Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isidor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Fedha na Mipango, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha ubunifu wa ukusanyaji mapato na usimamizi mzuri wa matumizi ya Serikali ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa miradi ya kimkakati na pia utayari wetu wa Ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.” Pia mapendekezo haya yanazingatia dhima ya bajeti 2023/2024 ambayo ni kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi, kuhimili na kukabili athari za mabadiliko ya tabianchi, na kuimarisha sekta za uzalishaji ili kuboresha hali ya maisha.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za uchumi katika nchi nyingi duniani yakiwemo mataifa makubwa, Tanzania imefanya vizuri katika kusimamia ukuaji wa pato la Taifa lilikua kwa asilimia 4.7 ukilinganisha na wastani wa asilimia 3.9 kwa nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara; mfumuko wa bei umeendelea kubaki katika wigo wa tarakimu moja ambapo kwa mwaka 2022 ulikuwa asilimia 4.3 ukilinganisha na wastani wa asilimia 11 kwa nchi za Afrika Mashariki; na thamani ya shilingi ta Tanzania dhidi ya dola imeendelea kuwa tulivu ambapo kwa mwaka 2022 ilibadilishwa kwa wastani wa shilingi 2,314.50 kutoka shilingi 2,309.2 kwa mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, pia pamoja na upungufu wa fedha za kigeni, bado akiba ya fedha za kigeni ilikuwa USD milioni 5,177.2 sawa na uwezo wa uagizaji wa bidhaa na huduma kwa miezi 4.7 kutoka akiba ya USD milioni 6,386 ya mwezi Desemba, 2021 sawa na miezi 6.6 ya uagizaji. Upungufu wa fedha za kigeni kwa kiasi kikubwa umesababishwa na mfumuko wa bei katika soko la dunia, ulipaji wa madeni ya nje, pamoja na kugharamia miradi ya kimkakati. Hali hii imepelekea kuongezeka kwa nakisi ya urari wa malipo kufika USD milioni 4,414.2 kwa mwezi Julai, 2022 kutoka USD 2,516.1 kwa Julai, 2021.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uhaba wa fedha za kigeni, napendekeza Serikali iendelee kwa kasi na jitihada za kununua na kutunza dhahabu kama sehemu ya fedha za kigeni. Ununuzi ulenge pia kununua dhahabu toka kwa wachimbaji wadogo hata kwa bei ya ushawishi ili kuzuia utoroshaji unaosababisha kupunguza mapato ya fedha za kigeni. Kutokana na mabadiliko ya kiuchumi kidunia, Benki Kuu nyingi duniani zimeanza kuwekeza zaidi kwenye dhahabu na hii ni ishara nzuri kwa bei ya dhahabu kuendelea kuimarika kwenye soko la dunia ambapo kwa mwezi Aprili, 2023 bei imepanda kwa zaidi ya asilimia 11 ukilinganisha na bei za Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua nzuri za kurudisha Mfuko wa Dhamana kwa Wakopaji Wanaozalisha Bidhaa kwa Soko la Nje (Export Credit Guarantee Scheme) ambayo itachochea kuongezeka kwa mauzo ya bidhaa nje. Pamoja na uanzishwaji wa mfuko huu, Serikali isimamie uzalishaji wa tija na pia kusaidia kupata masoko ya nje ili bidhaa zetu zipate bei ya kiushindani.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kulipa fidia ya wananchi wanaopisha Mradi wa Liganga na Mchuchuma. Baada ya fidia, napendekeza Serikali kuchukua hatua za kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa chuma (Liganga Iron Ore) ikiwa ni pamoja na makaa ya mawe (The Mchuchuma Coal Mining and Power Projects). Mradi wa Liganga na Mchuchuma unatarajia uwekezaji wa zaidi ya US$ bilioni tatu na kuzalisha ajira zaidi ya 30,000.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Mradi wa Liganga na Mchuchuma, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya Niobium ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja na reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapa kwetu. Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya Niobium ambayo yanapatikana Panda Hill Wilaya ya Mbeya, na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) yanaendelea kuwa makubwa duniani na hapa kwetu pia.

Mheshimiwa Spika, Serikali inahitaji kujiwekekea mikakati ya haraka (quick wins) ili kuhakikisha inaimarisha uchumi ikiwemo kupunguza urari wa malipo ambao umefika USD milioni 4,414.2 kwa Julai, 2022 kutoka USD 2,516.1 kwa Julai, 2021. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini yakiwemo ya chuma, makaa ya mawe, na Niobium, kuna fursa ya kuvutia uwekezaji wa nje (FDI) ambao ni zaidi ya USD bilioni tatu katika kipindi cha miaka miwili mpaka mitatu. Pamoja na fursa ya ajira ya zaidi ya 30,000 kwa Liganga na Mchuchuma kuna fursa ya kuvutia uwekezaji (FDI) wa zaidi ya USD bilioni tatu, wakati huo huo Niobium ina fursa ya uwekezaji wa zaidi ya USD milioni 200 na kuzalisha ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakuwepo ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000.

Mheshimiwa Spika, mradi utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (US$ 220 million) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka shilingi bilioni 50 (US$ 22 million) uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (Modern Manufacturing Plant and Smelter).

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki wakati dunia inapambana na changamoto za kiuchumi, napongeza hatua za Serikali kwa kuwasilisha Muswada wa Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria ya PPP, Sura 103 na ambayo yamepitishwa na Bunge tarehe 13 Juni, 2023. Serikali imeonesha utayari wa kujenga reli ya Kusini ya Mtwara – Mbambabay na reli ya Kaskazini (Tanga-Arusha-Mara) kwa njia ya ubia baina ya Serikali na sekta binafsi (PPP).

Napendekeza pia kuharakisha ujenzi wa barabara ya Kibaha – Morogoro (kilometa 205) na baadae Morogoro hadi Dodoma ili iweze kutekelezwa kwa utaratibu wa PPP, na iende sambamba na ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara ya mzunguko wa nje katika Jiji la Dodoma (kilometa 112.3).

Mheshimiwa Spika, pamoja na PPP napongeza Serikali kwa kuanza utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara saba zenye jumla ya urefu wa kilometa 2,035 zenye gharama ya takribani shilingi trilioni 3.7 kujengwa kwa kutumia mfumo wa Engineering, Procurement, Construction and Financing (EPC+F). Katika barabara hizo saba ni pamoja na barabara ya TANZAM kipande cha Igawa – Songwe – Tunduma (kilometa 218) pamoja na barabara ya mchepuo ya Uyole – Songwe (kilometa 48.9).

Mheshimiwa Spika, kutokana na fursa za uzalishaji mkubwa kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, napendekeza muendelezo wa uboreshaji wa barabara za Mbalizi – Shigamba – Isongole kutokana na uzalishaji wa mazao ya kilimo; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongolosi kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na madini; na pia barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete ambayo ni muhimu sana katika kusafirisha mazao ya kilimo ikiwemo maua, parachichi na viazi kwa soko la nje.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea kwa kasi ile ile na pia napongeza jitihada za kuendelea kutafuta vyanzo vya fedha vya masharti nafuu kugharamia ujenzi huo. Pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa, Serikali imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na huduma katika bandari zetu hususana Bandari ya Dar es Salaam ili kukabiliana na ushindani mkubwa wa bandari zingine za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Spika, Bandari ya Dar es Salaam inakumbana na ushindani mkubwa toka Bandari za Mombasa (Kenya), Beira (Msumbiji), Nacala (Msumbiji), Durban (Afrika Kusini), Lobito (Angola) na Walvis Bay (Namibia). Maboresho ya bandari zetu yaendane na kuondoa changamoto zingine ambazo zinasababisha gharama kubwa za usafirishaji kwa bandari zetu na kusababisha kupoteza biashara ya usafirishaji kwa bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, ufanisi wa bandari unategemea pia maboresho ya barabara, Reli ya Kati (TRL), Reli ya TAZARA, utendaji wenye tija wa wadau wote wa bandari na hata watumishi ili kupunguza gharama za usafirishaji kwa wateja wa bandari zetu. Kwa sasa karibu asilimia 70 ya mzigo wote wa nchi za nje unasafirishwa kwa kupitia Dar es Salaam Corridor ambapo DR Congo ni asilimia 38, Zambia asilimia 26 na Malawi asilimia sita. Pamoja na fursa za kijiografia ya bandari zetu, mzigo unaopita sasa kwenye Bandari ya Dar es Salaam, ni chini ya asilimia 50 ya biashara yote ambayo kwa sasa sehemu kubwa inashikiliwa na bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, napongeza Serikali kwa maboresho ya uwanja wa ndege wa Songwe, na kutokana na maboresho hayo napendekeza kujengwe maghala (cold rooms) kwa ajili ya kuhifadhi mboga mboga, matunda, nyama na samaki kwa soko la nje. Uwanja wa ndege wa Songwe upo kimkakati kwa kuhudumia wafanyabiashara wa hapa nchini na pia nchi jirani za Zambia, DRC na Malawi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ATCL iboreshe muundo wake wa utumishi kulingana na biashara iliyopo ya usafiri wa anga ili kupunguza mzigo wa gharama na kuongeza ufanisi. Pia ATCL ianzishe njia za safari za ndani na za nje zenye fursa ya kuongeza biashara kama vile safari za moja kwa moja za Mbeya – Dodoma, Mbeya – Lilongwe, Mbeya Lubumbashi na Mbeya – Lusaka.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iangalie upya mapendekezo ya kuboresha muundo wa mfuko wa asilimia 10 kwa ajili ya mikopo kwa vijana, wakina mama na makundi maalum. Napendekeza mfuko huu uboreshwe na uwe sehemu ya mpango wa kuwawezesha kiuchumi makundi lengwa kwa misingi ya huduma za kifedha shirikishi (financial inclusion). Msukumo uwe kwenye elimu ya ujasiriamali na kuwasimamia kwa karibu wakopaji ili kuongeza tija na pia kuboresha uchumi wa wakopaji na Tanzania kwa ujumla.

Napendekeza pia kujumuisha huu mfuko uwe kitaifa na uendeshaji uwe katika misingi ya taasisi za kifedha, lakini kwa masharti nafuu ikiwemo bila riba na Serikali iunganishe mifuko yote ya makundi maalum na yaunde taasisi moja imara chini ya Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.