Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Spika, nitaanza kwa kuomba kumpongeza Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwenye mambo mawili; jambo la kwanza, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye uongozi wake anafanya mambo kwa uwazi na kushirikisha Watanzania wote na Bunge lako hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Bandari Sura ya 166 ya mwaka 2004 kifungu cha 12(1)(b) na kifungu cha 5(e) kinaipa mamlaka Mamlaka ya Bandari kuingia kwenye mikataba ya upangishaji na uendeshaji. Kama Serikali ingeamua kufanya matakwa ya kisheria leo azimio hili lisingekuja Bungeni, lakini Mheshimiwa Rais kwa busara yake na kwa uongozi wake wa uwazi ameamua kuchukua njia ambayo inaonekana ni ndefu, lakini ni njia shirikishi leo tuko hapa tunajadali mkataba ama makubaliano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai juu ya uwekezaji wa bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili amesema Mheshimiwa Reuben Kwagilwa ni uhuru wa kujieleza kwenye Taifa letu. Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa uhuru mpana sana wa kujieleza. Watu wanasema mpaka wanavuka mipaka, lakini nikuthibitishie wanayosema maneno hayo ni wananchi wetu na sisi ni viongozi wa watu lazima tuwasikilize katika kuelekea kwenye maamuzi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya azimio hili kuletwa Bungeni na wewe kuilete kwenye Kamati ya Pamoja inayoundwa na Kamati zetu mbili, mijadala imekuwa ni mingi. Mijadala ni afya kwa Taifa letu lakini lazima tuseme, wako watu ambao walikuwa wana nia njema ya kutaka kuelemishwa, lakini lazima tuseme vilevile wako watu wanaopotosha jitihada nzuri ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuleta maendeleo ya uchumi katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze wanasiasa wakubwa wa nchi hii wakiwemo wa upinzani ambao walitoa maoni yao ya haki na hawakutumia fursa ya kupotosha umma juu ya azimio la makubaliano haya yalioko Bungeni. Maneno mengi yaliyosemwa amesema hapa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kakoso, ambao sisi kwenye Kamati yetu ya Pamoja tumepokea maoni ya wananchi wengi, pamoja na yale maoni yalitoka kwenye maeneo ya mitandao ya kijamii yalionyesha kuna hofu kubwa baina ya Watanzania. Hofu yao iko kwenye maeneo mengi, yakiwemo watu wana hofu ya ajira za Watanzania, wananchi wana hofu ya ardhi yetu, wananchi wana hofu ya mapato, wananchi wana hofu ya ukomo, wananchi wana hofu ya usalama wa bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nilitaarifu Bunge lako tukufu, azimio lililoko mezani mbele yetu ni makubaliano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai na si mkataba wa aina yoyote wa uwekezaji, uendeshaji wala ubia wa bandari. Naomba niseme hili na kaka yangu Kitila Mkumbo naomba na yeye vilevile nimshauri, ni ngumu sana na kwa nia njema kabisa kwa mtu asiyekuwa na taaluma ya sheria kutofautisha baina ya a contract and an agreement. Kwa lugha ya Kiingereza cha kawaida inaonekana ni nyaraka zinazofanana, lakini kilichopo mbele yetu ni makubaliano yanayojenga msingi wa Serikali kwenda kutengeneza mikataba ambayo ndio itakuwa na utaratibu wa uwekezaji baina ya Host Government Agreement na concession agreement za project moja moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi wengine elimu zetu za kwanza hazikuwa sheria, mimi nilisoma Electronic Science and Communication, nilienda kuongeza ujuzi huo tu katika nia ya kujaribu kufahamu nyaraka hizi unapozisoma kwa lugha ya kawaida inawezekana ikakupotosha ama mtu akakupotosha kwa makusudi. Zipo clip zinatembea za mwanasheria mmoja ukisikiliza lafudhi yake utajua nchi anayotokea, nchi ambayo tunashindana nayo kwenye shughuli hizi za bandari na ukisikiliza kwa makini hata usomaji wake anasoma kipengele kwa kukikatisha kipande ambacho anajua anaweza akapotosha umma kwa wale ambao hawajui legal interpretation ya kifungu kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini naomba niseme Kamati imetoa maoni na Wabunge wengi waliochangia wametoa maoni; Serikali inapoenda kutengeneza Host Government Agreements na inakwenda kutengeneza mikataba ya mradi mmoja mmoja itazingatia maeneo yote ya hofu za wananchi mliyoyataja pale juu kama Kamati ilivyopendekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko eneo naomba niseme na niwathibitishie Watanzania katika kipindi Bunge lina Spika mbobevu wa sheria ni kipindi hiki. Spika Dkt. Tulia Ackson Mwansasu ni Mwanasheria mbobevu. Wale wasiofuata historia amewahi kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ndiyo kipindi pekee usingeweza kuleta jambo lenye matatizo likaingia kwenye floor ya Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini naliomba Bunge kazi iliyoko mbele yetu ya azimio la makubaliano haya, ni kazi uliyoitaja kwa mujibu wa kanuni fasili ya 107 na fasili ya 111 kama inavyotohoa ibara ya 63(3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuridhia makubaliano ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai ili kutengeneza msingi wa Serikali kwenda kutengeneza mikataba ya Host Government Agreements na Concession Agreements ambazo ndiyo zitajenga msingi mzima wa aina ya uwekezaji. Hapa hatuna ubia, hapa hatuna partnership, hapa hatuna uendeshaji, yote hayo yataelekezwa kwenye mikataba ile ambayo Serikali itaenda kuandika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili ambalo nataka kulisema kwenye sheria niwaombe Waheshimiwa Wabunge na utatuongoza. Bunge linafanya kazi yake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tusijiingize kwenye kazi ya Serikali ya kuwa waandishi wa mikataba tutajiondolea wajibu wetu wa kuisimamia Serikali pale ambapo Serikali itakuwa imekosea. Najua ni matamanio na ni mihemko ya kuona kwamba Bunge hili kila kinachofanywa na Serikali, kila mkataba uletwe, siyo utaratibu wa kikatiba na wewe utatuongoza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwaambia umma wa Watanzania maana matatizo yote ya bandari yameelezwa na wengi, wapo wanaochangia ambao hawalitakii mema Taifa letu. Mchakato wa maendeleo siyo mchakato rahisi, amesema Mheshimiwa Tauhida hata maendeleo yako binafsi ametaja marafiki, ametaja majirani hata ndugu zako wenyewe wanaweza wakawa wanapinga maendeleo yako binafsi, lakini wako washindani wetu wa kiuchumi, wako washindani wa wenzetu tunaoingia nao kwenye makubaliano haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wako wengine ni clout chasers tu kwenye mitandao; clout chasers ni mtu anayetaka kupata na umaarufu, yuko mtu mmoja anaheshimika sana anaandika maandiko mengi juzi ameandika haiwezekani ukampa mtu bandari zote hiyo ni sole proprietorship. Hivi jamani hata ku-google tunashindwa? Maana ya sole proprietorship ni kumpa mtu bandari zote? Lakini ni mtu anaandika kwa kutafuta fame na watu wanamfuata wakimsikiliza. Lazima Bunge hili litoe uongozi na litoe ufafanuzi wa maeneo haya ili wananchi wetu wafahamu kabisa tuko hapa kwa ridhaa ya Watanzania. Tunaanza vikao vyetu kwa dua, tumeapa hapa kwa imani za dini zetu. Tunayoyafanya hapa yanahesabu kwa wananchi, lakini yanahesabu kwa Mungu wetu huko mbele ya haki. Tunafanya kwa uadilifu wa hali ya juu na wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nina maombi matatu; ombil la kwanza,...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 malizia kengele imeshalia.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, ombi la kwanza niliombe Bunge lako liendelee kumuunga mkono Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye mipango yake mema ya kujenga uchumi imara wa nchi yetu. (Makofi)

Ombi la pili, kuwaomba wananchi kuendelea kutuamini kwamba Wabunge wao wataendelea kusimamia maslahi yao kwenye maeneo yote katika kuishauri na kuisimamia Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi la tatu Serikali iendelee kutoa elimu kwa umma ili kuondoa hofu na izingatie maoni ya Kamati na maoni ya Wabunge katika kutengeneza mikataba mizuri yenye tija kwa Taifa letu na kulinda maslahi ya Taifa hili na wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)