Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

Hon. Joseph Anania Tadayo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuwa mchangiaji wa pili katika hoja hii muhimu sana iliyoko mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niishukuru sana Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kuendelea kupambana kutafuta majibu ya maswali magumu yanayosumbua uchumi na ukuaji wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bandari ni moja kati ya masuala magumu ambayo yana umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi yetu, kwa hiyo kitendo cha kuendelea kuhangaika kutafuta ufumbuzi juu ya suala hili ni jambo ambalo tunapaswa kuliunga mkono na kulipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo muwasilishaji hoja pamoja na mchangiaji aliyetangulia alivyosema hoja hii imekuja mbele ya Bunge lako chini ya Ibara ya 63(3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kujadiliwa na kuridhiwa na Bunge lako hili mwaka 2017 lilishapitisha mwongozo wa jinsi ya kujadili ambao umezingatiwa, Kamati imefanya kazi yake vizuri na tumeona taarifa yake na tunaipongeza kwa taarifa nzuri katika hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili kama alivyozungumza mchangiaji wa kwanza suala hili limeleta taharuki, limeleta hofu katika jamii yetu ya Tanzania moja kwa mambo ambayo pengine ni ya kisiasa yanayoenezwa na watu mbalimbali lakini hofu nyingine tu ni hofu ya kawaida ya hofu ya kitu kipya, hofu ya kitu usichokijua (fear of unknown). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inatokana tu na kwamba tumekaa na bandari yetu kwa miaka 60 tumekuwa tukiitumia wenyewe, tunapanda, tunashuka, tunakwenda, tunarudi miaka 60 siyo muda mchache, sasa ghafla unaposikia kwamba uendelezaji wake unachukua mfumo mwingine lazima kunakuwa na hofu ambayo sisi kama Wabunge tunalo jukumu la kuelewa na kuwaelewesha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitaangalia zaidi maeneo ambayo huwa yanahojiwa kwenye mkataba. Ukipewa mkataba uuchambue au utoe opinion mojawapo ya mambo ya kwanza kwanza kabisa kujiuliza ni wahusika wa mkataba (parties) kwamba hivi ni nani hawa wanaosaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkataba huu uko wazi kwamba umesainiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo hiyo hatuna hofu yoyote ya kuifahamu kwa sababu tunaijua ni Serikali yetu, lakini pia pale kwenye preamble imesainiwa na nchi inaitwa The Emirates of Dubai. Sasa the Emirates of Dubai ni sehemu ya Umoja wa Falme ya Nchi za Kiarabu au UAE United Arabs Emirates ambayo ni dola ya Kifalme inayoongozwa na Katiba, it is the constitutional monarchy.

Mheshimiwa Spika, Katiba yake ya mwaka 1971 kama ambavyo imerekebishwa mara nyingi mpka 2004 ndio toleo ambalo lipo sasa hivi inaunda shirikisho lenye hizi Emirates lenye hizi nchi saba ambayo ni Dubai tunayoizungumzia Sharjah, Abu Dhabi, Dubai, Ajman, Umm Al-Quwain, kuna Ras Al Khaimah na Fujairah. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hizi nchi ambazo zinaunda hili shirikisho, shirikisho lina bendera linaundwa Taifa, lakini hizi nchi shiriki zinazounda hili shirikisho pia zina bendera zake na mamlaka yake. Ibara ya 120 ya Katiba ya UAE inataja masuala ya Muungano (union matters) za UAE, inataja masuala ya Muungano ambayo yako 19 katika masuala hayo suala la uwekezaji si sehemu ya masuala ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la uwekezaji ni sehemu ya mamlaka ambayo imeachiwa hizi nchi moja moja hizi Emirates. Kwa hiyo, Mkataba wetu huu umesainiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwakilishwa na Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wetu wa Miundombinu kwa idhini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na upande wa The Emirates of Dubai imesainiwa kwa idhini ya Mfalme wa Dubai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende mbali kidogo, Dubai ni absolute monarchy yaani ni nchi ya Kifalme per see ambapo Mfalme akishasaini under seal chini ya ile lakiri yao huo ni mkataba ambao ni halali kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimelizungumza hili kwa sababu mojawapo ya hofu zinazoendelea ni kwamba mbona hapa Rais wetu amesaini na Waziri lakini kule amesaini mkuu wa ile port ni kwa sababu ile ni absolute monarchy na tayari Mfalme yule ameshasaini pale kwenye ule mkataba, ameshatoa idhini yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndivyo ambavyo wenzetu hawa wamekuwa wakiishi mpaka wakageuza jangwa likawa sehemu ambayo dunia nzima inaitamani. Wamenaishi hivyo na wameweza kufikia hatua hiyo katika nchi hiyo katika nchi hii I mean katika dunia hii. Kwa hiyo uwekezaji haupo chini ya yale mambo ya Muungano isipokuwa article 117 ya Katiba hiyo ya UAE inatoa mamlaka kwa kila nchi kushughulikia mambo ya ukuaji wa uchumi na biashara wa nchi zao ili waweze kuchangia kule kwenye union yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo sasa niendelee tu kusema kwamba haya ni makubaliano, makubaliano pia unaweza ukayaita mkataba, lakini haya ninayosema ni makubaliano ya uendelezaji wa bandari zetu chini ya Ibara ya 5(3) cha Mkataba huu, hizi taasisi mbili maana kama ilivyosema Tanzania inamiliki TPA na Dubai inamiliki DP World na hakuna mahali kwenye mkataba huu ambapo DP World imesaini ni hizi Serikali mbili zimesaini ili kujenga mazingira sasa ya haya makampuni yake mawili kushirikiana na chini ya ile Ibara ya 5(3) ya mkataba huu kila panapokuwa na project ambayo TPA na DP World wataingia mkataba kutakuwa na presentation na uwasilishi ambao utaletwa na DP World, TPA italipitia na kulijadili na kusaini mkataba tofauti kwa kila mradi ambao utakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha kushauri tu kama ambavyo mwenzangu Profesa Mkumbo alizungumza ni kwamba tunahitaji umakini mkubwa tu wakati wa kusaini hii mikataba mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikia Mheshimiwa Waziri akieleza mambo ambayo Serikali ime-undertake kuzingatia wakati wa kusaini huo mkataba. Mimi nakubaliana na yale mambo ambayo ameyaorodhesha ikiwa ni pamoja na suala la land right ambalo lipo huku, kwamba kama ambavyio mkataba huu unazungumzia kwamba land right ni juu possession na access na siyo ownership basi hilo liendelee kuzingatiwa hivyo hivyo kama ambavyo mkataba huu kubwa umeweza kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkataba huu unaruhusu marekebisho yaani amendment, unaruhusu termination na Ibara ya 21 inaruhusu matumizi ya sheria za Tanzania katika ile mikataba mmoja mmoja ambayo tutakwenda kuingia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi naunga mkono hoja, na ninawashawishi Wabunge wenzangu tuuridhie mkataba huu, ahsante sana. (Makofi)