Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nitoe maoni yangu kwenye hoja hii muhimu sana iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha mchakato huu wa mageuzi makubwa ya kiutendaji kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam na bandari nyingine hapa nchini. Haya ni mambo ambayo yalikuwa yamekwama kwa muda mrefu yalihitaji mtu mwenye uthubutu, mtu ambaye atakuwa tayari kutupiwa mawe ilimradi mambo makubwa kama haya yaweze kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimpe moyo Mheshimiwa Rais wetu na Mheshimiwa Waziri na timu nzima iliyolifikisha jambo hili hapa tulipofika kwamba wasikatishwe tamaa na watu ambao wanakusudia kutukwamisha, kwa sababu miongoni mwa wanao tukwamisha wengine siyo raia wa nchi yetu. Nilisikia clip moja inazunguka mtu ambaye alikuwa anajaribu kutaka kutukwamisha siyo hata Mtanzania, lakini pia wengine wanaotaka kutukwamisha ni wanasiasa kutoka upande wa upinzani, badala ya kuchangia hoja ambayo ni mkataba wanaleta hoja nyingine za ajabu ajabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme hapa kwamba Mheshimiwa Rais Samia hawezi kuwa mtu wa kwanza kupigwa mawe pale ambapo alithubutu kufanya jambo kubwa. Mambo haya yalianza toka Awamu ya Kwanza walisemwa viongozi wakuu. Mzee Mwinyi alisemwa miaka ile ya 1990 alipokuwa anaamua kuikwamua nchi kutoka kwenye mfumo wa centrally planned economy uliokuwepo wakati huo na kutuleta kwenye mfumo wa soko huria, aliambiwa amelikanyaga na kulichana Azimio la Arusha, aliziba masikio akasonga mbele. (Makofi)

Mzee Mkapa alipokuwa anaamua kutekeleza yale ambayo yaliamuliwa na Rais aliyemtangulia ambaye ni mzee wetu Mzee Mwinyi naye aliambiwa anauza mashirika ya umma, kelele zilikuwa nyingi lakini aliziba masikio akasonga mbele hakurudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Mzee Magufuli hapa juzi alipokuwa anataka kujenga Bwawa la Mwalimu Nyerere alipigwa vita sana, walikuwepo wenzetu upande wa upinzani, lakini naye aliamua kuziba masikio na akasonga mbele. Leo hii karibu tuanze kupata umeme megawati zaidi ya 2,150. (Makofi)

Kwa hiyo, mtu yeyote yule siku yoyote ile atakayoamua kufanya jambo zuri lenye manufaa atarajie atapingwa, atarajie atapigwa vita, hakuna watu ambao watakuwa tayari kumuunga mkono moja kwa moja kwa sababu nyingi mbalimbali mojawapo ni woga wa mabadiliko na nyingine ni woga wa kitu ambacho hawakijui. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kupingwa, kukosolewa sio mambo ya ajabu ni mambo ya kawaida, kwa hiyo napenda kumtia moyo Mheshimiwa Rais, lakini pia Mheshimiwa Waziri na timu nzima ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi ninapenda nijikite moja kwa moja kwenye kile kifungu cha 23 ili kujaribu kujibu hofu mbalimbali ambazo zililetwa, lakini kabla ya kifungu cha 22 labda nianzie kile cha nane ambacho kinahusu haki za ardhi (land rights). Kifungu hiki hakiendi kummilikisha ardhi huyu mwekezaji anayekuja, kinaenda kumpa haki za kutumia ardhi na sisi katika sheria zetu za ardhi hapa nchini, haturuhusiwi hata sisi wenyewe tuliozaliwa hapa haturuhusiwi kumiliki ardhi, tunapewa tu haki ya kutumia ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hata huyu mwekezaji anapokuja atapewa haki ya kutumia ardhi na haki atakayopewa yeye itapitia TIC kwa sababu sio mzawa. Kwa hiyo, atapata derivative rights, atapewa masharti ya namna ya kutumia ardhi atakayoitaka na ndio ataishia pale, lakini sio kumilikishwa ardhi.

Kwa hiyo, wanaowadanganya Watanzania huko nje kwamba ardhi yetu inauzwa na anapewa mwarabu wa Dubai waache tabia hiyo kwa sababu ni upotoshaji ambao haujengi Taifa, ila unaenda kutukwamisha kufanya mambo yetu ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine ambalo napenda kulisema linahusu upotoshaji ambao umewekwa kwenye eneo la kipindi cha mkataba na termination. Walikuwa wanasema kwamba tunauza kipande cha ardhi ya Tanzania kwa miaka 100, kwanza hakuna hicho kitu kwenye mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mkataba huu unaweka ukoma kwenye hicho hicho kifungu cha 23; wengi wanatia mashaka kwenye kile kifungu kidogo cha (4) ambacho bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Spika amekifafanua vizuri sintokirudia, lakini mimi napenda kutia msisitizo kwenye kile kifungu cha kwanza kwamba kifungu 23(1) inasema kwamba mkataba huu utaendelea kufanya kazi mpaka pale mambo kadhaa yatakapojitokeza. Moja ni shughuli za mradi zitakapoisha, lakini la pili ni mikataba ile midogo midogo ya utekelezaji itakapomaliza muda wake. (Makofi)

Sasa kama ile itamaliza muda wake na shughuli za mradi zitakuwa zimeisha automatically huu mkataba mama utakuwa hauna kazi, utakuwa umekufa, hautokuwepo tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kusema kwamba mkataba huu hauna mkomo sio sahihi, kwa sababu sisi tuwe makini tu kwenye ile mikataba midogo midogo ambayo Serikali wataenda kusaini huko mbele kwa maana ya Hosting Government Agreement ama Concession Agreement na hapo mimi na mapendekezo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwamba Serikali watakapoenda kujadili na hatimaye kupatana juu ya HGAs pamoja na Concession Agreements wawe makini kwenye kipindi kwenye mkataba. Wasizidishe miaka 30, naona imekuwa kama consensus hapa Wabunge wengi wamejadili hivyo na mimi napenda kuungana na wanaopendekeza miaka kati ya 25 ama 30. Kwa maana ya kwamba ikipita hicho kipindi cha miaka hiyo 30 maana yake kama hatujasaini mkataba mwingine na wala hakuna mkataba mwingine ambao uko hai maana yake hii IGA inakuwa imekuwa imekufa automatically. Hata kama itakuwepo haijafutwa lakini itakuwa imekufa kwa sababu ya hichi kifungu cha 23(1). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia napenda kupendekeza kwamba watakapoenda kusaini ile mikataba ya utekelezaji hizo Hosting Government Agreement pamoja na Concession Agreement, wawe makini wasije wakasaini mikataba ya kumpangisha kutumia ardhi, wasaini mikataba zaidi zaidi inayojielekeza kwenye kumpa haki ya usimamizi wa miradi husika, kwa maana ya kwamba sisi tubaki na haki za kumiliki ili mitambo, kumiliki hizo facilities ambazo watakuwa wamejenga, lakini tumpe tu mikataba ya operations, usimamizi, marekebisho kwa miaka hiyo atakayotaka na hapo tutakuwa tumelinda sana maslahi ya Tanzania kwenye mikataba hiyo, kuliko tukisema tunaenda kumpa aidha mikataba ya upangishaji kama tenant agreements ama CMS agreement.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ninalopenda kupendeza wakawenalo makini kwenye Bandari ya Dar es Salaam ukiangalia miradi iliyopo kwenye appendix I, phase one unaona pale kuna shughuli ambazo Serikali yetu imeshakopa pesa nyingi na zimekwishafanyika sema kuna mapungufu ya hapa na pale ambayo yanaenda kutekelezwa na mkataba huu. Sasa pale maana yake kuna uwekezaji wa Serikali. Kwa hiyo, mapendekezo yangu ni kwamba iundwe kampuni ya pamoja kati ya DP World na TPA ambayo Serikali itakuwa ina hisa zake na mwisho wa siku kabla ya kuunda hiyo kampuni utakuwa tumeshafanya valuation, tutakuwa tumefanya uthamini wa mali iliyoko pale. Kwa hiyo tutakapoenda kufunga naye mkataba tutapata share za kutosha kwa hiyo DP World ataendesha ndio, lakini na sisi tutakuwa wabia kwenye mkataba wa kuendesha Bandari ya Dar es Salaam kuliko kusema tunamwachia moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hiyo naweza nikapendekeza pia hio kampuni mpya itakayoundwa baina ya DP World na TPA iweze kuwa listed kwenye Soko la Hisa, ili katika ile local content Watanzania wengi zaidi waweze kununua hisa na waweze kupata matunda yanayotokana nan uwekezaji wa kimkakati katika Taifa letu. (Makofi)

(Kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili imeshagongwa, shukrani sana.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)