Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Awali ya yote, naungana na Wabunge wenzangu kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aliyetujalia kuiona siku ya leo na baraka zake kwa nyakati tofauti tofauti. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu maisha yetu ni rasilimali na hazina anayotujalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mji, nathibitisha kabisa kwamba mambo mengi niliyokuwa nimeahidi kwenye uchaguzi, yametekelezwa kwa asilimia kubwa sana. Nampongeza Mheshimiwa Rais, Mawaziri, kuanzia kwa Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wote. Kwa sababu mwaka jana 2022, wakati tunahitimisha Bunge la Bajeti nilikuwa nimesema nashika shilingi ya Mheshimiwa Waziri Mwigulu, akanitania siku moja akasema, “kwa umri wako ukishika Shilingi na hurudishi itakuaje?” Nikawa nacheka. Kwa maana ya kuona kwamba ninahofia yale mambo ambayo tuliyaandika kwenye bajeti na hayatatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa moyo wa staha na furaha kubwa kwa niaba ya wananchi, naipongeza sana Serikali kwa sababu kazi kubwa imefanyika, na pia ndani ya mwezi huu wa Sita nadhani, kuanzia tulipoanza hili Bunge letu la Bajeti mpaka sasa, Jimbo la Mbulu Mji limepokea fedha nyingi sana kutoka Serikalini. Fedha zilizopokelewa, nyingine hata hazikuwa kwenye mpango ule wa awali, zilikuwa zinazokuja kama fedha za kimkakati kwa ajili ya kutatua matatizo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa sababu Mbulu Mji, sisi wananchi wake kama Halmashauri, tunakusanya mapato madogo sana, lakini mahitaji yetu ni makubwa sana Serikalini, kiasi kwamba wakati fulani unajiuliza, sasa hayo tutayatatuaje? Kwa hiyo, natuma ujumbe huu kwa Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote kuwashukuru sana. Kwa sababu kila sekta katika mwaka huu wa bajeti ni takribani karibu Shilingi bilioni saba au nane zimepelekwa kwenye Jimbo la Mbulu Mji, katika robo hii ambayo tunamaliza sasa kama dakika za mwisho za kumalizia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Makamu wa Rais kwa ziara anazofanya katika majimbo yetu. Pia, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake ya hivi karibuni kule Jijini Arusha katika halaiki ya kanisa kwa ajili ya kuelezea hali halisi ya taharuki ambayo Watanzania wanaichukulia kwa hatua ya tofauti zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kutoa mchango wangu mchache sasa. Kwanza niungane na Wabunge wenzangu ambao walikuwa wanaipigia kelele dhana hii ya kuondoa au kupunguza kodi kwa bidhaa ya mafuta kutoka nje, na bidhaa nyingine, lakini tunataka kuingiza bidhaa hiyo, kupunguza na kujenga soko la ndani. Niseme tu kwamba, nchi yoyote ni lazima ijenge uchumi wake wa ndani ili iweze kwenda mbele, kwa sababu nchi nyingi zinajenga uchumi wa chini na uchumi wa kati na baadaye inaenda kwenye uchumi wa kuuza nje na pia kujenga uwezo wa wananchi katika rasimali walizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naungana na Wabunge wenzangu kwamba eneo hili la kupunguza kodi kwenye bidhaa za nje pengine itaua viwanda vya ndani na mwisho wake wananchi wetu watashindwa katika uzalishaji. Kwa sababu hali ya uzalishaji itatofautiana na ile ya kipato wanachopata hasa kwenye sekta ya kilimo na sekta zingine kwa ajili ya kupungua kwa gharama kubwa na uchumi kushuka na bidhaa zetu kushindwa kushindana na bidhaa zinazotoka nje. Kwa hiyo, rai yangu hapa ni kwamba tuangalie kwa umakini sana eneo hili na pia kulinda viwanda vya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita lile la miaka mitano, kwenye Halmashauri tulikuwa na viwanda vya ndani kama 100. Vile viwanda vilishafika hatua ya kuchakata na kufungasha malighafi za ndani, na pia viwanda vile vilikuwa vinatoa ajira kwa wananchi wa chini, wale waliioko kwenye majimbo. Vimekuja kufa kwa ajili ya matatizo ya wataalam na uelewa mdogo wa usimamizi, kutokana na kwamba hatukua na muundo mzuri. Hapa ushauri wangu ni kwamba tuangalie muundo wa SIDO na taasisi nyingine zitakazolinda viwanda vya ndani hasa hizi ndogo ndogo ambazo zinafungasha mazao ya wananchi. Pia kule kuna ajira za muda za wale wanaofanya vibarua, na pia maisha ya wananchi wetu yanaendelea na huduma za familia zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nashauri kama itawezekana, tuijengee uwezo SIDO, na tuwe na matawi ya SIDO kwenye wilaya zetu ili kuvilea viwanda vidogo vya chini kwa ajili ya kujenga uwezo wa wananchi. Tunapozungumza uwezo wa wananchi, tunachukua kundi kubwa la viwanda vidogo vidogo ambavyo watafanyakazi, watarudi makwao, lakini Maisha yao yanaendelea, wanasomesha watoto na pia wanapata huduma ya kila siku kupitia familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza sana Serikali kuondoa kodi. Miaka miwili iliyopita nilikuwa nimeuliza swali hapa Bungeni kwa ajili ya vijana wa vyuo vya chini na vyuo vya kati kuwa na gharama kubwa ya kuwasomesha, na vijana wengi wanashindwa na familia nyingi zinalemewa kwa ajili ya gharama. Kwa sababu tulikuwa tunakuta mwanafunzi anayesoma pengine Shahada ya Chuo Kikuu anasoma kwa gharama sawa na yule ambaye anasoma chuo cha cheti, wakati mwananchi yule anayemshomesha yule, gharama ile ilikuwa hailingani na kipato chake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunamshukuru Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ajili ya kuondoa ada hizi na gharama hizi katika baadhi ya vyuo. Rai yangu hapa ni kwamba tuangalie vyuo vingine pia ambavyo kwa uwezo wetu tukijijenga, tuweze kuwaweka na kundi hilo la vyuo vya cheti na vyuo vingine ili kujenga uwezo wa watendaji au watumishi ama wataalamu wa ngazi hizi za chini. Kwa sababu hata kufa kwa viwanda ni pamoja na hawa wataalamu wa ngazi za chini wanakuwa wachache. Kwa hiyo, tatizo hili ni kubwa kwa kadiri mnavyoona. Kwa vyovyote vile, hapa tunamwondolea mwananchi gharama kubwa. Alishamsomesha mtoto shule ya kata na sasa anaenda kwenye chuo kwa ajili ya kumjengea uwezo ili aweze kukabiliana na hali ya ulimwengu unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu haya ni majumuisho, katika taarifa yetu ya bajeti kuu, tumeongelea eneo hili la wastaafu. Wastaafu wa zamani pensheni yao ni shilingi 100,000 kwa mwezi. Yaani bima anayotakiwa ahudumiwe kwa maisha aliyonayo, inaweza kuwa shilingi 600,000, lakini yeye kwa mwezi anachopata ni shilingi 100,000 au shilingi 150,000. Nadhani Serikali itazame vizuri, iangalie namna gani watumishi hawa waliotumikia Taifa letu tunawaangalia ili nao basi wasiombolezee Serikali yetu, lakini pia wawe na amani wanapoelekea katika uzee wao na waweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee eneo la kuongeza ukusanyaji au utaratibu wa ukusanyaji wa mapato. Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kwenye kuhitimisha, angetuambia sisi Wabunge basi, kwa Serikali na taasisi za umma, ni lini siku ya mwisho ya matumizi ya mashine za POS kukusanya fedha za Serikali? Kwa sababu huko ndiko ambao fedha nyingi tunashindwa kukusanya na pia kuingia kwenye mfumo wa Serikali, kujenga uchumi wa nchi yetu na pia mapato yetu kuwa halisia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna fedha mbichi zinazopotea katika corridor hiyo au katika muundo huo na tutakapotoa tamko; kwa sababu kama tunafanya mambo makubwa sana hayo, tukumbuke kuwa hata na hilo la POS linawezekana kwa nchi yetu. Tutafute muundo wa maeneo yote hayo ambayo yanakusanya mapato ya Serikali, yawe yanaingia kwenye mfumo na kuweza kuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni kwamba bado tunahitaji kujenga uwezo wa wakusanyaji, kwa maana, kuna wilaya zetu nyingi hazina majengo ya wakusanyaji kwa maana ya TRA. Pia katika halmashauri hatuna Maafisa ambao wanaweza kukidhi haja na kujaza nafasi hizo ambazo ni muhimu sana katika makusanyo ya Serikali. Nilikuwa nafikiri hilo litatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwamba tumehangaika sana, hatuwezi kuwaajiri hawa vijana waliomaliza chuo, hawa ambao tayari wengine ni wa certificate wengine ni wa diploma, wengine ni wa degree. Serikali ione kwamba namna pekee ya hawa vijana kupata ajira ni kuangalia sheria za sekta binafsi za ajira, na maslahi katika sekta binafsi kwenye ajira, na pia namna ambavyo tutachochea kupitia viwanda ambavyo tutakuwa navyo ndani ya nchi na vijana wataajiriwa kutokana na taaluma zao ili kuondoa mzigo mkubwa uliopo kwa Serikali. Kwa sababu kwa vyovyote vile, mbele ya safari Serikali haitaweza kubeba jukumu hili la kuwaajiri hao vijana, kwa sababu kila mwaka wanamaliza masomo yao na wanapomaliza wanaiangalia Serikali kama baba yao ili iweze kuwaajiri na hawataajirika kwa sababu ya uchache wa nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika mwaka wa fedha unaokuja tuone namna ya kuajiri zile takwimu ambazo tumeziombea kwa ajili ya kupunguza idadi kubwa ya hao vijana. Tunajua hatuwezi kuajiri mara moja, lakini angalau tutafute madirisha ya kuajiri. Hata katika nchi zinazotuzunguka kwa uhusiano mzuri tulionao, basi tuwe na sehemu hiyo ya kulielezea jambo hili katika sura ambayo inaweza ikaleta tafsiri nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali, siyo kuilaumu tu; hata kwa hii hatua iliyoichukua ya mazao, kwa maana kuna muundo rasmi unaoandaliwa ili kuona kwamba angalau hata kama tutauza mauzo nje, Serikali itapata kodi, na pia hatutauza yote baadaye tukabaki na njaa ambayo ni janga la Taifa na mwisho wa siku haitawezekana. Kwa hiyo, nampongeza Mheshimiwa Waziri aliyekuwa anatoa tafsiri hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni Mamlaka ya Chakula na Lishe, kwa maana ya hasara inayotokea katika nchi yetu ni kubwa sana, kwa sababu ya uteketezaji wa bidhaa bandia na bidhaa ambazo zinazoingizwa nchini na tunazotengeneza kama bidhaa feki. Nilikuwa nashauri, kama itawezekana, tutazame muundo wetu wa kudhibiti uingizaji na utengenezaji wa bidhaa bandia, kwa sababu wanaoathirika sana sio wahusika, ni wale wafanyabiashara wa kawaida na wanapokamatwa kwa kukutwa na hiyo bidhaa, wanapata hasara kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muundo wa taasisi hii tukiutazama na namna ambavyo utaweza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nitachangia mengine kwa maandishi kwa sababu nina mambo mengi sana niliyaorodhesha katika mchango wangu wa leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)