Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Bajeti yetu Kuu. Kwa kuanza naomba nitambue kazi kubwa ambayo inafanyika. Si haba kupandisha pato la Taifa kutoka bilioni 69.9 mwaka 2021 kwenda bilioni 89.4 dola za Kimarekani ni kazi kubwa sana na matumaini ya kwamba bajeti yetu au pato letu la Taifa litaendelea kukua kwa asilimia 5.2, ni kazi kubwa imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya kilimo imeongezwa kutoka bilioni 294 mpaka kufikia bilioni 970.8 mwaka 2023/2024. Hapo tunajihakikishia kwamba tutapata pembejeo, viuatilifu vya kutosha, zana za kilimo lakini wakulima wetu wataendelea kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa afya tumejenga vyumba 111 vya huduma za dharura na pale Hanang sisi tumepata chuma kimoja ambacho kinakaribia kukamilika, vyumba vya wagonjwa mahututi 70 navyo vinakwenda kujengwa, navyo vinaenda kukamilika, nyumba za watumishi wa afya 150 zimejengwa na sisi Hanang tumepata nyumba moja na tumeipeleka pale Zahanati ya Gidagharibu pale Kata ya Simbay. Hii ni kazi kubwa imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepeleka vifaatiba katika maeneo mbalimbali. Hanang tumepata x–ray ya kisasa katika Hospitali ya Wilaya ya Tumaini, lakini vifaa kama CT-Scan zaidi ya 30 zimepelekwa, MRI na vifaa vingine. Hanang tunatarajia kupata ambulance mbili, ni kazi kubwa imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya nishati, miradi mikubwa inaendelea. Bwawa la Mwalimu Nyerere linaendelea kukamilika, lakini na miradi mingine inaendelea kukamilika ili kujihakikishia kwamba gridi yetu inakuwa na umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa imefanyika kwa upande wa TARURA, barabara nyingi zimejengwa. Tumejenga kilometa 798.1 za lami, lakini kilometa elfu 23.2 hizo za changarawe pamoja na madaraja kadhaa. Mpango wa kutengeneza P4R kwenye upande wa ujenzi wa barabara, hii itatusaidia sana. Ndio maana unasikia Wabunge hapa wanasifia kazi nzuri inayofanyika na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Wengine wanasema tumpe maua yake, naunga mkono maua yake apewe kwa kazi nzuri inayofanyika na sisi kwenye majimbo yetu kila sehemu amegusa, ni kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kukumbusha kwenye eneo la TARURA, tunayo majimbo tofauti. Kwenye Jimbo la Hanang kwa sensa ya sasa hivi tuna watu 367,391, kaya ziko karibu 70,000. Vilevile tuna majimbo mengine madogo ambayo hata watu 100,000 hawafiki, kupewa mgao sawasawa sio sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye upande wa nishati hilo pia limefanyika, kwamba kila Jimbo lipewe vitongoji 15 kwa mwaka huu wa fedha. Hilo sio sawa kwa sababu haitaleta tija, tumefanya sensa tumetumia fedha. Hii sensa itumike na wataalam ili hatimaye mgawanyo wa rasilimali uende sawia kwenye majimbo yetu, maendeleo yaende sawa sawa kwenye majimbo yetu. Idadi ya watu izingatiwe ndio maana tumeingia gharama, jiografia ya maeneo yetu izingatiwe ili hatimaye maendeleo yaende sawasawa kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewekeza sana kwenye sekta ya kilimo. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo anafanya kazi kubwa sana na timu yake. Nampongeza sana rafiki yangu Mheshimiwa Bashe. Hata hivyo, nimhakikishie tumeanza kuingia mashambani mwezi wa 11, kila mtu amepambana kwa namna yake, wengine wamepata na wengine wamekosa. Sasa hivi tuna changamoto na leo hii mimi niko hapa Bungeni kule kwangu wamekaa kikao, maelekezo ni kwamba ukitaka kusafirisha gunia moja la mahindi kwenda Babati, kwenda Arusha mpaka upate kibali kutoka kwa Mkuu wa Wilaya, hii inatoka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wameenda mashambani kipindi kile Serikali hatukuiona. Sasa hivi tumevuna, tumehangaika wenyewe mbona control zinakuwa nyingi? Kwa nini Serikali isiwe proactive inakuwa reactive? Sisi tunachotaka tukiingia mashambani, Wizara tumeweka fedha za kutosha, wachochee uzalishaji. Wasiende kudhibiti baada ya watu kuwa wamesota mashambani, wao wanazuia sijui watu wasiuze, sijui wasifanyeje. Hii si kazi ya Serikali, Serikali itusaidie tuzalishe zaidi na itusaidie kuweka mifumo mizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwa inajulikana kwamba kuanzia mwezi Machi hadi sasa tutavuna. Kwa nini mipango hai isiwepo kabla hata muda huu haujafika? Tusiwakwamishe wakulima. Sisi wana Hanang na Watanzania wengi wako kama wana Hanang wanategemea yale wanayopata mashambani, wanategemea mifugo yao kupeleka watoto shule, ni kipindi cha shule kufunguliwa. Sasa hivi biashara ya mazao haieleweki, mifugo tumeuza wakati tunakwenda mashambani. Sasa, unategemea watoto watarudije shule? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itusaidie wakati tunakwenda mashambani, watusaidie mbolea na vitu vingine ili angalau wakati huo tukishazalisha watutengenezee na masoko. Vile vile, kwenye eneo la masoko iwe streamline tuijue, suala la masoko yanakuwa Wizara ya Kilimo au Viwanda na Biashara ili mwishoni sasa tum–task Waziri wa Kilimo kwenye suala la uzalishaji ili upande wa viwana na biashara wahangaike kututafutia masoko. Watusaidie kwenye eneo hili mambo haya yanawachanganya wananchi wetu na hii haikai sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujawahi kumwona Mkuu wa Wilaya wakati tunakwenda mashambani na hatutarajii kumwona Mkuu wa Wilaya sasa hivi wala kwenda kuomba kibali kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kidogo suala la miundombinu. Pia kwenye eneo hili, kazi kubwa yamefanyika. Nikisoma kwenye upande wa uchukuzi, reli hesabu zinasomeka vizuri, lakini napata changamoto kubwa kwenye upande wa barabara. Mwaka 2022 kwenye bajeti kama hii, nilipata nafasi ya kukaa na Waziri wa Ujenzi, tukachorachora Barabara, lakini mpaka sasa sioni kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara inayotoka Kondoa inayokwenda Gisambalang inayotokea Nangwa tulichorachora na Mheshimiwa Waziri mwaka 2022, lakini hakuna kinachoendelea. Vilevile barabara ya Katesh – Haydom, mara zote nimeambiwa hapa Bungeni ni sehemu ya barabara inayotoka Karatu – Mbulu – Haydom – Mto Sibiti – Lalago mpaka Maswa. Juzi wamekwenda kusaini mkataba hata mwaliko Mbunge wa Jimbo la Hanang sikupata na tuna tawi letu hilo ambalo kila mwaka tunaambiwa ni sehemu ya barabara hiyo. Je, yale niliyokuwa naambiwa hapa nilikuwa nadanganywa au wananchi wa Hanang wanadanganywa au Mbunge nilikuwa nadanganywa? Naomba ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha alikuwa pale Katesh, babu zake nilivyosema hiyo barabara, nikawambia unabeba pochi ya Mama na yeye ni mtoto mwaminifu wa mama, hiyo pochi ambembeleze mama aifungue kidogo hiyo barabara ijengwe. Wana-Hanang ni wale waliopiga makofi Waziri akatikisa kichwa, lakini mpaka leo hakuna kitu alichoweka pale, hakuna kinachoeleweka. Sasa sisi tufanye nini? Kwenye bajeti hii nikisema naunga mkono bajeti, narudi Hanang wananipokeaje? Tusemezane tu ukweli si aliwambia mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahati nzuri Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Kampeni amesimama Bassotu, Katesh, Gehandu, tumeongea barabara hiyo hiyo. Tukirudi nyuma Dkt. Magufuli alifanya hivyo hivyo. Tukirudi nyuma Dkt. Jakaya Kikwete naye alifanya hivyo hivyo, mimi nikirudi sasa hivi naenda kuwaambia nini? Tuelezane tu ukweli, barabara hii tumeisema sana na si mimi wa kwanza kuisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2020 Dkt. Mary Nagu alisimama hapa Bungeni akidai barabara hiyo…

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Engineer Hhayuma kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Miraji Mtaturu.

TAARIFA

MHE. MIRAJI J. MTATURU Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji mtani wetu ambaye ametuita sisi babu zake kwamba, unapoambiwa barabara ni kiungo maana yake barabara kuu itakamilika feeder road itajengwa. Kwa hiyo, maana yake ndiyo hiyo tafsiri halisi ya barabara ambayo inaungiwa pale. Ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Engineer Hhayuma, unapokea taarifa?

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, namheshimu sana mjukuu wangu lakini naomba asitumie muda wangu na naomba tu unilindie muda wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara hii limesemwa mara nyingi kwamba ni feeder road na maneno yamekuwa ni mengi. Sisi tunachotaka barabara hiyo ijengwe na wala hatutaki maneno mengine na ili nijiridhishe kwamba kwenye bajeti hii tuko pamoja nipate maelezo ya kina na wala sina lingine zaidi ya hilo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako ndio umekwishayoyoma hivyo. Malizia sentesi yako.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi na naamini Mheshimiwa Waziri atakuwa na maelezo ya kina ili tukubaliane bajeti hii ni ya kwetu au ya kwake?

MWENYEKITI: Ahsante sana.