Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb) na Naibu wake Mheshimiwa Hamad Hassan Chande (Mb), Katibu Mkuu Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, Naibu Makatibu Wakuu Lawrence Mafuru, Jenifa Omolo na Amina Shaaban na wataalamu wa Wizara, Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara pamoja na wadau wa maendeleo wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayofanya katika sekta ya fedha na uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni ulizuka mzozo kati ya wafanyabiashara wa Soko la Kariakoo na Serikali ambapo wafanyabiashara walifunga biashara zao kwa takribani siku mbili. Mambo makubwa waliyolalamikia wafanyabiashara wa soko hili ni usajili wa store zao za mizigo wasioutaka, tuhuma za rushwa kwa watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wasio waaminifu, kamatakamata na kunyanyaswa na kikosi kazi (Task Force) cha TRA, viwango vikubwa vya makadirio ya kodi na utitiri wa kodi. Mpaka wafanyabiashara walipogoma, walijihisi kuwa Serikali iliwakamua sana na walikuwa na hofu ya kumaliza mitaji yao na biashara zao kufilisika kwani wakusanya kodi na ushuru walikuwa wanachukua zaidi ya kile walichokuwa wanazalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru sana Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb) kwa busara zake na kuutatua huu mgogoro kisiasa. Soko la Kariakoo linahudumia wafanyabiashara kutoka mikoa yote Tanzania na nchi za nje kama Demokrasia ya Watu wa Congo (DRC), Burundi, Malawi, Zambia, Rwanda na Uganda likiwa linaendeshwa na wafanyabiashara wakubwa, wadogo na wachuuzi. Wote hawa huliingizia Taifa letu kipato cha kutosha. Inakadiriwa kwamba soko la Kariakoo linaweza kuiingizia Serikali mpaka zaidi ya shilingi bilioni 10 kwa mwezi kama malipo ya kodi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, soko la Kariakoo likitetereka, matokeo yake ni mabaya kwani kwani litaathiri biashara nchi nzima na nchi za jirani ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa mapato hapa nchini. Kutokana na umuhimu wa soko hili kwa uchumi wa Taifa letu, ni vyema Serikali ikajipanga na kukwepesha mgogoro wa aina yoyote ule na hiki chanzo kikubwa cha mapato. Tujikumbushe kwamba ni mara ya kwanza toka tupate uhuru kuona tukio baya la mgomo katika soko letu la Kariakoo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna umuhimu mkubwa wa kuipa moyo na kuisaidia hii sekta binafsi ili waendeshe shughuli zao wakiwa na utulivu. Wakikatishwa tamaa na kuziacha biashara zao, madhara yake yatakuwa makubwa kwa Taifa letu. Kutokana na fundisho tulilolipata huko Kariakoo, naishauri Serikali ipeleke Bungeni sheria zinazolalamikiwa na wafanyabiashara na kuzifanyia marekebisho ili ukusanyaji ufanyike kwa kutumia sheria na kanuni rafiki za kikodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla, ni vyema kupitia upya na kuangalia baadhi ya vipengele vya Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sheria ya Kodi ya Mapato, Sheria ya Tozo za Huduma ya Bandari, Sheria ya Magari (kodi katika usajili na kuhamisha umiliki), Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, Sheria ya Forodha (Usimamizi na Ushuru) Sheria ya Rufaa ya Mapato ya Kodi, Sheria ya Serikali za Mitaa (Ukadiriaji) na Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Waziri akaja na mapendekezo yake katika kipindi hiki cha bajeti ili kuhakikisha Serikali inazikabili changamoto za kibiashara kwa wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, napendekeza utafiti unaofanywa na Wizara uwe endelevu na ulenge kuibua fursa mpya za mapato ya kodi na yasiyo ya kikodi ili kuongeza wigo wa walipakodi na kuondokana na kuwategemea walipakodi wachache kuiendesha nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.