Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Kwanza kabisa mimi naomba nisiipongeze Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wetu wa Ukanda wa Pwani hali zao ni duni sana kiuchumi na wote ni mashahidi. Mkoa wetu wa Tanga tuna bahari Wilaya ya Mkinga, Tanga, Muheza na Pangani katika Mkoa wetu wa Tanga. Mkakati waliokujanao mwaka jana ambao ndiyo mwaka wa fedha huu tunamalizia, walikuja na mikakati mizuri sana na mipango mizuri. Ukisikiliza mikakati yao ya mwaka jana mwaka wa fedha 2021/2022 na mipango yao ya mwaka 2021/2022 unasema basi hawa Wavuvi sasa hawaendi kutafuta kazi nyingine ya kufanya. Lakini cha kusikitisha mikakati ile ya mwaka jana ambayo walikuja nayo hakuna mkakati hata mmoja ambao wameutekeleza. Sasa Napata wasiwasi kama mikakati ile yam waka wa fedha 2021/2022 haikutekelezwa, sasa hivi tunakwenda kupitisha bajeti ya 2022/2023, sasa sijui hiyo watatekeleza vipi napata wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ukiangalia mikakati yao ya mwaka jana walituambia kwenye Bunge hili wataweka miamba ya kuvutia Samaki ili kuongeza uzalishaji kwenye ukanda wetu ule wa pwani kwa Mikoa ya Tanga, Pwani, Dar-es-Salaam, Lindi na Mtwara. Hiyo miamba siyo kuiona tu hata kuisikia huko Pwani mimi ninakotoka sijaisikia! Sijaisikia na haipo. Hata Waziri wakati anasoma hotuba yake hakutaja kabisa pia hakutaja kwenye mwaka wa fedha huu anaohama nao kuwa labda tulishindwa mwaka huu, lakini mwaka unaokuja tutafanya, hawakusema! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye bajeti yao ya mwaka 2021/2022 walituahidi hapa watatengeneza vichanja kwa ajili ya kukaushia samaki na dagaa ili kuhakikisha wanapunguza upotevu wa mazao haya ya samaki. Baada ya kutuahidi yale kwa sababu niliuliza mpaka swali mwaka jana na nilijibiwa hapa nikaambiwa vichanja vile vinapelekwa, mimi nikaenda kule nikawaambia wanawake wenzangu wa Mkoa wa Tanga jamani jipangeni vichanja vinakuja na watu wamejiandaa vikundi viko kule wanasubiria vichanja. Vichanja mpaka leo havijaenda, imebakia miezi miwili tunamaliza hii bajeti hakuna kichanja kimekwenda. Sijasikia tena kwenye mpango wao hata kwenye hotuba sijasikia kuwa mwaka jana tuliahidi hivi lakini tumeshindwa na mwaka huu tutaendelea. Sijasikia na haipo na vichanja havipo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mwaka jana hapa walituahidi wakasema wataongeza uzalishaji wa barafu na kujenga cold rooms kwa ukanda, tena walisema siyo cold rooms tu cold rooms za kutosha kwa Ukanda mzima wa Pwani kuanzia Tanga mpaka Mtwara. Mpaka leo hivi ninavyosema sijaona cold rooms hata moja hata tu ya mfano huko ninakotoka haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia walituahidi hapa watakuja kuweka hizi cold rooms kwa sababu kama tunavyofahamu mazao ya samaki huwa yanaharibika kwa muda mfupi sana, sisi tunaotoka Ukanda ule wa Pwani samaki huwa hawavuliwi siku zote ndani ya mwaka mzima, kuna siku samaki wanapatikana kwa wingi na kuna siku samaki hawapatikani kabisa, kwa hiyo lengo lao lilikuwa ni zuri kuwasaidia hawa wavuvi kwamba, zile siku wanazopata samaki kwa wingi wangeweza kuhifadhi hata zile siku ambazo hawapati samaki bado wangeweza kuendelea kufanya biashara, lakini haipo, haijatekelezwa, sijaisikia kwenye mpango uliopita na sijaisikia kwenye mpango huu tunaokwendanao, sasa sijui imepotelea wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia walituahidi hapa mwaka jana watakuja kujenga soko la kisasa la samaki, baadhi ya maeneo likiwepo soko la samaki la Kipumbwi, Wilayani Pangani. Nalo nimesikia wamelisema, mwaka jana walisema watajenga kwa bajeti ile ya 2021/2022, hakuna msingi uliojengwa, hakuna hata soko lililoanza kujengwa. Kwenye bajeti hii wamesema tena tutajenga soko, wameliweka tena kwenye bajeti ya 2022/2023. Kwa hiyo, mwaka jana hata msingi tu, labda wangesema tumeanza tutaendelea, hata msingi tu haupo! Kwa hiyo, sasa napata wasiwasi sana na bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti yao pia ya 2021/2022 walituahidi hapa watanunua boti ya uvuvi kusaidia kule wavuvi wetu, sasa safari hii sijalisikia, badala yake sasa wamekuja kutuambia watanunua meli kubwa za uvuvi. Sasa kama yale boti hazikununuliwa hivi wataweza kweli kununua meli? Hapo napata wasiwasi? Badala yake sasa wametuambia walinunua boti za doria, siyo ya uvuvi tena. Wamesema tumenunua boti za doria, sasa nikawa sielewi nachanganyikiwa kabisa! Kwa hiyo, boti zilishindikana safari hii tutanunua meli kubwa za uvuvi, sijui ni meli tatu, sijui tano? Sasa napata mashaka kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Wizara kwa sababu mambo mengi hawajayatekeleza yale waliyotuahidi mwaka jana, naomba sasa watueleze mikakati yao hasa madhubuti ya mwaka huu 2022/2023 watakwenda kufanya nini ili kuongeza uzalishaji wa wavuvi hawa kwa maeneo yetu yale ya Pwani na maeneo mengine hata ambayo siyo ya Pwani lakini kwa wavuvi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia watatuhakikishia vipi, ni upi mkakati wao wa kuhakikisha wanawaunganisha wavuvi hawa na masoko? Waje hapa tuwe na mkakati wa uhakika, wavuvi wanahangaika sana, wanavua samaki wanazunguka nao kutwa nzima, mara wameoza, anakwenda anamwaga samaki. Sasa sielewi wakati kuna nchi kibao za jirani hazina kabisa bahari na wangependa wapate samaki kutoka kwetu, sasa sijui, Waziri aje na mkakati. Ni mkakati gani wa kuhakikisha wanawaunganisha wavuvi wetu na masoko ya uhakika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia waje watumabie hapa ni mkakati gani wanaokuja nao wa kuhakikisha wanawawezesha wavuvi wetu kuongeza thamani mazao yao haya ya bahari? Waje hapa na mkakati wa uhakika watuambie ni mkakati gani wameuweka wa kuhakikisha watawaunganisha hawa wavuvi wetu na taasisi hizi za kifedha ili waweze kupata fedha za kuendelea kufanya shughuli zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wetu wale wa Ukanda wa Pwani pia wamehamasika sana kulima zao hili la mwani. Kwenye hotuba ya Waziri sijasikia kabisa akiongelea, hajagusa kabisa! Lakini ninawashukuru Wizara walikuja kama mara mbili, mara tatu, kupitia Naibu Waziri wa Uvuvi kwa wakulima wetu wale wa mwani waliwaletea vifaa kama vile viatu na kamba. Waliwawezesha, lakini changamoto bado ni kubwa sana, zao hili la mwani kwa Wabunge wasiofahamu ni zao muhimu sana, linatengeneza vitu vingi sana. Kwa mfano tunaweza kutengeneza sabuni ya unga…

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako Mheshimiwa.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia hili zao la mwani tunaweza kutengeneza sabuni ya unga, sabuni ya maji, sabuni ya kipande, mafuta ya mgando, mafuta ya maji na juice pia, Mheshimiwa Ulega anafahamu. Kwa hiyo, ninaomba sasa Wizara waje watuambie watawasaidiaje hawa wakulima wa mwani kupata masoko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba niunge mkono hoja. (Makofi)