Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kupata nafasi ya kuchangia katika Bajeti hii Kuu ya Serikali kwa mwaka 2023/2024. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ya kuleta maendeleo anayoifanya katika nchi yetu. Niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara. Kazi mnayofanya ni kubwa na Mungu aendelee kuwatia nguvu ya kulitumikia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa sababu ni sikivu na inasikiliza sana maoni ya Waheshimiwa Wabunge. Waheshimiwa Wabunge wengi walilalamika juu ya faini za bodaboda na zilipunguzwa kutoka 30,000 mpaka 10,000. Mimi leo nakuja mbele yako kuomba sasa Wizara na Serikali waangalie pia faini zinazochajiwa katika bajaji za mizigo. Bajaji za mizigo zinachajiwa faini ya shilingi 250,000 kwa kukosa stika ya usafirishaji. Hii imekuwa ni kwa sababu bajaji hizi kwenye sheria zimewekwa kwenye class moja na malori ya mizigo. Ni kitu cha ajabu sana kuweka kifaa kinachonunuliwa shilingi milioni tano mpaka sita kwenye class moja ya malipo sawa na kifaa kinachonunuliwa zaidi ya milioni 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkurugenzi wa LATRA alitangaza kwamba sasa watu hawa waanze kuchajiwa faini ya shilingi 25,000 lakini jambo hili halitekelezwi na watendaji wa chini na hii ni kwa sababu ya mapungufu yaliyoko kwenye sheria. Mimi niiombe Serikali kama tulivyosikia kilio cha waendesha bodaboda tusikie kilio cha waenda bajaji za mizigo. Hawa ni vijana wanaotaka kujikomboa, wanaotaka kujikwamua, tuwashike mkono. Shilingi 250,000 ni fedha nyingi tupunguze fedha hii ifike shilingi 25,000 na tu-reflect mapungufu haya kwenye sheria zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze pia Serikali kwa sababu ilisikia kilio cha wafanyabiashara hasa wa soko la Kariakoo kwenye kero mbalimbali walizokuwa wanapitia kwenye biashara na mengi yamerekebishwa; mimi niwapongeze sana. Hata hivyo niiombe Serikali yetu, changamoto zilizoelezwa na wafanyabiashara wa Kariakoo ni changamoto ambazo wanazipitia wafanyabiashara sehemu zote nchi nzima. Kero walizozieleza wafanyabiashara wa Kariakoo ni kero ambazo wanazipitia wafanyabiashara almost wote nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusisubiri wafanyabiashara wa sehemu nyingine pia wagome ili twende tukatatue changamoto hizo. Mimi naomba yale mliyoyafanya kwa wafanyabiashara wa Kariakoo yaende yakafanyike kwa wafanyabiashara wengine wote nchi nzima. Tutoe mafunzo na maelekezo kwa watumishi wetu wa TRA, lugha wanazotumia na approach wanayotumia kwa wafanyabiashara wetu si rafiki sana, waende wakarekebishe ili wafanyabiashara na TRA waanze kufanya kazi kwa harmony na kwa amani kujenga nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kati ya vitu ambavyo Mheshimiwa Rais ameendelea kuwa anasisitizia ni namna gani ambayo tunaweza tuka-widen tax base kwenye nchi yetu ili tusiumize wale wachache wanaoendelea kutuchangia na kutusaidia katika kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina jambo la kushauri, kuna kitu kinaitwa carbon credit, alizungumza Mheshimiwa Kakoso. Wilaya ya Tanganyika peke yake kwa vijiji nane tu inalipwa takribani bilioni nne mpaka tano kwa malipo haya ya carbon credit. Sasa hivi dunia inakoelekea hot topic ni climate change, mabadiliko ya tabianchi; na itaendelea kuwa hot topic kwa sababu ndiko tulipo na ndiko tunakoelekea. Sasa, kwa nchi kama za kwetu za uchumi wa chini tutaendelea kuwa wahanga wakubwa wa mabadiliko haya ya tabianchi. Namna gani tunaweza kufaidika na wale wanaochafua mazingira kutusaidia na sisi kuweza ku-deal na athari za mabadiliko ya tabianchi ni kupitia hiki kitu kinachoitwa carbon credit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hi kuna nchi, nitolee mfano nchi ya Ghana, kwa miezi sita tu kuanzia Juni mpaka Desemba 2019 wamepokea malipo ya dola za kimarekani milioni 4.9 kwa carbon payment, miezi sita tu; na wao wamelipwa fedha hizi kwa hekta milioni sita tu za misitu. Takwimu katika nchi yetu zinaonesha kwamba sisi tuna hekta milioni 48 za misitu. Kama tukisema tunaanza ku-tap malipo katika carbon credit za misitu hii hekta milioni 48 naamini tunakwenda kukusanya fedha nyingi sana. Kuliko kuendelea kuongeza kodi kwa wale walipa kodi wachache kuendelea kuwaumiza kuna namna nyingine ya kuongeza tax base kwa kupokea fedha kutoka katika rasilimali ambazo tumeshapewa na Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amekuwa kinara wa mfano wa namna gani tunaweza yukaongeza mapato kupitia rasilimali zetu kwenye Royal Tour. Sisi twende mbele zaidi, tuunge mkono juhudi zake, tutumie hizi carbon credit kuzalisha mapato kwa ajili ya kuendelea kuleta maendeleo na kukabili matokeo mabaya au matokeo hasi ya mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuchangia katika Bunge hili na nitaendelea kusema; kwamba hatuwatendei haki wakandarasi wazawa wa ndani. Ripoti ya CAG inaonesha kila mwaka kwamba wakandarasi hawa hatuwalipi kwa wakati. Lakini ni uhalisia, hawa watu wako katika majimbo yetu, tuna malalamiko ya kutosha. Lakini kubwa zaidi wale ni vijana wenzangu na hivyo nina jukumu la kuwasemea. Nilisema na nitaendelea kusema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amekwishakutoa maelekezo, tutoe kipaumbele kuwalipa wakandarasi wa ndani. Hawa ni wazalendo, fedha tunazowalipa zinabaki hapa ndani, mzunguko wake unabaki hapa ndani, wanaajiri Watanzania wenzetu. Tusiendelee kufilisi Watanzania wenzetu kwa kuchelewa kuwalipa ilihali hawa watu wana malipo kwenye commercial banks. Ninaomba sana Serikali twende tukaangalie suala hili tuwalipe kwa wakati wakandarasi wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mimi niende kwenye fedha za 4:4:2. Ukurasa wa kumi wa bajeti yetu unaonesha kwamba Serikali iko katika mchakato wa kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais, na pale tutakapokuwa tayari kukamilisha utaratibu wa kupitishia fedha hizi benki utakuja kutupa taarifa. Mimi niwapongeze sana kwa hatua ambazo mnaendelea nazo. Nina machache ya kushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati vijana, wanawake na watu wenye ulemavu wanakwenda kuchukua fedha katika halmashauri zetu, fedha hizi za 4:4:2 hawakujua kwamba benki zipo, walijua; lakini walikwenda kule kwa sababu kuna changamoto kadha wa kadha kwenye kupata fedha kwenye benki zetu. Kuna changamoto za muda, ukiritimba, gharama, kuna rushwa na nyingine nyingi. Mimi niiombe sana Serikali, inapokuwa inaangalia namna gani ya kupitishia fedha hizi tuangalie pia namna ya kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto hizi, ili hawa watu ambao tunataka tuendelee kuwawezesha kiuchumi kupitia sasa kwenye benki zetu tuhakikishe tunaendelea kuwajengea mazingira yaliyo salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana issue ya gharama, kuna gharama kubwa sana na usumbufu mkubwa sana kwa mtu kwenda ku-apply mkopo benki. Cha kwanza tusiwaengue maafisa maendeleo moja kwa moja, tuendelee kufanya kazi kwa karibu sana kati ya benki ya maafisa maendeleo. Pili benki sasa tunakwenda kuzipatia mtaji ambao wao hawana hata ile cost of funds, tunakwenda kuwaongezea capital kupitia hizi fedha za 4:4:2. Niwaombe sasa ikiwezekana zile gharama za mikopo benki wazibebe wenyewe, wasiwabebeshe vijana wanawake wala watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe sana suala la muda, vijana wengi pia hawana dhamana, benki nyingi zinahitaji dhamana, tuliangalie suala hili. Kule kwenye halmashauri zetu walikuwa wanatubeba kwa nafasi zetu kama tulivyo. Leo hii Mheshimiwa Bashe anajaribu kuanzisha BBT ili tusaidie vijana kumiliki ardhi tupate dhamana kuingia benki. Sasa niombe sana hizi fedha zinapopitishiwa benki tuwe makini na kale kautaratibu ni jambo zuri, lakini tuhakikishe pia hatuumizi wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa utaratibu huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni zuri, mimi nampongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu ni kweli kulikuwa na changamoto nyingi, CAG ameonesha upotevu mkubwa uliokuwa unatokea kwenye halmashauri zetu. Tunaamini fedha hizi zikipita huku zinakuwa na ufanisi mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe kuwepo na timu za watu ambao wataendelea kuwa-monitor hawa vijana. Hata kama wakishapewa hizi fedha waendelee kuwafatilia ili wahakikishe kwamba fedha hizi zinazaa na zinakuwa na ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia Mheshimiwa Rais nimpongeze sana na nimshukuru kwa sababu alitenga fedha shilingi bilioni 20 ili kuhakikisha mikoa ya Kanda ya Ziwa inaweza kunufaika na rasilimali ziliozoko katika Ziwa Victoria. Walikuja watu wa wizarani tuliunda vikundi vya vijana katika Mikoa ya Mwanza, Kagera, Simuyu, Geita na Mara. Vikundi viliundwa vikawa vetted tukaandika maandiko, maandiko yakaenda Wizarani, yakapitiwa yakafanyiwa vetting watu wa Wizarani wakaja wakatoa mafunzo kwa vijana na mwisho wa siku ikaja list ya vikundi ambavyo vime-qualify kupata fedha na idadi ya fedha ambayo vikundi hivyo watapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza cha kushangaza tarehe 13 Juni wamekuja tena watumishi wa Wizarani kule Mwanza kuzungumza na vijana; na badala yake wamekuja kutuambia mambo ambayo ni tofauti kabisa na vile tulivyokuwa tumekubaliana. Vikundi hivi vilitakiwa vianze kufuga samaki kwa njia ya vizimba kwenye Ziwa Victoria. Kwenye makubaliano ya Mwanza vikundi hivi kwenye fedha zile milioni 130 kwa kila kikundi, vilitakiwa vipewe vizimba, samaki, chakula pamoja fedha kwa ajili ya kufanya doria na kutunza vile vizimba kwa miezi nane ili baada ya hapo fedha hizi waweze kuzirejesha, na fedha hizi zilikuwa zinapitia TADB.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza wamekuja watumishi wa Wizara kuja kuwaambia vijana kwamba tofauti na walivyokuwa wamekubaliana, kwamba venders wa hivi vizimba, chakula cha Samaki na vifaranga itakuwa ni makubaliano kati ya vijana na Wizara; na fedha ile hawatapewa vijana itaenda kulipwa kwa wale venders moja kwa moja; na jambo hilo vijana wamekubali. Changamoto inakuja watumishi wa Wizara wamkuja kuwaambia vijana kwamba wao wenyewe ndio watakaochagua venders. Wao ndio watachangua venders wa vizimba, Samaki, na chakula. Lakini experience inatuonesha kwamba watu wengi wameshaanza kufuga Samaki kwa vizimba na wamefeli. Wamefeli kwa sababu ya uduni wa ubora wa vizimba, uduni na udumavu wa vifaranga pamoja na chakula kisicho bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii watu Wizara wanakuja kutuambia tutafanya haya, kama hamtaki acheni. Je, hii ndiyo lugha ambayo Mama Samia amewatuma kuja kuwaambia vijana? Hii ndiyo lugha ambayo Mama Samia ametoa bilioni 20 ili vijana waje waambiwe hivyo? Leo hii vipi kuhusu hivi vizimba vikiletwa na havina ubora? Je, vifaranga vikiletwa na vikadumaa au chakula kisicho na ubora. Mikopo hii wanabebeshwa vijana wao ndio walipe, wanalipaje vijana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka ni kwamba makubaliano ya mwanzo yabaki vilevile. Vijana wakae na kujadiliana venders na Wizara ili wale watakaoridhia ndio wapewe tender ya kuleta hivyo vitu ili hata mwisho wa siku hivi vitu vikiwa si bora vijana waweze ku-own makosa yao na kulipa fedha hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia vijana wamekuja kuambiwa na watumishi wa Wizara kwamba hatutalipa tena fedha kwa ajili ya doria, fedha za kujikimu kwa kila kijana kwa hii miezi nane wakati mnafatilia huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongelea mradi wa miezi nane, vijana wakati wanafatilia mradi huu watakuwa wanatumia nini? tunatishia vijana kuweza kutekeleza miradi hii ili kwenda kutafuta fedha za kujikimu. Lakini fedha hizi hawapewi bure ziko ndani ya mikopo ambayo maandiko ya wizara yalikuwa yameshakubalia kuwapa fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, samaki ni kitu ambacho soko lipo. Mwanza sasa hivi as we speak wanaboresha airport iwe ya kimataifa. Tuna Daraja la Magufuli ambalo linatusaidia kutoa Samaki kupeleka nchi za jirani. Tuna SGR ambayo pia itatusaidia kusafirirsha bidhaa hizi kwa wepesi. Tuna viwanda vingi sana vya minofu ambavyo mpaka sasa malighafi haitoshi. Zao hili tunaloenda kutoa kwenye Ziwa Victoria wala soko lake halina mashaka. Kwa nini Wizara inapata kigugumizi kutoa fedha hizi kwa vijana kama tulivyokuwa tumekubaliana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zinasema fedha hizi milioni 130 kwa kila kikundi zimetoka, hizi fedha ambazo Wizara sasa inasema hazitowapa vijana zimeenda wapi? tunahitaji tuambiwe na hii lugha ya kuwaambia vijana kwamba tutafanya hivyo la sivyo kama hamtaki acheni, basi acheni kwa sababu mnawatengenezea vijana bomu la kuwapa miradi ambayo itashindwa kuwa sustainable. Leo hii tunatengeneza vile vizimba vya zaidi ya milioni 60 mpaka 100 kuweka ndani ya Ziwa Victoria halafu unamnyima kijana milioni mbili tatu ya kijikimu ili kukifatilia kile kizimba. Leo hii mtu anatakiwa kukodi boti ya kwenda kufanya doria za ulinzi na kulisha wale Samaki shilingi 60,000 mpaka 80,000 kwa siku ndani ya miezi nane kijana anapata wapi hizi fedha? Atapata wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwatengenezee mazingira vijana ya kuonekana wao hawawezi kufanya kazi, tusiwatengenezee mazingira vijana ya kuonekana wao si wasikivu na wala si wachapakazi. Vijana wanayo nia tuwashike mkono na tufate maelekezo kama Mama Samia anavyotaka. Tusimchonganishe Mama na Vijana wake, hatutakubali. Vijana tumemwelewa Mama tutampigia kura kwa nguvu 2025 kwa sababu tunajua chote anachokifanya ni kuhakikisha vijana wa Tanzania tunanufaika na matunda ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nitafurahi sana kama Mheshimiwa Waziri akija katika kuhitimisha hoja yake akatupa majibu vijana wa mikoa hii mitano. Kwamba hii project itaishia wapi na nini kinaenda kutokea kwenye zile fedha ambazo Wizara imetuambia kwamba haitazileta ilihali tunajua zimetoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)