Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji katika hotuba ya bajeti ya Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Wizara ambayo ipo mezani kwetu tunayoijadili leo ni Wizara inayoenda kugusa hali halisi za watanzania kwa jina lingine kule mitaani hii tunapenda kuita Wizara ya kitoweo kwa sababu Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwa bajeti yako kwa kiasi fulani imefanya kazi na imejibu hoja kwa kiwango kikubwa ambacho Wabunge tulitarajia kusikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri wewe ni rafiki yangu sana na urafiki wetu umekuja kutokana kwamba wewe unatoka eneo linalotoka wavuvi na mimi natoka maeneo yanayotoka wavuvi kule Zanzibar. Lakini ni ukweli kabisa sina lengo la kuzuia shilingi kwa namna yoyote ila wakati ambapo utapoweza kuwasilisha bajeti hii na kuja kutuhutubia kwa mara ya mwisho kufunga hotuba yako ukishindwa kutuelezea yale matarajio ambayo Wabunge sisi tulitarajia kuyasikia yawepo katika hotuba yako basi sisi tutaacha kujadili hotuba yako baadaye tutakuja yale ambayo wananchi wametutuma tuje tuyazungumzie hapa kwasababu wao ndio wanapenda wayasikie hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni miongoni mwa nchi tatu bora ambazo zimejaaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji katika Bara la Afrika, Tanzania tumebahatika kuwa na mito mingi, kuwa na bahari kuu kuwa na maziwa mengi tu inasemekana hata chanzo cha mto Nile kinapatikana Tanzania na ndio maana nchi za jirani zetu zinazotuzunguka kama vile nchi za Malawi, Kongo, Zimbabwe zinategemea sana kupata samaki wao kupitia Tanzania kwa mfano Kongo na Malawi ni wafanyabiashara wakubwa sana wa dagaa kwa nchi ya Tanzania naizungumza hii kwasababu ya kuonesha jinsi gani umuhimu wa sekta hii ya mifugo ilivyo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake dagaa kwa kiasi kikubwa hata akinamama na wavuvi wadogo wadogo wana uwezo wa kuifanya hii shughuli, licha ya umuhimu wa sekta hii lakini bado sisi kama Serikali hatujawa serious katika kuwekeza na kutafuta wawekezaji watakaoweza kuja kui-support sekta hii na sina doubt na utendaji wa Mawaziri. Kwasababu wakati mwingine tunaweza kuwabebesha mzigo mkubwa Mawaziri nimejifunza kitu leo Waziri wa Uvuvi na Mifugo unatuwasilishia bajeti katika bajeti iliyopita utekelezaji wake maana yake fedha iliyokuja katika utekelezaji wa miradi ya bajeti ni asilimia 3.3 katika miradi ya maendeleo lakini kwenye mishahara asilimia 66. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi haya tunayoyapanga kwenda kutekeleza kama fedha usipopewa unakwenda kutekeleza nini, maana yake wakati mwingine tuna uwezo wa kumbebesha lawama mtu ambaye hastahili ingawa sio lengo, sasa kama kweli tunataka kunyanyua mifugo yetu kama kweli tunataka kuendeleza sekta ya uvuvi ni lazima Serikali tuangalie utaratibu wa kuwawezesha wavuvi wetu, hivi sheria na hizi taratibu za uvuvi ambazo zinaonekana kwamba ni kikwazo kwa wavuvi wadogo na wavuvi wakubwa hakuna haja ya kuendelea nazo Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu leo hii unaweza ukatunga sheria ukamwambia mtu usivue sehemu fulani, nyavu fulani usitumie kuvua lakini ukashindwa kumpa mbadala wake hakuna anayependa kufanya uhalifu lakini mazingira wakati mwingine yanalazimisha na sheria ngumu zikachangia katika hayo. Mheshimiwa Waziri Serikali ione haja ya kuwarahisishia upatikanaji wa pembejeo za uvuvi itafute njia na ikae na wawekezaji watakaoweza kuisaidia sekta hii ya uvuvi watakaoweza kuwapatia wavuvi wetu vifaa vya uvuvi kama vile mashine, na pembejeo nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wavuvi wetu wanavua uvuvi ambao ni wa holela mtu anatoka anakwenda kuvua lakini hajui wapi anapokwenda anakwenda kubahatisha hajui samaki wapi anakwenda kuwakamata huku tutoke kwenye njia hizi za local sasa hivi twende na utaratibu unaokubalika tulingane na wavuvi wenzetu wa dunia za nchi nyingine. Katika hili nioneshe mfano mmoja nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kwa jitihada kubwa anazozifanya kupitia sera ya uchumi wa bluu lazima tumpongeze kwa hilo. Yeye sasa hivi ameshaandaa takribani boti 557 kwenda kuwawezesha wavuvi wadogo wadogo na vi-holi vile vya kuvunia mwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hali kama hii wananchi wamekuwa wanavua maji madogo samaki wengi tunawaacha katika uvuvi wa maji marefu au bahari kuu lakini kule watafikaje? Vyombo wanavyotumia ni mtumbwi, mtumbwi hauwezi ukautumia kwa uvuvi wa maji marefu au uvuvi wa bahari kuu na ndio maana unasikia kesi nyingi zinakuja, Mamba kala Mtumbwi na abiria aliyekuwepo ndani yaani huu ndio ukweli ulivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu sasa katika mazingira kama hayo ndio tunasema tunawathamini na kuwa-support wavuvi wetu sasa katika suala hili bajeti ya killimo ipo vizuri kwasababu asilimia kubwa imewagusa wananchi wadogo lakini sekta nyingine ipi inayowagusa wananchi wadogo na wakombozi wa maskini, ni sekta hiyo ya uchumi wa bluu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wale watu ambao wanaonekana hawana ajira watu ambao wanaharakati wanaona kwamba bamba gumu kwa upande fulani wa kimaisha wanajikita katika sekta hizi ya uvuvi na mifugo. Maana yake na sisi kama Serikali tuwatafutie njia sahihi tukae na tujue tunawa-support vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikwambie kitu kimoja tujifunze kutoka kwa wenzetu nchi kama Norway iliyokuwepo Bara la Ulaya ni miongoni mwa nchi zinazojulikana kama Nordic Countries hii nchi inazalisha gesi nyingi nchi hii inazalisha mafuta mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kiukweli asilimia 70 ya uchumi wao inategemea uvuvi kwanini, wao wamewasaidia wavuvi wao na wakaipa thamani inayostahiki sekta hii ya uvuvi. Mheshimiwa Waziri katika hili unapozungumzia suala la zima la uvuvi, kilimo, ufugaji maana yake unazungumzia vitu tofauti na mazingira yatatofautiana, kwa kule Zanzibar sisi sekta ya uvuvi ndio mkombozi wetu, kwa sababu ardhi yetu sisi ni ndogo ukilinganisha na idadi ya watu. Lakini kwa huku upande wa bara kilimo lazima kitakuwa na tija na kitapewa support kubwa sasa sisi tunategemea hii sekta ya uvuvi zaidi ikilinganishwa na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hali kama hii Mheshimiwa Waziri kumekuwa na changamoto kubwa mno kwa wavuvi wetu hususani katika masuala haya ya hawa wanaohusika na huu uvuvi wa bahari kuu, changamoto za leseni ni bei kubwa mno Mheshimiwa Waziri kwa maskini, leseni za uvuvi wa bahari kuu maana yake ni changamoto kwa wavuvi, lakini isitoshe suala la kuwachaji mara mbili wavuvi wanaotoka Zanzibar regardless aina gani ya uvuvi kwa sababu vyombo vile wanakuwa wamevikatia leseni wanapokuja huku wanachajiwa tena leseni, matatizo kama haya ni masuala ya kukaa na kushirikiana na wale wenzenu wa Zanzibar kutafuta zile changamoto kuondosha hili migongano isiyokuwa ya lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri najua Wizara yako ukiangalia waajiriwa wengi sio rasmi na hii ningependa unipatie ufafanuzi kitu kimoja Mheshimiwa Waziri, kuna suala zima la mvuvi na changamoto zinazowakabili lakini research fupi niliyoifanya kwamba changamoto hizi zinatokana kwamba wewe na Wizara yako humjui mvuvi ni nani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii ninazungumza na kama sio kweli basi ningeomba unifafanulie hakuna sheria ya Tanzania hii inayomtafsiri moja kwa moja maana ya mvuvi ni nani, naizungumza hii kwa hoja yangu. Hapa unaomba fedha kwenda kuwasaidia wavuvi unaomba fedha hizi kwenda kuwasaidia wavuvi lakini wavuvi ni nani wakati hatuwatambui katika sheria, umeweka tu katika sheria taratibu za uvuvi ukaweka aina za uvuvi lakini hakuna maana leo hii inapotokea fursa za mikopo…

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako Mheshimiwa.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja inapotoka fursa za mikopo zinaenda kwa wafugaji na wawindaji wa paa zile nyavu badala ya kwenda kuwindiwa baharini kwa sababu mtu leo atoke na mshipi aende kuingia chomboni utahesabu kama ni mvuvi kwa mujibu wa sheria zenu. Sasa hizi fedha badala ya kuomba kwenda kuwasaidia hawa wavuvi tuletee yaani omba fedha hizi kwa ajili ya kurekebisha kwanza angalau hizi changamoto ndogo ndogo zinazotokana na… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashirikia kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)