Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan; Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Mchengerwa; Mheshimiwa Naibu Waziri, dada yangu Pauline; Katibu Mkuu, ndugu yangu Abbas; lakini Naibu Katibu Mkuu, ndugu Yakubu pamoja na watumishi wote ndani ya Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. Ukiona Serengeti Girls wanafanya vizuri na wanaenda World Cup, ukiona Tembo Warriors wanafanya vizuri, wanaenda world cup na maeneo mengi wasanii wanafanya vizuri hiyo ni kazi kubwa imefanyika.

Mheshimiwa Spika, kama wenzangu walivyotangulia kusema kwamba angalau uhai wa Wizara tumeuona, baada ya Waziri kuchakarika, tumekuwa naye kwenye Kamati, ametuambia sasa anaenda mtaa kwa mtaa, anaenda kijiji kwa kijiji hatimaye kata kwa kata, wilaya kwa wilaya kupeleka salamu za Mama kwenye michezo. Tunamsubiri, hiyo salamu njema ya Mama itufikie.

Mheshimiwa Spika, kipekee nizipongeze sana timu zetu hizi zinazofanya vizuri. Jana nilikuwa miongoni mwa waliokuwa Amani kushuhudia Serengeti Girls wakiicharaza Cameroon, siyo kazi ndogo Cameroon ni timu kubwa, jina lake ni kubwa kwenye mpira lakini vijana wetu wamefanya vizuri sana, nawapongeza sana. Hata hivyo, siku za karibuni pia tumeanza kufanya vizuri hata kwenye riadha. Nalisema hili mahususi, nchi hii ukitafuta medali nyingi, zipo Hanang. Tunayo kumbukumbu nzuri ya mzee wetu Gidamis Shahanga ameleta medali mbili za dhahabu za Commonwealth, lakini kijana wetu mahiri Emmanuel Giniki amevunja rekodi iliyodumu kwa miaka nane ya Warsaw Peace Half Marathon, ni kazi kubwa inafanyika.

Mheshimiwa Spika, nikizungumzia eneo hili, ninachoomba Hanang iangaliwe kipekee kwenye eneo la riadha. Nimeona orodha ya michezo ya kipaumbele, mpira wa miguu, netball, mpira wa kikapu, mpira wa wavu, riadha, mpira wa mikono. Sisi tuanze na riadha kwa Hanang kwa sababu tunayo record ukitafuta medali Tanzania hii Hanang tunaongoza, tunaomba tupewe kipaumbele cha kuangaliwa kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, michezo hii yote ya vipaumbele ambayo imewekwa, ili ifanikiwe naishauri sana Wizara washirikiane na TAMISEMI kuboresha eneo la michezo mashuleni, UMITASHUMTA na UMISSETA. Kazi inafanyika lakini ukienda kwenye shule zetu hakuna vifaa vya michezo. Bila vifaa vya michezo itakuwa ni hadithi kuimba, kwamba tutaibua vipaji, ukienda kwenye shule zetu mipira bado wana matambara shule nyingi. Tusaidiane kutatua changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu eneo la wataalam wa michezo, wenzangu wamelisema sana hili. Ukiangalia hakuna motisha yoyote wanayopewa Walimu ambayo wanajihusisha na michezo. Tuwatambue, tuwape motisha, lakini tuwape mafunzo mahusus ili wawafundishe vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amekuja na mpango mzuri wa shule 56 mahususi kwa ajili ya michezo. Mambo ambayo nimeeleza kwa ajili ya Hanang naomba shule ya kwanza ikajengwe Hanang. Wakashirikiane vizuri lakini bila kutatua changamoto ya upatikanaji wa wataalam, upatikanaji wa vifaa, bado changamoto ni kubwa. Wizara waanze na suala la kutatua changamoto ya vifaa na wataalam ili hizo shule sasa zitakapokuja ziweze kuwasaidia na tutengeneze vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia michezo yetu ukitoa kwenye mfumo huu wa shuleni, UMITASHUMTA na UMISSETA. Baada ya hapo, vijana wakienda vijijini wanazagaa tu. Kwa sisi wakulima na wafugaji kuanzia mwezi Aprili mpaka mwezi Desemba hatuna shughuli mahususi, kwa hiyo, vijana wengi wanakaa vijiweni. Lazima tuje na mkakati mahususi wa kuwapelekea michezo kwenye mitaa ni mkakati muhimu sana naomba ukatekelezwe. Waziri aje ili tuwaokoe vijana na changamoto za kukaa vijiweni. Vijana wengi wakienda vijiweni wanafundishana mambo ya ajabu. Ndio unakuta watoto wadogo wamejifunza kunywa pombe utotoni tunapoteza nguvu kazi ya Taifa kwa sababu hatuna shughuli za kuwaweka na kuwatoa kwenye vijiwe. Kwenye vijiwe kuna mambo mengi.

Mheshimiwa Spika, suala la ujenzi wa viwanja; kwenye bajeti ya Wizara wana viwanja saba ambavyo wanavikarabati, lakini mahitaji ya viwanja nchi hii ni makubwa sana. Tunachoomba kwenye eneo hili hatusemi Wizara wajenge viwanja kila sehemu, kwa sababu wanao uzoefu kwenye eneo la michezo, watutengenezee mpango ambao halmashauri zetu zitafuata wa PPP ili tuwekeze na viwanja hivyo viweze kujengwa, tuweze kuwaendeleza vijana wetu na tuwe na facilities za kufanya mazoezi, lakini ni sehemu ya kutambua vipaji vya vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaweza kutohoa kutoka kwenye Wizara ya TAMISEMI, wao walielekeza kila halmashauri inayokusanya zaidi ya bilioni tatu ijenge kituo cha afya cha milioni 400. Kwa sababu tunapoenda kwenye kituo cha afya tunaenda kutibu watu, lakini ukiwa na maeneo ya michezo unawakinga watu na maradhi. Sasa tuangalie namna ambavyo tunaweza kutohoa na namna ambavyo tunaweza kutekeleza, tukajaribu kuwekeza kwenye eneo la kuwakinga Watanzania na maradhi wakati huo huo tukiendeleza utaratibu wa kupelekea huduma kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili linawezekana wakiunganisha na mpango mahususi wa PPP na halmashauri zetu ili kuondoa burden kubwa na uhaba wa viwanja tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la utamaduni; ukiangalia sasa Watanzania kama wengi tunaanza kusahau asili zetu. Niombe Wizara ianzishe siku mahususi ambako watu watarudi kwenye tamaduni zao, kutakuwa na michezo mbalimbali, wasukuma watakuwa na mambo yao ya kiutamaduni, lakini Wairaki watakuwa na mambo yao ya kiutamaduni, Wakurya watakuwa na mambo yao ya kiutamaduni pia ndugu zangu Wanyaturu watakuwa na mambo yao ya kiutamaduni. Tuchague siku mahususi ili tuweze kuhamasisha tamaduni zetu. Hiyo itatusaidia sana ili angalau watu tusisahau na tamaduni zetu zisipotee.

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa kutoa pongezi kwenye makampuni ambayo yanaweka au wanafadhili kwenye michezo.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nicodemas Maganga. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa tu Mheshimiwa mchangiaji, mchango wake ni mzuri sana, naomba Wizara iuzingatie. Kwa kweli kwenye utamaduni hapo kama kweli Wizara ikipashika vizuri, Wasukuma tunacheza ngoma vizuri sana. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mhandisi Hhayuma. (Kicheko)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nafikiri anaongezea kwenye yale ambayo nimesema, ni mambo ya msingi sana ambayo Mheshimiwa Maganga ameyagusia.

Mheshimiwa Spika, namalizia kwa kusema, wale ambao wanawekeza kwenye michezo, wanaofadhili michezo mbalimbali, wanaofadhili sanaa, tutambue mchango wao. Nasema tu kwa wachache tu, nitaje Azam, Mohamed Enterprises, Sports Pesa, juhudi zao tumeziona. Huko nyuma Serengeti waliwekeza kwenye michezo, lakini Tanzania Breweries pia wamewahi kuwekeza kwenye michezo na wengine ambao wanagusa maeneo hayo. Hao wadau tutambue mchango wao, utatuhamaisha wengi zaidi kwenye eneo la michezo kwa sababu inagusa zaidi upande wa sekta binafsi. Tuweze kuhamasisha wengi ili kwenye sekta ya michezo kuwe na fedha ya kutosha na tuweze kuendeleza vipaji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)