Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kutoa maoni katika hoja iliyopo mbele yetu. Ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya za kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi mikubwa ya kimikakati. Naomba nimtie Mheshimiwa Rais moyo, tuko pamoja naye kazi anayoifanya inaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mwigulu pamoja na Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na jukumu kubwa la kutafuta fedha lilipo katika majukumu ya Wizara ya Fedha. Kazi ya kutafuta fedha ni ngumu, kazi ya kuchangisha kodi ni ngumu. Naomba niwatie moyo, tuko pamoja na ninyi, na naomba Watanzania hususan wananchi wa Jimbo la Meatu tuielewe hii Wizara katika suala zima la ukusanyaji wa kodi, kwani fedha nyingi sana zinazoletwa katika Jimbo la Meatu zinatokana na kodi hizi tunazochangia wananchi. Zinatokana na fedha zinazotafutwa za mikopo ya masharti nafuu nje. Naomba tuiunge mkono Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja iliyopo mbele yetu. Niishukuru Serikali hivi karibuni Jimbo la Meatu tumeletewa milioni 857.7 kwa ajili ya upanuzi wa shule ya wasichana Nyalanja Sekondari ambapo yatajengwa mabweni manne, matundu 18 ya vyoo pamoja na madarasa 12. Shule hii ni high school, kwa hiyo kuwepo kwa high school pia kutachangiza watoto wale wa form one hadi form four kupenda kujifunza kwa sababu kutakuwa na wasichana wengi wanaotoka sehemu tofauti za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naishukuru Serikali wiki iliyopita imesaini mikataba saba ya ujenzi wa barabara za kimkakati ikiwemo barabara yetu ya Sibiti, Mwanuzi, Lalago Maswa kwa kiwango cha lami. Niombe Serikali yetu kusaini mikataba si maana yake fedha ziko mezani, maana yake Serikali iendelee kutafuta fedha. Fedha nyingi zinatakiwa kwa ajili ya hii miradi saba takribani trilioni tatu. Fedha hizi zinatokana na kodi zetu, fedha hizi zinatokana na tozo zetu tunazotozwa pamoja na mikopo ya masharti nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru Serikali, mwishoni mwa mwezi Mei, Wizara ya Maji ilienda kusaini mradi wa kimkakati wa maji wa kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi. Kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hoja yake aliahidi, kwamba angeenda kusaini mkataba, ni kweli amesaini mkataba wa bilioni 440 kwa ajili ya kutoa maji Ziwa Victoria na kuyaleta katika Wilaya za Mkoa wa Simiyu. Naamini sasa maji haya yatafika katika Wilaya ya Meatu ambayo imeathiriwa kabisa na mabadliko ya tabianchi. Nimshukuru Mheshimiwa Aweso wakati, huo alitupatia milioni 500 kama nilivyoomba wakati nachangia Wizara ya Maji kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la kati ya Mwambajimu pamoja na Lukale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe wananchi wa Jimbo la Meatu, bwawa hili litajengwa kati ya Kijiji cha Lukale na Mwambajimu ambako watu wetu hawapati maji kutokana na chumvi. Kuna ziwa Eyasi pale ambalo lina chumvi kabisa; wananchi wanasafiri mpaka siku nne kuyapata maji kwa ajili ya kunywesha mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite sasa kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nishukuru Serikali kwa program ya mikopo kwa wanafunzi wanaochaguliwa na Serikali kusoma kwenye vyuo vinavyotoa elimu katika fani za kipaumbele. Jambo hili ni zuri kwa watoto wanaotoka kwenye familia duni. Hii ni kwa sababu wengi walichaguliwa kwenda kwenye vyuo vya kati walishindwa kuhimili ada kwa ajili ya kulipa masomo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kuna fani ambazo zimeachwa. Kwa mfano katika Jimbo la Meatu wanafunzi wametoka Sekondari ya Kimali na Mwamalole, wengine wameenda chuo cha IFM kilichopo Bariadi, wengine wameenda vyuo vya maji. Lakini, wanafunzi hawa wamepata division nzuri, wamepata division two wamepelekwa katika hivi vyuo vya kati lakini havipo kwenye vyuo vya kipaumbele. Wanafunzi hawa wanatoka kwenye familia zenye maisha duni kwa hiyo ndoto yao inaweza ikakatishwa pale katikati kwa kukosa ile ada. Kwa macho tunaweza tukaiona ile ada ni ndogo lakini ipo jamii ambayo haiwezi kuilipa hiyo ada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanafunzi walitamani waende A-level kwa sababu kule elimu ni bure hakuna ada angalau waliweza kubaingiza kwa kutafuta nauli wengine walikaa miaka miwili shuleni bila kurudi nyumbani ili waweze kuhitimu katika ile miaka miwili na hatimaye waende chuo kikuu ambako kuna mikopo. Kwa hiyo kwa kuwapeleka kwenye vile vyuo wanaweza kupoteza ndoto zao kwa ajili ya kukwamua zile familia zao. Niiombe Serikali iende zaidi, ipanue wigo, ione vyuo vya kati vingine kwa sababu kuna wengine wamepata division three wameenda form five wakatimiza ndoto zao, waliopata division two wanaenda chuo cha kati wanaweza wakapoteza ndoto zao pale katikati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la upatikanaji wa fedha za kigeni limekuwepo katika kipindi hiki cha hivi karibuni na Serikali imebainisha sababu za kuwepo changamoto hii lakini ninaunga maoni ya Kamati ya Bajeti yote. Imechambua, ikaona sekta kuu tatu ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa katika ongezeko la fedha za kigeni ikiwemo sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee mazao ya kimkakati ambayo mojawapo lipo zao la pamba na zao la alizeti ambayo ni mazao ya kimkakati katika Mkoa wetu wa Simiyu katika Wilaya yetu ya Meatu. Mwaka jana wananchi walifurahi baada ya kuona bei ya pamba imefikia hado 2000. Wananchi wengi walijitokeza na kulima pamba hiyo, lakini mwaka huu bei yake ni 1,000, inazidi kuwanyongonyesha na kuwakatisha tamaa wananchi wetu wa Mkoa wa Simiyu hususan katika Wilaya ya Meatu. Kwa hiyo wananchi wamekuwa wakitangatanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana waliona bei ya alizeti ilipanda wengine waliacha pamba wakaenda kwenye alizeti lakini tunaona bei ya alizeti imeshuka zaidi ya asilimia 50 kwa wakulima wetu. Kwa hiyo wananchi hawajui cha kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto nyingine, katika yale mazao tunayoyalima bado Tembo wanakuja kuyavuruga yale mashamba yao. Tuone namna gani tunaenda kuwasaidia wakulima hawa wa pamba na alizeti. Pamoja na mwaka jana Serikali ilipeleka tani 28 za mbegu katika Wilaya ya Meatu, lakini tani 8 tu ndizo na zilinunuliwa tani 20 zilirudishwa na ASA kwa sababu zilienda kwa kuchelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo pia wananchi walipanda mbegu hazikuwa na tija nak ama mbegu zingekuwa zina tija pamoja na kuporomoka kwa bei zingeweza kuwasaidia zaidi. Huenda wenye viwanda wanashindwa kununua labda mbegu hazina tija, tuliangalie suala la tija katika mbegu za alizeti. Serikali iliagiza mafuta inawezekana zaidi ya upungufu uliokuwepo. Tukiangalia Serikali iliagiza mafuta ghafi ya michikichi kwa ajili ya kuja kuchakata na kwenda kuyauza nchini na mengine kuyauza nchi ya Malawi, Rwanda, Burundi na DRC. Niiombe Serikali ifatilie takwimu na kuangalia, je, yale mafuta yanayochakatwa kwa ajili ya kuuzwa katika nchi nilizozitaja yanauzwa kweli? ama yanazunguka ndani ya nchi na kuleta ongezeko kubwa la mafuta na kukosesha bei ya mafuta ya alizeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la Tembo. Suala la Tembo linavuruga mashamba yetu, ya wakulima wetu mpaka wanakosa vyakula. Nimshukuru Mheshimiwa Rais mwaka huu alituletea mahindi yenye bei nafuu. Nishukuru wepesi wa Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Bashe pamoja na Naibu walitusikiliza Wabunge kwa urahisi na kuyaleta yale mahindi. Lakini bei ile ya mahindi bado ni ndogo ukilinganisha na gharama ya fidia ya ekari ya mahindi ambayo wananchi wanalipwa, na fedha hizi zinaletwa kwa kuchelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imesema inaweka mbinu ya kukabiliana na tembo, imesema inaleta radio caller. Radio caller katika hifadhi ya makao ziliwekwa lakini hazikuwa na ufanisi kwa sababu ziliweza ku-detect ni wapi Tembo wapo kwa kuangalia kwenye mtandao lakini walikosa vifaa vya risasi, walikosa radio kwa hiyo yaliendelea kuwa kama ni mapambo tu ilhali radio caller moja inatumia fedha nyingi sana za kigeni. Serikali imesema wakulima wa kando kando ya hifadhi walime mazao ambayo si rafiki kwa tembo; lakini, hakuna mazao ambayo si rafiki ya tembo. Hata pamba inavurugwa na tembo, alizeti inavurugwa na tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena niiombe Serikali ile habari ya kusema kwamba wananchi wamejenga katika ushoroba, na mimi niwaulize. Je, Tembo zamani walikuwa wanakula matikiti yalipandwa na nani? wanakula viazi vilipandwa na nani? kwa hiyo Serikali ikubali mabadiliko ya hali ya hewa na mabadiliko ya maisha hata kwa hawa tembo ianze kukabiliana nao badala ya kuanza kusemea ushoroba, ushoroba, ushoroba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. LEAH J. KOMANYA: …tumechoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)