Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Uvuvi na Mifugo. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza, niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu na Watendaji wote katika Wizara kwa kazi wanayoifanya na hasa kwa hotuba yao waliyowasilisha leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 wakati kama huu na wakati nachangia hotuba ya Wizara hii, nilishauri juu ya umuhimu wa Wizara kuwekeza kwenye ufugaji wa samaki kupitia vizimba. Nimefarijika angalau kwenye hotuba iliyosomwa leo kuna mabadiliko yanaonekana angalau jitihada zimeweza kufanyika na kuongeza idadi ya vizimba, dhamira ikiwa ni kuimarisha ufugaji wa samaki na kuongeza mazao ya ziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado hatujafanya vizuri sana kwenye uzalishaji wa mazao ya samaki na ndiyo maana kama mchangiaji mmoja alivyosema hapa wakati anachangia ukiangalia mazao tunayozalisha na kusafirisha kwenda nje Tanzania pamoja na advantage tuliyonayo ya kuwa na maziwa, kuwa na bahari, bado hatujafanya vizuri sana. Ndiyo maana ukiangalia kwenye sources mbalimbali katika idadi ya nchi ambazo zinazalisha na kusafirisha samaki kwa wingi, kwa mfano Morocco ndiyo inaongoza kwa Afrika, Namibia, South Afrika, Mauritius na Senegal, lakini Tanzania kwenye tano bora bado hatumo, bado hatujafanya vizuri sana. Pamoja na kwamba kwa mwaka huu kwa takwimu zilizosomwa na Mheshimiwa Waziri, tumezalisha metric ton karibu 415,000. Mwaka juzi 2020 tulikuwa na metric ton karibu 393,000, ninaamini bado tunastahili kufanya zaidi ya hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri tu kwamba pamoja na jitihada hizi tunazozifanya kuimarisha ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba, ni vizuri tukaangalia vile vile athari hasi za vizimba ili tuweze kuzifanyia kazi zisije kuathiri ufugaji wa asili wa samaki. Kwa sababu tunaweza kuwa tunalalamika samaki wanapungua, kumbe ni matokeo ya athari hasi za vizimba hizi; kunaweza kuwa na athari za kijenetiki na kadhalika. Kwa hiyo, ni vizuri tukaangalia vile vile kiutafiti kama zipo athari hizo, basi tuweze kuzifanyia kazi ili wakati tukiendelea na mpango huo ili wavuvi wetu wa asili wasije kuathirika na ufugaji wa vizimba ambao tunawekeza hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nilitaka kulichangia ni juu ya uvuvi wa samaki aina ya dagaa. Dagaa ni samaki wanaopatikana kwenye maziwa tuliyonayo kwenye nchi yetu hii; Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa na Ziwa Victoria; na kwa sehemu kubwa inatoa ajira nyingi sana kwa wananchi wetu hasa akina mama na vijana. Hata hivyo kumekuwa na shida kubwa sana, na kwa mtizamo wangu Serikali haijawekeza ipasavyo katika kuongeza thamani ya mazao ya samaki hawa aina ya dagaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, kwa mfano, mwaka 2021, Shirika la Chakula Duniani (FAO) kwa mujibu wa ripoti yao iliyotolewa mwezi Desemba inaonesha samaki hawa aina ya dagaa, pamoja na kuzalishwa lakini post-harvest loss ipo kwa karibu asilimia 16 na wakati wa masika/wakati wa mvua inaenda mpaka asilimia 60 jambo linaloifanya Serikali yetu kukosa mapato ya karibu Shilingi bilioni 50 kila mwaka kwa sababu ya kushindwa kuwekeza kwenye uvuvi huu na kuweza kuongeza thamani ya mazao haya yaweze kuuzwa na kusafirishwa nje ya nchi na kuweza kusaidia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naombe sana kama nilivyotangulia kusema, hii ni ajira kubwa sana ya wananchi hasa vijana na akina mama. Kwa takwimu mlizotoa kwenye hotuba yenu, wananchi karibu milioni nne wanapata kula yao na maisha yao kutokana na uvuvi. Pia uvuvi huu wa dagaa unaajiri karibu asilimia 70 ya wananchi na kutengeneza mzunguko mkubwa sana wa kipato kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali kupitia kwenye Wizara, wekezeni kwenye uvuvi huu wa dagaa mwasaidie wananchi wetu, tusiwe tunatoka tu kwenda kufanya operation na kuathiri maisha ya uvuvi wa watu wetu. Tuwekeze vile vile, tuweze kuwaelimisha na kuongeza mitaji yao wafanye uvuvi wa kisasa na kuongeza thamani ya mazao ya samaki hawa hasa dagaa. Kwa sababu ikiongezeka thamani ya dagaa kama nilivyotangulia kusema, itaboresha sana maisha ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mchango wangu ulikuwa kwenye maeneo hayo mawili. Naomba sana wekezeni kwa kiwango kikubwa sana kwenye uvuvi wa dagaa. Tunapokuwa tunapoteza kwa mwaka Shilingi bilioni 50, ni pesa nyingi sana ambazo tungeweza tukafanyia mambo mengine mengi. Kwenye eneo kama la kwangu la Ukerewe pale, sehemu kubwa, zaidi ya asilimia 90 ya vijana na akina mama wanapata maisha yao kutokana na uvuvi wa dagaa, tuwawezeshe, tuwasaidie, tuongeze thamani ya mazao yao. Leo dagaa wanaovuliwa wanaanikwa kwenye mchanga, wakati mwingine wakati wa mvua hawakauki, inaathiri kipato kwa ujumla na maisha ya wananchi wa eneo langu la Ukerewe, naamini na kwenye maeneo mengine katika Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Serikali kupitia Wizara wekezeni kwenye eneo hili muweze kuwasaidia wavuvi wetu wa dagaa tuongeze thamani ya mazao yao, itasaidia sana uchumi wao na uchumi wa Taifa kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naungana mkono hoja. Ahsanteni sana.