchi ambao tulikuwa tunashirikiana kwa majukumu mbalimbali siku zilizopita, bado wanaikumbuka Tanzania na wanaona kuna fursa nyingi za kuweza kushirikiana nasi. Kwa hiyo, naomba hilo nalo liingie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna utalii wa mapango. Kati ya mwaka 1994 na mwaka 2000 kulikuwa na Wataalam wa Kijerumani walikuja hapa nchini wakafanya utafiti kwenye mapango 25, wakiongozwa na Albert Daniel Galabawa. Walianzia Tanga, wakafanya exploration ya mapango tisa yakiwemo nane ya Amboni, lakini kulikuwa na mapango mengine Zanzibar moja, kule wanaita Mangapwani, pia walikwenda katika Milima ya Matumbi ndani ya Jimbo langu Kilwa Kaskazini, walifanya exploration na utafiti kwenye mapango 15, likiwemo Pango la Nang’oma ambalo ni kubwa, namba moja katika Afrika Mashariki kulikuwa na Pango la Naliotoke, kulikuwa na pango la Kiongolo, Mpachawa, Kilindima, Namaingo, Lupondo, Kibwe, Shingya, Kimambo, Nampombo, Likolongomba pamoja na pango la Mtumbukile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu ule utafiti umefanyika, hakuna uendelezaji wowote uliofanyika. Hata Waheshimiwa Mawaziri tu, nakumbuka Waziri mmoja tu alifika mwaka 2021 katika Pango la Nang’oma lile ambalo nimesema ni kubwa kuliko yote Afrika Mashariki. Kwa hiyo, nilifikiri hapa tunapaswa kujenga Information Center, lakini vilevile tuone namna ambavyo tutaendeleza hivi vyanzo vya utalii. Nina hakika nchi yetu itapiga hatua katika sekta ya utalii na vilevile tutaweza kupata pesa mara tatu hadi mara nne inayotokana na hivi vyanzo ambavyo inaonekana vimesahaulika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikenda kwenye sekta ya mifugo, naomba niwaeleze Waheshimiwa Wabunge wenzangu. Sisi Tanzania hapa hatufugi, tunachunga. Hii imepelekea changamoto kubwa. Kuna uharibifu wa mazingira ambao unapelekea kuwepo kwa athari za tabianchi lakini pia kumekuwa na mapigano ya mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha tuna mifugo isiyopungua milioni 28.3, lakini mifugo hii inachungwa, imezagaa tu nchi nzima. Ni lazima tuwe na mipango mizuri ya kuendeleza sekta hii ya mifugo, vinginevyo tutaendelea kushuhudia majanga, tutaendelea kushuhudia matatizo; achilia mbali migogoro ya wakulima na wafugaji ambayo imejaa kule hasa Mkoa wetu wa Lindi katika Wilaya za Kilwa, Nachingwea pamoja na Wilaya ya Liwale. Pia hata miundombinu ya hii mifugo haipo. Tumesomewa hapa kwenye taarifa, kuna ujenzi wa majosho 246. Sasa majosho 246 kwa mifugo milioni 28.3, wapi na wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna utoaji wa chanjo, mifugo 696 imetolewa kwa mwaka uliopita. Hii mifugo 696 kwa mifugo milioni 28.3 wapi na wapi? Bado hatujafanya juhudi za kuhakikisha kwamba tunaidhibiti hii mifugo, lakini tunaifuga katika namna ya kisasa ili iweze kuzalisha kwa kiwango cha kutosha. Kwa hiyo, nimeangalia hata ulaji wa nyama, inaonekana sisi katika top ten hatumo…

MWENYEKITI: Ahsante, kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ichukue hatua za kutosha ili kuzuia haya mapigano ya wafugaji na wakulima, na pia kuruhusu sekta nyingine nazo ziweze kushamiri na kutuleta fedha nyingi, kuzalisaha ajira na kutuletea maendeleo katika nchi yetu, ahsante sana. (Makofi)