Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuhitimisha hoja ambayo niliiweka mezani mnamo tarehe 15 Juni, 2023 ambapo niliwasilisha katika Bunge lako Tukufu Hali ya Uchumi kwa mwaka 2022, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2023/2024 na Mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe mwenyewe pamoja na Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge, kwa kuendesha mjadala huu kwa umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu hoja mbalimbali za Wabunge, napenda kutumia fursa hii kupaza sauti tena kwamba Mama apewe maua yake kwa sababu ya kazi nzuri anazowafanyia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wale ambao hawajazoea kufuatilia mambo yanavyofanyika wanaona Waheshimiwa Wabunge wanaposimama kusifia kazi nzuri, wanafanya tu hivyo kama ni utamaduni. Hata hivyo, naomba dakika chache tu niseme baadhi ya mambo kwa ufupi.

Mheshimiwa Spika, fedha zinazokwenda kwenye shughuli za maendeleo kwenye Wizara zetu, mikoa yetu, wilaya zetu, majimbo yetu kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo, ni kiwango kikubwa cha fedha ambacho hakijawahi kutokea tangu uhuru.

Mheshimiwa Spika, fedha zilizokwenda TARURA kutengeneza barabara za mijini na vijijini ili wakulima waweze kupitisha mazao yao, watoto wanaokwenda shule wasisombwe na maji mvua zinaponyesha, akinamama wajawazito wasifariki njiani kwa sababu ya kukosa barabara za kuwafikisha kwenye vituo vya afya ni fedha nyingi kuliko zilizowahi kutokea tangu TARURA ianzishwe. Hivyo ndivyo Mama anavyowajali Watanzania na anavyowajali wananchi wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha zilizokwenda kutengeneza barabara zinazosimamiwa na TANROADS na hivi juzi tumesaini mikataba ya barabara zile saba pamoja na ya nane ikiwa imekaribia kukamilika, ni barabara zenye urefu mkubwa kuliko barabara zilizowahi kusainiwa Afrika kwa mara moja tangu Nchi zote za Afrika zipate uhuru. Hivyo ndivyo Mama anavyowatumikia Watanzania. Mama apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha zinazokwenda kwenye Elimu bila Malipo, Mikopo ya Elimu ya Juu, Miundombinu kuanzia Shule ya Msingi, Sekondari na Vyuo Vikuu, ni fedha nyingi ambazo zimewahi kwenda kwa mara moja katika mwaka wa fedha tangu nchi hii ipate uhuru. Hivyo ndivyo Mama anavyowajali watoto wa Watanzania maskini.

Mheshimiwa Spika, fedha zinazokwenda kwenye afya, kwenye kazi za Sekta ya Afya, Miundombinu ya Sekta ya Afya, vitendea kazi kwenye Sekta ya Afya ni fedha nyingi Kwenda katika mwaka wa fedha kuliko kipindi chochote kile.

Mheshimiwa Spika, fedha zinazokwenda kwenye kilimo. Fedha zinazokwenda kwenye miundombinu ya umwagiliaji, mbegu bora, maghala ya uhifadhi wa chakula, fedha zinazokwenda kwenye kuendeleza vijana katika ku–modernize kilimo, ni fedha nyingi zilizowahi kutolewa katika Sekta ya Kilimo kwenye mwaka wa fedha kuliko kipindi chochote tangu tupate uhuru. Hivyo hivyo, katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi na hivyo hivyo katika sekta nyingine.

Mheshimiwa Spika, hata fedha ambazo zimekwenda kwenye Sekta ya Maji. Usambazaji wa maji, magari ya kuchimba visima, mitambo ya kuchimba mabwawa, fedha zilizokwenda kwenye kujenga miundombinu ni fedha nyingi zilizowahi kwenda katika mwaka wa fedha kwa mara moja kuliko kipindi chochote tangu tupate uhuru. Hivyo ndivyo Mama anavyowajali Watanzania. Mama yuko kazini, Mama apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha zinazokwenda kwenye utekelezaji wa Miradi ya Kimkakati. Reli, Bwawa la Mwalimu Nyerere, fedha zinazokwenda kwenye kutekeleza miradi mingine kama mafao ya wastaafu, mtakumbuka mwaka 2022 tuliweka hati fungani zaidi ya trilioni mbili. Maslahi ya watumishi wa umma, kukuza sekta binafsi, kuvutia uwekezaji pamoja na uboreshaji wa vyombo vya ulinzi na usalama, ni fedha nyingi kuliko kipindi chochote katika mwaka wa fedha wowote utakaoutaja.

Mheshimiwa Spika, nimetaja tu sekta chache, lakini kuna sekta nyingine huu ndio utaratibu na hivyo ndivyo fedha zilivyokwenda. Pia, hapa ndipo Watanzania wajiulize, kuna Watanzania wengi sana ambao wamekuwa wakiwaaminisha watu wengine kana kwamba kumekuwa na wizi mwingi wa fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, hivi fedha kama zimwekwenda nyingi hivyo kwenye miradi ya maendeleo na Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kila jimbo limepata fedha nyingi kuliko kipindi chochote kile. Hivi kama wizi umeongezeka, katika kipindi ambacho wizi haukuwepo hizo fedha zilikuwa zinakwenda wapi? Kama sasa zimekwenda nyingi kuliko kipindi chochote, katika kipindi ambacho wizi haukuwepo hizo fedha zilikuwa zinakwenda wapi?

Mheshimiwa Spika, Watanzania watofautishe na tusichanganye uwazi katika matumizi ya Serikali kuongezeka, ni tofauti na wizi kuongezeka. Nirudie tena kusema kwamba, haya niliyoyasema ni kwenye baadhi ya sekta tu, lakini maendeleo yametokea katika sekta nyingi na Watanzania wote ni mashahidi. Hata Yanga kufika fainali na kuchukua vikombe vyote ni hatua ya maendeleo ambayo haijawahi kufikiwa. Hata lile la mataifa walilichukua kwa sababu chanya moja na chanya moja ziko sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru tena wewe pamoja na Naibu Spika wako kwa jinsi ambavyo mmendesha vikao vizuri. Vile vile, niwashukuru Wenyeviti na nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Mheshimiwa Daniel Baran pamoja na Mheshimiwa Omari Kigua ambaye ni Makamu Mwenyekiti pamoja na Kamati nzima ya Bajeti. Pia, napenda kuwashukuru Mawaziri wote ambao walitoa ufafanuzi wa hoja za kisekta siku ya Ijumaa.

Mheshimiwa Spika, pia, napenda kumshukuru Naibu Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Hamad Hassan Chande, Naibu Waziri wa viwango kabisa na ananisaidia vema katika kutekeleza majukumu haya. Vile vile, nawashukuru watendaji wote wa Wizara ya Fedha wakiongozwa na Katibu Mkuu, Dkt. Natu Mwamba, Daktari Bingwa kabisa wa masuala ya uchumi pamoja na timu yote ya wataalam ambao wanasaidia katika shughuli hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali imeanzisha Mafungu mapya matatu kwa lengo la kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mipango, uwekezaji na ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi. Mafungu hayo ni :-

(i) Ofisi ya Rais Uwekezaji;

(ii) Tume ya Mipango; pamoja na

(iii) Kituo cha Ubia kati ya Serikali na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, hivyo, napenda kutoa taarifa kwamba bajeti za mafungu haya zimetengwa kupitia kasma ya Matumizi ya Kitaifa (National Expense) iliyopo Fungu 21 Hazina. Kwa muktadha huo Sheria ya Matumizi ya mwaka 2023 (Appropriation Bill, 2023) itajumuisha bajeti za mafungu haya baada ya Serikali kukamilisha taratibu zote.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye ufafanuzi wa mafungu nitaomba uridhie niende kwa hoja kwa sababu ya wingi wa hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Waheshimiwa Wabunge wengi wameongea kuhusu masuala ya maendeleo kwenye Majimbo yao yanayohusisha sekta zao, wameongelea kwenye maji, wameongelea kwenye elimu, wameongelea kwenye afya, wameongelea kwenye miundombinu.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hoja zenu zote hizo tumezipokea na mara tutakapoenda kuna zile ambazo mmeziwasilisha kwa maana ya udharura na ulazima katika maeneo hayo. Wizara ya Fedha tutakaa na Wizara za Kisekta ili tuweze kuona utekelezaji wake tunaweza tukaufanya namna gani. Liliongelewa kwa sauti kubwa suala la Uwanja wa Ndege wa Mwanza Ndugu yetu Musukuma alilisema na bahati nzuri Uwanja wa Ndege wa Mwanza hiyo center wote tunaijua.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge tumelipokea tutakaa na Wizara ya Kisekta taratibu za kutafuta fedha ni taratibu endelevu tutaendelea na tutaweka uzito unaostahili katika jambo hilo na Mheshimiwa Mbunge uliongelea kushika shilingi hata usishike shilingi, Uwanja wa Ndege wa Mwanza hata mimi naupenda na ni nyumbani kwetu, kwa hiyo tutakaa na Wizara za Kisekta tuweze kuangalia ili tuweze kuona namna ya kulitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili Mheshimiwa Rais alishalielekeza siku nyingi, nakumbuka alipokuwa ziara kule katika Nchi za Umoja wa Ulaya ni moja ya maeneo ambayo alikuwa anayasisitiza kila wakati sisi Wizara ya Fedha tuweze kukaa na wenzetu tuweze kuyafanyia kazi hiyo.
Mheshimiwa Spika, yaliongelewa masuala barabara Ndugu yangu Mheshimiwa Taletale, Mheshimiwa Mwenyekti Kihenzile, Mheshimiwa Bilakwate, Ndugu yangu Mheshimiwa Waziri mwenzangu Jafo, Ndugu yangu Mheshimiwa Asenga, Ndugu yangu Mheshimiwa Kamamba tumepokea barabara zote ambazo waheshimiwa Wabunge mmeziwasilisha. Waheshimiwa Wabunge barabara zingine mlisema zimetengewa fedha kidogo, tunapoweka fedha kidogo hatuna maana kwamba katika mwaka huo tutatekeleza mradi wa barabara kwa kutumia fedha hizo, fedha zingine ni kwa ajili ya upembuzi lakini maeneo ambako upembuzi ulishafanyika kama kule Nyororo tumeweka fedha kwa sababu zoezi la kutafuta fedha ni endelevu, tunaendelea kukamilisha masuala ya fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuliweka fedha kwa ajili ya kushikilia kifungu ili wakati wa kutekeleza kuwe na kifungu ambacho kilipitishwa kwenye bajeti. Kwa maana, hiyo barabara zote ambazo zitatekelezwa kwa P4R ni kwamba fedha zitakapatikana zitaendelea kutoka kadri utekelezaji unavyoendelea. Kwa hiyo, hatuna maana kwamba tutatekeleza kwa kiasi kidogo kile ambacho kimewekwa, kile kinashikilia kifungu ili tutakapokwenda kutekeleza tuweze kutekeleza kwa kutumia kifungu ambacho kilipitishwa na kwa utaratibu wa P4R ambapo fedha inaendelea kutoka kufuatana na utekelezaji wa mradi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge miradi yote ile mliyoitaja ya barabara, miradi ya maji, miradi ya afya tumeipokea tutakaa na Wizara za Kisekta kama ambavyo Mawaziri wa Kisekta walizisema siku ile wakati wanahitimisha.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee niwapongeze Wabunge wote ambao walihimiza wananchi pamoja na viongozi kwenye suala la kulipa kodi. Suala hili la kulipa kodi ndilo linalotutambulisha kuhusu kujitegemea, ndilo linalojitambulisha kuhusu uhuru wetu, ndilo linalotutambulisha sisi kuhusu uwezo wetu wa kutekeleza miradi ya maendeleo. Mheshimiwa Bilakwate ulisema kabisa ulikpokuwa unaomba ilikuja hiyo kama ndoto na ilikuja ikakuelekeza hivyo nilimsikia Mheshimiwa Kwagilwa, Mheshimiwa Matiko, Mheshimiwa Mnzava, Mheshimiwa Subira, Mheshimiwa Riziki Mama yangu na Wabunge wote ambao mmeongelea kuhusu hamasa hii.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge, twendeni tukawaelimishe wananchi wetu, tukawahamasishe kwamba jambo la kulipa kodi ni jambo letu sisi sote, ni jambo la Watanzania, ndiyo maendeleo yetu na jambo hilo kama wananchi wote wataitikia mwito huo nchi yetu itashusha viwango vya kodi.

Mheshimiwa Spika, leo hii viwango vya kodi ni vikubwa kwa sababu wanaolipa kodi ni wachache, maana yake mzigo wa maendeleo, mzigo wa huduma za jamii unabebwa na wachache. Kwa maana hiyo twendeni tukawahamasishe na kama kila mmoja atalipa kodi, kila mmoja atatumia mashine za kilektroniki, kila mmoja atadai risiti, kila mmoja atatoa risiti, anapouza maana yake tunaianza safari ya kupunguza viwango vya kodi. Leo hii kila mfanyabiashara anaona viwango vya kodi ni vikubwa lakini hii vicious cycle inatakiwa kukatwa kwa kuanzia kila mmoja alipe kodi ndipo tutakapoweza kupunguza viwango hivyo vya kodi.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye hoja nyingine ambayo iliongelewa kwa kiwango kikubwa na Waheshimiwa Wabunge ilikuwa ni hoja ya ngano. Na nilimsikia Mheshimiwa Mbunge wa Makete akiongea kwa sauti kubwa sana pamoja na Wabunge wengine wote ambao waliongelea suala la ngano. Waliona kama vile Wizara ya Fedha imeshusha kiwango cha kutoka asilimia 35 kwenda asilimia kumi.

Mheshimiwa Spika, nikuambe kwamba jambo hili tumekaa na Wizara ya Kisekta tuko na sauti moja kwenye jambo hili, kinachotokea hiyo ni terminology ambayo inatumika kwenye masuala hayo ya kikodi. Kama ambavyo huwa tunafanya kwenye sukari, ile sukari ya gap sugar inapoagizwa, pale ambapo huwa tuna upungufu ama wazalishaji au waagizaji huwa wanapewa nafuu kwa hiyo hata hii duty remission ni lugha ya kitaalamu inayomaanisha kwamba wale wote ambao watanunua ngano ya ndani. Ngano ya ndani ikishaisha anapewa ruhusa ya kuagiza Ngano ya nje kwa bei iliyo nafuu.

Mheshimiwa Spika, hicho ndicho kilichofanyika hakijapunguzwa ili aagize nje aache ngano ya ndani, ila anapewa nafuu pale atakapokuwa amenunua. Kwa hiyo, anapewa motisha ya kununua ngano ya ndani, kwa maana hiyo atakapokuwa amenunua ngano ya ndani ikaisha anapewa ruhusa ya kuagiza Ngano ya nje kwa kiwango ambacho kiko chini ya kile cha kawaida, mtu mwingine yeyote yule ambaye hanunui ngano ya ndani hanufaiki na hiyo duty remission. Kwa maana hiyo, hii ni motisha ambayo sisi Wizara ya Fedha pamoja na wenzetu wa Wizara ya Kilimo tuko na sauti moja na uagizaji wake utaratibiwa na Wizara ya Kisekta ya Kilimo kwamba yule ambaye amemaliza kununua ngano ndiye ambaye atapewa hiyo duty remission kama motisha ya wale ambao wananunua ngano ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge kwa hiyo niwaombe mkubali hilo pendekezo liko sawa na huo ndiyo utaratibu ambao ni standard na ile ni lugha ya kitaalam ambayo imetumika. Hatujapunguza ili tuue wakulima wa ndani, tumepunguza kumpa motisha yule atakayenunua ngano yote ya ndani, ile iilikuwa ilitolewa kwa sababu kuna wakati watu walikuwa wanapendelea kununua ngano za nje ngano za nje, kwa hiyo, ikaleta unafuu kama motisha kwa yule ambaye atanunua ngano ya ndani, hiyo ndiyo maana ya duty remission

Mheshimiwa Spika, kuna Wabunge wengine waliongea kwa sauti kubwa kuhusu upande wa mafuta ya kula. Tumeliangalia jambo hili na kwa jinsi ambavyo tumeliangalia tumeenda kutoa unafuu kwa wale wazalishaji wa ndani ili mafuta ya ndani yasije yakazidiwa na yale mafuta ya nje, kwa hiyo tutaleta kwenye schedule of amendment nafuu ambayo tumeitoa kwa wazalishaji wa ndani kama motisha ya kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana ndani ya Serikali kwamba jambo hili tutaendelea kulifuatilia kwa ukaribu, lakini kingine ambacho ndani ya Serikali tunakubaliana tukasema tuanze nalo hilo kwa uzito mkubwa ni kudhibiti uingiaji wa mafuta kwa njia ambazo siyo rasmi, ambao ndiyo ambao unaleta hiyo flooding ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeiongea kwa sauti kubwa. Tumepokea nakumbuka ndugu yangu Mheshimiwa William aliongea na Mheshimiwa Kunti na wengine wote akina Mheshimiwa Musa na wengine wote wanaotokea katika maeneo ya wakulima wa alizeti, tumeyapokea na tutakaa na wazalishaji tutakaa na vyombo kuhakikisha kwamba uingiaji wa mafuta kiholela unadhibitiwa ili kuondoa hiyo flooding ambayo ndiyo inaleta tatizo kubwa la bei ya mafuta ya kula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge mkubali mapendekezo hayo na Mheshimiwa Rais anawajali wakulima ndiyo maana anaweka uwekezaji mkubwa katika sekta hizo za kiliomo.

Mheshimiwa Spika, kuna Waheshimiwa Wabunge wengine waliongelea kuhusu kuboresha kuboresha mazingira ya kufanyia biashara, tumeyapokea ninayo orodha ndefu ya wale Wabunge ambao walisema mazingira yawe rafiki, tunaendelea na hayo ndio maana hata katika mapendekezo yetu kuna maeneo ambayo tumeyaboresha zaidi na tunaenda full swing kwenye utekelezaji wa blue print. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Wabunge ambao waliongelea kuhusu Wakandarasi kulipwa, kuna walioongelea kuhusu makundi maalum, Sheria ile ya Manunuzi kutekelezwa, kuna wale walioongelea kuhusu kuwianisha mapato na matumizi. Tumeyapokea hayo na nadhani katika Bunge lijalo kama itakupendeza tunaleta Sheria ile ya Manunuzi ambayo itaangalia hivi vitu vyote, pia Serikali ya Mheshimiwa Samia iliona hilo tatizo ambalo linajitokeza kwenye upande wa riba zinazojitokeza kufatana na wakandarasi kutokulipwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, chimbuko la tatizo hilo ni pale ambapo miradi mingi inaingiwa mikataba kwa mara moja kwenda kwenye utekelezaji ambayo haioani, haiwiani na fedha ambazo zinapatikana za kulipa hiyo. Kwa hiyo, kama madai ni makubwa kuliko fedha zilizopo ni dhahiri kwamba watalipwa wachache na wengine ambao hawajalipwa watenda kwenye kudai riba. Ndiyo maana Mheshimiwa Rais ameona afufue Tume ya Mipango na ijitegemee ili utekelezaji wa miradi uwiane na mipango iliyopo, kama utekelezaji wa miradi utawiana na mipango iliyopo ni dhahiri kwamba miradi inayotekelezwa itakuwa inawiana na uwezo wa Serikali wa kuilipia miradi ile na kama uwezo wa kuilipia miradi ile utaweza kuendana na miradi inayotekelezwa ni dhahiri patakuwa hapana riba.

Mheshimiwa Spika, kinachojitokeza ni kama miradi inayotekelezwa kama certificate zilizoiva ni nyingi kuliko fedha zilizopo, ni dhahiri huwezi ukazilipia zote na wale ambao hawajalipwa ni dhahiri watadai riba. Kwa hiyo, hicho ni kitu ambacho Serikali imeenda kwenye utekelezaji wake lakini ndiyo maana pia Mheshimiwa Samia akaona aweke utekelezaji wa miradi ya barabara kwa EPC+F ambapo baada ya kukamilika kwa maridhiano ya Serikali na Benki inayotoa fedha hizo, fedha zitaanza kutolewa moja kwa moja kwenda kwenye mradi kwa hiyo hapatakuwepo na utaratibu wa fedha ambazo zilipangwa ziende kwenye mradi, kuweza kutumika labda katika maeneo mengine ambayo yanapunguza uwezo wa Serikali labda kulipa katika miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo ambalo tumekaa ndani ya Serikali tunaliangalia kwa ukaribu ni vile tuna madeni ya ambayo yalishazalishwa siku nyingi hatuwezi tukayaacha wala hatuwezi kuyakana tunaendelea kulipa mafungu kwa mafungu na tutaendelea kutoa taarifa hiyo kwenye Kamati ya Kisekta, Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mengine aliyasema Mheshimiwa Mpina akiwa anapinga hatua ambazo Serikali inazichukua. Napenda kumshauri rafiki yangu jirani yangu maana Iramba na Meatu zinapakana. Si ubingwa na wala si ustaarabu kusema na kupinga kila kitu hata ambacho hakistahili kupingwa.

Mheshimiwa Spika, namuelewa sana Rais Samia anapoleta hatua hizi za kikodi namuelewa sana, mwenzangu asipokuwa anaelewa haya si mbaya pia ukimuona Mbunge mwenzako Kibunge tu ukamuuliza hili linamaana gani? kuliko aibu ya kusema jambo, unapinga jambo ambalo lina maana kubwa sana kwa mazingira ya sasa.

Mheshimiwa Spika, Rais Samia anapendekeza kwamba tuache utaratibu wa kufunga biashara ama shughuli ya uzalishaji, kwa sababu shughuli ya uzalishaji mle ndani kwenye shughuli za uzalishaji kuna watu ambao hata siyo wamiliki lakini maisha yao yanategemea hiyo shughuli ya uzalishaji. Tuache kufunga biashara kwa sababu huyo ni mtu anayeendesha biashara ni mtu ambaye ameamua kuisaidia Serikali, badala ya kukaa kutafuta ajira yeye ameamua kujiajiri na ameamua kuwatafutia ajira na Watanzania wengine.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais anasema badala ya kufunga biashara, kama kuna makosa yapo tukae na yule anayetakiwa kutatua yale makosa na penalty imewekwa kwa mtu ambaye hatasikia taratibu za kisheria zichukue mkondo wake, lakini Mheshimiwa Mpina anaona jambo hilo halina maana anasema tuendelee kufunga biashara kwa sababu yeye kwa hulka yake anafurahia watu wakiumia.

Mheshimiwa Spika, tunakumbuka jinsi alivyokuwa anafanya sherehe kwa kuchoma nyavu bila kudhibiti nyavu zile kuingia, tunatambua jinsi alivyokuwa anafurahia kwenda kufunga viwanda anafika tu anakuta mchirizi hivi anasema hiki nimeshafunga mpaka mwezi ujao. Kwa nchi ambayo ina tatizo kubwa la ajira ambalo tunataka sekta binafsi ikue ili tupate kodi huo siyo utaratibu ambao mtu yeyote mwenye hekima anatakiwa kuupigia debe. Angalieni nchi ambazo zimeendelea zilizokuza sekta binafsi zinaishi vipi, ni watu ambao wana adabu kwenye sekta binafsi, watu wanaheshima kwenye sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, Rais Samia anachotufundisha, anatufundisha kwamba sekta ya umma na sekta binafsi siyo maadui, hawa ni wabia wa kuendesha nchi. Hawa ni wabia siyo maadui, lazima tufanye mtu kufanya shughuli ya kujiajiri aione ni shughuli yenye heshima. Sasa hivi nchi nzima watu wanataka tu watoto wao waende kufanya kazi Serikali, kila mtu anataka watoto wake waende Serikalini na wengine wanakuwa specific zaidi wanataka tu watoto wao waende TRA kwa sababu gani? ukiwa Serikalini ndiyo shughuli pekee ambayo ina heshima, watu wote wanaheshimu hiyo peke yake, lakini Mheshimiwa Rais Samia anachotaka kutufundisha anataka kutufundisha shughuli yoyote ya uzalishaji iheshimiwe na yule anayefanya hiyo shughuli aheshimiwe, hata pale ambapo panapoonekana pana matatizo pawe na utaratibu wa kiungwana wa kurekebisha.

Mheshimiwa Spika, sasa unafunga shughuli ya uzalishaji kuonesha tu ubosi unafika tu unafunga na kuondoka, umevaaa zako tai, hautambui hata kwamba hiyo tai uliyovaa pamoja na suti hiyo na mshahara unaopokea unaupokea kwa sababu ya huyo huyo uliyemfungia biashara yake. Mheshimiwa Mpina kwa uelewa wake hilo halioni kabisa, hajui kabisa kama Serikali hata Bunge tulipokaa hapa mchango wa sekta binafsi upo. Mchango wa sekta binafsi ili Bunge likae upo, hayajui haya.

Mheshimiwa Spika, mimi naunga mkono kama Waziri niliyepewa dhamana ya kusimamia uchumi, maoni haya ambayo Mheshimiwa Rais anataka kuyaweka ni maoni ya msingi yataikuza sekta binafsi yatakuza tax base na yataongeza ajira pamoja na hamu ya watu kujiajiri, lazima mtu ambaye hatma ya wenzake aheshimiwe na apewe jina lililojema ili aweze kuvutia na wengine waweze kujiandaa nalo kwenda na hilo wazo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili tunasema tuache kukamata mizigo, tuache kushikilia mizigo na vitendeakazi vya watu. Mheshimiwa Mpina anasema na hilo ni baya tukamate tu anasema taasisi hizo zinafanya vizuri sana. Hebu niambieni Waheshimiwa Wabunge ninyi ni wawakilishi wa wananchi hebu fikiria mzigo ambao siyo mali haramu, eti tumetofautiana kodi siyo sumu, eti tumetofautiana kodi badala yake tunakaa nayo mwezi wa kwanza, wa pili, wa tatu, wa nne, wa tano, wa sita, mwaka wa kwanza, mwaka, wa pili, hebu niambieni. Je hivi tungepokea kodi ile ambayo hatubishani nayo halafu tuandikishiane ile ambayo tunatofautiana, halafu huyu mtu bidhaa yake apewe aendelee na biashara, niambieni kwa miaka mitatu ambayo tumeshikilia mzigo tungeshapokea kodi ngapi? Mheshimiwa Mpina anasema wakamatiwe tu huo utaratibu Serikali mnaotaka kuufanya ni mbaya. Ni lazima tuheshimu mitaji ya watu!

Mheshimiwa Spika, niambieni ni wafanyakazi wangapi unaweza ukashikilia mishahara yao kwa miaka miwili halafu wasilalamike ukae tu? Kwa sababu yule mwenye mtaji wake ile biashara ndiyo mshahara wake. Ili tuweze kukuza sekta binafsi kama wapo ambao hawajaelewa maoni, mawazo ya Mheshimiwa Rais kama Mheshimiwa Mpina tunawakosea sana watoto wa Kitanzania ambao hatma yao inategemea sekta binafsi kukua.

Mheshimiwa Spika, ni lazima nchi hii na viongozi wote wa Serikalini walitambue hilo, lazima tuheshimu mitaji ya watu, huwezi ukakaa na mtaji wa mtu umeushikilia tu, wewe fikiria mtu amekopa amekopa akaenda kufuata bidhaa hiyo, bidhaa imefika wewe unaishikilia yeye amekopa ameweka rehani nyumba, nyumba inaenda kuuzwa wewe umeshikilia bidhaa yake. Umeshikilia tu kwa sababu unayomamlaka na uko ofisini na unalipwa mshahara halafu Rais anasema tuondoe huo utaratibu tutafute njia mbadala ya kushughulikia matatizo ambayo hayajakubalika, Mbunge anayelipwa kwa kodi ya sekta sinafsi anasema hili jambo siyo zuri, ninyi endeleeni kukamata tu. Sasa Mheshimiwa Mpina kwa sababu ni jirani yangu usikute yale mambo kaambiwa kule wanakoamini sana mambo yale kwambe wewe pinga kila kitu tu. Si kila kitu kinafaa kupingwa mambo mengine ni lazima tutumie logic ilipo.

Mheshimiwa Spika, tumeondoa pia utaratibu na tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge, Wabunge walikuwa wanasema kule kwenye Halmashauri kwa nini kila taasisi ya Serikali inakwenda yenyewe kudai? Tumeandaa blueprint imeeleza kwamba tukitaka kukuza sekta binafsi tuondoe ule utaratibu wa kuwafanya watu wa sekta binafsi siku nzima kusikiliza ama kuhudumia Serikalini tu. Anatoka wa fire anaenda wa OSHA, anatoka wa OSHA anaenda wa TFDA, anatoka wa TFDA anaenda wa TBS, anatoka wa TBS anaenda…, utitiri wa watu wote wanaotoka Serikalini. Tukasema tutengeneze dirisha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo mifano ambayo tumefanikiwa kwenye hilo, tumeweza kufanikiwa kwenye upande wa mafuta, tunakusanya mara moja, tukishakusanya kuna fedha inaenda REA, kuna fedha inaenda reli, kuna fedha inaenda TANROADS, tuna fedha inaenda maji, tuna fedha inaenda TARURA lakini imekusanywa mara moja. Sio kila taasisi inaenda kukusanya maana yake na katika dunia hii ya kidijitali inawezekana. Hata zile kaguzi zilizo rasmi si vyema kila mtu anaenda kwa wakati wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wengine hawajaona sana tatizo tulilonalo kwenye nchi hii. Mimi namwelewa sana Rais Samia, watu wengine wanataka tuishi kama ile enzi niliielezea sana kwenye hotuba siku ile. Mheshimiwa Rais alitupa dira tatizo anavyoliona na jinsi anavyoona tunaweza kulitatua.

Mheshimiwa Spika, pale zamani Watanzania walikuwa wachache tuko milioni tisa, vyuo vikuu una wataalam 12; una wataalam wawili, una wanafunzi 42. Hao wanafunzi huna kuumiza kichwa kuhusu ajira zao, lakini mazingira ya sasa eneo pekee ambalo linaweza likaajiri Watanzania wengi ni sekta binafsi. Sasa tuna kazi, tuna kazi ya kuifanya sekta binafsi ikue, tuna kazi ya kuwafanya watu waone ni heshima kufanya kazi kwenye sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ilivyo sasa kuna watu ambao hata wako sekta binafsi hawaoni kama wako kazini, kwa sababu ya jinsi ambavyo tunai–treat sekta binafsi na kwa jinsi ambavyo tunaweka majina kwa watu wa sekta binafsi, lakini kama wote tutaipa heshima sekta binafsi, kama wote tutakuwa na lengo la kumuunga mkono Mheshimiwa Rais katika kukuza sekta binafsi, naamini watu watakuwa wanaona ni heshima kwenda kufanya sekta binafsi na tutakuza tax base.

Mheshimiwa Spika, tusipokuza sekta binafsi kodi zote zitabebwa na wanyonge, kwa sababu hauwezi ukaleta kodi mpya bila shughuli mpya ya uzalishaji, maana yake kama hatutakuza sekta binafsi tax base yetu itaendelea kubakia wafanyakazi wataendelea kubakia wachache ambao wanalipa kodi. Niliona niseme na hiyo ili tuweze kuelewana.

Mheshimiwa Spika, kuna Wabunge ambao waliongelea kuhusu taasisi zetu za Maliasili, Wizara ya Kisekta ilishafafanua na kama walivyosema Wizara ya Kisekta tumekaa nao na kwa kweli kuna mapendekezo ambayo tumeyaweka ambayo yataenda kutusaidia tuweze kupiga hatua kubwa kuliko pale ambapo tulikuwa.

Mheshimiwa Kakoso hewa ya ukaa pamoja na wenzake tumelipokea, tutakaa na Ofisi ya Makamu wa Rais kuweza kukimbizana na hili ili liweze kuwahi kufika hatima njema.

Mheshimiwa Spika, jambo la ETS limeongelewa sana na lenyewe tulikubaliana kwenye kikao cha Kamati ya Uongozi na kikao ambacho Serikali ilikuwa inafanya mashauriano na Bunge, tumekubaliana tunapokuja Bunge lile lingine tunatarajia na Mungu atusaidie tutakuja na utaratibu ambao tunaamini itakuwa hatua nzuri ambayo itatutoa hapa tulipo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwepo na maeneo mawili yaliongelewa kwa nguvu; eneo moja lilikuwa la mafuta, tozo ya shilingi 100 kwenye mafuta; mimi niwaombe Wabunge na Waheshimiwa Watanzania, Serikali inafanya simulation/inafanya ufuatiliaji wa ndani kuhusu Soko la Dunia kwenye masuala ya mafuta (fuel), kwenye suala la mafuta ya kutumia nishati ile ya mafuta. Tena Watanzania hata msiwe na hofu na hii shilingi 100; kwa sababu gani? Kuna wakati ambapo mafuta yalipanda kwenye Soko la Dunia sio hata kwa ajili ya shilingi 100, Serikali ikaweka ruzuku ili mwananchi asipate shida. Sasa ikitokea mafuta yanashuka kwenye Soko la Dunia, si mbaya Serikali ikikusanya fedha hizo na ikapeleka kwenye miradi ya kimkakati, kwa sababu hata ikipanda kwa sababu nyingine ambayo sio hii ya shilingi 100 Rais Samia amekuwa akiwapa nafuu wananchi. Kwa nini upate shida? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna wakati mafuta yamepanda hata sio kwa ajili ya shilingi 100 na Rais akatoa unafuu. Sasa kama Soko la Dunia mafuta yanashuka ile difference Serikali ikikusanya ikatekeleza kwenye miradi kuna shida gani. Wanasema huenda yakapanda kule mbele, sasa kama mafuta yakipanda na Rais amekuwa anatoa unafuu kwa wananchi wake, hofu yako ni nini? Angalieni kwa nchi zote za SADC na EAC muone jinsi tofauti ya Rais Samia na maeneo mengine ambavyo walifanya. Kwa hapa aliweza kuweka ruzuku shilingi bilioni 100 kila mwezi na hapo sio kwamba Serikali ilikuwa imepandisha, yalipanda kwenye Soko la Dunia kule. Maana yake kama sio mtu anayejali wananchi wake angekuwa na sababu ya kutosha kabisa kusema yamepanda kwenye Soko la Dunia, kwa hiyo tupambane na hizo hali, lakini yeyye akasema wananchi wasipambane na hali zao, akawapambania kwa kuweka shilingi bilioni 100 kila mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo niwasihii wananchi wenzangu wa Tanzania kwamba hii ni jambo jema kwa maana linataka kutunisha mifuko ya Serikali katika kutekeleza miradi ya kimkakati. Niwakumbushe Watanzania na Waheshimiwa Wabunge miradi ambayo Tanzania inatekeleza, miradi ya maendeleo ambayo Tanzania inatekeleza, hakuna nchi nyingine yoyote, majirani zetu na ukanda wote huu wa Afrika wanaotekeleza miradi mikubwa kwa mara moja kama Tanzania inavyotekeleza, hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo wala tusitoetoe sana mifano mingine mingine, tunaweza tukawa tunatolea mfano kwa watu ambao hawa mradi hata mmoja mkubwa. Unaweza ukasema mbona hawa wanaishi hivi, unaweza ukawa wale unaowatolea huo mfano hawana hata mradi mmoja wa maendeleo, lakini sisi tuna miradi mikubwa ambayo tunatakiwa tujionee heshima kutekeleza miradi ya aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ukubwa wa miradi hiyo unatuonesha sisi ni nchi ya aina gani na vision ile ya viongozi wetu katika kutekeleza shughuli zinazolenga kuwakwamua wananchi kimaendeleo na Waheshimiwa Wabunge miradi hii mtaiona faida yake ikikamilika. Tunapojenga barabara za lami hatuna maana kwamba barabara hiyo tutaenda kukusanya hela, lakini shughuli zile zinazorahisisha katika kutembeza zile shughuli za kimaendeleo ndizo ambazo zinatuletea tija kubwa.

Kwa hiyo, hata hii miradi yote, bandari, reli madaraja, linalolengwa ni hilo, twendeni tuunge mkono wala tusirudi nyuma ndio patakuwepo na mzigo mzigo hivi lakini tuubebe tunaubeba kwa ajili ya nchi yetu na maendeleo yetu.

Mheshimiwa Spika, niwaombe Watanzania haya ni mambo mema yanatutofautisha na watu wengine. Tunataka tunapomaliza dira ile nyingine inayofuata nchi yetu iwe imeshatoka kwenye zile nchi zinazokuwa kwenye lile kundi la nchi maskini zaidi.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo ilitokea kwenye upande cement; Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote naomba watuelewa Serikali kwenye jambo hili, iko namna hii, nchi yetu ilijengwa kwenye misingi ya ujamaa na kujitegemea, watu wengi hizi concept mbili huwa hawazielewi sawa sawa. Ujamaa ni undugu kwamba usifurahie tu wewe pekee yako kufanikiwa huku wengine wakiwa wanapata shida. Sisi tuliokulia kwenye maji, Mheshimiwa Doto anafahamu ile mkijifunika nguo mmoja ilikuwa inaitwa Japan ukiigusa tu hivi inafyatuka inawakimbia wote, kipande kimoja cha Japan mnajifunika watu watano. Kwa hiyo, hapo anapata faida ni yule wa katikati wanakuwa wanapambana hawa wa pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajua usifurahie wewe kufanikiwa pekee yako, lazima umbebe na mwingine wa chini ni jukumu lako, hivyo ndivyo ilivyo. (Makofi)

Sasa niambieni Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukilia dakika zote hapa kuna watoto wanapangwa elimu ya kati pale, wanapangwa waende vyuo vya kati pale, niambieni ninyi wenyewe anapangwa mtoto wa maskini aende vyuo vya kati pale. Vyuo vingine vyote tumewapa waweze kupata mikopo wote, lakini kwa idadi tu ya wingi wa watoto wa Kitanzania kwamba hawawezi wote tena wakaenda kidato cha tano na sita, haujafikiwa huo uwezo labda kwa sababu ya ongezeko linaloongezeka. Hivi tunavyoanza hivi kutoka mwezi wa tano mpaka sasa hivi tangia matokeo yametokea tumelazimika kujenga madarasa ya kuweza kukidhi lile ongezeko, ongezeko la watoto waliofaulu wametoka 75,000 mpaka 192,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuna maeneo mengine kama hivyo vyuo vya kati hivyo MUST, Arusha Technical pamoja na DIT vipo ni vyuo vinavyozalisha wataalam tena wanaotakiwa na uelekeo wa nchi yetu katika kukuza sekta ya ualishaji, lakini watoto wa kimaskini wakienda kule wanakutana na ada. Mheshimiwa Samia akasemaje tutafute kwa yeyote aliye na kaunafuu unafuu atoe shilingi 20 kwa kilo, atoe shilingi 20 tupeleke elimu bure kwenye vyuo vyetu vya kati na tupeleke tuanze kutoa mkopo kwenye vyuo vya kati kwa sababu hata wanaokwenda kwenye vyuo vya kati ni watoto wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutatoa wapi fedha ya kusomesha watoto wetu wa Kitanzania wanaokwenda vyuo vya kati. Ni lazima Watanzania tutagusana tu, ni lazima tutagusana, ndio tutagusana tu. Ndio inaweza ikakuongezea ka gharama, lakini ni lazima tumjali mtoto huyo. (Makofi)

Mimi baba yangu alikuwa na uwezo wa kuuza ng’ombe mmoja naenda sekondari, lakini nilipofika Chuo Kikuu kama nisingepata dirisha lile la grant, nisingeweza kufika kule Chuo Kikuu. Familia za aina hiyo bado zipo, mzazi wa mtoto maskini wa kijijini akiambiwa atoe shilingi milioni tatu, shilingi milioni nne, milioni ngapi, tena wengine wanasomea masomo ambayo tunayahitaji sana, sekta za afya, sekta hizi za uzalishaji. Watanzania tutakuwa tumeonesha mfano mbaya sana wa kizazi hiki cha leo tukishindwa kuwalipia watoto hao kwa sababu tu tunataka tujilimbikizie sisi ambao tumeshapata nafasi hiyo, kwamba wewe uwe hata na nyumba tano, uwe na nyumba kadhaa, lakini wale pale uwaache kabisa kwa sababu tu tunaogopa kubeba mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watoto wa Watanzania ni watoto wetu ni lazima tubebe huo mzigo, nawaomba Watanzania wote tukubaliane na maoni hayo hata kama yanatuongezea mzigo, inatuongezea mzigo kwa ajili ya watoto wetu. Hizo ni fedha ambazo zinakwenda kwenye kutengeneza Taifa lililo bora katika sasa na miaka inayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe Watanzania urithi tuliopewa wa kuthaminiana ni urithi mkubwa sana katika Taifa letu. Hicho ndicho Rais Samia anachokisisitizia kwamba kama una unafuu, haujenda mbali sana, lakini una unafuu wasaidie na wengine walioko chini waweze kupanda, hicho ndicho anachojaribu kutuelekeza kwa kutumia taritibu hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunatambua tunapoenda kuongeza tozo mahali ama kuongeza kodi mahali, ni kweli tunatambua kiwango kile kinaweza kisibaki kile kile. Tunaomba Watanzania wote tuelewane, ni lazima tutekeleze miradi ya kimaendeleo na ni lazima watoto wetu waweze kupata fursa hiyo.

Mheshimiwa Spika, nchi hii imewahi kupita kipindi ambacho watoto walikuwa wanafaulu vizuri halafu wanaambiwa hawajachaguliwa. Wengi wa rika letu hili watafuteni rafiki zetu, wengi walikuwa na akili na walifaulu, lakini waliambiwa hawajachaguliwa kana kwamba kwenda kidato cha kwanza ama kidato cha tano ni uchaguzi, unaambiwa huyu hajachaguliwa.

Mheshimiwa Spika, watoto wameongezeka sana baada ya elimu bila malipo. Tusiirudishe nchi yetu kwenye upungufu wa miundombinu ama upungufu wa uwezo wa kuweza kuwasaidia watoto wanaokwenda elimu ya juu, ama vyuo vya kati, ama sekondari kwa sababu za kibajeti. Ni lazima tuwabebe watoto wetu wote wapate elimu, tena elimu inayolingana, hiyo ndio future ya Taifa letu, ndio maana Rais Samia akaongeza boom elimu ya juu, boom sio lilelile ameongeza, ameongeza elimu bila ada kidato cha tano na sita, ameongeza elimu bila ada kwenye vyuo vile vya sayansi na ameongeza vyuo vya kati viingie hatua kwa hatua kwenye mikopo. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, hata hilo la hatua kwa hatua wala msilichukulie kwa negative na Watanzania wala msilichukulie kama wazo hasi, ni wazo chanya hata sasa kwenye elimu ya juu, sasa hivi kwenye elimu ya juu tulianza kwanza na watoto waliopangiwa vyuo vya Serikali, ndivyo tulivyoanza. Hatukuanza anza tu siku ya kwanza tukaanza vyuo vyote, tulianza na wachache, lakini tukawatumeanza, ikapiga hatua tukaongeza idadi, ikafika hatua tukaongeza vyuo, ikafika hatua tukaenda vyuo vya sekta binafsi ndio wabia wetu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivi sasa tukianza na wachache hii ni bajeti moja ya mwaka huu, mwaka unaofuata ndio na hii hamasa tunayoijenga na hii kukuza sekta binafsi na miradi mingine itakuwa imeisha, miaka miwili ijayo hatutakuwa na commitment za Bwawa la Mwalimu Nyerere. Tutakuwa tumemaliza, uzalishaji utaongezeka, ile saving ambayo tunapeleka trilioni 1.6 kila mwaka haitakwenda tena kwenye bwawa, maana yake tutaongeza uwezo wa kuwapeleka watoto walioko vyuo vya kati vya Serikali na visiovyo vya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais Samia aliona tuwe na mahali pa kuanzia, fikirieni lipi ni jema je, angesema uwezo hauruhusu tukaacha kabisa vile vyuo vyote vya sayansi tukaacha kabisa, vile vya kati tukaacha kabisa, ili tusibiri uwezo utakaporuhusu, la hasha! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yeye akaona twendeni tuanze kidogo kilichopo tuanze hatua kwa hatua kama tulivyoanza zamani. Zamani mikopo ilikuwa inapatikana Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Allied Universities, nadhani Muhimbili pamoja na UCLAS baadaye baadaye ikaja na Mzumbe, baadaye baadaye ikaja UCLAS. Ikaenda ikiwa inakuwa mpaka ikaenda na vyuo vya sekta binafsi. Niwaombe mridhie huu ni utaratibu mzuri utaenda kuwagusa watoto wa Watanzania. Tusiridhike tukiwa tumekosa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo hiyo concept na inatumika sana hata kwenye masuala ya uwekezaji. Siku moja niliona kikatuni cha Kipanya kile, nilikiona kikatuni kile ni kama vile kuna mama mmoja alikuwa anaulizwa, Kipanya anamuuliza hivi katika nchi hii kuna matajiri na kuna maskini, wewe unapendaje, upandishwe uwe tajiri au matajiri washushwe wote wawe maskini? Yule akawaza it’s sadistic mind akasema, kwa kuwa kutajirika ni kugumu mimi naomba washushwe wote tuwe maskini tu. Hilo si wazo jema, kama wanaweza wakapata wachache waanze, tutaenda tukikuwa waanze tunaenda tukikuwa yule ambaye haukuguswa mwaka huu ama kile chuo ambacho hakikuguswa kwa maana labda ni cha sekta binafsi wajue ndivyo tulivyoanza hata vile vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutaenda na miradi fulani fulani tunaimaliza kama nilivyosema Daraja la Busisi linaelekea kuisha na Bwawa la Mwalimu Nyerere linaelekea kuisha. Kwa hiyo, tutaenda tukimaliza miradi hiyo na tutakapokuwa tumemaliza maana yake uwezo wa Serikali utaongezeka. Yule ambaye anakuwa na mashaka kuhusu utekelezaji wa mambo haya ya Rais Samia anajipa mashaka yeye mwenyewe tu. Miaka miwili tu aliyoingia Rais Samia mikopo ya elimu ya juu ilikuwa chini ya shilingi bilioni 500 ilikuwa bilioni mia nne naa, hivyo tunavyoongea imeshafika shilingi bilioni mia saba naa, hilo ni ongezeko kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tunavyoongeza na hii ya vyuo vya kati hii inaenda kwenye shilingi bilioni 800 maana yake anavyomaliza miradi ile mama ni mama mpeni maua yake. Hatuna haja ya kuwa na mashaka. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, Chief Whip amesema nirudie. Mama ni mama, mama yuko kazini mama apewe maua yake. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwenye Biblia wale walienda wakamtembelea Yohana Mbatizaji alipokuwa amefungwa kule wakaenda wakamuelezea kwamba amepita Yesu amefanya hivi na hivi halafu yeye akawatuma, nendeni mkamuulize; je, wewe ni yule tuliyekuwa tunakusubiri au tuendelee kumsubiri mwingine? Yesu hata hakupata shida kuwaelezea zaidi akasema tu, “Wagonjwa wanapona, viwete wanatembea; nendeni mkawaambie heri wale wasio na mashaka na mimi.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa wale wengine wote, wale wengine wote wanaojadili kuhusu 2025. Ndugu zangu nimewatajia miradi yote hii na mambo ambavyo yameongezeka kwa kiwango cha mvua ile ambayo hamuwezi mkaonana nae, kwa kiwango cha mafuriko, unajadilije kuhusu uchaguzi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mengine niliyoyataja hapa kuna mengine hata sikuyataja ambayo Rais anafanya. Unajua mzigo mzito ukibebwa na mwenye nguvu kuna wakati huwa unaweza kuanza kuonekana ni mwepesi. Mambo anayofanya Rais Samia siyo kila mtu anaweza kuyafanya, siyo kila mtu anaweza kuyafanya. Kuna mengine siyo fedha, siyo fedha, siyo fedha lakini kama Kiongozi wa Nchi amesimamia tu mtu apatae haki yake lakini faraja anayoitengeneza kwa watu hao ni kubwa sana na inawaongezea umri wa kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, demokrasia ndani ya nchi kwa sababu ni jambo la kikatiba na kwa sababu imeonekana wazi ni jambo linaloleta maendeleo, jinsi ambavyo Rais amewaunganisha Watanzania ni mtaji mkubwa sana wa maendeleo kwenye nchi yetu na hili watu wote wanapaswa kuliheshimu. Mambo mengine Mheshimiwa Rais anafanya kwa hekima yake yeye kama yeye. anafanya yeye kama yeye na Mungu alivyomjalia anafanya kama kiongozi lakini anasaidia kuiunganisha nchi, anasaidia kuvutia uwekezaji lakini pia anaisaidia nchi kueleweka hata kwenye taasisi za kifedha sisi tukienda kule tunasikilizwa na fedha zinakwenda kwenye majimbo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hayo anafanya kwa hulka yake. Ni mengi tu hata sitaweza kuyataja kwa hiyo ni vyema tukamuheshimu na ni vyema tukamuunga mkono tusije tukafanya kama majuzi ambavyo ilianza kuonekana watu wanaweka weka vimaneno maneno. Mheshimiwa Rais ameonesha mfano ambao ni wa kiongozi na ni wa upekee hata hapa kwenye ukanda achilia mbali Tanzania, hata kwenye ukanda tu wa nchi majirani hakuna ambaye amefanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Katiba ya Nchi iliyoweka vyama vingi hakuna sehemu iliposema Mwenyekiti wa chama tawala aende kwenye chama kingine kwenye shughuli ya chama kingine, ni hulka yake na upendo wake amefanya hivyo. Hata kiwango cha uhuru wa kutoa maoni alichokitoa na hata wengine wakaamua kumsema yeye mwenyewe ni hulka yake na mimi niwakumbushe Watanzania tusije tukafanya kazi ya kuwatengenezea viongozi roho mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapohama kwenye hoja, Mheshimiwa Rais anakaribisha sana hoja lakini unapoondoka kwenye hoja za maendeleo ukaenda kwenye personalities hizo ni jitihada za kutengeneza roho mbaya kwa kiongozi. Tunasahau mapema sana, tunasahau mapema sana kwamba Katiba hii haijabadilika ni hii hii kama kuna wakati umenyimwa uhuru ni Katiba hii hii na kama kuna wakati umepewa uhuru wa kuweza hata kunyoosha kidole namna hiyo na kusema chochote namna hiyo na kubeza namna hiyo na kubagua namna hiyo na kutumia lugha ya kibaguzi namna hiyo ni Katiba ni hii kwenye Lugha ya Kiswahili. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, ni kwamba pamoja na Katiba kuwepo unatakiwa utambue kuwa kiongozi pia amekufanyia uungwana kwamba angeweza kufanya kingine lakini kakufanyia uungwana. Kwa hiyo, Lugha ya Kiswahili inasema, “Usitukane mamba kabla ya kuvuka mto.” Tusifanye jitihada, tusifanye jitihada za kutengeneza roho mbaya kwa viongozi wetu, tuwalipe uungwana. Tuwalipe uungwana, inapokuwepo hoja tujadili hoja kwa Lugha ya Wanairamba tunasema usimfuate mamba kwenye kina kirefu cha maji. Twendeni tuwe tunajikita kwenye hoja tumepewa fursa ya kujadili hoja tuwe tunajikita kwenye hoja. Tuache kuongelea, tuache kuvuka mipaka, tuache kuongelea hoja zinazoweza kuligawa Taifa letu. (MakofiVigelegele)

Mheshimiwa Spika, niliona nilipazie sauti hilo kwa sababu sisi wengine wa rika lako na wadogo zako hatujawahi kuijua nchi nyingine tunaijua Tanzania tu na Mtanzania wa kona yoyote ya nchi ni Mtanzania hakuna nusu Mtanzania na hakuna Mtanzania na nusu. Mtanzania aliyeko kona yeyote ya nchi hii ni Mtanzania. Twendeni tuwe tunajadili hoja zinazoweza kuboresha utekelezaji wa masuala ya maendeleo badala ya kujadili watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa sababu nimesikia kengele. Tumezipokea hoja zote, hoja za kisekta zingine zimejadiliwa na Mawaziri wa Kisekta. Hoja zingine Waheshimiwa Wabunge mmezitoa moja moja, sisi Wizara tutakaa na Wizara za wenzetu za kisekta tutajadili hoja moja moja na zingine Waheshimiwa Wabunge mmekuwa mkifanya kazi nzuri sana na Wapigakura wenu watambue mmekuwa mkifanya kazi nzuri sana za kwenda kwenye Wizara moja kwa moja, mmekuwa mkifanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna Mbunge ambaye hajaenda kumwona Waziri wote mmekuwa mkifanya hivyo mnaenda kufuatilia hoja moja kwa moja kwenye Wizara za kisekta. Kwa hiyo, hata zingine ambazo hatujazijibu ninawatangazia wananchi wenu kwamba Wabunge tutaendelea kukaa kwenye sectors na zile ambazo zinahusu Wizara ya Fedha tutakutana Wizara pamoja na Mbunge kwa eneo mahususi, mradi mahususi ili tuweze kutekeleza na hayo ndiyo ambayo Mheshimiwa Rais amekuwa akitutuma na mengine Mawaziri wa kisekta pamoja na watendaji watakuja kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisisitize moja la mwisho, twendeni tuendelee kuhamasishana kwa ajili ya kulipa kodi na kule watendaji tuendelee kusimamia miradi kwa ukaribu ili fedha hizi ambazo zinakwenda kule ziweze kutimiza malengo yaliyokusudiwa. Watendaji wote wa Serikali mnapopokea kule kwenye wilaya zetu, mnapopokea fedha watendaji wote mnapopokea fedha wajulisheni Wabunge hawa ambao wanafuatilia fedha huku kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haikupi gharama kumwambia Mbunge fedha zile ulizokuwa unafuatilia zimeshakuja na tunaanza utekelezaji haina gharama. Ni uungwana, yeye kafuatilia, yeye kafikisha mpaka kwa Rais, Rais amemjibu, fedha zimekuja kwenye jimbo lake ni jambo dogo tu mjulishe kwa sababu fedha zinaweza zikaja kabla ya vikao vile rasmi ambavyo vinakaa, mjulishe. Mimi ndivyo ambavyo wenzangu kule Iramba wamekuwa wakiniambia, wanawaambia madiwani, wanawaambia Mwenyekiti wa halmashauri, wananijulisha na mimi nashiriki na nikifika kwenye vikao tunaenda sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, watendaji wote, wakurugenzi wote wajulisheni Wabunge fedha zinapofika. Mama amewasikiliza Wabunge ameleta fedha kwa ajili ya shughuli za maendeleo, wajulisheni kama zimekuja kabla ya kikao, msisubiri kuja kusema wakati wa vikao ili waendelee kutafuta fedha zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge mpokee salamu za Mheshimiwa Rais, yuko nanyi bega kwa bega tulipokuwa tunapitisha, tulipokuwa tunatoa briefing ya kikao hiki alisema yuko nanyi bega kwa bega na anawaomba mkitoka hapa mpeleke salamu kwa wananchi wote na yeye anawatakia kila la kheri. Anawaunga mkono, mko naye pamoja mtakapokuwa mnaelekea majimboni mwenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika na baada ya kusema hayo sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naafiki.