Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwanza ninaomba kuchukua fursa hii kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maono yake na jinsi anavyojitoa katika kuwahudumia Watanzania. (Makofi)

Napenda pia kutoa pongezi na shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Phillip Isdor Mpango, Makamu wa Rais kwa namna anavyomsaidia Mheshimiwa Rais. Pia napenda kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba kukushukuru sana kwa kunipa tena nafasi hii na mimi kuchangia kwenye hoja hii iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa ninaomba kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba pia kipekee nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mheshimiwa Selemani Moshi Kakoso na Waheshimiwa Wabunge wote, Wajumbe wote wa Kamati kwa hoja nzuri walizozitoa za Kamati. Aidha, ninamshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mitaji ya Umma - Mheshimiwa Jerry Silaa na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati ya PIC kwa michango yao mizuri. Kamati hizi mbili zilifanya kazi kubwa ya kuchambua azimio hili, ninaomba kuwahakikishia maoni yao yote pamoja na maoni ya wadau wote waliopitisha maoni yao kwenye Kamati hizo mbili tumeyapokea na tunakwenda kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado muda tunao, fursa kubwa ya kuyafanyia kazi ipo na tunawahakikishia kwamba tutayafanyia kazi maoni yote na ya Watanzania wote kwenye mikataba ya miradi na mkataba wa nchi mwenyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda kutumia fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hoja hii. Naomba sasa nianze kuhitimisha hoja yangu kwa kutoa ufafanuzi wa kijumla kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamechangia kwa hisia kali kuhusu azimio la makubaliano haya kuhusu uendelezaji na uboreshaji wa utendaji kazi katika bandari Tanzania na Waheshimiwa Wabunge wanakubaliana wote na azimio la makubaliano lililoko mbele yetu. Ninaomba kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni yenu na maelezo yenu na tunawaambia kwamba tunaenda kuyafanyia kazi, tunao muda na tutayafanyia kazi kama mlivyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamefanya hivyo kwa kuchangia kwa hisia kali kwa sababu wanafahamu kwamba Bandari ya Dar es Salaam ndiyo lango kuu la uchumi wetu kwa sasa. Kama walivyosema wengi 37% sawa na shilingi trilioni 7.78 ya makusanyo ya mapato ya kiforodha ya TRA yanakusanywa kwenye bandari zetu hasa Bandari ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, bandari zetu ni muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye hotuba yangu mikataba kwa kila mradi itakayoandaliwa itapewa bayana kipindi cha utekelezaji wake na ukomo kila mradi tukianzia mradi wa uendeshaji utapewa muda wake, tukianzia kama kuna mradi wa ujenzi pengine gati la abiria tutaupa muda wake na ninaomba nichukue fursa hii hili jambo la muda tuwaachie wataalam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, mwekezaji anayendesha bandari na mwekezaji anayejenga bandari wanapewa muda tofauti. Huwezi mtu anayeendesha bandari ukampa miaka kumi, anayejenga bandari ukampe miaka kumi; siyo sahihi hata kidogo, kwa sababu mmoja anawekeza sana, mmoja anafanya operation, kwa kweli naomba hili ni jambo la kitaalamu, sisi tutalichukua na tuna wataalamu wazuri ambao watalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla kwamba tutaweka muda wa marejeo. Tutaweka time ya kufanya review kwa kila mradi. Miradi mingine tutafanya review kila baada ya mwaka mmoja, na miradi mingine tutafanya review kila baada ya miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tutaweka viashiria muhimu vya ufanisi wa kiutendaji yaani key performance indicators kwa kila mradi na ninaomba Waheshimiwa Wabunge niwaeleze key performance indicators hizi ndiyo zilizomtoa TICTS. TICTS alikuwa asitoke, lakini TICTS alishindwa kufikia vigezo tulivyomuwekea na ikawa hana njia lazima aondoke tu. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba sana muwaamini wataalamu wetu tunaamini wataalamu wazuri na ninaamini kwa kila mradi wataweka hizo key performance indicators na mkandarasi yoyote ama muwekezaji yoyote kama atashindwa kutekeleza tutaachana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba tuwahakikishie kwamba uandaaji wa mikataba ya miradi utafanywa na timu chini ya usimamizi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narejea tena, tuna vijana wazuri ambao wana uwezo mkubwa wa kutengeneza miradi kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliopata kuona ule mkataba wa TICTS, ule mkataba ulikuwa non-starter, ilikuwa hatuwezi kutoka lakini vijana wale wale tuliokuwa nao jana waliupitia mradi ule na TICTS mwezi wa Desemba aliondoka bila matatizo yoyote, bila mgogoro wowote kwa vile tunao vijana wazuri wana uwezo mkubwa na watafanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nijielekeze kwenye utendaji wa Bandari ya Dar es Salaam. Wabunge wengi wameongea hapa kwamba Tanzania imeelekeza au Tanzania imewekeza takribani shilingi trilioni moja. Serikali imeelekeza ama iliwekeza karibuni shilingi trilioni moja kwenye Bandari ya Dar es Salaam, lakini ufanisi kwenye bandari yetu bado ni changamoto kubwa. Nitawapa mfano, kwa mfano kitengo chetu cha makasha kuanzia gati namba tano mpaka namba saba ambayo inahudumiwa na TICTS mwaka uliopita iliweza kuhudumia makasha 150,000 tu wakati pale malengo ilikuwa tuhudumia takribani makasha 600,000. Hii haiwezekani, hatuwezi tukafanya hivyo kuwaachia watu ambao uwezo wao siyo mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna sababu za msingi ambazo zimefanya utendaji wa Bandari ya Dar es Salaam hasa kwenye kitengo kama cha makasha uwe ni dhaifu. Sababu ya kwanza kabisa tumeshindwa kuwekeza kwenye mitambo mikubwa ya kushushia makontena au makasha kwenye meli. Mheshimiwa Ezra amesema hapa ukitaka kununua ship to shore crane moja unahitaji takribani shilingi za Kitanzania bilioni 45 mpaka 50 na kwa meli moja unahitaji ship to shore cranes nne kwa wakati mmoja ndiyo utaweza kufanya hiyo kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine tuliyonayo pale sote tunafahamu, tumekuwa na changamoto kubwa sana la mifumo ya TEHAMA na kila Mheshimiwa Mbunge aliyesimama hapa amezungumzia mambo ya TEHAMA. Sasa tunakwenda kupata mwarobaini kwa ajili ya changamoto hizi.

Mheshimiwa Spika, pia Bandari yetu ya Dar es Salaam tumekuwa na changamoto kubwa ya utafutaji masoko. Haya makontena hayaji tu hivi hivi kama watu wanavyofikiria, lazima uwe na mtu ambaye ana uwezo mkubwa, ana network kubwa aweze kwenda nje kuleta mizigo mingi zaidi. Kwa vile tuna amini kwa mtazamo tunaokwenda nao wa DP World, sasa tunaweza kwena kupata mwekezaji ambaye atatutoa hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema majibu ya changamoto hii ni kuleta mwekezaji mahiri na sisi tunaamini kwamba DP World ni mwekezaji mahiri na anaweza kututoa hapa tulipo. (Makofi)

Ninaomba nieleze machache tu kuhusu bandari tunazoshindana nazo. Sisi sote katika ukanda huu tunapambania soko la Zambia, Malawi, Rwanda na Uganda pamoja na DRC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mshindani wetu mkubwa namba moja kwa sasa kwa hapa karibu ni port au Bandari ya Mombasa. Bandari ya Mombasa ina gati 19 wakati sisi Dar es Salaam tuna gati 12 tu. Magati ya kawaida wanayo 13 na magati sita ni kwa kuhudumia makasha. Sisi tunazo gati sita, lakini zote ni ndogo kulinganisha na Mombasa.

Mheshimiwa Spika, lakini wenzetu Mombasa sasa na wao wameshaanza kwenda kutafuta private sector kuendesha bandari hiyo hasa sehemu ya makasha. Container Terminal Number Two kwa sasa ambao wameijenga kwa mkopo na wao kutoka JICA kwa gharama ya dola za Kimarekani 280 tayari sasa hivi inaendeshwa na Kampuni ya Mediterranean Shipping Company ya Italy. Kampuni hii inamilikiwa na familia tajiri ya Kiitaliano Bwana Aponte ambaye yeye ni tajiri mkubwa kwenye mambo ya meli.

Mheshimiwa Spika, bandari hii vilevile ina gati ambayo inaendeshwa na private sector ambayo kazi yake kubwa ni kuhudumia nafaka.

Mheshimiwa Spika, Bandari ya Durban; Bandari ya Durban inamilikiwa na Transnet National Port ya South Africa ina magati 50; magati 31 ni ya kawaida ya kuhudumia makontena ni magati 10 na magati ya mafuta na chuma ni magati tisa. Magati 31 ya kawaida na magati 10 yanahudumiwa na Transnet Port Terminal siyo Transnet National Port Authority ni mtu tofauti ni kampuni ya South Africa lakini tofauti. Magati tisa yaliyobaki ya mafuta na mawe na chuma yanahudumiwa na private sector.

Mheshimiwa Spika, mshindani wetu mwingine ni Beira kutoka Msumbiji. Bandari ya Beira yenyewe ina magati 11; magati ya shehena za mchanganyiko pamoja na magati ya kuhudumia makontena yanahudumiwa na private sector (Conal Eda Mozambique) ni kampuni ambayo inatoka huko Uholanzi.

Mheshimiwa Spika, mshindani wetu mwingine ni Bandari ya Vizag...

SPIKA: Mheshimiwa Waziri dakika tatu malizia.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwa ufupi tu niseme bandari zote sasa hivi hasa kwenye maeneo ya kontena zinahudumiwa kwa asilimia mia moja na private sector. Ukichukua Angola, ukichukua Egypt, ukichukua Ghana, ukichukua Nigeria kila mahali wanafanya private sector kwa sababu wanafahamu private sector ina uwezo mkubwa wa kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, tuliamua kuleta private sector na tukaamua tulete private sector ambaye ana uwezo wa kufikia viwango vya kimataifa pamoja na awe na ufanisi katika utekelezaji wa Bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, sifa ya pili ambayo private sector tunataka tumlete awe na uwezo wa kutoa ufumbuzi katika mnyororo mzima wa usafirishaji; sifa ya tatu awe na mtandao mpana wa kupata mizigo kutoka soko la usafirishaji duniani; na sifa ya nne awe na uwezo wa kimataifa katika kuendeleza na kuendesha shughuli za kibandari.

Mheshimiwa Spika, majibu yote yako kwa DP World. Kampuni ya DP World ina uwezo mkubwa katika uendeshaji wa shughuli za bandari duniani kuanzia Afrika, Asia, Ulaya, Marekani ya Kaskazini na Kusini, kwa ufupi anao mtandao mkubwa sana duniani.

Pili, DP World ina uzoefu na utaalamu wa kuchagiza mnyororo mzima wa usafirishaji kutoka maeneo ambayo bidhaa zinatoka mpaka kufikia kwa walaji. Kampuni ya DP World inamiliki kampuni kubwa ya meli (P&O) ambayo ina takribani meli 100 na zinafanya kazi biashara duniani kote. Tunaamini kwa kwenda na DP World tutaweza kufanikiwa kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya DP World inaendesha maeneo mengi maalum ya kiuchumi karibu na bandari, inasafirisha usafirishaji baharini na inafanya kazi kwenye nchi kavu nyingi na hivi sasa tunavyozungumza kule Rwanda wana logistic park kubwa ambayo tunaamini DP World ikija Tanzania mizigo yote ya Rwanda itakuja au itapitia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema leo kwamba baada ya kazi hii ya kumleta DP World kuna matokeo makubwa tutayapata kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam. Ninaomba nimalizie haya mawili.

Kwanza tunaamini tutapunguza muda wa meli kukaa nangani kutoka masaa manne mpaka matano mpaka kufikia saa 24 kwa siku. Meli inaingia sasa hivi jioni, kesho inaondoka.

SPIKA: Ngoja, ngoja, hapo mwanzoni nadhani ulikusudia kusema siku umesema masaa sasa nadhani tutakuwa tuna…

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimesema siku nne mpaka tano za sasa mpaka masaa 24 kwa siku. (Makofi)

Pili, kama tutafanikiwa, na naamini tutafanikiwa kumleta DP World tutapunguza muda wa ushushaji wa makasha yaani kutoka siku nne kwa sasa mpaka kufikia siku moja na nusu yaani meli itaingia pale baada ya siku mbili inaondoka. Pia tunasema kama tutamleta DP World tunaweza kuongeza mzigo kutoka tani milioni 20.8 za sasa mpaka kufikia tani milioni 47.57 ifikapo mwaka 2032/2033.

Mheshimiwa Spika, jambo muhimu ambalo tutafanikiwa nalo ni kuweza kuongeza mapato yanayotokana na kodi ya forodha. Kwa sasa tunakusanya takribani shilingi trilioni 7.756 kupitia TRA kama tutaweza kumleta mwekezaji DP World tutaweza kwenda mpaka shilingi trilioni 26.709 sawa na 62% ya bajeti ya nchi yetu, pia tutaweza kuongeza kwa kiasi kikubwa ujaji wa meli katika bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niaomba mwisho kabisa niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Wabunge mtuamini sana kama tunaenda kuifanya kazi hii kwa uadilifu mkubwa na ninyi wenyewe matokeo mtayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo sasa ninaomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.