Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kukushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia katika bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2022/2023. Nachukua fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu Rahim kwa kunijalia uhai, na kwa kunipa afya ya kuniwezesha kusimama hapa leo ili nami nitoe mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti, kwa uongozi wake bora na kwa mwaka huu kutuletea mapendekezo ya bajeti yanayoakisi maslahi na matlaba yaani expirations za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, nichukue fursa hii kumpongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu, Naibu Waziri Mheshimiwa Hamad Hassan Chande, Katibu Mkuu wa Wizara na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bwana Emmanuel Mpawe Tutuba na Manaibu Katibu Wakuu na wote katika Wizara ya Fedha kwa kutuletea bajeti nzuri yenye ubunifu na inayozingatia mahitaji na matarajio ya wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba yangu binafsi na ya wananchi wa Jimbo la Kilosa ambalo nimepata heshima ya kuwawakilisha, namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi ambazo ametupatia wana Jimbo la Kilosa katika mwaka huu wa fedha 2021/2022 katika sekta ya afya, elimu, maji, barabara, madaraja, mawasiliano vijijini, kilimo cha umwagiliaji na kadha wa kadha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa elimu, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupatia jumla ya Shilingi 2,347,000,000/= kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Berega ambayo tumepata Shilingi bilioni moja. Shule ya Sekondari ya Berega itakuwa ni ya aina yake. Kwa upande wa O‘Level ni shule ya Kata kwa upande wa A’Level wao ni shule ya Kitaifa kwa ajili ya wavulana Bweni, Sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupa Shilingi milioni 470 kujenga Shule ya Kata ya Maguha. Wote mnaosafiri kwenda Dar es Salaam, mara baada ya kupita Mtumbatu ambako mnanunua nyanya, vitunguu, maharage na vinginevyo, mtaiona Shule ya Berega na mtaiona Shule ya Maguha. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa jumla ya Shilingi bilioni 2.405 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya na zahanati. Namshukuru kwa namna ya kipekee kwa kutoa jumla ya Shilingi milioni 900 kujenga kituo cha afya katika milima ya Uponera. Wale wanaoifahamu milima ya Uponera haifikiki kwa urahisi. Kutoka Gairo mpaka Uponera ni muda wa saa nne. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Maisha ya akina mama wengi waliofariki wakati wa kujifungua wakishuka kwenda Mamboya mwendo wa saa nne au kwenda Gairo mwendo wa saa tano, sasa yanakwisha kwa Shilingi milioni 900 ambazo Mheshimiwa Rais ametoa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Uponera katika Kata ya Mamboya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nashukuru kwa kituo cha afya cha Kata ya Chanzulu Ilonga; Shilingi milioni 515 na Kituo cha Afya cha Ntembo Kata ya Mabula Shilingi milioni 450; pia kwa Shilingi milioni 200 kwa ajili ya kujenga ICU katika hospitali ya Wilaya ya Kilosa, bila kusahau zahanati mbili za pembezoni mwa Jimbo letu ambalo ni kubwa sana, yaani Zahanati ya Unone Kata ya Rudewa Shilingi milioni 80 na Zahanati ya Lumbiji kwa Shilingi milioni 80.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa madaraja, namshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa upendeleo wa aina yake. Kwanza kwa kutupa fedha ya kujenga daraja la Berega katika Mto Mkundi ambalo linagharimu Shilingi 7,900,000,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni kuenzi jitihada alizozifanya Rais wa Awamu ya Pili, Benjamin William Mkapa aliyejenga daraja, kwa bahati mbaya likasombwa na maji; pia Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete aliyejenga daraja ambalo bado lipo lakini limevunjika. Kwa hiyo, Shilingi bilioni 7,900,000,000/= zitajenga daraja hilo, nasi kwetu tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwa ajili ya Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga daraja la Masombawe Kata ya Berega; na Shilingi milioni 160 kwa ajili ya kujenga daraja la watembea kwa miguu, bodaboda na baiskeli kwa Kijiji cha Ruwemba ambacho kukifikia unatumia mwendo wa saa nne kupita wilaya tatu ili kufika Kijiji cha Ruhemba katika Kata ya Kidete. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunamshukuru kwa fedha aliyotupa kwa ajili ya miradi ya maji hasa katika Mji Mdogo wa Dumila. Kwanza alitupa Shilingi 1,200,000,000/= na sasa ametupa Shilingi bilioni 530 ili kuhakikisha Mji wa Dumila unapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa Shilingi milioni 700 kwa ajili ya kujenga tanki la maji na mfumo wa maji katika Kata ya Rudewa katika Jimbo la Kilosa. Hii ni baadhi tu ya miradi ambayo imepatiwa fedha na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan katika mwaka huu wa fedha na katika mwanzo wa uongozi wake. Sisi wana Kilosa tunamshukuru sana na kwa lugha ya Kikaguru nimwambie Kwimage Lugano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nategemea kabisa katika bajeti hii tunayoijadili sasa barabara ya Rudewa kwenda Kilosa itakamilika kwa ujenzi wa madaraja manne yaliyosalia; daraja la Mto Kobe, daraja la Mto Kilonga na daraja la Mazinyungu na hatimaye daraja kubwa la kuvuka Mto Mkondoa kwenda Mikumi na baadaye kwenda Iringa, Mbeya, Tunduma na Zambia. (MakofI)

Mheshimiwa Spika, vile vile tunashukuru sana kwa fedha ambayo tunajua imepangwa kwa ajili ya kuanza kujenga barabara ya Kilosa kwenda Mikumi. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu na itasaidia sana katika utalii, na pia katika mazao ya miwa na mazao mengine yanayolimwa katika Jimbo la Kilosa na Mikumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa bajeti tunayoijadili, napenda sana kumshukuru Waziri wa Fedha, kwa kupendekeza kusamehe kodi ya ongezeko la mtaji, (Capital Gain Tax), kwenye uhamishaji wa haki na taarifa za madini kwenda kwenye kampuni za ubia zinazoundwa baina ya Serikali na wawekezaji na uhamishaji wa hisa, (Free Carried Interest) kutoka kampuni ya ubia kwenda kwa Serikali. jambo hili litarahisisha utekelezwaji wa mikataba hiyo, pia litarahisisha mazungumzo kwa sababu lina faida kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kumshukuru tena Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa heshima kubwa sana aliyonipa na kwa kuniamini kwa kiasi kikubwa sana kunikabidhi majukumu ya kuwa Mwenyekiti wa Timu Maalum ya Rais ya Majadiliano ya Serikali, yaani kwa kiingereza (Special Presidential Government Negotiation Team). Ni heshima kubwa sana ambayo sitaisahau katika maisha yangu yote nitakayokuwa duniani. Sijawahi kupata heshima kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua hizi ambazo Waziri wa Fedha amezichukua kwenye suala hili la capital gain tax litatusaidia sana. Tuna aina mbili ya free carried interest na ningeomba nitumie nafasi hii kuzifafanua. Iko aina ya free carried interest, yaani hisa ambazo Serikali inapewa bila kulipiwa za aina mbili, iko ambayo ni diluted free carried interest shares na iko ambayo ni non dilutable free interest carried shares; nini tofauti yake?

Mheshimiwa Spika, ile ya kwanza ambayo siyo dilutable, kila mwekezaji anapoongeza hisa wewe usipoongeza mtaji thamani ya hisa zako inashuka na mwisho inaweza kufifia kabisa. Tanzania tumechukua aina ya pili ya non dilutable free carried interest maana yeke nini? Yeye kila anpoongeza mtaji wewe unabaki na asilimia 16 ileile katika ule mtaji ulioongezeka. Maana yake thamani ya hisa zako haishuki. Nchi nyingi za kiafrika na ninaomba nisizitaje kwa heshima ya nchi hizo, zilichukua aina ya kwanza ya dilutable ndiyo maana nyingine zilianza na asilimia 50 leo zina asilimia Mbili. Nyingine zilianza na asilimia 20 leo zina asilimia Tano, lakini sisi kwa aina hii ya hisa tutaendelea kuwa na asilimia hiyohiyo katika maisha yote ya mgodi au mradi huo bila hisa hizo kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo tumelifanya katika Mabadiliko ya Sheria ya 2017 ya kuunda kampuni za ubia za madini kati ya Mwekezaji na Serikali. mara nyingi tunasahau jambo hili muhimu sana, iko tofauti kati ya rasilimali na mali. Madini ni rasilimali, lakini ili yawe mali ni lazima yatolewe leseni kama ambavyo ardhi ni rasilimali, lakini ili ardhi hiyo iwe mali ni lazima upewe Tittle Deed, yaani Hati ya Umiliki. Huko nyuma sisi tulibaki na rasilimali, lakini license au leseni zilipewa kampuni za nje. Kwa hali ya sasa katika majadiliano yote yanayoendelea leseni sasa zinamilikiwa na kampuni ya umoja ya ubia. Maana yake sasa unamiliki leseni ambayo ni mali na madini ambayo ni rasilimali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hilo ningependa nifafanue, ile free carried interest sio kwai le kampuni hodhi ni kwa mgodi husika na mradi husika. Kwa hiyo, kwa mfano katika kampuni ya Twiga Minerals Serikali ina asilimia 16 katika Mgodi wa Bulyankulu, ring fenced, asilimia 16 katika Mgodi wa North Mara, ring fenced, na asilimia 16 katika Mgodi wa Buzwagi ambao unakaribia kufungwa, ring fenced na asilimia 16 katika Kampuni ya pamoja. Maana ya ku-ring fence ni kwamba, faida au hasara ya mgodi mmoja haiwezi kuathiri faida au hasara ya mgodi mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefanya pia hivyo katika Kampuni ya Tembo Nickel, itayaoanza kuchimba madini ya nickel ambayo ni madini ya kimkakati kule Kabanga. Serikali ina asilimia 16 kwenye Mgodi wa Kabanga, lakini pia ina asilimia 16 katika smelter itayaojengwa Kahama, pia ina asilimia 16 katika kampuni hodhi. Hivyohivyo ndivyo tumefanya kwa kampuni nyingine za Nyati Sand Minerals, lakini pia Kampuni ya Faru itakayochimba madini ya graphite huko. Kwa hiyo, maamuzi hayo yaliyochukuliwa na Waziri wa Fedha yanatusaidia kutoka katika kawaida tuliyoizoea ambayo imekuwa haitupi faida zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kengele ya pili imegonga. Na nisikuweke mahali pagumu kuamua nikae au nisikae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nitachangia katika maandishi tofauti ya aina tatu za mikataba ya concession ya PSA na mikataba ambayo sasa tunaingia. Hiyo, nitachangia kwa maandishi au nikipata nafasi nyingine wakati wa bajeti hii kabla ya kupiga kura, kama inaruhusiwa, nitaomba tena nipate nafasi nilieleze hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa heshima hii na ninamshukuru sana Waziri wa Fedha kwa ubunifu na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa heshima aliyonipa, lakini kwa upendo kwa wana-Kilosa. Naunga mkono hoja. (Makofi)