Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali ambayo ipo ndani ya Bunge letu na sisi kama Wabunge tunaendelea kuichangia na kuiunga mkono asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba Waziri wa Fedha na timu yake nzima ya Wizara yake kwa namna ambavyo wamejipanga kuhakikisha kwamba wanaleta mapinduzi ya kweli katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa bajeti iliyokuja sina mashaka nayo na mimi nawatakia kila la kheri Mwenyezi Mungu aendelee kuwaongoza katika kuhakikisha kwamba trilioni 41 na zaidi iweze kupatikana ili mipango ya kimaendeleo katika nchi yetu iweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anachapa kazi lakini kwa namna ambavyo ametekeleza miradi mikubwa ya kimkakati na ya kimaendeleo inayogusa jamii yetu. Sisi kama Wabunge kupitia majimbo yetu tumeshuhudia kuona miradi mbalimbali imetekelezwa na tumeendelea kupiga hatua kubwa. Mheshimiwa Rais wetu ni mzalendo wa kweli na kweli anataka kuleta mapinduzi ya kweli kuhakikisha kwamba anapunguza umaskini nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze ndugu zetu wa TRA kwa namna ambavyo wameendelea kuleta ufanisi katika ukusanyaji wa mapato kwa miaka mitatu mfululizo kama taarifa ya Kamati ilivyotueleza. TRA wanatufanyia kazi nzuri, lakini kulipa kodi ni uzalendo. Wako wafanyabiashara ambao mteja anapoingia dukani kununua bidhaa na kumuuliza kwamba unataka bei ya risiti ama bei isiyokuwa ya risiti, huu si uungwana. Ninawaomba wafanyabiashara Watanzania tuwe wazalendo wa kweli tuhakikishe kwamba tunaiunga mkono Serikali kwa kutoa risiti. Watanzania wanapaswa wawe wazalendo kwa nchi yao kuhakikisha kwamba wanaponunua bidhaa basi waweze kudai risiti ili kwa pamoja tuungane kuhakikisha kwamba nchi yetu inasonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Wizara ya Nishati; Wizara ya Nishati wanafanya kazi nzuri na sisi tunaiona, na mimi naendelea kuwabariki kwa sababu tunaendelea kunufaika na suala zima la nishati. Lakini wamekuja na mpango mahususi wa kumtua mama kuni kichwani. Mpango huu ni mzuri, Watanzania sasa tumechoka kutumia kuni na mkaa, na Watanzania walio wengi wanapenda kutumia umeme na gesi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani. Hasa sisi wanawake wa Mkoa wa Lindi na Mtwara tumechoka kutumia kuni na mkaa. Kwanza vinaathiri afya yetu ule moshi tunaovuta ukiingia ndani ya mapafu tunaathirika afya zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe sana Waziri wetu wa Fedha kuhakikisha kwamba vifaa vya matumizi kama majiko ya gesi, majiko ya umeme, pasi na vinginevyo vinaondolewa ama vinapunguzwa kodi ili wananchi Watanzania waweze kumudu kununua majiko haya na waachane na matumizi ya mkaa na gesi. Wenzetu wameanza na kampeni nzuri na Wizara ya Fedha tuunge mkono kampeni hii inayofanywa na Wizara ya Nishati kwa kuhakikisha kwamba vifaa hivi vinapunguzwa bei ili Watanzania waweze kumudu kununua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Wizara ya Kilimo. Niwapongeze Wizara ya Kilimo kwa sababu wameongezewa bajeti ya milioni 900. Tuna mfumo wa ununuzi wa pembejeo, ninaomba Serikali waangalie kwa sababu mfumo huu hauendani na kalenda ya upuliziaji wa dawa ya mikorosho. Kwa hiyo ninaomba wabadilishe mfumo huu wa manunuzi wa pembejeo ili uendane na kalenda ile ambayo wakulima wanahitaji pembejeo kutumia katika zao hili la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pia ndugu zetu wa TAWA pamoja na ASA aongezewe bajeti yao kuhakikisha kwamba wanaendelea kufanya utafiti wa kuzalisha mbegu bora ili wakulima waweze kupata mbegu yenye kuleta tija katika uzalishaji wa mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie suala la wazalishaji wa chumvi. Wazalishaji wa chumvi mpaka unapata kiroba cha kilo 25 gharama yake inafika takriban shilingi 4,500. Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto mbalimbali, chumvi isiyotiwa madini joto maana yake haiwezi kutumika. Wizara ya Afya walitoa mafunzo na madini joto yalitolewa bure, lakini ikaenda madini joto kilo moja ikafika shilingi 30,000, na sasa hivi madini joto kilogram moja ni 150,000. Hii imekuwa ni changamoto na ni hatari tunaweza tukatumia chumvi ambayo haina madini joto kwa sababu ya gharama kubwa ambayo wanaifanya hawa wazalishaji wa chumvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali kama ambavyo tunatoa pembejeo basi kwenye wazalishaji wa chumvi tutoe madini joto kwa ruzuku ya Serikali ili wazalishaji wa chumvi waweze kupata unafuu na urahisi wa kutumia madini joto na chumvi yetu iweze kutiwa madini joto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la ujenzi. Nipongeze Serikali kwa hatua mbalimbali tunazoendelea nazo za kuhakikisha kwamba njia ya kukua kiuchumi zinaboreshwa. Lakini tunayo changamoto, naomba tufanye mapitio tena ya sera na kuangalia sera ya barabara. Barabara hizi ambazo zinaunganisha Bandari na nchi jirani, barabara kuu za kiuchumi hazijengwi kwa ubora ule unao stahili, ama zikijengwa hazichukui hata mwaka tayari zimekufa. Pamoja na kwamba tunayo mizani ya kudhibiti uzito wa magari barabarani lakini bado barabara zetu zinaendelea kuwa mbovu na Serikali inatumia gharama kubwa sana kuhakikisha kwamba kila mwaka barabara zinafanyiwa ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe Serikali kuhakikisha kwamba tunaweka mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba barabara hizi zinakuwa imara na zinaweza kudumu zaidi ya miaka miwili mitatu ili kuokoa fedha ya Serikali na iweze kwenda kufanya kazi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwazungumzie wakandarasi wa Tanzania hasa wale walioanzia class seven. Tunajua kwamba wao wanapata kazi ndogondogo lakini bado wana changamoto, kwanza wanapopata mradi wanakwenda kusajili mradi TRB, pia wanasajili mradi OSHA, na bado wanalipa madini, kokoto, mchanga na mawe wanalipa SBL kwa maana ya Levy kwa vibarua lakini bado wanalipa fire, wanalipa NEMC, bado wanalipa kodi ya TRA. Utakuta mlolongo wa tozo unakuwa mkubwa sana kwa hiyo wanatumia gharama kubwa lakini wakati mwingine viwango vinakuwa tofauti tofauti kila mara. Niombe Serikali kuhakikisha kwamba viwango basi viwe vinafanana kila wakati visiwe vinabadilika. Kwa hiyo niombe sana Serikali kuhakikisha kwamba wanaendelea kuwatazama wakandarasi hawa ili nao wawe wakubwa ili waendelee kufanya kazi zetu na wasaidie watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu. Tumeona matunda mazuri katika maeneo yetu, tumefarijika sana. Miradi mikubwa ya maendeleo iko katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)