Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Fedha na Mipango, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha ubunifu wa ukusanyaji mapato na usimamizi mzuri wa matumizi ya Serikali ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa miradi ya kimkakati na pia utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miezi kumi, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango imesimamia kwa ufanisi ukusanyaji mapato na utekelezaji wa miradi mingi ya miundombinu ya barabara, reli, bandari na kaadhalika. Napongeza Serikali kwa mwendelezo mzuri wa utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa umeme Mto Rufiji, Mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR pamoja na uboreshaji wa bandari utaimarisha kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi yetu. Umeme, reli na bandari ni nguzo imara ya kiushindani katika uchumi wa Tanzania na nchi za Maziwa Makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi hiki wakati dunia inapambana na athari za vita vya Urusi na Ukraine na pia janga la corona virus (covid-19), tumejifunza umuhimu wa kuwepo kwa mikakati mbadala kutokana na nchi nyingi tunazoshirikiana kibiashara na kiuchumi kukumbwa na mtikisiko wa kiuchumi. Biashara zilizoathirika kwa kiasi kikubwa ni za usafirishaji hasa wa anga uliathirika sana na napongeza mkakati wa shirika la ndege kwa utendaji wenye tija na hata kununua ndege mpya ya mizigo na kujipanga kuanza kutumia ndege zake kusafirisha mizigo. Mkakati huu ambao umetumiwa na hata mashirika makubwa ya ndege duniani, utawezesha usafirishaji wa mazao yetu ya kilimo kufikia masoko kirahisi na hapo hapo uhakika wa mapato kwa shirika la ndege hasa kipindi hiki kukiwa na uhutaji mkubwa wa usafirishaji mizigo kwa ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Msajili wa Hazina anapaswa kuendelea kuimarisha mitaji kwa mashirika ambayo yatachochea ukuaji wa uchumi ikiwemo Benki za TADB, TCB, TIB na ATCL ili iweze kusimama kibiashara ikiwa ni nguzo muhimu hata kwa sekta zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali kwa kurudisha Tume ya Mipango na hata maboresho ya Ofisi ya Msajili wa Hazina. Tume ya Mipango ni nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa nchi yetu hasa katika kipindi hiki tunapotekeleza miradi mingi ya kimkakati. Upangaji na utekelezaji wa miradi unahitaji kuwa na chombo madhubuti kinachoweza simamia miradi kitaifa badala ya kusimamiwa kisekta. Msajili wa Hazina anapaswa kupewa nguvu zaidi ili asimamie mashirika ya umma ili yaendeshwe kibiashara na kwa tija ya kiushindani kwa hapa nchini na hata nje ya nchi. Kuongezeka kwa tija kwenye mashirika ya kibiashara itapunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa mapato ya kikodi na hata mikopo kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea hata kwa kutafuta vyanzo mbadala vya fedha kugharamia ujenzi huo, kwa vile kutakuwa na fursa kubwa za usafirishaji. Pamoja na ujenzi wa SGR, napendekeza kuendelea na kuboresha reli ya TAZARA na uboreshaji wa bandari zetu ikiwemo ujenzi wa bandari kavu ikiwemo ya Inyala, Mbeya ambayo ina fursa kubwa katika kipindi hiki ili kupunguza gharama za kusafirisha pembejeo na mazao. Serikali ichukue hatua za haraka kuinusuru reli ya TAZARA hata ikibidi kurekebisha mikataba ya umiliki na uongozi ili mradi iendeshwe kwa tija. Kuna umuhimu mkubwa kuchukua hatua za makusudi kwa kutumia zaidi TAZARA kusafirisha mizigo ambayo imeelemea hata uwezo wa barabara zetu. Usafirishaji wa mizigo kwa kutumia TAZARA ilenge kupunguza gharama za usafirishaji mizigo kwa wateja wa bandari kutoka Zambia, DRC, Malawi na hata kwa kupunguza gharama za usafirishaji wa pembejeo kwa wakulima na wakati huo kupunguza gharama za kusafirisha mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza Serikali iwekeze angalau shilingi bilioni 200 kwa mwaka kwa kipindi cha miaka mitatu kwa ajili ya kuboresha mindombinu ya reli na karakana. Uwekezaji huu utawezesha TAZARA kujiendesha kwa faida na hata kuipunguzia Serikali mzigo wa kulipa zaidi ya shilingi bilioni 15 kwa mwaka ikiwa ni mishahara ya wafanyakazi wa TAZARA. Uwekezaji huu unahitajika haraka wakati Serikali za Tanzania na Zambia zinaendelea na jitihada za kurekebisha mikataba ikiwemo wa uendeshaji wa TAZARA. Pamoja na kuboresha TAZARA, napendekeza kukamilisha taratibu za ujenzi wa Bandari Kavu ya Inyala, Mbeya ambapo Mamlaka ya Bandari kwa kipindi kirefu wamewahakishia wananchi kulipa fidia ya eneo lao wanalolichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna fursa nyingi za muda mfupi za kuongeza mapato kupitia hatua za kiutawala ikiwemo ya kuondokana na matumizi na malipo ambayo hayana tija kwa Serikali na hata walipakodi. Kutokana na mahitaji makubwa ya uwekezaji kwenye miradi ya kimkakati, uchumi wetu utaendelea kuwa na mahitaji makubwa ya mikopo ya pesa za kigeni na wakati huo huo kulipa mikopo iliyoiva. Serikali iweke mkakati wa kuhakikisha mapato ya fedha za kigeni yanaongezeka kupitia mazao ya kilimo, madini na utalii. Kuongezeka kwa mapato ya fedha za kigeni yatasaidia kuimarisha uhimilivu wa deni la Taifa na pia kuendeleza utulivu wa shilingi yetu dhidi ya sarafu kuu za kigeni na hata kuhakikisha utulivu wa mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ihakikishe kipaumbele cha kuwekeza kwenye kilimo ikiwemo pembejeo na umwagiliaji kwa lengo la kuongeza tija na pia kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kulinda mfumuko wa bei. Serikali inashauriwa kuchukua hatua zaidi za kuimarisha sekta za kilimo, utalii, na madini ili kukabiliana na athari za kiuchumi wa kidunia. Kutokana na athari za kiuchumi uliokumba dunia nzima ikiwemo changamoto za upatikanaji wa fedha za kigeni, hatua za kuimarisha sekta hizo hapo juu, inaweza kuwa fursa kwa Serikali kuvutia uwekezaji zaidi kwenye madini hasa dhahabu, viwanda vya mbolea kutokana uwepo wa malighafi za madini ya calcium carbonate, lime na phosphate. Dhahabu ina historia ya bei kutoyumba kwenye soko la dunia kwa vile mabenki yanatumia dhahabu kwenye kuwekeza na kutokana pia na kuyumba kwa thamani ya shillingi na hata dola ya Marekani, Serikali inaweza kutumia dhahabu kama mbadala wa kuwekeza amana zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mabadiliko ya kiuchumi kidunia, Benki Kuu nyingi duniani zimeanza kuwekeza zaidi kwenye dhahabu na hii ni ishara nzuri kwa bei ya dhahabu kuendelea kuimarika kwenye soko la dunia ambapo kwa mwezi Aprili, 2023 bei zaidi ya asilimia 11 ukilinganisha na bei za Desemba, 2022. Serikali ijielekeze kununua dhahabu kwa shilingi toka kwa wachimbaji wadogo na kisha kuzitafutia soko la kigeni la moja kwa moja na hatua hii itapunguza na kuzuia uvujaji wa mapato ya fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Mradi wa Liganga na Mchuchuma, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya Niobium ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja na reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa kimataifa. Kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapa kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya Niobium ambayo inapatikana Milima ya Pandahill Wilaya ya Mbeya na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) yanaendelea kuwa makubwa duniani na hapa kwetu pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inahitaji kujiwekekea mikakati ya haraka (quick wins) ili kuhakikisha inaimarisha uchumi ikiwemo kuboresha urari wa biashara kukabiliana na athari za Covid-19 na sasa vita vya Urusi na Ukraine. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini, Serikali inaweza kutengeneza fursa nyingi na kupitia Mradi wa Niobium na Kiwanda cha Ferroniobium, ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakuwepo na ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (US$ 220 million) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka ni shilingi bilioni 50 (US$ 22 million) uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (modern manufacturing plant and smelter).

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuingiza teknolojia hii adimu na ujuzi (skills transfer) pia itakuwa itachangia huduma za kijamii (Corporate Social Investment in Community) na chanzo cha fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upotevu mkubwa wa fedha za Serikali ikiwemo miradi ya Serikali Kuu na Halmashauri, napendekeza Serikali kuimarisha Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani ili kuongeza ufanisi na uhuru wa Wakaguzi wa Ndani. Serikali ihakikishe Mkaguzi wa Ndani wakati wote anakuwa huru kutoka kwa Afisa Masuuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakaguzi wa Ndani wa Halmashauri wasimamiwe na Mkaguzi Mkuu wa Mkoa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Serikali iimarishe uhuru wa Mkaguzi Mkuu wa Ndani (Internal Auditor General) na napongeza Serikali kupandisha hadhi ya Ofisi kuwa na Fungu la Bajeti linalojitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.