Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa mwisho kwa mchana huu wa leo kwenye bajeti hii ya Serikali.

Kwanza niseme kwamba naunga mkono kauli ya Mheshimiwa Mbunge wa Singida Mashariki, Mheshimiwa Miraji Mtaturu kwamba wapo watu katika nchi hii wanaona taabu mtu akipongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwakumbushe Watanzania, mtu asiyependa kupongeza ni mtu mwenye wivu au ni mtu msahaulifu kwa mema aliyofanyiwa. Kwa hiyo, nimesoma bajeti hii ya Wizara ya Fedha na nimejiuliza swali moja tu: Je, bajeti hii inajibu kero za wananchi wangu wa Lupembe? Nimekuta jibu ni ndiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti hii imebeba matumaini makubwa, imebeba miradi ya umeme kwa wananchi, imebeba miradi ya barabara, imebeba miradi ya maji ya Kichiwa, Maduma na Tagamenda, Nyombo, Matigangila, na kadhalika. Bajeti hii ya Wizara ya Fedha imebeba fedha ya kupeleka mbolea ya ruzuku kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, hii ni bajeti muhimu. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kwa ajili ya Taifa letu. Nami kwa niaba ya wananchi wa Lupembe, namwombea Mheshimiwa Rais afya njema na siha njema ya kufanya kazi kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Mchemba, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara hii. Kwa mara ya kwanza Watanzania wameshuhudia kwenye majimbo yetu, tunayo miradi mingi mpaka imefika mahali wakandarasi hawapatikani, fedha ziko nyingi sana. Mambo haya yamefanikiwa kwa sababu, Waziri wetu wa Fedha bila shaka amekuwa ni mshauri mzuri sana kwa Mheshimiwa Rais. Nasi tunamuunga mkono, tuendelee kupeleka fedha wananchi wapate maendeleo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kukishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi, na kipekee namshukuru Katibu wetu wa CCM, Comrade Daniel Godfrey Chongolo kwa kusimamia vizuri Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Wabunge tumeshuhudia mahali pengi, Katibu wetu Mkuu na timu yake wanatembea kwenye majimbo yetu wakitoa hamasa kwa wananchi na kutoa wito wa ilani kutekelezwa. Hongereni sana Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chingolo na timu yako yote ya chama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye mchango wa bajeti. Nianze kwenye eneo la changamoto za wafanyabiashara. Nimesoma kwenye Bajeti hii ya Serikali na nipongeze kwamba Serikali imetambua umuhimu wa kukuza sekta binafsi. Kutambua sekta binafsi ni kwa sababu sekta binafsi inalipa kodi kubwa sana Serikalini. Namwomba Mheshimiwa Waziri, Serikali imefanya uamuzi mzuri. Kwanza tulimsikia Mheshimiwa Rais akiwaambia wafanyabiashara wanaoanza biashara mpya kupewa muda angalau wa mwaka mmoja ndipo waanze kulipa kodi. Huu ni uamuzi mzuri sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tumemsikia Waziri hapa ndani akisema anataka wafanyabiashara wenye madai ya kodi wasibughudhiwe, wasifungiwe biashara, badala yake waelimishwe jinsi ya kulipa kodi zao. Haya ni maamuzi mazuri, yanaonesha kulea na kukuza sekta binafsi ya wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, kumekuwa na kero kubwa sana kwa wafanyabiashara. Kule kwangu Lupembe na Mkoa wa Njombe kwa ujumla, wafanyabiashara wengi wanasumbuliwa sana magetini na Maofisa wa TRA. Mageti kama ya Migori na Mikumi, kuna usumbufu mkubwa sana kwa wafanyabiashara, mpaka Wabunge tupige simu ndiyo watu waachiwe. Kwa hiyo, imekuwa kama kufanya biashara kwenye nchi hii ni kero, ni usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri kwa uzito kabisa, kwa sababu Wizara ya Jinsia na Watoto wanalo dawati maalum la kushughulikia masuala ya jinsia, nakushauri Mheshimiwa Waziri, anzisha dawati maalum la wafanyabiashara kwenye Wizara hii, ili wafanyabiashara wapate fursa ya kutoa kero zao moja kwa moja kwako Wizarani. Hili jambo likifanyika hivyo, Mheshimiwa Waziri utakuwa karibu sana na wafanyabiashara na kujibu kero zao kwa wakati. Dawati hili ni muhimu, aajiriwe mtu maalum kupokea kero za Watanzania hasa wafanyabiashara. Hii ni kuhusu wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu kilimo. Nimeongea mara nyingi hapa ndani kwamba Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Hussein Bashe ni msemaji wa wakulima, ni mkombozi wa wakulima wa Tanzania. Mheshimiwa Bashe anafanya kazi nzuri sana. Mwaka 2022 Mheshimiwa Bashe ametangaza maeneo kadhaa hapa nchini kwamba, mkulima wa Tanzania aachwe kuuza mazao yake anakotaka. Aachwe kama walivyo wafanyabiashara wengine wa soda, sukari, na kadhalika. Nataka nikuhakikishie uamuzi ule wa Serikali wakulima wetu waliupokea vizuri sana. Sasa ushauri wangu ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa siku za karibuni huu mkanganyiko wa wafanyabiashara kutokwenda kununua haya mazao, hizi taarifa kwamba wamezuiwa kununua mazao na kwenda nje, Mheshimiwa Waziri, asubuhi na jana ametoa kauli nzuri sana hapa ndani kwamba, Serikali haijazuia wananchi kuuza mazao popote wanakotaka. Nimhakikishie Mheshimiwa Waziri, kuna jambo moja kubwa sana nyuma ya hili suala, kuna urasimu mkubwa wa kutoa vibali vya wafanyabiashara wa haya mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara wanazinguliwa sana huko maofisini. Vibali havipatikani, leseni hazipatikani. Namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa sababu jambo hili limeshakuwa kero, kule kwangu Lupembe, watu wa Ikondo, Ninga, Mtwango, Kichiwa, Igongolo, Ikula, na kadhalika, mahindi yameanza kushuka bei kutoka shilingi 15,000, wameanza kuuza kwa shilingi 5,000. Ni mporomoko mkubwa sana. Namwomba Mheshimiwa Waziri mambo mawili; jambo la kwanza atangaze mamlaka yetu ya kununua nafaka ianze mara moja kununua nafaka kwa wananchi; pili, atoe bei elekezi, wanunue kwa bei gani kwa wakulima? La tatu,…

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, naomba sana Serikali iongeze fedha za kununua haya mahindi kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa ameamua kuwasaidia wakulima wa Tanzania, afuatilie kwa ukaribu upatikanaji wa vibali vya kununua mahindi na mazao kwa wananchi wetu… (Makofi)

MWENYEKITI: Kabla hujamaliza, nafikiri kuna Taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kuhusiana na hoja hiyo.

TAARIFA

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge wa Lupembe na wakulima wa Tanzania. Wakala wa Chakula wa Serikali (National Food Reserve Agency) ameshaanza kununua mahindi, na bei ya chini anayonunulia ni shilingi 600 mpaka shilingi 700 na tumeanza kufungua vituo katika Wilaya zote na Serikali itatoa tangazo. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Mfumo wa kutoa vibali vya export kwa watu wote watakaokuwa na Business License, badala ya kutoa leseni manually, tutaanza kutoa leseni za export na kuuza mazao kuanzia tarehe 1 Julai kwenye mtandao ili kuondoa hiyo adha anayoisema kwamba, Wilayani wanasumbuliwa. Kwa hiyo, leseni zote zitatoka online kuanzia tarehe 1 mwezi wa saba. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Swalle unaipokea Taarifa?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa heshima kubwa sana. Nilisema hapa ndani kwamba, mzigo mzito wa kulima amepewa Mnyamwezi, Mheshimiwa Bashe, hongera sana, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye suala zima la ajira. Hili jambo la ajira limesemwa mara nyingi na watu wengi hapa nchini. Sisi kama chama, tumeahidi ajira milioni nane kwa Watanzania. Kwa takwimu zilizopo, kila mwaka karibu Watanzania milioni moja wanaingia kwenye soko la ajira kutafuta ajira, lakini uwezo wetu wa kuajiri hauzidi 70,000 pengine. Sasa maana yake kundi kubwa halipo kwenye mfumo rasmi wa ajira. Ushauri wangu ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, juzi hapa ndani tumetunga sheria kama Bunge ya kuanzisha Tume ya Mipango kwa ajili ya kushauri mipango mbalimbali ya Serikali. Ninaomba Serikali kupitia tume hii ikaanzishe mpango maalum wa kufufua viwanda vingi ambavyo vimekufa. Sisi kule Njombe kwa mfano, tulikuwa na kiwanda cha maziwa ambacho kingetoa ajira nyingi sana, kimekufa. Tulikuwa na kiwanda cha parachichi (Urivado) kimekufa. Viwanda vya chai vina hali mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoweka mpango wa kufufua viwanda vilivyokufa, hatuwezi kuongeza ajira. Serikali duniani kote haiwezi kuajiri wananchi wote wakapata ajira rasmi Serikalini. Kwa hiyo, hili ni jambo la kwanza ambalo Tume yetu ya Mipango lazima iliangalie kwa ajili ya kuongeza ajira kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nataka niseme kuhusu barabara yangu ya muhimu sana; barabara ya Kibena – Lupembe mpaka Madeke. Hii barabara imekuwa na ahadi ya muda mrefu. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, mwaka 2022 Rais wetu amekuja Njombe na Mheshimiwa Waziri alikuwepo. Barabara hii Mheshimiwa Rais ameagiza ianze ujenzi. Nimeambiwa mchakato wa kuandaa tenda umeanza. Nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye bajeti hii ambayo mimi naiunga mkono, barabara hii ianze kujengwa kwenye bajeti hii ya 2023/2024 ili kusudi mwakani tukija hapa tukupongeze kwa kazi nzuri ambazo unafanya huko Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, naona umeinua mic, natoa rai kwa Waziri wetu wa TAMISEMI pamoja na watu wa fedha, wananchi wetu wanayo maboma mengi ya zahanati, maboma mengi ya madarasa, vituo vya afya, na kadhaliak. Wekeni mpango maalum wa kumaliza maboma haya ili kuwatia moyo wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)