Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hoja iliyopo mezani ya bajeti ya Serikali ya trilioni 44.38. Kwanza nianze kwa pongezi kwa bajeti hii ambayo imeenda kutoa majibu kwenye maeneo mengi. Vilevile naomba niungane na wenzangu kuipongeza Serikali kwa mafanikio makubwa ya uchumi. Uchumi wa nchi yetu umepanda kutoka dola bilioni 69.9 mpaka dola bilioni 85.4. Mapato ya Serikali yamezidi kukua na hii imepelekea nchi yetu kupata rating za juu kwa kampuni zinazoheshimika duniani za Fitch Writing na Moody’s Investors Service.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi tu, kampuni kama hizi ni sawa na timu zetu zinavyopata faraja, zinapopata rating ya FIFA ama rating ya CAF. Huku duniani huwezi kufanya mwenyewe ukajipa viwango mwenyewe, kwa hiyo kwa rating hizi za kampuni hizi yanayoheshimika duniani nchi yetu imeongezeka viwango vya kukopesheka nani pongeze kubwa kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, uwezo mkubwa wa Serikali katika ukusanyaji wa mapato umeiwezesha Serikali kuwa na uwezo mkubwa wa kutekeleza miradi ya kimkakati na miradi mikubwa. Kwa mfano Bwawa la Kufua Umeme la Mwalimu Nyerere tumeoneshwa hapa inatekelezwa kwa asilimia 86 na inakaribia kukamilika, ujenzi wa SGR unaendelea bila kukoma vipande vyote vina wakandarasi, Daraja la Kigongo – Busisi liko katika hatua nzuri na litakamilika kwa muda uliopangwa, grid za umeme zinaendelea kusambazwa nchi nzima. Ni kazi kubwa kwenye miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi ya kati pia. Sisi kule Dar es Salaam kuna Bwawa la Kidunda ambalo litasambaza maji Dar es Salaam ambao inaenda ku-complement ile miradi ya maji usambazaji wa maji ambayo hata kwenye Jimbo la Ukonga ipo. Upo mradi wa mwendokasi awamu ya tatu Gongo la Mboto - Kariakoo. Jimbo la Ukonga ni wanufaika na unajengwa kwa kasi kubwa. Serikali pia haijasimamisha hata mradi mmoja ile miradi midogo, madarasa yanajengwa, vituo vya afya vinajengwa, zahanati zinajengwa na hii ni pongezi kubwa kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba niongelee maeneo machache. Kwanza nikuendelea kuishauri Serikali kuongeza wigo mpana wa ukusanyaji wa kodi. Tumeoneshwa hapa kwenye hotuba, nchi hii watu wenye TIN ni watu milioi 4.45, na hizi ni TIN zinazo-include zile leseni na wale wanaolipa PAYE kwenye mishahara yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TIN za biashara zimekomea milioni 1.641 na tumeambiwa hapa katika hizi TIN za biashara asilimia 80 ya makusanyo inatoka kwenye TIN asilimia 20; yaani watu kama laki nne ndio wanatuendeshea nchi kwenye makusanyo haya ya takribani trilioni 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima Serikali iendelee kuboresha mifumo ya ukusanyaji wa mapato na mifumo hii, nimemsikia Mbunge mmoja hapa nadhani kwenye mjadala wa bajeti ya Wizara ya Fedha, aliongelea mfano wa Estonia. Estonia ni nchi ambayo imeweza kuwa na central ledger ambayo shughuli zote za kiuchumi na kijamii ziko kwenye eneo moja. Hii inasaidia Serikali kuweza ku-monitor shughuli za wananchi ili kuweza kuwa na utaratibu mzuri zaidi wa ukusanyaji wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mlimsikia hapa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, leo mtu ana-export mahindi lakini hasomeki sehemu yoyote. Lakini leo mfanyakazi mwenye threshold inayozidi 270,000 na kwenye mapendekezo yao 370,000 analipa PAYE kwenye mshahara wake. Leo kuna mtu anasafirisha mahindi tani kwa tani halipi kodi. Leo kuna mtu ana mifugo maelfu kwa maelfu halipi kodi. Mimi nadhani Serikali iendelee kuboresha mifumo lakini iendelee kwenye kulenga kuwa na central ledger, maana kila mtu anaandika mfumo wake; na ndiyo inakuja hoja ya mifumo ya kusomana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Bashe amekuwa na mfumo wake anagawa pembejeo, lakini mfumo ule hauwezi kwenda kumsoma ni mkulima yupi amepata pembejeo kiasi gani na leo mahindi yake ameuza wapi na anaingiza kiasi gani kwenye Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ipo mifumo mingine kwa mfano Mfumo wa ETS. Kila mtu anakubaliana na mimi na takwimu zipo, kwamba tangu ufungwe ETS makusanyo ya kodi yameongezeka, zile exercise duty zinazotozwa kwenye biashara zinazozalishwa nchini zimeongezeka. Na SICPA ni moja ya kampuni reputable duniani ambayo si tu inafanya mifumo ya kodi lakini pia imeaminika kwenye printing hasa ya vitu kama noti au fedha kwenye nchi mbalimbali na inafanya kazi kwenye nchi nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tutakapokuwa na mifumo ya kisasa, na maeneo mengine Wizara ya Fedha ama Serikali isione tabu; Mheshimiwa Rais alishawahi kusema, nadhani alipokuwa akipokea ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali mwaka jana, kwenye maeneo ambayo tunakwama sisi ndani tusipate tabu kutafuta utaalam wa nje kwa sababu yako maeneo yanahitaji ubobezi. Mimi naamini tukiwa na mifumo bora zaidi makusanyo yataongezeka kama tulivyoona kwa mfano wa ETS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko eneo ambalo mimi nitaomba kutoa ushauri kwa Serikali, na ninadhani kama sitopata majibu ya msingi tutakutana kwenye Finance Bill. Serikali inapendekeza kufuta kodi ya VAT kwenye gaming odds na gaming software. Iliwahi kuwekwa huko nyuma kwenye Section 64 ya Value Added Tax Act Cap.149 ya 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia gaming odds maana yake ni unazungumzia michezo yote ya kubahatisha. Bidhaa pekee inauzwa ni gaming odds. Serikali inapotaka kuchukua gaming odds ikaisamehe VAT, na ukizingatia gaming odds ina michezo mingi ya kubahatisha ni kampuni za kimataifa ambayo Serikali na Bunge hili liliweka ile Section 64 ili kampuni zile zipate representative hapa nchini waende wakalipe VAT; na ndiyo kodi pekee inakusanywa kwenye eneo hili. Ukisha iondoa, ukachukua gaming odds ukaipeleka kwenye jedwali la kusamehewa, ambao kule kumejaa kilimo, mifugo na maeneo mengine ya uzalishaji, maana yake unaenda kujikuta kwenye shughuli hii ya michezo ya kubahatisha kwenye kampuni za nje hatutakusanya hata shilingi moja kwa sababu wale wanaofanya michezo hiyo ya kimataifa ni non-resident kwenye tax base yetu. Kwa hiyo, mimi ningependa kusema wazi kabisa siliungi mkono na ninadhani nitapata majibu ama tutakutana kwenye finance bill.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa uchache kabisa, siku ya jumamosi tarehe 17 tulikuwa pale Mlimani City, Mheshimiwa Rais alipokea Hundi ya shilingi bilioni 45.5 kutoka benki ya NMB. Huwezi kuzungumzia benki ya NMB bila kuzungumzia walipa kodi wakubwa, benki hii kwa mwaka wa fedha huu walitoa gawio, wamelipa kodi shilingi bilioni 453.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi ukaizungumzia benki ya NMB bila kuzungumzia mkakati wa Serikali ulioanza kwenye awamu ya tatu ya ubinafsishaji. Tuliwahi kuuza hisa zetu Label bank mwaka 2004. Jambo hili lilikuwa na kelele kubwa; bodi ya NMB iligoma, ilipelekea Serikali kuvunja bodi hiyo ya Wakurugenzi ya NMB. Lakini tangu uwekezaji ule ufanyike benki imezidi kuboreka, mifumo imeimarika na gawio limeongezeka. Tangu gawio la shilingi bilioni nne mwaka 2009 mpaka gawio la shilingi bilioni 45.9. Maana yake nini; Serikali hailipi mishahara NMB, Serikali hailipi umeme NMB, Serikali imeenda kupata gawio la bilioni 45.5 na kodi ya bilioni 453.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuendeleza nchi hii bila kushirikiana na sekta binafsi, na mimi niombe Serikali, tulipitisha hapa Azimio la IGA ya bandari yetu ya Tanzania, kelele zimekuwa ni nyingi. Nishukuru Serikali imeendelea kutoa elimu, na elimu kubwa ni kwamba IGA sio mkataba wa utekelezaji na yeyote anayeenda nje ya hapo ana nia yake ovu maana wa kuelewa ameshaanza kuelewa. IGA ni makubaliano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai juu ya uwekezaji utakaoenda kufanyika kwenye bandari zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba ya kwenda kutekeleza miradi (Host Government Agreement) na zile concession agreement bado hazijaingiwa na concern zote za wananchi Serikali iliahidi hapa Bungeni na inaendelea kuahidi, na juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema, watazi-consider kwenye kuingia mikataba yenye maslahi na Taifa. Mimi naamini kabisa ufanisi wa bandari ukiongezeka na takwimu zipo uchumi wa Taifa utakua, forodha itaongezeka, kilimo kitachachuka, sekta zote za uchumi zitaenda kuboreka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaiomba Serikali, kama vile Rais wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa Hayati Benjamin Mkapa alivyokubali kupigiwa kelele mwaka ule 2004, leo tunapokea Hundi pale Mlimani City jina lake halikutajwa hata mara tatu. Niombe Serikali ikubali ushauri, isikilize wananchi lakini wakati mwingine isikubali kuyumbishwa na watu wenye nia zao za kuitaka nchi yetu isiendelee kiuchumi; ikubaliane na hizo hoja za msingi za kuendeleza Taifa tuwe na uwekezaji na kushirikisha sekta binafsi kwenye maeneo ambayo wenzetu wamebobea tupate uendeshaji mzuri wa bandari. Miaka ijayo tutakuja hapa kupongeza na wakati wote nawajua binadamu hata wale walioshiriki jambo hilo hawatatajwa, sifa zitakwenda kwa wale watakaokuwepo wakati huo lakini ndiyo kazi ya viongozi kuweza kusimamia uongozi wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda mwisho, niombe Serikali iendelee kushirikiana na sekta binafsi, lakini kama nilivyosema iendelee kuboresha mifumo ya nchi yetu. Mifumo hii ikiwa bora kero zote tunazozisikia hata zikiwemo hizi za mahindi zilizotajwa hapa Bungeni na Mheshimiwa Mwenisongole na kupata majibu ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo zitafika wakati zitakwisha na kila mtu atachangia katika uchumi wa Taifa lake kwa kadri anavyochochea kwenye uchumi wa Taifa lake. Isiwezekane kukuta mfanyakazi analipa kodi kwenye mshara wake kwenye threshold ndogo ya laki mbili na elfu sabini analipa kodi lakini kuna mtu mwingine anafanya biashara kubwa zaidi na hasomeki kwenye uchumi wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)