Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafsi hii nichangie hii bajeti ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2023/2024. Nianze kwanza kwa kuungana na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anawafanyia Watanzania, juhudu zake tumeziona katika kujenga Diplomasia ya Uchumi, Royal Tour na mambo haya yamefanya nchi yetu sasa imepanda ilikuwa Namba Sita kiuchumi Afrika, tumeondoka kwenye dola bilioni 69.9 mwaka 2021 na sasa tumefikia dola bilioni 85.4 kufika mwezi Aprili, haya ni mafanikio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anategemea sana wasaidizi wake wa karibu na kwa ajili hiyo nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu wake Mheshimiwa Chande pia na Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Mkuu pale Wizarani wote, hawa wanafanya kazi nzuri, ndiyo wametufikisha hapa tulipo kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuja na bajeti ya trilioni 44.39 fedha ambazo zinatakiwa zikusanywe na kutumika kwa mwaka huu wa fedha, sina mashaka kwamba hizo fedha zitapatikana kwa sababu nimesoma mikakati ya kuzitafuta lakini pia na mikakati ya usimamizi. Nimpongeze sana Waziri kwa kujipanga sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya salamu hizo za pongezi naomba nizungumze kidogo kwenye Wizara za Kisekta nikianzia kilimo. Wenzangu wamesema kwamba Kilimo kinaajiri Watanzania wengi lakini mchango wake kiuchumi bado uko chini sana. Mimi nipongeze kwa kweli juhudi za Serikali katika kukiboresha na kukiinua kwa kuongeza bajeti kutoka bilioni 294 mwaka juzi sasa tuko bilioni 970 ambazo zimependekezwa hapa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba kilimo chetu kinakuwa cha kisasa, kwa maana ya mbegu bora, pembejeo lakini pia na kuhakikisha kwamba tunaachana na kilimo cha kutegemea mvua. Nirudie kusema tena kwamba kwa kweli tutafanikiwa tu kama nchi hii tutaachana na kufanya kilimo cha kukaa na kusubiri mawingu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kule Arusha Meru Tarafa za King’ori na Mbuguni kwa miaka mingi zimekuwa ndiyo kapu la chakula kwa ajili ya Jiji la Arusha na viunga vyake lakini pia hata kwa nchi za Jirani. Lakini sasa hivi Tarafa zile zimeathiriwa sana na mabaliliko ya tabianchi, na kwa hiyo nishauri Serikali ichukue hatua za haraka yajengwe mabwawa kwenye Tarafa hizo na kujenga skimu za umwagiliaji sambamba na kuendelea kutoa mbegu bora na pembejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani sana miaka ya 1970 kule Kisimiri Juu tulikuwa tunalima Pareto na tulikuwa na Kiwanda cha Pareto kule Arusha, yale mashamba yalifungwa na siku hizi yale mashamba wananchi wanalima bangi. Kwa hiyo, Serikali imekuwa inahangaika sana kupambana na kilimo cha bangi kule Kisimiri Juu. Ushauri wangu kwa Serikali, tufufue Kilimo cha Pareto kule Kisimiri Juu, hali ya hewa inakubali kwa ajili ya kilimo cha Pareto nina taarifa kwamba Iringa wameanza ujenzi wa Kiwanda cha Pareto kama sijakosea, lakini kuna umuhimu wa kuhakikisha kwamba tunafufua kile kilimo cha Pareto ili wananchi waachane kilimo cha bangi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Serikali imekuja na mipango mingi tu, nimshauri Waziri, kule abeleke hii program ya BBT zile familia ziunganishwe, wasaidiwe kimtaji na kuhakikisha kwamba hicho Kilimo cha Pareto kinafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mashamba ya maua ambayo yalikuwa yanaongeza sana Pato la Taifa, yalikuwa yanatuingizia fedha nyingi za kigeni. Haya mashamba yamefungwa na wananchi wafanyakazi kule wamebaki wanahangaika kutafuta ajira, lakini pia wamekuwa maskini. Nishauri pia kwamba Serikali ije na mpango wa BBT kwenye yale mashamba ya maua, wale watumishi waliokuwa kwenye yale mashamba waunganishwe wachanganywe na vijana, wapewe pesa kazi iendelee na maisha yawe bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kupongeza Wizara ya Ujenzi kwa kuja na mpango wa kuboresha Bandari ya Dar es Salaam. Sasa hivi Serikali inajenga SGR ambayo tunahakika kabisa kwamba itakuwa na uwezo mkubwa sana wa kubeba mizigo lakini kama bandari ile isingeboreshwa ile Reli ingebakia kama white elephant, jambo ambalo lingekuwa si zuri kwa sababu soko la huduma za bandari kwa nchi yetu ni kubwa sana. Bandari ya Dar es Salaam ina soko kubwa sana ya kutoa huduma landlocked counties za Malawi, Zambia, DRC, Burundi, Rwanda, Uganda na wakati mwingine Msumbiji. Kwa hiyo, uboreshaji wa ile bandari ni kama ni lazima ifanyike kazi kubwa ya kuiboresha na nashukuru Mungu kwamba Serikali imeshaanza mchakato kwa kusaini mkataba wa EGA kati ya Tanzania na Dubai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu nilikuwa na Waziri Mkuu juzi kule Jimboni kwangu alizungumza vizuri sana na kusema ile kweli alinisaidia sana mimi kama Mbunge kule kwa sababu sitakuwa na kazi kubwa sasa ya kwenda kuelimisha wananchi kuhusu hilo la bandari. Alizungumza alikaa kama Mwalimu akafundisha na watu wote waliomsikiliza waliondoka pale wana amani kwamba kumbe nchi haiuzwi, bandari haiuzwi bali inafanyiwa maboresho ili iweze kufanya kazi efficiently.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi kwa sababu ya muda na mimi naunga mkono hoja, ahsante sana.