Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya. Anafanya kazi kubwa sana mama yetu. Tunampongeza na kumtia moyo. Tunajua kwenye uongozi kuna changamoto nyingi sana, yako mengi yanazungumzwa, mikataba kuingia hakuanza yeye walianza wengi, lakini maneno yanakuwa mengi. Mimi ninamtia moyo Mheshimiwa Rais aendelee kwa nia yake nzuri ya kutaka kuiopeleka Tanzania mahali pazuri, basi aendelee kufanya kazi na Mungu azidi kumbariki na kumpa afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote kwenye bajeti zao, Waheshimiwa Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu wote kwa utendaji wao mzuri mpaka leo hii tunafikia mwisho wa bajeti yetu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi alivyoli – handle suala zima la Kariakoo. Nitakuwa mkosefu wa fadhila mimi Mbunge ambaye natoka Kariakoo. Kwa kweli amefanya kazi kubwa na niiombe Serikali yale madai yao wayaangalie kwa sababu miongoni mwa wafanyabiashara wa Karikakoo wengi ni wakinamama. Kwa hivyo, niwaombe muangalie akinamama wale jinsi gani wanaweza kusaidiwa ili kuondoa kero ile, wafanye biashara zao. Wana mikopo na mambo mengi tu lakini niiombe Serikali na nina imani Serikali hii sikivu itayatekeleza yale waliyoyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti hii mchango wangu utajikita katika ukurasa wa 21, 19, 12, 23, 34, 25 na 26 kama muda utaniruhusu, hivyo nitaelekea kwenye miundombinu maji, kilimo, uvuvi na nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na upande wa miundombinu napenda kuishukuru Serikali, kwa kweli hali ya Mkoa wa Dar es Salaam kwa upande wa madaraja tumefanyiwa mambo mazuri. Tuna daraja Tanzanite, tuna daraja la Kijazi Interchange, kuna TAZARA, kuna Chang’ombe VETA, kuna Kurasini pale Uhasibu kulikuwa na kero kubwa sana. Magari yalikuwa yanajaa pale Kurasini, sasa hivi tumepata daraja, magari yanakwenda na yanaenda vizuri na tunapata muda wa kwenda kufanya shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna madaraja mengine madogo tumejengewa, pale kutoka Bendera Tatu kwenda Gerezani, kuna watu hawakutarajia kama lile jambo linaweza kuwa, ukilinganisha na ile miundombinu ya reli pale chini, watu hawakutarajia. Leo hii pale ukienda utasema siyo Dar es Salaam hii ambayo tumeizoea, huwezi kujua kama hapa ni Keko. Ni jambo la kumshukluru Mungu na tunaishukuru sana Serikali na Mheshimiwa Rais wetu. Miradi ile mingi iliachwa katika awamu iliyopita lakini imeenda kwa kasi katika awamu hii, pia kuna miundombinu ya mwendokasi ya kutoka Mbagala mpaka Gerezani. Hiyo imekamilika tunashukuru sana lakini miundombinu ya kutoka Gerezani tena pia mpaka Gongo la Mboto nao watu wako site, wafanyakazi wako site na kazi inaendelea. Tunapongeza kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto kubwa. Mkoa wa Dar es Salaam hatulimi, tunachotaka kwetu ni barabara. Tunaomba Serikali mradi wa DMDP pamoja na kuzungumza juhudi zako Mheshimiwa Waziri tunaziona hongera sana, tunakaa na wewe, tunakaa na Wizara mbalimbali miundombinu kujua hilo, lakini tunaomba DMDP tu, ije Dar es Salaam. Nasema hivyo kwa sababu Dar es Salaam kama Mji tuna miji yetu. Kwenye Wilaya ya Kinondoni sehemu kama Hananasif - Kinondoni, Kinondoni - Shamba, Mwananyamala, Kijitonyama, Mwenge maeneo yale kwa sasa hayapaswi kuwa na barabara za vumbi, yale ndiyo maeneo yetu ya kujidai katika Mkoa wa Dar es Salaam, kwa hiyo, tunomba Serikali iangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Ilala Kata ya Mchikichini, Kata hii bado iko katika Wilaya ya Ilala na iko mjini sana, lakini ukiingia kule ndani vumbi tupu. Kwa hiyo, tunaomba sana mradi huu wa DMDP uje ili tuboreshe. Kwenye Jimbo la Segerea, maeneo ya Buguruni, Segerea yenyewe na Kata ya Tabata. Haya ni maeneo ambayo ya kwetu kweli ni maeneo ambayo yana uwekezaji mkubwa na watu wana shughuli kubwa za kiuchumi tunaomba tupate lami. Ukonga yenyewe, maeneo ya Ukonga Kata ya Ukonga pale Magereza, bado ukiingia humo ndani tafrani, hakujatimia, kuna barabara ile moja inayoenda markasi sijaona barabara nyingine, ninaomba Wilaya ya Ukonga nayo pia ipatiwe barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbagala Rangi Tatu ndiyo center ya Mbagala isipokuwa ukiingia ndani Mbgala kwenye ile Kata ya Kibondemaji ni huruma, hakuna barabara ya lami. Tunaomba tuletewe barabara ya lami kutoka Mbagala Shule ya Rangi Tatu kuelekea Kwa Ndunguru kule bondeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sasa niende kwenye suala zima la nishati. Nimeona Serikali jinsi gani imeweza kuwapatia wananchi wake majiko na kuhamasisha watu kutumia mitungi ya gesi. Lakini mimi niombe kwa vile gesi asilia imeshakuja katika Mkoa wa Dar es Salaam, maeneo ya Mikocheni tayari inatumika, wameshuka mpaka Msasani, niiombe Serikali wawekeze katika gesi asilia. Gesi ile ishuike mpaka Tandale, ishuke iende Manzese, ishuke iende Ubungo, ishuke iende Temeke, ishuke iende Mbagala, ishuke iende Ukonga, ishuke iende Segerea, gesi ishuke iende maeneo ya Buguruni ambako kuna wananchi wengi Watanzania ambao wanaweza wakatumia na hali zao ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama gesi ile mtu ukiwekewa ndani kwa mwezi unaweza ukalipa 10,000 tu kama matumizi yako madogo. Ni kwamba itawapunguzia gharama Watanzania. Kwa hiyo, tunaomba sana tunajua mmetuambia miundombinu yake ya gharama lakini ni uwekezaji, gharama ile italipwa polepole kama tunavyolipa umeme na mambo mengine ina Watanzania pia watakuwa wamenufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije sasa kwenye upande wa maji. Kwenye suala zima la maji tunaipongeza Serikali, kwa kweli miundombinu ya maji inaridhisha, tumepata visima vile vya Mpera na Kimbiji, tunapata maji. Lakini bado kuna changamoto. Wakati wa kiangazi maji Dar es Salaam inakuwa shida. Ni lazima nilitaje Bwawa la Kidunda, tukiwekewa Bwawa la Kidunda hao wananchi wanaotoka mitaa hii ya Mbezi, Kimara, Chuo Kikuu wote wale wanapata maji kutoka Ruvu. Kwa hiy,o tukichimbiwa lile bwawa pale Ruvu itakuwa halikauki. Wakati Mto Ruvu unakauka wataenda kufungulia lile bwawa wananchi wa Dar es Salaam na Mikoa ya Pwani tutapata maji kwa wakati wote. Naiomba sana Serikali waendeleze kama walivyoanza Mheshimiwa Rais amethubutu kwa jambo hili kubwa la kuweka Bwawa la Kidunda kulijenga sasa basi nawaombea heri tufanikiwe hili ili tuweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala zima la uvuvi; Dar es Salaam imezungukwa na Bahari Kuu, Bahari ya Hindi imezunguka katika Mkoa wa Dar es Salaam, lakini wavuvi wetu bado. Katika maeneo ya Pemba Mnazi, tunaita Pemba Mnazi ina maana bahari (ukienda pale baharini unakuta bado wavuvi wanavua na vingalawa vidogovidogo) lakini ukienda Kimbiji unakuta kuna bahari, ukija Mji Mwema kuna Bahari, ukienda hapa Feri ndiyo kwenyewe lakini bado utakuta wavuvi wetu hawana vyombo vizuri vya kuvulia samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo niiombe Serikali na Wizara husika, waende wakawaone wavuvi wetu wa Mkoa wa Dar es Salaam, hata vile vianikio vya kuanikia dagaa wanaanika katika vitu visivyoeleweka na wengine wanaanika tu chini. Niombe hivi huu uwezeshwaji wa hawa wavuvi sijui wa nini, ni akina nani? Mbona kwetu hatujaona wapate hata boti za kisasa. Tunaomba sana Serikali iwasaidie wavuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuja kwenye suala zima la afya. Kwenye afya, kweli Mkoa wa Dar es Salaam jamani tumejengewa Zahanati na Vituo vya Afya na Hospitali kubwa lakini maboresho ya Haospitali za binafsi yamefanyika ni jambo jema. Hospitali zipo na zipo kweli lakini changamoto kubwa ni Madaktari pamoja na Madaktari Bingwa. Ninashukuru mpango wa Serikali wa kuwazungusha wale Madaktari Bingwa wanatengeneza timu wanahama, leo wanaenda hospitali ya Kigamboni, kesho wanahamia Temeke, kesho kutwa wanahamia Ubungo, keshokutwa wanahamia Amana, Mwananyamala. Hivyo ndivyo wanavyofanya lakini haitoshi ukilinganisha na idadi ya watu walioko Mkoa wa Dar es Salaam ambao sasa tunaelekea kwenye milioni sita kwa mujibu wa sensa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunahitaji huduma nyingi sana za afya na Madaktari wengi waje watutibu. Nawapongeza kwa hilo lakini naomba tupewe Madaktari na Wauguzi pia. Wauguzi wanafanya kazi kubwa kwenye hospitali zetu tunawapongeza na Madaktari wetu wote, wanafanya kazi nzuri tunawapongeza sana lakini bado tunahitaji ziada. Ziada siyo mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Mwenyezi Mungu akubariki, ahsante sana. (Makofi)