Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ili kuweza kuhitimisha hoja hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa hoja ambazo wamezitoa na nianzie ufafanuzi wangu kwenye eneo hilo la jumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili na Watanzania wajue, leo hii tunayoijadili ni Wizara ya Fedha, Bajeti ya Serikali itakuja wiki ijayo. Kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge tumepokea hoja zote, na waridhie zile zinazoangukia kwenye hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali, kwa sababu matayarisho yake bado yanakamilika kamilika zikiwepo zile za hatua za kikodi, waridhie kwamba tumezipokea na tutakuwa na mjadala mpana tutakapokuwa tumewasilisha yale ambayo tumeyaweka maoni yao na yale ambayo watatamani tuyabadilishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo yale masuala yote ambayo yamejitokeza yanayohusisha masuala ya kikodi niwaombe waridhie kwamba tutayajadili kwa upana baada ya kuwa tumeshawasilisha kile ambacho tumekiandaa katika kauli ya Serikali, ambayo tutaiotoa tarehe 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, pia kwa manufaa ya ufafanuzi ili na wananchi waelewe; bajeti ya maendeleo ambayo tunaiongelea kwenye muktadha huu hapa ni bajeti ya maendeleo kwa Wizara ya Fedha na taasisi zake. Huwa inatokea tukisema bajeti ya kawaida ni mathalan hapa shilingi trilioni 15, wanatokea wengine wanasema bajeti ya maendeleo ni kidogo, kama hivi iko shilingi bilioni karibu 500, inazidiwa na bajeti ya matumizi ya kawaida. Kwa leo hii hapa tunapoongea bajeti ya matumizi ya kawaida ndani yake ina takribani shilingi trilioni 10 ambazo zinaangukuia kwenye Deni la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Deni la Taifa kama tulivyotoa kwenye ufafanuzi wa majukumu ya Wizara linasimamiwa na Wizara ya Fedha. Kwa hiyo tuna trilioni 10 ambazo zenyewe ni Deni la Taifa kwa mwaka, na bilioni 500 wanayoiona hiyo ni bajeti ya maendeleo kwa Wizara ya Fedha na taasisi zake. Bajeti ya Maendeleo ya Nchi nzima tutaitaja tutakapotoa Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Deni la Taifa wanaloliona, hizo shilingi trilioni ni Deni la Taifa kuanzia awamu ya kwanza. Awamu ya kwanza, awamu ya pili, awamu ya tatu, awamu ya nne, awamu ya tano na kwa awamu ya sita kwa mikopo hii ya roll over pamoja na ya ndani kwa sababu za mikopo ya nje bado hazijaiva ndiyo inayoleta jumla ya deni la hilo la shilingi trilioni 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Fedha pia ndani yake pia kuna Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi ambapo na yenyewe fungu lake tunaliomba pamoja na mafungu haya mengine, na tuna ofisi zingine kama tulivyoziorodhesha wakati wa kuwasilisha taarifa hii rasmi ya leo. Kwa hiyo uwiano ule wa fedha za matumizi ya Kawaida kuwa kubwa na uwiano wa matumizi ya maendeleo kuwa ndogo ni kwa sababu matumizi ya kawaida yanahusisha Deni la Taifa ambalo ni la awamu zote. Na matumizi ya maendeleo namba yake ni ndogo kwa sababu tu inahusisha matumizi ya Wizara ya Fedha na taasisi zake na matumizi ya maendeleo ya jumla yatakuja kwenye Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepokea ushauri wa kamati, na maeneo yale kama nilivyosema mengine yamejikita kwenye sera za masuala ya kikodi kwa hiyo tutatoa tamko tutakapokuja wakati wa tamko la Bajeti ya Serikali. Tumepokea hoja kubwa ambayo imejadiliwa kwa mapana na Wabunge wengi kuhusu ukaguzi wa ndani. Wabunge watakumbuka mwaka jana walitupitishia mabadiliko ya kimuundo ya Ofisi ya Ukaguzi wa Ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilichokuwa kinatokea kabla ya huo muundo wa mwaka jana ambao tulipitishiwa mapendekezo na Bunge, Wakaguzi wengi wa Ndani walikuwa ni sehemu ya management. Kwa sababu Fungu lao, vote yao ilikuwa inaangukia kwa wale wanaowasimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufikia mwaka jana tulibadilishiwa muundo, Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani ilipewa vote yake na mtiririko wake. Sasa baada ya Bunge kupitisha, ilienda kwenye hatua za kutengeneza muundo wake ambao wanaweza wakaona labda haijaweza kuwa na kiwango kikubwa. Kwa sababu ndiyo kwanza mwaka huu ambao tumeumaliza ndiyo tumepata ridhaa ya Bunge baada ya kupitishiwa mapendekezo na tukaenda kwenye kutengeneza muundo na muundo ambao umefanyiwa kazi ni kwamba taarifa zote zile sasa hazitakuwa zinapelekwa kwa yule anayekaguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilivyokuwa mwanzo ilikuwa ukimkagua yule unayemkagua ndiyo unampatia ile taarifa ya ukaguzi, lakini kwa sasa watatoa ushauri kwa wale wanaofanya nao kazi. Kama ni halmashauri watatoa ushauri kwa Mkurugenzi, kama ni ofisi yeyote ile watoa ushauri kwa mkurugenzi. Lakini taarifa itaenda kwenye ofisi ya juu ya yule aliyekaguliwa, za halmashauri zinaenda mkoani na siyo kwa Mkaguzi Mkuu wa upande wa mkoa lakini ni kwa mkoani kwa maana kama Mbunge alivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa zile ambazo zinakwenda juu kwa maana ya ngazi ya Taifa, tulizipeleka ziende kwa Mkaguzi Mkuu wa Taifa ili baadaye yeye ndiye anayehusika kwenda kuwasilisha kwa Kamati ya Baraza la Mawaziri la kazi, ambalo linaongozwa na Waziri Mkuu ambaye ndiyo coordinator wa Shughuli za Serikali. Hapo ndipo ambapo tuliona yule Mkaguzi Mkuu wa Ndani anatakiwa aende kuziwasilisha. Hii tumeiweka pale kwa sababu tuna taarifa za halmashauri, tuna taarifa za local government, tuna taarifa za Serikali Kuu na tuna taarifa za Mashirika ya Umma, kama ambavyo zinaweza kuwasilishwa kwa upande wa CAG.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeongelea upande wa nyongeza ya fedha kwa upande wa CAG. Tukishamaliza bajeti hii tutakuwa na mashauriano ya Serikali na Kamati, kwa hiyo yale yote yanayohusisha nyongeza tumeyapokea na tutaenda kuyaandalia majibu kupitia mashauriano ambayo yatafanyika kati ya Kamati na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepokea ushauri kuhusu masuala ya fedha haramu, tumepokea ushauri kuhusu kufanya marejeo masuala ya pensheni, yote yale tumeyapokea na Naibu Waziri amejibu. Tumepokea maoni ya Mheshimiwa King yanayohusisha masuala ya mgao pamoja na mahusiano. Yote hayo yanafanyiwa kazi na yako hatua nzuri yatakapokuwa yamekamilika tutatoa kauli na yataenda moja kwa moja kwenye utekelezaji ambao utakuwa umeshafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala ya kimfumo, kazi kubwa inaendelea kwa upande wa mifumo ya TRA na kwa upande huu ambao Waheshimiwa Wabunge wameongea ETS na yenyewe yanafanyiwa kazi. Tunajua mifumo na yenyewe hawafanywi mara moja, kujenga mfumo si jambo la mara moja. Unatakiwa kutathimini aina ya mifumo, kusimika mifumo, kuweka mifumo iweze kusomana na hilo ndiyo jambo kubwa ambalo linafanyika hata lile alilosema Mheshimiwa Kishimba la dola tutalitolea kauli tunaposoma Hotuba kubwa, kwa sababu kazi yake kubwa imeendelea kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, alilolisema Mheshimiwa Katimba la suala la manunuzi, Sheria ya Manunuzi tunaileta upya, imeshasomwa kwa mara ya kwanza. Itakuja hapa na itajadiliwa kwa mapana yake na tunaamini kwamba itakuwa na ushauri wote ule ambao Mheshimiwa Mbunge amesema.

Mheshimiwa Naibu Spika, ameongelea Mheshimiwa Nusrat, masuala ya kodi na yenyewe nimeishasema tutayaongelea kwa mapana tutakapoleta kodi na lile alilosema kuhusu kutoa elimu. Tunatarajia tufanye semina kwanza kwa Waheshimiwa Wabunge, tuwaelezee haya masuala ya kodi na jinsi ambavyo yanawiana na maendeleo yetu na jinsi ambavyo inawiana, kwamba watu wengi sana wakilipa kodi itatuwezesha kupunguza ukubwa wa kodi. Kwa kadri wanavyolipa kodi watu wachache ndivyo tunavyofanya mzigo ule uwe mkubwa zaidi, kwa sababu unabebwa na wachache.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuwa tumeshafanya semina Waheshimiwa Wabunge wakaelewa, tutaomba ninyi wenyewe ndiyo mkawe mabalozi kila mtu kwenye Jimbo lake kama tulivyofanya kwenye Sensa na tukaona mafanikio makubwa, yakajitokeza katika Sensa ile tuliyoifanya mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea yale ya Mheshimiwa Hasunga. Tumepokea yale ya real time ya Mheshimiwa Songe, Mbunge makini, tumepokea yale ya Mheshimiwa Swai, ya Mheshimiwa Kwagilwa nimeshajibu, ya Mheshimiwa Sillo Mwenyekiti wangu kabambe kabisa nimeshajibu, ya Mheshimiwa Hassan king nimeshajibu. Tumepokea yale ya Hotel Levy Mheshimiwa Kilumbe na tulikuwa kwenye zana na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI. Kwa sababu tutakuwa na mashauriano na tutaangalia upya haya masuala ya kikodi, niombe Wabunge waridhie kwamba yote hayo tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea hoja za Wabunge wote waliochangia kwa kuongea na wale waliochangia kwa maandishi na yote yale tutayafanyia kazi, kwa sababu bado tutakuwa na muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.