Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika maazimio haya mawili, Azimio la Kigosi pamoja na lile la Ruaha.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kumpongeza kwa moyo wa dhati Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, lakini pia kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu.

Mheshimiwa Spika, hakika sisi Wanakamati tunaona sasa namna gani sekta ya maliasili na utalii inakwenda kuwa na tija katika Taifa letu, na hasa kwa kuendelea kutatua migogoro ambayo imekuwa ikiikabili sekta yetu ya maliasili na utalii.

Mheshimiwa Spika, nitaanza kuchangia kwa eneo la Ruaha kwa maana ya kule Mbarali. Niendelee kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa ekari zaidi ya 74,000 na kuweza kuwagawia wananchi. Mheshimiwa Rais ana nia njema na Watanzania na ndiyo maana ameweza kutoa sehemu hii ya eneo hili ili wananchi hawa waweze kwenda kujiendeleza kimapato kwa maana ya kuyatumia sasa maeneo haya kwa uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutumie nafasi hii kuendelea kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuungana na Kamati na kwenda Mbarali na kuona tatizo na changamoto ambayo imeweza kuwakuta wananchi, kero ambayo ilikuwa Kapunga I kupitia Kapunga II ambayo amepewa mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kuipongeza Serikali kwa kuwa sikivu kwa kuona sasa ni busara kutoa baadhi ya maeneo na kuikabidhi Serikali ili wananchi waweze kupatiwa na kuendelea kutatua mgogoro kati yao na zile hisia walizokuwa nazo kuhusu kupendelewa kwa mwekezaji. Kwa hiyo, niipongeze Serikali kwa kuitoa hiyo sintofahamu kwa wananchi kuhusu kupendelewa kwa mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, sasa tuiombe Serikali, wananchi wanakuwa na mgogoro na mwekezaji kwa sababu eneo lake lina manufaa, lina miundombinu ya kutosha ambayo inaweza kumzalishia na kumpatia kipato. Tuombe sasa na upande huu wa wananchi ambapo ni eneo la Kapunga I liweze kuwekewa miundombinu, na hii Wizara ya Kilimo pia ishirikishwe ili wananchi wale lile eneo ambalo wamepatiwa liweze kuwa na tija ya uzalishaji na kuondoa migogoro ambayo imeweza kuonekana kati yao na mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, eneo lile likiwekewa miundombinu litaendelea kuwapunguzia wananchi gharama kwa sababu hata kwa sasa kule kwa mwekezaji wanakodisha lakini wanakodisha kwa gharama kubwa sana. Wakipewa eneo lao hili wataweza kupata ghrama nafuu na kuweza kunufaika nalo.

Mheshimiwa Spika, tuendelee kutoa rai kwa timu ya Mawaziri nane. Tumeona mfano leo Azimio hili limeweza kuingia huku Bungeni na linakwenda kupita kwa sababu ni azimio ambalo lina tija kwa Watanzania. Ile timu ya Mawaziri nane ina kazi sasa ya kuleta kile ambacho wamekwenda kukifanya kwa sababu ni maeneo makubwa na mengi wameweza kwenda kuyafanyia kazi, Serikali imegharamika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa waje watuambie ni maeneo yapi ambayo tayari migogoro imekwisha ili wananchi kuendelea kuondoa sintofahamu na wabaki wakiendelea kuifurahia Serikali yao kama ambavyo wanaifurahia sasa huko Mbarali pamoja na Kigosi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, niende sasa kwenye eneo lingine la Kigosi. Tunaipongeza sana Serikali na tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 2.5 kuwekeza miundombinu ya kisasa kwa ajili ya viwanda vya kuchakata asali.

Mheshimiwa Spika, hii italeta tija sana kwa wananchi na hasa wananchi wa maeneo ya Mlele, Kibondo, Nzega, Sikonge, Bukombe. Nitoe rai kwa wananchi hao, Mheshimiwa Rais ana nia njema, eneo hili limeenda kutolewa kwa wananchi, basi tuombe Serikali kupitia TFS ambayo ndio inaenda kuwa msimamizi kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanapewa nafasi ya kuingia na wasipewe vikwazo, tusianze habari ya vibali vingi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wafuate utaratibu na Wizara watumie nafasi hii sasa kutoa elimu kwa wananchi, nini ambacho wanatakiwa kufuata na taratibu zipi za Kiserikali zinatakiwa kufutwa ili wananchi hawa sasa waende kunufaika kama ambavyo walikuwa wakinufaika mwanzo kwa kufanya matambiko, lakini pia kuweka mizinga yao. Pia bila kusahau wahakikishe kwamba wanaenda kuhakikisha vijana wanakwenda kupewa elimu ili na wao, hili eneo ambalo limetolewa na Mheshimiwa Rais liweze kuwa na tija ya kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuipongeza Wizara kwa kuendelea kutafuta masoko China pamoja na Marekani. Bado malighafi, nyingi zitahitajika hapa kwa hiyo ni jukumu la Wizara sasa kwenda kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi ili maeneo haya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa yaweze kwenda kuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuipongeza sana Wizara kwa kuendelea kutatua changamoto na huu ni mfano mzuri, sisi kama Kamati tutaendelea kuwaunga mkono katika kuhakikisha kwamba tunalinda rasilimali zetu, tunazitunza, tunazihifadhi lakini pia tunatoa fursa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja kwa maazimio yote mawili. Ahsante sana. (Makofi)